Mwenyekiti wa Vipaji Promotion Network (VPN), Haji is Mrisho
(kulia) akimkabidhi zawadi ya saa Naibu Meya wa Temeke, Juma Rashid wakati wa
hafla hiyo.
Sehemu ya watoto wanaofadhiliwa
na Vipaji Promotion Network (VPN) wakifuatilia matukio yaliyokuwa yakiendelea katika hafla fupi iliyoandaliwa na taasisi ya Vipaji Promotion Network (VPN) kwa lengo la
kuchangia vijana wenye vipaji ili kuwawezesha kusoma, ambayo iliambatana na
tukio la kufutarisha lilifanyika Mei 25, 2019 jijini Dar es Salaam.
Mmoja wa kinamama washiriki wa hafla hiyo akitoa mchango
wake wa mawazo ili kuboresha taasisi hiyo ili iwe na uwezo wa kusaidia vijana
wengi zaidi.
Na. Mbaraka Kambona,
Mwenyekiti wa Mtandao huru (VPN) wa kubaini na kuwafadhili
vijana wenye vipaji lakini familia zao
hazimudu kuwasomesha, Haji Mrisho amewaomba watanzania kuunga mkono jitihada za taasisi hiyo ili kusaidia vijana
hao kupata elimu nchini.
Mrisho alitoa wito huo Mei 25, 2019 jijini Dar es Salaam
katika hafla fupi iliyoandaliwa na
taasisi hiyo ya Vipaji Promotion Network (VPN) kwa lengo la kuchangia vijana
wenye vipaji ili kuwawezesha kusoma, ambayo iliambatana na tukio la kufutarisha.
Mwenyekiti huyo alisema kuwa tangu kuanzishwa kwa taasisi
hiyo mwaka 2015 mpaka sasa wameshafanikiwa kuwapeleka shule watoto tisini na
nne (94) ambao wako katika shule zilizopo mikoa ya Tanga, Dar es Salaam, Kigoma
na Tabora.
Mrisho aliendelea kusema kuwa
lengo la taasisi hiyo ni kupeleka shule watoto Mia moja (100) kila mwaka,
hivyo alitoa wito kwa watanzania wenye mapenzi ya kusaidia watoto kusoma
wajitokeze kuunga juhudi zilizoanzishwa na VPN.
“Serikali peke yake haiwezi kufanya kila kitu, niwaombe ndugu
zangu watanzania wajitoe na kuungana na sisi katika harakati hizi za kumkomboa
kijana, kwani kijana akiachwa tu mtaani bila kusaidiwa anaweza kujiingiza
katika makundi yasiyofaa na ikawa ni hasara kwa jamii na taifa pia”, alisema
Mrisho
“Lakini vijana pia wanaopata fursa hii ya kusoma wahakikishe
wanaitumia vyema kwa manufaa yao na kwa taifa, wajue kuwa hili ni deni kwao kwa kuwa jamii inajitolea
rasilimali zao ili wao wasome na kuja kuiendeleza nchi yao”, aliongeza
Mwenyekiti huyo
Pamoja na mafanikio hayo waliyofikia mpaka sasa, Mrisho
hakusita kueleza changamoto wanazopata ikiwa ni pamoja na ufinyu wa bajeti, na
pia taasisi hiyo kutofahamika vizuri kwa
watanzania walio wengi kwa kuwa bado ni
changa.
Katika hatua nyingine, Naibu Meya wa Halmashauri ya Temeke,
Juma Rashid Mkenka ambaye ndiye alikuwa mgeni rasmi
akimuwakilisha Meya wa Temeke alisema kuwa
kazi inayofanywa na taasisi hiyo ni kubwa sana hivyo wasiifanye peke yao
peke yao, wapanue wigo kwa kushirikisha wadau wengi zaidi ili wapate uwezo wa
kusaidia vijana wengi.
“Tanzania kuna wadau wengi sana wanaopenda kusaidia katika eneo
la elimu, hivyo mfanye jitihada za kuimarisha ushirikiano na wadau hao ikiwemo
Serikali ili muweze kupanua wigo wa kuwasaidia vijana wengi zaidi nchini”,
alisema Naibu Meya huyo
Aidha, Mwenyekiti wa VPN alisema kuwa mipango yao ya baadae
ni kuwa na uwezo wa kuchukua vijana wenye vipaji nje ya masomo ifikapo mwaka
2020, pia kuwa na shule ya sekondari ya VPN ifikapo mwaka 2025 na kuwa na chuo
kikuu ifikapo 2035.
Vipaji Promotion Network (VPN) ni Mtandao huru unaojiendesha
bila faida ambao ulioanzishwa mwaka 2015
na vijana wa kitanzania kwa lengo la kuwabaini
na kuwafadhili vijana wenye vipaji lakini familia zao hazimudu kuwasomesha
vijana.
No comments:
Post a Comment