Waziri
Mkuu Wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa akimsikiliza
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mhandisi Patrick
Mfugale akisoma taarifa ya Ujenzi
wa mradi wa Jengo la Tatu la Abiria la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha
Julius Nyerere (JNIA), hivi karibuni alipowasili kukagua maendeleo ya ujenzi
huo.
Kiongozi
Mkuu wa Timu ya Wataalam wa Ujenzi wa Jengo la Tatu la Abiria la Kiwanja
cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Mhandisi Julius
Ndyamukama (aliyenyoosha mkono) akimuonesha Waziri Mkuu Mhe. Kassim
Majaliwa ukumbi wa abiria wanaoondoka katika jengo la tatu la abiria la
Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), alipotembea
hivi karibuni.
Waziri
Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa akiangalia aina ya viti vya abiria
vitakavyotumika kwenye Jengo la tatu la abiria la Kiwanja cha Ndege cha
Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) alipotembelea hivi karibuni. Kulia kwa
Waziri Mkuu ni Bi. Sophia Mjema, Mkuu wa Wilaya ya Ilala na wa pili
kushoto ni Mhandisi Julius Ndyamukama, akifuatiwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar
es Salaam Mhe. Paul Makonda.
Menejimenti
ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania wakiongozwa na Kaimu Mkurugenzi
Mkuu Bw. Vedastus Fabian (watatu kulia) wakitoka katika jengo la tatu la
abiria la Kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) mara
baada ya ziara ya waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa kumalizika hivi karibuni.
Na
Mwandishi Wetu
WAZIRI
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa amesema hivi
karibuni kuwa ameridhishwa na ujenzi wa mradi wa Jengo ka Tatu la abiria la Kiwanja
cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA-TB III), wakati alipotembelea
kukagua maendeleo ya ujenzi huo.
Mhe.
Majaliwa amesema amefarijika kusikia ujenzi wa jengo hilo umekamilika kwa asilimia
95.05, ambapo imebaki asilimia 4.5 pekee kukamilika.
“Nawapongeza
wakandarasi, Tanroads na wote mliopata ajira ya ujenzi wa jengo hili naamini
sasa mmekuwa wataalam hodari, kwani jengo ni zuri, linavutia na lenye ubora
nimeona maeneo muhimu pale pa kuondokea abiria, sehemu ya kupokelea mizigo na
kwenye madaraja ambapo kote nimefarijika kwa kiasi kikubwa ujenzi unakwenda
vyema,” amesema Mhe. Majaliwa.
Amesema
mbali na ujenzi huo pia amefurahishwa na ukuta unaotambulika kama “Wall of
Tanzania” ambao unaonyesha picha za vivutio mbalimbali ukiwemo mlima mrefu
Barani Afrika, Mlima Kilimanjaro, Bahari, Majahazi, minazi, wamasai, wanyama
Twiga, Tembo, Pundamilia, Nyumbu, Simba na Chui, ambao hutambulisha wageni kuwa
tayari wamewasili Tanzania na wataweza kuona vivutio hivyo, ambavyo ni alama na
nembo ya nchi.
“Hizi
picha ni nembo ya Kitanzania, na hapa zimekaa sehemu nzuri sana kila mgeni
anapowasili na kufika eneo hili la kuchukulia mizigo anaona kweli amefika
Tanzania kwani zinawakaribisha wageni, na hii ni faraja kwa kuwa jitihada za
serikali za kuleta maendeleo zinafanyika vyema,” amesema Mhe. Waziri Mkuu.
Mhe.
Majaliwa pia amekuwa na faraja kubwa kusikia jengo hilo litaweza kuhudumia
abiria milioni sita (6) kwa mwaka, na kwa majengo yote likiwemo Jengo la Kwanza
na la Pili jumla yataweza kuhudumia abiria milioni nane (8) kwa mwaka, ambapo
pia kumekuwa na miundombinu kwa ajili ya watu wenye mahitaji maalum.
Hatahivyo,
ameitaka
Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) ianze
kukamilisha taratibu za kuanza kutumika kwa jengo hilo, ili
mkandarasi anapolikabidhi kwa serikali ifikapo tarehe 31 Mei, 2019 lianze
kutumika mara moja.
Naye
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), ambao ndio wasimamizi
wa ujenzi Mhandisi Patrick Mfugale awali alimweleza Mhe. Majaliwa kuwa ujenzi
wa jengo hilo umekamilika kwa asilimia 95.05, ambapo eneo la maegesho ya ndege
linaweza kuegesha ndege 19 za darala C, na 11 daraja E na jengo linaweza
kuhudumia abiria 2,800 kwa saa muda ambao abiria ni wengi.
Hatahivyo,
Mhandisi Mfugale amemhakikishia Mhe,. Majaliwa kuwa ujenzi huo utakamilika kwa
wakati na viwango vilivyowekwa, amesema jengo hilo litakabidhiwa kwa serikali
tarehe 31 Mei, 2019.
No comments:
Post a Comment