Habari za Punde

Uzinduzi wa Skuli ya Msingi na Maandalizi Ng'ambwa Kisiwa cha Uzi.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Mama Mwanamwema Shein na kulia Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibaer Mhe. Riziki Pembe Juma, wakipiga makofi baada ya kuondoa kipazia kuashiria kuweka Jiwe la Msingi la Skuli ya Ng'ambwa leo , akiwa katika ziara yake Wilaya ya Kati Unguja. 


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  amesema kuwa si muda mrefu kisiwa cha Uzi kitafumbuka kwani Serikali anayoiongoza itahakikisha inaimarisha huduma za maendeleo ikiwemo kujenga barabara na daraja kutoka Unguja Ukuu Kaepwani hadi Uzi.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika ziara yake ya Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja wakati alipotembelea kisiwa cha Uzi na kuweka jiwe la Msingi katika Skuli ya Maandalizi na Msingi ya Ng’ambwa na baadae kuwahutubia wananchi wa Uzi.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ina mipango kabambe ya kuhakikisha wananchi wa Kisiwa cha Uzi wanapata huduma zote muhimu kwa uhakika ikiwemo usafiri wa barabara, Skuli ya Sekondari pamoja na kuimarisha huduma za masi safi na salama.

Alieleza kuwa barabara ya Kutoka Unguja Ukuu Kaepwani hadi Uzi kwa kujengwa daraja linalokadiriwa kuwa na urefu wa mita 400 inawezekana kwani Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeshatekeleza miradi mikubwa kuliko huo.

Rais Dk. Shein aliwataka wananchi wa kisiwa hicho kufanya subira kwani Serikali itajenga daraja hilo kuelekea usawa wa bahari hatua ambayo itawaondoshea wananchi wa kisiwa hicho usumbufu wa usafiri wa barabara.

Aliongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzbar inampango wa kukopa fedha kutoka Benki ya Maendeleo ya ya Afria AfDB kwa ajili ya kutekeleza mradi mkubwa wa maji katika kisiwa hicho cha Uzi ambao utaondoa kabisa uhaba wa huduma hiyo.

Akieleza kuhusu azma ya Serikali kuimarisha sekta ya elimu katika kisiwa hicho cha Uzi, Rais Dk. Shein ameeleza kuwa Serikali anayoiongoza itahakikisha inajenga Skuli ya Sekondari ya Uzi Ng’ambwa pamoja na kupeleka samani.

Aidha, Rais Dk. Shein aliwaelezea wananchi wa kisiwa hicho juu ya suala zima la magendo linavyofanyika katika eneo hilo alisema kuwa Serikali kupitia Kikosi chake cha KMKM kiko macho kupambana na wale wote wanaofanya magendo.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kukipongeza kikosi hicho cha KMKM kwa kazi nzuri inayofanya kwani watu wamekuwa wakifanya makosa kwa kusafirisha bidhaa kama vile unga,mchele, sukari na mafuta bila ya kufuata taratibu na sheria za nchi.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliwaahidi wanaCCM wa Uzi kuwa tawi lao atalizindua na kuliweka jiwe la msingi baada ya kumaliza ujenzi wake kwa hoihoi na nderemo huku akiwataka wananchi wa Uzi kutogombana wala kutohasimiana kwa sababu ya vyama vya siasa kwani wao wote ni ndugu wa asili moja.

Alisema kuwa kuwepo kwa mfumo wa vyama vingi kunatokana na mujibu wa sheria na taratibu kutokana na Katiba ya mwaka 1984 hivyo hakuna haja ya kugombana wao wenyewe kwa wenyewe na kuwataka wapendane na waishi kwa amani na utulivu.

Aliwaeleza wananchi hao kuwa kisiwa cha Uzi kitapiga hatua kubwa za maendeleo  iwapo wataendeleza amani na utulivu sambamba na kuimarisha umoja wao kwani siasa ni mpito lakini damu na uasilia bado unabaki pale pale. Aliwataka kufanya siasa bila ya kubughudhiana na kutukanana.

Mapema Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Riziki Pembe Juma alipongeza juhudi za Rais Dk. Shein katika kuimarisha sekta ya elimu nchini.

Akiwa huko Uzi Rais Dk. Shein alimtaka Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) Mussa Ramadhan Haji kueleza mikakati ya Serikali iliyoiweka katika kuimarisha huduma ya maji safi na salama ambapo alieleza kuwa Mamlaka yake inachukua hatua za dharura hivi sasa ikiwa ni pamoja na kulifanyia ukarabati tangi lililopo kwa kuliziba ili lisipoteze maji.

Aidha, alisema kuwa  ZAWA inampango wa kuongeza uzalishaji wa maji kwa kuongeza idadi ya visima kwani vipo baadhi ya visima ambavyo vimeshachimbwa na vinaweza kutumika kuzalisha maji ili kusaidiana na kisima kiliopo na kusaidia kupeleka huduma hiyo huko Uzi pamoja na kuweka mtandao mpya wa maji katika kisiwa hicho.

Kwa upande wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji Mustafa  Aboud Jumbe alisema kuwa sehemu ya barabara inayotoka Unguja Ukuu Kaepwani hadi Kisiwa cha Uzi ina urefu wa km 2 na inapita kwenye bahari ya Hindi ambapo hali yake si nzuri.

Aliongeza kuwa kutokana na Wizara kuliona hilo imepanga kutafuta Mshauri Mwelekezi kwa ajili ya kulipatia ufumbuzi suala hilo ikiwa ni pamoja na kuangalia uwezekano wa kujenga daraja kwenye eneo ambalo nguzo za umeme zimewekwa ambalo linakadiriwa kuwa na urefu wa mita 400 tu kutoka kisiwa cha Uzi hadi Unguja Ukuu Kaepwani.

Alisema kuwa Wizara imekusudia kumpatia kazi za ziada Mshauri Mwelekezi Kampuni ya Dar Al Handasah ya Misri inayoendelea na kazi za upembuzi yakinifu, sanifu na kuandaa zabuni ya barabara ya Tunguu-Makunduchi, Fumba-Kisauni na Mkoani Chake Chake ambapo makisio ya kitaalamu ya gharama za ujenzi wa daraja na barabara yatajulikana baada ya Mshauri Mwelekezi kukamilisha michoro yake.

Akiwa katika majumuisho ya ziara yake hiyo pamoja na mazungumzo na viongozi wa CCM wa Wilaya hiyo huko katika ukumbi wa Hoteli ya Coconut Tree, Marumbi, Wilaya ya Kati Unguja, Rais Dk. Shein aliupongeza uongozi wa Wilaya hiyo kwa kutoa ripoti nzuri ambayo imemridhisha.

Aliwasisitiza viongozi wa Wilaya hiyo kuzigeuza changamoto chache zilizopo kuwa mafanikio kwa kufanya kazi kwa pamoja na kwa mashirikiano huku akitumia fursa hiyo kupongeza mashirikiano yaliopo kati ya uongozi wa Serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Rais Dk. Shein ambaye pia, ni Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar aliipongeza Wilaya hiyo ya Kati kwa kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM kupitia Wizara zote 14 za Serikali huku akieleza azma ya Serikali ya kuzijenga barabara za Jumbi hadi Koani, Dole-Kizimbani-Miwani hadi Kiboje, Tunguu-Ndijani na Jozani Charawe- Ukongoroni ambazo zote zitajenwga kwa kiwango cha lami.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza changamoto ya wizi wa mazao, wizi wa kuvunja nyumba ambao alisema ni miongoni mwa maombo ya uhalifu yaliyomo katika Wilaya hiyo ambayo yanahitaji kukomeshwa.

Nae Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ Haji Omar Kheir alieleza hatua zitakazochukuliwa katika kuajiri wafanyakazi katika sekta ya kilimo, elimu na afya ambapo ajira zitazingatia mahitaji ya maeneo maalum.

Rajab Mkasaba, Ikulu
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.