Na.
Paschal Dotto-MAELEZO.
Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Dkt.John Pombe Magufuli,
ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa upanuzi wa Uwanja wa Ndege Mtwara na
kuagizi Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Isack Kamwelwe na Waziri wa
Fedha na Mipango, Dkt.Philipo Mpango, wakutane ndani ya siku tano ili kutoa
pesa ya mradi wa ujenzi huo kwa Mkandarasi.
Rais Magufuli alisema
kuwa aslimia 15 ya pesa za mradi huo ambazo ni sawa na shilingi Bilioni 7.5,
zinatakiwa kutolewa ndani ya siku tano ili kumwezesha mkandarasi kuendelea na
kazi na kumaliza kazi kwa muda uliopangwa kwenye mkataba wa mradi huo.
“Mimi leo naagiza,
wewe Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano na Waziri wa Fedha na Mipango, asilimia 15 ya pesa za mradi huu ambazo ni sawa na shilingi Bilioni 7.5,ziwe
zimefika hapa ndani ya siku tano, kwa sababu najua fedha hizo zipo sasa kwa
nini mkandarasi hajaletewa pesa hizo”, Rais Magufuli alisema.
Rais Magufuli
amlitaka Mkandarasi huyo kufanya kazi
yake kwa umakini mkubwa mara atakapopata
pesa hizo za mradi asilimia 15, huku ikielezwa kuwa mradi mzima utagharimu Shilingi
bilioni 50.4 mpaka kukamilika kwa mradi mwaka 2020, pia imeelezwa mradi uko
nyuma ya muda.
“Nataka akishapata pesa hizo afanye kazi usiku na
mchana na siyo kubabaisha kama alivyofanya katika Uwanja wa Ndege Mwanza,
ingawa sasa yuko asilimia 98 kumalizia mradi ule, ila mwanzoni alisuasua, sasa
nakueleza Waziri wa Ujenzi, Mkurungezi Mtendaji, Tanroad na Mkandarasi wa mradi
huu, mfanye kazi usiku na mchana, najua
mpaka sasa hivi mmeishachelewa siku kadhaa, lakini wananchi wa Mtwara wanataka
kuona uwanja umekamilika”, Rais Magufuli.
Aidha Rais Magufuli
alieleza utekelezaji wa miradi mingine ya Serikali kwa wananchi wa Mtwara,
ikijumuisha ujenzi wa mradi wa barabara ya Mikindani, kilometa 3, stendi,
kadhalika maeneo ya kupumzikia, soko, pamoja na mfereji wa maji, itagharimu
Tsh.bilioni 23.843.
Miradi mingine ni
ukarabati ama ujenzi wa vituo vya afya, utakaogharimu Tsh.bilioni 10.3, lakini
pia utekelezaji wa mradi wa maji wa Makonde ambao utakarabatiwa na kuwa nguzo
ya upatikanaji wa maji katika miji ya Newala, Nanyumbu, Tandahimba, Mtwara na
vijiji 309.
“Nafahamu kuwa moja
ya changmoto katika mkoa huu ni upatikanaji wa maji kwani kwa sasa ni asilimia
4, ingawa kwa mjini ni asilimia 80, lakini tatizo hili linasababishwa na
uchakavu wa miundombinu katika mradi wa maji wa makonde, kwani mahitaji ya maji katika meneo haya ni lita za
ujazo milioni 18.3 wakati mradi una uwezo wa kuzalisha lita milioni 24.3,
lakini kutokana na uchakavu, mradi huu hutoa lita milioni 6.7, kwa hiyo
asilimia 60 ya maji inapotea”, Rais Magufuli alisema.
Katika utekelezaji wa
miradi ya maji kwa miji 28 nchini, ambapo Serikali inapata mkopo wa kugharamia miradi
hiyo kutoka Serikali ya India, zikiwa zaidi ya Trioni 1.2, mradi wa maji
makonde umetengewa dola za Kimarekani milioni 70, sawa na Tsh.bilioni 160.
Rais Magufuli pia
alisema kuwa Serikali inaendelea na utekelezaji wa kuwalipa wakulima wa korosha
katika mikoa ya kusini wanakozalisha korosho, huku wakulima 39,765 waliokuwa na
korosho chini ya kilo 1500 ambazo zilikuwa ni tani 16,669.3, walitengewa
Tsh.Bilioni 521.8 na baada ya uhakiki walilipwa pesa zao.
“Watanzania sisi ni
wataalam kwenye hewa, kwa hiyo ilibidi tukae macho tusije tukawa na korosho
hewa tukalipa malipo hewa, ndiyo maana tulihakikisha kila mkulima anafanyiwa
uhakiki ili kupata haki yake”, Rais Magufuli
Rais Magufuli
aliongeza kuwa wakulima 373,149 wamelipwa, kwa hiyo asilimia 99 ya wakulima
wenye korosho chini ya kilo 1500 wamelipwa, huku uhakiki wa wakulima wenye kilo
zaidi ya 1500 ambao walikuwa 18,103,
waliobainiwa kwenye uchambuzi wa pili umekamilika na wataanza kulipwa, lakini
katika hao, majina 780 walikuwa hawana mashamba wala mikorosho.
“Najua kuna watu
wamenunua korosho tangu zikiwa mashambani, ninafahamu imekuwa ni biashara
ambayo inaendelea huko japo siyo biashara nzuri kwa sababu imekuwa ikiwadhulumu
wananchi, kwa wale watakaokiri kwamba wao ni makagomba Serikali itawasamehe na kuwalipa pesa zao”, alisema Rais
Magufuli
Akihimiza malipo kwa
wakulima, Rais Magufuli alitoa maagizo kwa Waziri wa Kilimo kupeleka bilioni 50
kuanzia kesho ili wakulima wenye korosho zaidi ya kilo 1500 waanze kulipwa mara
moja.
No comments:
Post a Comment