Habari za Punde

Makamu Mwenyewkiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Shein, Azungumza na Viongozi wa CCM Wilaya ya Chakechake Pemba.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ina mpango wa kujenga uwanja wa ndege wa kisasa kisiwani Pemba ikiwa ni moja ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM.

Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika ukumbi wa Kiwanda cha Makonyo Wawi Chake Chake Pemba wakati alipofanya mazungumzo na viongozi wa CCM wa Wilaya ya Chake Chake pamoja na kufanya majumuisho ya ziara ya Wilaya hiyo ambapo viongozi mbali mbali wa Chama na Serikali walihudhuria akiwemo Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein.

Katika maelezo yake Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Rais Dk. Shein alieleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inayoongozwa na CCM ni kujenga uwanja mpya na wa kisasa wa ndege kisiwani Pemba utakaoruhusu kutua ndege kubwa za aina zote.

Alieleza kuwa uwanja huo utakuwa wa kisasa na mkubwa utakaoruhusu ndege za aina zote kubwa kutua katika kiwanja hicho hatua ambayo itasaidia kwa kiasi kikubwa usafiri wa anga katika kisiwa hicho na Zanzibar kwa jumla.

Alieleza kuwa tayari mchakato wake wa mwanzo umeanza na ameshatuma Mawaziri kumi kwenda kwa wananchi wanaoishi katika maeneo ya pembezoni mwa uwanja wa ndege kisiwani Pemba wakiwemo wananchi wa Mfikiwa, Furaha na Mvumoni ili wakae tayari mara tu ujenzi utakapoanza waweze kuondoka katika eneo hilo na kupewa fedha kwaajili ya mali zao.

Rais Dk. Shein alisema kuwa tayari upembuzi yakinifu umeshafanywa kwa ajili ya uwanja huo mpya wa ndege na karibu TZS milioni 500 zimetumika na hivi sasa Serikali imo katika hatua za kutafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi huo na kuwataka wananchi kuwa na subira hasa wale wanaoishi pembezoni mw auwanja huo na kuahidiwa kupewa fidia mara tu ujenzi utakapoanza.

Aidha, Dk. Shein amewasisitiza Wawakilishi wa CCM wa Majimbo yaliyomo katika Wilaya ya Chake Chake kuongeza kasi ya kushirikiana kwa kwenda kufanya kazi nyumba ili kuwashughulikia wananchi kwa azma ya kutatua changamoto walizonazo.

Makamu Mwenyekiti huyo wa CCM alitoa pongezi kwa taarifa nzuri zilitolewa na Wilaya hiyo ikiwemo ile ya Chama na Serikali pamoja na kuzipongeza taarifa zote za Mikoa yote miwili ya Pemba na Wilaya zake nne.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa ujenzi wa barabara ya Chake Chake-Mkoani pamoja na barabara ya Chake Chake-Wete azma ya ujenzi huo iko pale pale kwani barabara zote hizo zimetajwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 na tayari mchakato wake umeanza.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alisisitiza haja kwa viongozi kuzisoma Sheria zote zinazopitishwa katika Baraza la Wawakilishi ili iwe rahisi katika utendaji wa kazi zao pamoja na kuwaelekeza wananchi juu ya mamabo mabli mbali ambayo hawayajui.

Rais Dk. Shein alisisitiza haja kwa viongozi wote wa Serikali wakiwemo Maofisa wa Vikosi kufanya kazi zao kwa uadilifu kwa kufuata taratibu, Kanuni na Sheria zilizopo kwa lengo la kuimarisha utekelezaji wa kazi zao na kuleta ufanisi zaidi.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein ameendelea kueleza kuwa ardhi yote ya Zanzibar ni mali ya Serikali hivyo hakuna haja ya kuendelea kuwepo kwa migogoro ya ardhi.

Ameeleza kuwa ziara hiyo imefana sana na mafanikio aliyoyaona ni mengi kuliko changamoto zilizopo huku akisisitiza haja ya kutekelezwa kwa maagizo yote aliyoyaelekeza na kuahidi kufanya ziara nyengine baada ya miezi minane.

Nao viongozi wa CCM wa Wilaya ya Chake Chake pamoja na Mkoa mzima wa Kusini Pemba walitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa ziara yake hiyo ambayo imewapa ari kubwa katika utendaji wa kazi zao.

Viongozi hao walitumia fursa hiyo kutoa pongezi za pekee kwa Rais Dk. Shein kwa kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa vitendo na kusisitiza kuwa tayari Makamu huyo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar ameshatekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 kwa asilimia mia moja.

Walieleza kuwa ziara yake hiyo ambayo aliianza katika kisiwa cha Unguja mnamo Februari 12 mwaka huu 2019 na kuanza kisiwani Pemba mnamo Februari 21 mwaka huu 2018 imeleta tija kubwa na mafanikio sambamba na kuzidisha mashirikiano kati ya uongozi wa Chama cha CCM na Serikali.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.