Na John Mapepele, Dodoma
WAZIRI wa Mifugo na Uvuvi,
Luhaga Mpina ameitaka Sekta Binafsi nchini inayojishughulisha na
biashara ya mifugo na mazao yake kujitathmini na kurekebisha kasoro
zilizopo miongoni mwao ili kuiwezesha sekta hiyo kutoa mchango
unaostahili katika uchumi wa nchi hasa katika kipindi hiki cha Tanzania
ya Viwanda.
Amesema Serikali ya awamu ya tano inathamini na
kutambua mchango wa sekta binafsi katika maendeleo ya nchi na ndio maana
iko tayari wakati wowote kushughulikia changamoto zilizopo ili kuweka
mazingira wezeshi ya kufanya biashara nchini.
Akizungumza
katika kikao cha wadau wa tasnia ya Nyama, Maziwa na Ngozi jijini
Dodoma, Waziri Mpina ameelezea kusikitishwa kwake na kitendo cha wadau
wa sekta binafsi kutopendana na kuhujumiana na ndio sababu ya Serikali
kushindwa kutatua kwa wakati changamoto zinazoikabili sekta hiyo.
Waziri
Mpina amesema baadhi ya wadau wa sekta binafsi wamekuwa wakiwayumbisha
watendaji wa Serikali na watunga sera na sheria kwa kila mmoja kuvutia
upande wake huku wakiwa na mitazamo tofauti hata kama wako kwenye tasnia
moja huku baadhi yao wakipenda njia za mkato na kushindwa kufuata
taratibu na sheria zilizowekwa jambo ambalo limekuwa likisababisha
ucheleweshaji wa maamuzi serikalini.
Pia ameeleza
kuchukizwa na kitendo cha wenye viwanda vya mazao ya mifugo kuwanyonya
wafugaji kwa kununua bei ndogo mazao yao akitolea mfano maziwa na ngozi
ambapo kwa upande wa maziwa wenye viwanda hununua lita moja kwa sh 700
na baada ya kusindika wanauza sh 3,500 kwa lita, huku wenye viwanda vya
ngozi nao wakinunua kwa mfugaji kipande cha ngozi kwa sh 1,000 na baada
ya kuichakata wao wanauza kwa zaidi ya sh 60,000 jambo ambalo Serikali
haiwezi kukubali liendelee.
Mpina alisema wako baadhi ya
wenye viwanda vya maziwa,nyama na ngozi ambao hawana hata shamba la
mifugo wala maeneo ya kuhifadhia hali inayoifanya Serikali kuamini kuwa
bado sekta binafsi nchini haijaweza kujipanga vya kutosha kuwekeza
katika sekta hiyo.
Alisema ni lazima sekta binafsi na yenyewe
ifanye mageuzi ya kiuendeshaji na kimfumo ili kwenda sambamba na
mabadiliko yanayofanywa na Serikali ili kuiwezesha sekta hiyo kukua kwa
haraka na kutoa mchango unaostahili kwa maendeleo ya Taifa.
Mpina
alisema tayari Serikali iko kwenye hatua za mwisho za kupitia upya
changamoto zote zinazoikabili sekta binafsi ikiwemo za utitiri wa kodi
na tozo mbalimbali zinazotozwa kutoka kwenye taasisi mbalimbali za
Serikali ili kuharakisha ufanyaji kazi kwenye sekta hiyo.
Kuhusu
suala mikopo na mitaji kwa wawekezaji wa mazao ya mifugo amesema
Serikali itahakikisha Benki ya Maendeleo Kilimo nchini inakopesha wadau
hao ili kuongeza mnyororo wa thamani wa bidhaa wanazozalisha na kukuza
uchumi kwa haraka kwani kwa muda mrefu taasisi nyingi za kifedha
zimekuwa zikiwabagua wafugaji na wavuvi.
Mpina alisisitiza
kuwa ni mategemeo ya Serikali kuona baada ya miaka mitano Tanzania iweze
kushindana na dunia katika uzalishaji wa ya maziwa na bidhaa nyingine
za mifugo kutokana na fursa kubwa zilizopo nchini.
Aidha
Waziri Mpina alisema hatua zinazochukuliwa na Serikali kuzuia biashara
holela ya mazao ya mifugo nchini hazilengi kumkomoa mtu bali kuiwezesha
sekta binafsi nchini iweze kufanya biashara vizuri na kwa ushindani sawa
na waingizaji bidhaa hizo kutoka nje nchi.
Pia Waziri Mpina
amesema kutokana na kuripotiwa kuwepo mlundikano wa ngozi katika
maghala yaliyopo nchini na kukosa soko la kimataifa amelazimika kuunda
kamati ndogo ili kupitia na kufanya tathmini ya kina kuhusu kasoro
zilizopo kwenye tasnia hiyo ili kuwepo uelewa wa pamoja baina ya
Serikali na wadau wa ngozi, Kamati hiyo itahusisha Wizara ya Mifugo na
Uvuvi, Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji pamoja na Wizara ya
Fedha.
Hivyo aliwahakikishia wawekezaji hao kuwa pamoja na
changamoto zote zilizopo kwenye sekta binafsi nchini Serikali ya awamu
ya tano chini ya Rais Dk. John Pombe Magufuli iko pamoja nao katika
kutatua shida zote na ndio maana Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeitisha
mkutano huo ili kuwasikiliza na itaendelea kufanya hivyo mara kwa
mara.
Kwa
upande wake Katibu Mkuu Mifugo, Dk. Maria Mashingo alisema lengo la
mkutano huo ni kutambua changamoto zilizopo kwenye mnyororo wa thamani
katika sekta ya mifugo ili kuweiwezesha sekta hiyo kuzalisha bidhaa
zenye ubora na kukuza pato la Taifa
Pia aliwataka wadau wa
sekta ya maziwa kwenda kujifunza katika Kiwanda cha Maziwa cha Tanga
Fresh ili kuwezesha kuanzisha vikundi vya wafugaji wadogo ili kuwa na
uhakika wa ukusanyaji wa maziwa.
Naye Meneja Mkuu wa Tanga
Fresh, Michael Karata aliomba Serikali kuangalia uwezekano wa kuondoa
kodi ya ongezeko la thamani VAT ili kuiwezesha sekta hiyo kukuwa kwa
haraka na kuweza kushindana na mataifa mengine.
Alisema
Serikali ikiweka kiwango cha kodi sifuri gharama za uzalishaji
zitapungua na kuweza kuuza bidhaa zao kwa bei nafuu tofauti na sasa
ambapo huuza lita moja ya maziwa ya muda mrefu kwa sh 3,500.
No comments:
Post a Comment