Habari za Punde

Uzinduzi wa Skuli ya Msingi Chimba Wilaya ya Micheweni Kisiwani Pemba Leo Ikiwa ni Shamra Shamra za Miaka 55 ya Mapinduzi ya Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akikata Utepe kuashiria Uzinduzi wa Skuli ya Msingi Chimba Wilaya ya Micheweni Shehia ya Chimba, ikiwa ni shamra shamra za Miaka 55 ya Mapinduzi ya Zanzibar, zilizoaza leo Kisiwani Pemba.kushoto Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mhe. Riziki Pembe.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein  amewataka wananchi kuiunga mkono Serikali yao ya Mapinduzi ya Zanzibar ambayo imeamua kwa makusudi kutoa elimu bure kuanzia Chekechea, Msingi hadi Sekondari.

Dk. Shein aliyasema hayo leo huko Chimba, Wilaya ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba katika uzinduzi wa Skuli ya Msingi ya Chimba ikiwa ni miongoni mwa shamrashamra za maadhimisho ya miaka 55 ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964.

Alisema kuwa Serikali ya Mapianduzi ya Zanzibar itaendelea kutoa elimu bure na kuwataka wazazi wasitoe fedha kwa ajili ya matumizi ya ufagio na wala kununua chaki na badala yake kazi hiyo ni ya Wizara na Serikali itatoa gharamia gharama zote.

Alisema kuwa jambo hilo ni kubwa na Serikali itaendelea kugharamika kwa wananchi wake kwa kila hali na lisilobudi litafanywa na kusisitiza kuwa elimu haina mbadala.

Rais Dk. Shein aliwakata wazee kutochangia chochote na kama kuna mapungufu basi Serikali itafanya kazi wenyewe la wala sio wao.

Alisema kuwa elimu inatolewa bure kuanzia Chekechea, Msingi hadi Serkondari na kuwataka wananchi kuwaepuka wale wanaosema uongo kuhusu Serikali yao ambayo imekuwa ikiendelea kuimarisha sekta za maendeleo kila pembe ya Zanzibar.

Alieleza kuwa hadi mwisho wa mwaka jana uchumi wa Zanzibar umekuwa kwa asilimia 7.7 na sio kweli wale wanaosema kuwa uchumi wa Zanzibar umeanguka na kueleza kuwa kama ni hivyo Serikali isingeweza kutoa elimu zote bure.

“Msiwasikilize waongo wengine ni waongo na watu wazima hawaambiwi waongo....vile vile nataka kukwambieni kuwa afya pia bure...kwani Serikali imeamua afya nayo kuwa bure ”alisema Dk. Shein.

Dk. Shein alishangazwa na baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa kutoa takwimu za uongo na kuwataka wananchi kuwasikiliza viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kuachana na wale wanaosema uongo kwa kuwadanganya wananchi.

Rais Dk. Shein aliwasisitiza wananchi kuwaendeleza watoto wao kusoma ili waweze kujipatia manufaa wao na nchi yao.

Aidha, alisema kuwa wananchi wanaposhikana maendeleo makubwa yanapatikana na iwapo neema watazibeza Mwenyezi Mungu huleta mtihani na kusisitiza kuwa hapana haja ya kuleta utani katika elimu kwani imetukuka.

Alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haina mbadala na elimu  na itasimama kidete katika kuhakikisha sekta ya elimu inaimarika huku akitumia fursa hiyo kuwaahidi wananchi wa Chimba kuwa skuli yao itajengwa hadi elimu ya Sekondari  katika kijiji chao.

Rais Dk. Shein  alisema kuwa kazi kubwa ya kuwapelekea maendeleo wananchi wa Zanzibar inafanywa na CCM, hivyo aliwataka wananchi wa Chimba wasidanganyike kwani hakuna mbadala wa elimu.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alisema kuwa lengo la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuwasomesha watoto wote ili waje kuwa wataalamu na kuwataka wazee kukaza kamba na walimu nao kwa upande wao wawasaidia watoto.

Pia, aliwataka walimu kuwasomesha na kuwasaidia vyema watoto pamoja na jamii nzima kwani zamani watoto wakilelewa na Kiambo jambo ambalo hivi sasa halipo na kuitaka jamii kuishi kwa mapenzi na kulea kwa pamoja watoto wao.

Rais Dk. Shein aliiagiza Wizara ya Elimu kutafuta walimu haraka na kuwapeleka katika skuli ya Chimba kutokana na upungufu wa walimu uliopo kwani Serikali inataka kwenda na kasi ya CCM katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 ikiwa ni pamoja na kuimarisha sekta ya afya.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein  alieleza kuwa umuhimu wa elimu Zanzibar umeelezwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na chama cha ASP.

Alieleza kuwa wakati kunaanzimishwa miaka 55 ni lazima kukubukwe mambo makubwa mazito yaliyofanywa katika kupata ukombozi na uhuru wa Zanzibar.

Alisema kuwa ASP ilipigania uhuru ili wananchi wa Zanzibar waishi bila ya kutawaliwa na kuondosha madhila kwani wakoloni walikuwa wakipokezana katika kuitawala Zanzibar.

Alisema kuwa zaidi ya karne nne Zanzibar ilitawaliwa na kabla ya hapo Zanzibar haikutawaliwa na ilikuwa huru na licha ya kutafuta uhuru kwa demokrasi haukupatikana na ndipo yakafanyika Mapinduzi ya Januari 12, 1964 chini ya ASP na uongozi wa  Mzee Karume.
  
Alisema kuwa mambo makubwa aliyoyaahidiwa Rais Abeid Karume yalitekelezwa ikiwa ni pamoja na elimu ambayo itakuwa yenye manufaa kwa watu wote tena bila ya ubaguzi, ardhi yote itakuwa mali ya serikali na leo ndivyo ilivyo pamoja na wananchi kupata heka tatu tatu, afya kuwa bure pamoja na elimu bure.


Alieleza kuwa mnamo mwezi Machi mwaka 1965 Rais Abeid Karume alitangaza afya bure na hadi hivi leo miaka 54 afya hailipiwi isipokuwa wananchi wanachangia tu jambo ambalo hakuna hata nchi moja duniani inayofanya hivyo kama ilivyo kwa Zanzibar.

Alisema kuwa maendeleo yote yanaletwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ikiwemo sekta ya elimu.

Nae Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Riziki Pembe Juma alieleza kuwa  wananchi wote wa Chimba wamefarajika kwa kuona kwamba jengo hilo aliloliweka jiwe la msingi Rais Dk. Shein amelifungua mwenyewe.

Alisema kuwa tayari Wizara yake imeshajenga madarasa mengi sana na kutoapongezi kwa Dk. Shein kwa uongozi wake kwa kuwapelekea maendeleo wananchi wote bila ya kujali vyama vyao vya siasa, dini, rangi wala kabila.

Alisema kuwa tayari madarasa mengi yameshajengwa yakiwemo madarasa ya kwenye skuli mpya za ghorofa ambapo hadi sasa kuna skuli zisizopungua 600, na kutoa shukurani huku akiahidi Wizara yake itaendelea kumuunga mkono Rais Dk. Shein  katika kuhakikisha malengo ya Mapinduzi yanaendelea kusimamiwa.

Mapema Katibu  Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Dk. Idrisa Muslih Hija alieleza kuwa skuli hiyo ni miongoni mwa skuli zilizopo katika Wilaya ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba ambapo wazo la kuanzisha skuli hiyo lilitokana na wananchi wenyewe ikiwa ni hatua ya kukabialiana na tatizo la wanafunzi wanaoishi vitongoziji vya Bule, Jichwa, Maziwa njia na Pombwe kwa kwenda masafa marefu.

Alieleza kuwa katika ziara yake Rais Dk. Shein kijijini hapo mnamo Julai  22 mwaka 2017  wakati wa ziara yake alipokwenda kuweka jiwe la msingi kituo cha afya  Chimba ambapo wananchi walipata fursa ya kueleza changamoto yao ya skuli na Rais aliahidi kuwa Serikali itaunga mkono na Wizara pamoja na Halmashauri, wananchi , Mbunge na Mwakilishi pamoja na wananchi wapenda maendeleo walitoa michango yao.

Alisema kuwa wanafunzi wanaotarajiwa kuandikishwa darasa la kwanza katika maeneo ya Chimba ni 185 ambapo hadi hivi sasa wanafunzi  walioahikishwa ni 145   wakiwemo wanafunzi 76 wanaotoka katika vituo vya TUTU na wanafunzi 69 wanaotoka mitaani.

Alieleza kuwa upande wa wanafunzi wa maandalizi bado wanaendelea kuandikishwa katika vituo vya TUTU ambavyo viko vitatu vilivypo katika Shehia ya Chimba na hadi sasa vimeshaandikisha jumla ya wanafunzi 86.

Alisema kuwa Ujenzi wa Skuli ya Chimba ulianza rasmi mnamo Juni 23 mwaka 2012, ambapo skuli hiyo ina madarasa 4, vyoo,ofisi za walimu na hadi kukamilika kwa ujenzi huo umegharimu Shilingi za Tanzania milion 92.5.
  
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.