Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk Ali Mohamed Shein. Akabidhiwa Cheti Maalum Kwa Kazi Nzuri na Shukrani Kwa Uongozi Wake.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akikabidshiwa Cheti Maalum Kwa Kazi Nzuri na Shukari kwa Uongozi wake na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Balozi Seif Ali Iddi, kilichotolewa na Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora Zanzibar, wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Utumishi wa Umma Zanzibar, iliofanyika katika ukumbi wac Sheikh Idrisa Abdulwakil Kikwajuni Zanzibar. 


UONGOZI wa Ofisi ya Rais na Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kushirikiana na Chuo cha Utawala wa Umma (IPA) umetakiwa kuandaa programu maalum ya mafunzo ya muda mfupi kwa ajili ya Viongozi, Watendaji Wakuu na Watumishi wengine wa Serikali.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo katika ufunguzi wa kongamano la maadhimisho ya Siku ya Utumishi wa Umma Zanzibar yaliyofanyika katika ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdul wakil, Kikwajuni mjini Zanzibar.

Katika hotuba yake hiyo, Rais Dk. Shein alisema kuwa  programu hiyo ya mafunzo ya muda mfupi kwa ajili ya viongozi hao yana lengo la  kuongeza ufanisi katika Utumishi wa Umma ili wapate masomo ya kuwakumbusha majukumu yao na kuweza kuwahudumikia vyema wananchi.

Rais Dk. Shein katika hotuba yake hiyo alieleza kuwa ubunifu ni muhimu katika utumishi wa Umma na ndio utakaowafanya watumishi kuacha kufanya kazi kwa mazoea.

Alisisitiza kwamba bila ya kuwa wabunifu  Zanzibar inaweza kubaki nyuma katika karne hii ya sayansi na teknolojia ambapo kwa bahati mbaya miongoni mwa watumishi wapo wachache ambao ni wagumu kubadilika katika kutimiza majukumu yao ya utumishi.

Aliongeza kuwa watumishi wa aina hiyo ni lazima wabadilike na wahakikishe wanakwenda na kasi ya kutoa huduma zilizo bora na kutoa nasaha zake za kuhakikisha watumishi wanakuwa wabunifu wa kutafuta njia bora, rahisi na nzuri ya kuwatumikia wananchi ambao ndio waajiri.

Rais Dk. Shein alisema haja ya kuwepo kwa Chuo cha Utumishi wa Umma ambacho kutokana na mahitaji maalumu ya kitaalamu, maadili, fikra, mawazo na tabia zinazohitajika kwa wafanyakazi katika sekta ya umma nchi zote duniani zina vyuo maalum vya kutoa mafunzo maalum kwa watumishi wa umma. 

Alieleza kuwa utumishi wa Umma ulio bora ni chachu muhimu katika kuongeza kasi ya maendeleo hapa nchini kiuchumi na kuuimarisha ustawi wa jamii hasa kwa kutambua kuwa utumishi wa Umma ni kigezo muhimu cha misingi ya Utawala Bora.

Alieleza furaha yake jinsi ya watumishi wa Umma wanavyowahudumia wananchi na kuwapongeza wafanyakazi wote nchini na kueleza kwamba mwamko umebadilika na watumishi wengi wanazingatia umuhimu wa kuwatumikia wananchi kwani wao ndio wenye nchi na wanaoiweka Serikali madarakani.

Rais Dk. Shein alisistiza haja ya kuendelea kufanya kazi kwa kujiamini na kutofanya kazi kwa gati gati kwani watumishi wanaujuzi, wanajua na wanaweza kutekeleza vyema kazi zao na kusisitiza kutofanya kazi kwa mazoea na kuwataka kuwa wabunifu.

Alisisitiza haja ya kuwepo kwa mabadiliko kwa kila yule anayepewa dhamana kwa lengo la kuimarisha Utumishi wa Umma.

Akieleza juu ya ujumbe wa mwaka huu usemao “ Matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) Uwajibikaji na Ubunifu ndio chachu ya Maendeleo katika kuimarisha Utumishi wa Umma”, na kueleza kuwa iwapo ujumbe huo utazingatiwa na kufanyiwa kazi mabadiliko makubwa yatapatikana na kusisitiza haja ya kuufanyia kazi kwa vitendo ujumbe huo.

Alieleza haja ya Taasisi inayoshughulikia Serikali Mtandao kuwaelimisha wananchi pamoja na kuwaelisha watumishi wa Umma Serikalini na kwenye taasisi nyengine maana ya Serikali Mtandao na madhumuni yake kwani unarahisiha utendaji wa kazi.

Aliitaka Taasisi hiyo Kuwaeleza wananchi juu ya huduma gani wanazipata hasa ikizingatiwa kuwa Serikali imetoa mamilioni ya fedha kwa ajili ya Serikali Mtandao huo.

Rais Dk. Shein aliwataka viongozi na watumishi wa Umma kufanya kazi kwa mashirikiano ya pamoja huku akieleza kuwa Serikali inapiga vita suala la rushwa na uhujumu wa uchumi na ndio maana kuna Sheria maalum juu ya suala hilo na kueleza umuhimu wa maadili kwa viongozi .”maadili ndio chachu ya kutoa mwelekeo wa kuongoza watu”, alisisitiza Dk. Shein.

Rais Dk. Shein alisema kuwa katika kuendeleza juhudi za kuhakikisha kwamba viongozi wa umma wanashikamana na maadili ya umma sambamba na kuwajibika kwa uwazi na kwa kuzingatia  misingi ya sheria, kwa lengo la kutoa huduma bora kwa wananchi.

Alisema kuwa Serikali iliunda Tume ya Maadili ya viongozi wa Umma Zanzibar ambayo ina jukumu la kutekeleza na kusimamia Sheria ya Maadili ya viongozi wa Umma, namba 4 ya mwaka 2015 ambapo pia, inawataka viongozi wote wa Umma kujaza na kurejesha Fomu ya Tamko la Mali na Madeni..

Alieleza kuwa jumla ya viongozi 16,20 walijaza fomu na kuzirejesha katika mwaka 2016/2017 na viongozi 1,664 walifanya hivyo katika mwaka 2017/2018 na katika mwaka 2018/2019 jumla ya viongozi 1,727 walitimiza wajibu wao huo wa kisheria.

Nae Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora Haroun Ali Suleiman aliahidi kuendelea na jitihada za kuimarisha utumishi wa Umma hapa nchini na kutumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Shein kwa uongozi wake bora na jinsi anavyowajali watumishi wa Umma.

Alisema kuwa kwa upande wa Zanzibar tokea mwaka 1964 masuala ya Utumishi wa Umma utekelezaji wake ulianza lakini mageuzi makubwa yametokea mwaka 2010 katika uongozi wa Rais Dk. Shein baada ya kafanywa mageuzi na kufanya programu maalum ya matumizi ya Utumishi wa Umma ikiwa ni pamoja na Sera, Sheria na Kanuni ambayo yote hayo ni matunda ya Rais Dk. Shein.

Alisema kuwa mageuzi hayo yametokea na kuundwa kwa Wizara maalum kamili ya Utumishi wa Umma huku akitumia fursa hiyo kuwataka viongozi wa taasisi kuhakikisha inawapa stahiki zao wale wote wanaomaliza masomo.

Alieleza kuwa Zanzibar ina Awamu Saba na kila awamu imefanya mambo yake makubwa lakini katika suala la Utumishi wa Umma maabadiliko makubwa ya watumishi yamefanyika kuanzia mwaka 2010, ambapo katika hotuba zake Dk. Shein alikuwa akisema kuwa atahakikisha watumishi wa Umma anawawekea mazingira bora.

Aidha, Rais Dk. Shein aliwatunuku vyeti Katibu Mkuu wa Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee, Haji Omar Kheir;Waziri wa Mwanzo katika Wizara ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora pamoja na Waziri Haroun Ali Suleiman.

Pia, wakati huo huo Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd alimkabidhi Cheti maalum Rais Dk. Shein kutokana na kazi nzuri aliyoifanya na shukurani kwa uongozi wake uliotukuka sambamba na mchango mkubwa wa kuimarisha sekta ya Umma uliopelekea kuwepo kwa ufanisi.

Nae Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Mary Machuche Mwanjelwa alitumia fursa hiyo kuipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kufanya maadhimisho hayo kwani yana faida nyingi kwa utumishi wa Umma.

Alieleza kuwa kwa upande wa Tanzania Bara katika kuadhimisha wiki hii Ofisi yake ilikukutana na watumishi wa Umma kwa kuangalia wametoa huduma zao vipi kwa watumishi hao na kufanya maonyesho ambayo ndio sehemu ya watumishi wa Umma na kukutana kwa pamoja na kuona mrejesho wake na kuepuka kufanya kazi kwa mazoea.

Alieleza kuwa maadhimisho hayo ya Siku ya Utumishi wa Umma Zanzibar pia, ni sehemu ya kuuenzi Muungano uliopo ambao umeasisiwa na Marehemu Mzee Abeid Amani Karume na Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Nae Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora Yakuti Hassan Yakuti alieleza kuwa maadhimisho hayo yana lengo la kukuza ushirikiano na nchi kadhaa za Afrika.

Alisema kuwa nchi za Afrika kila mwaka huanzimisha siku hii kila ifikapo tarehe 23 Juni ya kila mwaka kwa kutambua mchango wa watumishi wa umma katika nchi husika.

Alisema kuwa Maadhimisho hayo kwa upande wa Tanzania yalianza mwaka 2003 baada ya kukubaliwa na Umoja wa Afrika ambapo Tanzania iliainisha kama ilivyo kwa nchi nyengine ikiwa ni pamoja na kuandaa makongamano na kuonekana haja ya kuanzishwa hapa Zanzibar mwaka huu.

Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa kuanzia mwakani kuanzia tarehe 17 Juni hadi 23 kwa kushirikiana na Taasisi zote za Serikali na kuomba kuzikumbusha Wizara na Taasisi zote za Umma kujiandaa mapema kwa ajili ya shughuli hii ambayo itakwenda sambamba na maonyesho, makongamano na kutoa tunzo kwa watumishi waliofanya vizuri katika kazi.

Katika kongamano hilo mada mbali mbali zilitolewa ikiwa ni pamoja na mada isemayo, Mafanikio yalipatikana katika Utumishi wa Umma Zanzibar, Mchango wa Chuo cha IPA katika Utumishi wa Umma Zanzibar, Mchango wa Srikali Mtandao katika Utumishi wa Umma Zanzibar na Uwajibikaji katika Utumishi wa Umma.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.