Kwa kutambua umuhimu wa michezo kwa maendeleo ya Zanzibar
Awamu zote Saba za uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zimefanya
jitihada mbali mbali za kuimarisha sekta ya michezo ikiwemo miundombinu ya michezo
hasa ujenzi wa viwanja.
Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein ameyasema hayo leo
huko katika uwanja wa Gombani Pemba mara baada ya kushiriki kikamilifu katika
Bonanza maalum la Mazoezi ya Viungo ambalo lilianzia Wawi Matrekta hadi uwanja
wa Gombani Chake Chake Pemba.
Mazoezi hayo ya viungo
yalivishirikisha vikundi mbali mbali vya mazoezi kutoka Unguja, Tanzania Bara
pamoja na wenyewe kutoka Pemba ambapo pia, yaliwashirikisha viongozi mbali
mbali wa vyama vya siasa na Serikali akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd pamoja na
wananchi.
Katika hotuba yake aliyoitoa
mara baada ya mazoezi hayo ambayo hufanyika Kitaifa kila mwaka mnamo tarehe
mosi ya mwezi wa Januari, Dk. Shein alisema kuwa katika Awamu ya mwanzo ya
Marehemu Mzee Abeid Amani Karume ulijengwa uwanja wa Amaan ambao ni wa kisasa
wenye viwango vya Kimataifa uliofunguliwa rasmi mwaka 1970.
Aidha, katika Awamu ya
Nne Marehemu Sheikh Idriss Abdulwakil alianzisha ujenzi wa uwanja wa Gombani
Pemba.
Katika utekelezaji wa
Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka 2015-2020, Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar, Awamu ya Saba imefanya jitihada kubwa za kuimarisha miundombinu ya
michezo ikiwa ni pamoja na kukifanyia matengenezo na kukiwekea majani ya bandia
na mpira wa kukimbilia kiwanja cha Amaan na Gombani.
Vile Vile, Rais Dk.
Shein alisema kuwa kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China
kimejengwa upya kiwanja cha michezo cha Mao Tse Tung ambacho kinaweza kutumika
kwa michezo mbali mbali .
Kwa maelezo ya Rais Dk.
Shein kiwanja hicho kinaweza kutumika kwa michezo ya mpira wa mikono, mpira wa
wavu, mpira wa vikapu, mpira wa pete na mpira wa miguu hatua ambayo itaondokana
na tatizo la uhaba wa viwanja vya michezo na kusaidia kuimarisha sekta ya
michezo.
Pia, Rais Dk. Shein
alieleza kuwa Serikali imeanza hatua ya ujenzi wa kiwanja kimoja cha michezo
kwa kila Wilaya ya Zanzibar kama ilivyoelekezwa katika Ilani ya CCM ya Uchaguzi
Mkuu ya mwaka 2015-2020.
Aliongeza kuwa Serikali
imekamilisha ujenzi wa uwanja wa
Kitogani katika Wilaya ya Kusini, Mkoa wa Kusini Unguja na hatua za
ujenzi wa kiwanja cha michezo cha Kishindeni katika Wilaya ya Micheweni na
kiwanja cha Kangani katika Wilaya ya Mkoani zinaendelea.
Rais Dk. Shein alieleza
kuwa maandalizi ya ujenzi wa uwanja wa Wilaya ya Kaskazini A huko Mkokotoni
nayo yataanza hivi karibuni.
Pamoja na hayo, Rais Dk.
Shein alisisitiza kuwa bado ana imani kuwa iwapo utawekwa mbele uzalendo,
ubunifu na kurudisha ari na hamasa ya kupenda timu za nyumbani kuliko za nje
timu za nyumbani zitaweza kufanya vizuri katika mashindano.
Aliwahimiza wananchi
kuzionea ufahari na kuzipenda timu za za nyumbani kwani mtu kukipenda chake si
ila isipokuwa ni wajibu jambo ambalo ni ishara ya uzalendo na litasaidia kuwapa
moyo wachezaji ili michezo iimarike zaidi nchini.
Rais Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kutoa wito kwa wafanyabiashara na sekta binafsi kuziunga mkono
juhudi za Serikali katika sekta ya michezo kwani michezo ina nafasi nzuri
katika kuzitangaza biashara na inasaidia katika matamasha na kampeni za
shughuli zinazofanywa na asasi za kiraia.
Alieleza jinsi
anavyothamini jitihada za wawekezaji wote walioahamasika kuweka huduma za
michezo katika hoteli za kitalii akiwemo Said Salim Bakhressa aliyeanzisha
kichezo ya maji katika hteli ya Verde pamoja na mwekezaji Subash Patel
aliyejenga kiwanja cha gofu katika hoteli ya Sea Cliff, Magapwani.
Sambamba na hayo, Rais
Dk. Shein alitoa wito kwa Wizara ya
Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na Wizara ya Habari, Utalii na Mambo
ya Kale kuendelea kushirikiana ili walitumie Tamasha la Utalii la Zanzibar la
kila mwaka katika kukuza michezo na kuimarisha sekta ya utalii ambayo
inachangia pato la Zanzibar.
Dk. Shein aliupongeza
uongozi wa Wizara ya Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Baraza la Taifa la
Michezo pamoja na Chama cha Mazoezi ya Viungo (ZABESA) kwa maandalizi mazuri ya
bonaza la mwaka huu ambalo kwa mara ya kwanza limefanyika kisiwani Pemba.
Nae Waziri wa Vijana,
Utamaduni, Sanaa na Micezho Balozi Ali Abeid Karume alieleza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
katika kuimarisha sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya michezo.
Mapema Kamishna wa
Michezo Sharifa Khamis alieleza kuwa Wanamichezo wamefarajika na juhudi za Rais
Dk. Shein anazozichukua katika kuhakikisha michezo inakua na kuendelea na ndio
maana akaamua kufanya matengenezo ya viwanja vya Amaan, Gombani, Mao Tse Tung.
Nao Uongozi wa ZABESA
katika risala yao walieleza umuhimu wa mazoezi kwa mwanaadamu huku wakitumia
fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Shein kwa kuwakubalia maombi yao likiwemo
kufanyika kwa Bonanza hilo kisiwani Pemba mwaka huu.
Pia, ujenzi wa viwanja
vya kila Wilaya, kuwapatia eneo kwa ajili ya ujenzi wa Uwanja wa Taifa pamoja
na kuziwezesha timu za Taifa kushiriki mashindano ya Kitaifa.
Pia, Kamishna huyo
alimuarifu Rais Dk. Shein kuwa eneo la ujenzi wa Uwanja wa kisasa wa michezo
wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 60,000 huko Tunguu Wilaya ya Kati Mkoa wa
Kusini Unguja limeshapatikana na limeshaanza kupimwa.
Katika hafla hiyo Rais
Dk. Shein alitoa vyeti maalum kwa Vikundi Shiriki pamoja na waazilishi na
viongozi wa ZABESA ambapo pia, Balozi Seif Ali Idd nae alitoa vyeti maalum kwa
wadhamini wa Bonanza hilo.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment