Bw.
Faustine Edward Msimamizi wa kituo cha Tohara cha
Katoro Bw. Faustine Edward, akizungumza na wakazi wa Katoro waliojitokeza
kupata huduma hiyo ya bila malipo, inayotolewa na Taasisi ya kimataifa
inayojihusisha na masuala ya Afya ya IntraHealth katika kituo cha afya Katoro,
ambapo wanatahiri watu 20 hadi 30 kwa siku. Hapa hupewa elimu kabla ya
kufanyiwa tohara.
Wakazi wa Katoro wakisubiri kupata
huduma ya Tohara ya bila malipo, inayotolewa na Taasisi ya Kimataifa
inayojihusisha na masuala ya Afya ya IntraHealth katika kituo cha afya Katoro.
kutahiriwa Madaktari wakimtahiri mmoja wa wakazi
wa Katoro,wakati wa huduma hiyo ya bila malipo inayotolewa na Taasisi ya
kimataifa inayojihusisha na masuala ya Afya ya IntraHealth katika kituo cha
afya Katoro.
Ikiwa
zimesalia siku chache kabla ya kumalizika kwa robo ya kwanza, ya Kampeni ya
Toharakinga kwa Wanaume wenye umri kuanzia miaka kumi na kuendelea inayoendeshwa
mkoani Geita, kundi la wanawake limebainika kuwa chachu ya kufanikisha mpango
huo kutokana na wengi wao kuwahimiza wanaume wao na watoto kwenda kufanyiwa Tohara.
Hadi
kufikia Sepetemba 2018, wanaume 115, 000 kati ya 119, 000 waliolengwa kufanyiwa
tohara Mkoani Geita walikuwa wamefikiwa na kuhudumiwa katika kampeni
inayoendeshwa na Serikali kwa ushirikiano na Shirika lisilo la kiserikali la
IntraHealth International kwa ufadhili wa Mfuko wa Rais wa
Marekani wa Kupambana na Maambukizi ya Virusi vya UKIMWI (VVU) PEPFAR kupitia
CDC,
Kituo cha Afya Katoro
ni kati ya vituo 23 vya muda na 13 vya kudumu vinavyotoa huduma hiyo ambayo
kabla ya kutolewa wanaume wanaofika kufanyiwa tohara hupitia hatua kadhaa
ikiwemo kuandikishwa, kuelimishwa na kupimwa virusi vya UKIMWI kabla ya huduma.
Msimamizi
wa Kituo hicho, Bw. Faustine Edward alisema muitikio wa wananchi umekuwa mkubwa
kiasi cha kuwafanyia tohara wanaume kati ya 10 hadi 30 kwa siku.
“Mwitikio ni mkubwa sana, wateja ni wengi,
hadi tunafikiria kuongezewa muda kwakuwa tulianza zoezi hili mwezi Novemba 15,
2018 na mwisho ni mwezi Desemba 15, 2018; Lakini pia niwapongeze akinamama,
wamekuwa mabalozi wazuri kwa kuwaleta watoto wao lakini pia kuwashawishi waume
zao kuja kufanya Toharakinga salama hadi kutuwezesha kupata watu 10 hadi 30 kwa
siku,” alisema Bw. Edward
Pamoja
na muitikio huo, Bw. Edward Alisema zipo baadhi ya changamoto zinazoikabili
kampeni hiyo ikiwemo upungufu wa miundombinu ya jengo la kutolea huduma kwa
sasa, imani potofu kutoka kwa baadhi ya wananchi kuhusu tohara na kutozingatia
ushauri wa kitaalam kwa baadhi ya wanaofanyiwa tohara kutumia njia za asili za
kutibu vidonda.
“Baadhi ya wanaotahiriwa wakirejea majumbani husikiliza
na kutumia ushauri wa mitaani ikiwemo kutumia kinyesi cha Ng’ombe kupakwa
kwenye kidonda wakiamini husadia kupona haraka, jambo linalosababisha madhara
kiafya. Tunakabiliana na tatizo hili kwa kutoa elimu kwa wananchi na tiba
sahihi tatizo linapojitokeza,”alisema Edward
Kwa
upande wake Bi. Winfrida John, Mkazi
wa Ludete Stooni amekuwa shuhuda wa kupitia mtoto wake kutosumbuliwa na
maambukizi kwenye njia ya mkojo (UTI) baada kufanyiwa Toharakinga aliyosema inasaidia
usafi na kuepusha magonjwa mbalimbali ya zinaa huku akiwaasa wanawake na
wananchi kwa ujumla kujitokeza kuunga mkono kampeni hiyo.
Bw. Masunga Maduhu ni mmoja wa wanaume waliofanyiwa Toharakinga
wakiwa na umri wa miaka 34, ambaye katika mahojiano alisema hakupata madhara
wala kusikia maumivu wakati wa tohara na kuiomba Serikali na wadau wengine
kuendeleza huduma hiyo hadi maeneo ya vijijini.
“Pamoja
na faida ya kujiepusha na maambukizi ya UKIMWI kwa asilimia 60, tohara pia
imeniongezea kujiamini kiasi cha kuweza kujisaidia haja ndogo bila hofu mbele
ya watu wengine kulinganisha na awali nilipokuwa naona aibu nikijificha kwa
sababu nilikuwa sijafanyiwa tohara,” alisema Maduhu
Naye
Bw. Peter Ngaseba, Mkazi wa Katoro
Stooni amesema, usafi na kuepuka maambukizi ya virusi vya UKIMWI kupitia hamasa inayoendelea kufanywa na wataalam mtaani
wakiwapa elimu na vipeperushi ndiyo imempa msukumo.
Alienda
mbali zaidi kwa kusema tohara imeongeza hamasa na uwezo wake katika tendo la
ndoa kutokana na kujiamini.
Vilevile,
tunatakiwa kuelewa kwamba Toharakinga salama inazo faida kemkem zikiwemo
kupunguza uwezekano wa kupata magonjwa ya zinaa ambayo nayo huchangia kwa kiasi
kikubwa maambukizi ya virusi vya UKIMWI, kupunguza uwezekano wa kupata saratani
ya kichwa cha Uume, saratani ya mlango wa kizazi kwa akina mama, kukosa uwezo
wa kutungisha mimba, uvimbe wa kichwa cha Uume na magonjwa mengine ya zinaa.
No comments:
Post a Comment