Habari za Punde

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Tanzania Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji :Atembelea Ujenzi wa Vituo Vya Afya Wapamba Moto Nchini Kote.

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), akipewa maelezo ya Ujenzi wa Kituo cha  Afya Kiganamo katika Halmashauri ya Mji wa Kasulu,  Mkoani Kigoma, kutoka kwa Mganga Mkuu wa Halmashauri hiyo, Dkt. Mshana Dastan, alipotembelea na kufanya ukaguzi wa Kituo hicho
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) akikagua mradi wa ujenzi wa Kituo cha Afya Kiganamo, kilichopo katika Mji wa Kasulu mkoani Kigoma.
 Mganga Mkuu wa  Halmashauri ya Mji wa Kasulu Mkoani Kigoma, Dkt. Mshana Dastan (kushoto),  akitoa maelezo kuhusu ujenzi wa Chumba cha kuhifadhia maiti ikiwa ni sehemu ya majengo mapya yaliyojengwa na Serikali kwa gharama ya shilingi milioni 500, likiwemo jengo la wodi ya akina mama, maabara, nyumba ya mganga na miundombinu mingine, wakati Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), alipofanya ziara kukagua maendeleo ya ujenzi wa miundombinu ya kituo hicho cha afya.
Muonekano wa majengo mapya ya Kituo cha Afya Kiganamo, yaliyojengwa  katika Halmashauri ya Mji wa Kasulu,  Mkoani Kigoma, ambayo yapo katika hatua za mwisho za kukamilika.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb),  akikagua wodi ya wazazi katika Kituo cha Afya Kiganamo Wilayani Kasulu, Mkoani Kigoma  akiwa katika ziara ya kukagua miradi mbalimbali iliyopewa fedha na Hazina.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) akifurahia maelezo ya Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Mji wa Kasulu Mkoani Kigoma Dkt. Mshana Dastan, kuhusu namna walivyojipanga kuhakikisha kituo hicho kinaanza kutoa huduma kwa wakati kutokana na umuhimu wake kwa wakazi wa Kasulu na maeneo yanayoizunguka Wilaya hiyo.

 (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Fedha na Mipango)

Na.Benny Mwaipaja, Kasulu, Kigoma
Serikali imepanga kujenga zaidi ya vituo 120 vya afya nchini kote katika mwaka wa fedha 2018/19 ili kusogeza huduma za afya karibu zaidi na wananchi ikiwemo huduma ya mama na mtoto.
Hayo yamesemwa Mjini Kasulu, mkoani Kigoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Ashatu Kijaji, alipotembelea na kukagua ujenzi wa majengo mapya ya Kituo cha Afya Kiganamo, yaliyo gharimu shilingi milioni 500.
Amesema kuwa tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani imeongeza bajeti ya Wizara ya Afya kutoka shilingi bilioni 30 hadi kufikia shilingi bilioni 369, hatua iliyolenga kuboresha afya za wananchi kwa kuwa hakuna maendeleo kama wananchi watakuwa na maradhi.
“Awamu ya Tano ilianza na ujenzi wa vituo 44 vya afya na kufuatiwa na vituo 74 na sasa  vituo takribani 120 vinaendelea kujengwa maeneo mbalimbali ili kutimiza lengo la kuwa na Kituo cha Afya kwa kila Kata”, alieleza Dkt. Kijaji.
Dkt. Kijaji, alisema Serikali imeweka utaratibu wa Kata ambazo zipo jirani kutumia kituo kimoja wakati lengo kuu la kujenga kituo kimoja cha afya kwa kila   Kata likiendelea kutekelezwa katika uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano.
Aidha amebainisha kuwa Sekta ya Afya inatazamwa kwa upana wake na ndio sababu Serikali inaboresha pia miundombinu ya Maji ili wananchi waweze kupata maji safi na salama ili kuimarisha Afya zao.
Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Mji wa Kasulu, Dkt. Mshana Dastan, amemweleza Dkt. Kijaji kwamba kukamilika kwa majengo hayo mapya ya Kituo cha Afya  Kiganamo, kutaimarisha utoaji wa huduma za afya kwa kuwa, kinategemewa na idadi kubwa ya watu wanaotoka ndani na nje ya Halmashauri ya Mji wa Kasulu.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mji wa Kasulu, Bi. Fatina Laay, amesema kuwa wagonjwa katika zahanati hiyo wamekuwa wakilala zaidi ya watatu kwenye kitanda kimoja na kwamba kukamilika kwa ujenzi wa majengo hayo yaliyokamilika kwa zaidi ya asilimia 98 kutaondoa changamoto hiyo.
"Mbali na Serikali kutupatia kiasi hicho cha shilingi milioni 500, mwisho mwa mwaka wa fedha uliopita, Serikali imetupatia kiasi kingine cha shilingi milioni 400kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Hedu Juu, kitakacho saidia kutoa huduma wa watu walioko pembezoni" Alieleza Bi. Laay.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Ashatu Kijaji, yuko mkoani Kigoma kwa ziara ya kikazi kutembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo inayopatiwa fedha na Hazina pamoja na kuzungumza na jumuiya ya wafanyabiashara.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.