RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Balozi wa Kuwait Nchini
Tanzania Mhe.Mubarak Mohammed Alsehaijan, alipofika Ikulun Zanzibar kwa
mazungumzo na kujitambulisha leo.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali
Mohamed Shein, akizungumza na mgeni wake Balozi wa Ethiopia Nchini Tanzania
Mhe. Yonas Yosef, alipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo na kujitambulisha.leo
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali
Mohamed Shein, akizungumza na mgeni wake Balozi wa Misri Nchini Tanzania Mhe.Gaber
Mohamed, alipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo na kujitambulisha leo
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein amekutana na kufanya mazungumzo na Mabalozi wa nchi za
Kuwait, Ethiopia na Misri ambapo mazungumzo hayo yalijikita zaidi katika
kuimarisha uhusiano na ushirikiano sambamba na kuendelea kuiunga mkono Zanzibar
katika juhudi za kujiletea maendeleo.
Mazungumzo hayo
yalifanyika kwa nyakati tofauti Ikulu mjini Zanzibar ambapo Mabalozi hao
walifika kwa ajili ya kujitambulisha kwa Rais Dk. Shein, miongoni mwao ni Balozi wa Kuwait nchini
Tanzania Mubarak Mohammed, Balozi wa Ethiopia nchini Tanzania Yonas Yosef na
Balozi wa Misri nchini Tanzania Gaber Mohamed.
Katika mazungumzo yao
Mabalozi hao walipongeza mafanikio yaliofikiwa Zanzibar na kuahidi kuendelea
kuyaunga mkono huku wakitumia fursa hiyo kutoa pongezi maalum kwa Rais Dk.
Shein pamoja na wananchi wote wa Zanzibar kwa kufanikisha Sherehe za miaka 55
ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya Januari 12, 1964 ambazo zilifana kwa kiasi
kikubwa.
Akizungumza na Balozi
wa Kuwait, Rais Dk. Shein alitoa pongezi kwa nchi hiyo kwa kuendelea kuiunga
mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo na kuupongeza
Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait
kwa kuiunga mkono Zanzibar.
Rais Dk. Shein alisema
nchi ya Kuwait imekuwa ikiiunga mkono na
kutoa ushirikiano mkubwa kwa Zanzibar katika kuimarisha sekta za maendeleo
ikiwemo sekta ya afya, elimu, kilimo na nyenginezo huku akiwakaribisha
wawekezaji wa nchi hiyo kuja kuekeza Zanzibar .
Nae, Balozi wa Kuwait
nchini Tanzania Mubarak Mohammed alieleza azma ya nchi yake ya kuendelea
kushirikiana na Zanzibar kwa lengo la kukuza uhusiano na ushirikiano uliopo na
kuelezea azma ya kusaidia kuimarisha
sekta za afya, elimu na Kilimo hapa nchini.
Rais Dk. Shein pia,
alifanya mazungumzo na Balozi wa
Ethiopia nchini Tanzania Yonas Yosef ambapo katika mazungumzo hayo, Balozi huyo
alimueleza Dk. Shein mafanikio yaliofikiwa na nchi yake kiuchumi, kisiasa na
kijamii ikiwa ni pamoja na kukua kwa Shirika la ndege la ‘Ethiopia Airlines’, pamoja na kurejesha
uhusiano kati ya Ethiopia na nchi jirani ya Eritrea.
Aidha, Balozi huyo
alimueleza Rais Dk. Shein kuwa kurejea kwa uhusiano kati ya nchi yake na
Eletria kutaimarisha shughuli za kimaendeleo sambamba na kukuza hali ya amani
katika ukanda wa nchi hizo pamoja na nchi jirani za Sudan, Djibout.
Balozi huyo pia,
alimueleza Rais Djk. Shein kuwa kuimarika kwa sekta ya usafiri kupitia Kampauni
ya ndege ya ‘Ethiopia Airlines’ , kutaongeza idadi ya watalii wanaofika Zanzibar
pamoja na kutoa huduma bora za usafiri kwa wananchi wa pande mbili hizo ambapo
pia, Balozi huyo alieleza mafanikio yaliofikiwa na Serikali ya Ethiopia katika kuweka
usawa wa jinsia katika nafasi za uongozi.
Nae, Rais Dk. Shein
alitumia fursa hiyo kumueleza Balozi huyo kuwa Ethiopia na Tanzania zina historia ya muda
mrefu katika ushirikiano na uhusiano tokea wakati wa mapambano ya kudai uhuru
ambapo waasisi wa nchi mbili hizo akiwemo Haile Salassie na Mwalimu Julius Kambarake Nyerere walishirikiana.
Dk. Shein alieleza
kuwa Zanzibar inathamini sana juhudi za kiongozi huyo ambaye ni muasisi wa
Ethiopia katika harakati zake za ukombozi wa Mwafrika na ndio maana Zanzibar ikaweka
alama kwa kuiita jina la kiongozi huyo skuli ya Sekondari ya Haile Salassie
iliyopo mjini Zanzibar.
Katika maelezo hayo,
Rais Dk. Shein alisema kuwa kabla ya ukoloni Bara la Afrika lilikuwa moja na
ndio maana hadi hivi leo licha ya kuwepo nchi mbali mbali ndani ya Bara hilo
lakini bado Waafrika wote ni ndugu na wamekuwa wakiendeleza ushirikiano wao.
Alitumia fursa hiyo
kutoa pongezi kwa Waziri Mkuu mpya wa Ethiopia Abiye Ahmed kwa kurejesha hali
ya uhusiano na ushirikiano kati ya Ethiopia na Eritrea hatua itaakyoimarisha
maendeleo kati ya pande hizo sambamba na kukuza uchumi na kujenga udugu wa
wananchi wake pamoja na wananchi wote wa Bara la Afrika.
Rais Dk. Shein
alieleza mafanikio makubwa yaliopatikana hapa Zanzibar kwa kuwepo huduma za
usafiri wa ndege za Kampuni ya ‘Ethiopia Airlines’ ambazo zimeweza kuongeza
idadi ya watalii wanaokuja kuitembelea Zanzibar hasa ikizingatiwa kwamba sekta
hiyo ina umhimu mkubwa kwa uchumi wa Zanzibar.
Aidha, Dk. Shein alieleza
haja kwa nchi hiyo kufungua Ubalozi wake mdogo hapa Zanzibar huku akipongeza
ahadi za Balozi huyo kwa nchi yake kuendelea kutekeleza Makubaliano ya Mkataba
kati yake na Tanzania ambayo alisema yatazidi kufungua milango ya ushirikiano.
Wakati huo huo,Rais Dk. Shein
alikutana na Balozi wa Misri nchini Tanzania Gaber Mohamed ambaye Balozi huyo
alitumia fursa hiyo kumuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Misri itaendelea kuiunga
mkono Zanzibar katika kuendeleza sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya kilimo,
mafunzo na uwezeshaji wa programu mbali mbali kupitia sekta hiyo na nyenginezo.
Balozi huyo wa Misri
alimueleza Dk. Shein kuwa nchi yake iko tayari kuanzisha maeneo mengine ya
ushirikiano kwa azma ya kukuza uhusiano na ushirikiano uliopo huku akiahidi
juhudi zitaongezeka kushajihisha watalii kutoa Misri kuja kuitembelea Zanzibar.
Aidha, Balozi huyo
alieleza hatua zitakazofuata katika kuhakikisha kunakuwepo ushirikiano kati ya
wafanyabiashara na wenye Kampuni wa Misri na Zanzibar kwa kuwaweka pamoja kwa
lengo la kubadilishana mawazo na kutafuta njia bora za kukuza biashara na uwekezaji.
Nae, Rais Dk. Shein
kwa upande wake alitumia fursa hiyo kuipongeza Misri kwa kuendelea kushirikiana
na Zanzibar na kueleza kuwa ushirikiano na uhusiano huo ni wa muda mrefu tokea uwepo
wa waasisi wa nchi mbili hizo akiwemo kiongozi wa Misri Gamal Abdulnasir ambaye
alikuja kuitembelea Tanzania, pamoja na kufika Zanzibar.
Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kuipongeza Misri kwa kuleta wataalamu hapa Zanzibar wakiwemo
wataalamu wa kilimo ambao walisaidia sana kutoa mafunzo ya kilimo hapa nchini
huku akisisitiza haja kwa nchi hiyo kuleta wataalamu wakiwemo Madaktari bingwa
wa afya kupitia programu maalum.
Aidha, Rais Dk. Shein
alieleza haja kwa Misri kuleta wataalamu katika sekta ya michezo hasa
ikifahamika kwamba hapo siku za nyuma nchi hiyo imeshawahi kuleta wataalamu
wake na kuja kutoa mafunzo ya michezo hapa nchini hasa kwa timu ya vijana
katika mchezo wa mipira wa miguu
Pamoja na hayo, Rais
Dk. Shein alieleza kuwa Wanazuoni, Masheghe na Maulamaa wengi wa Zanzibar
walipata elimu zao za dini ya Kiislamu kutoka Misri, hivyo ipo haja kuendeleza
utamaduni huo wa kushirikiana kati ya nchi hiyo na Zanzibar ili mafunzo hayo ya
elimu ya dini yaendelee na kuzidi kuleta tija kwa jamii.
Rais Dk. Shein
alisisitiza haja ya kuwepo kwa mashirikiano kati ya Chuo Kikuu cha Taifa cha
Zanzibar (SUZA) na Chuo Kikuu cha Elexandria cha nchini Misri pamoja na kuendeleza
mradi wake wa umeme wa kutumia nguvu za jua ambao unaweza kuwa mkombozi wa nishati
ya umeme kwa Tanzania pamoja na Zanzibar.
Sambamba na hayo, Rais
Dk. Shein aliwaahidi Mabalozi hao wote kuwa yeye pamoja na Serikali
anayoiongoza wataendelea kufanya kazi nao vizuri kwa lengo na azma ile ile ya
kukuza uhusiano na ushirikiano kati ya nchi hizo na Tanzania ikiwemo Zanzibar.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment