Habari za Punde

Sheria Kali Zinahitajika Dhidi ya Ukatili wa Watoto.


Na.Laila Abeid -Maelezo.

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeweka sheria, taratibu na miongozo ambayo inashirikiana na mashirika yasiyo ya kiserikali kuhakikisha usalama na ustawi wa watoto nchini Tanzania.

Hata hivyo, pamoja na yote hayo bado ukatili dhidi ya watoto umeendelea kushamiri pamoja na wahusika kuchukuliwa hatua za kisheria. Hii inatupa picha kwamba bado kunahitajika mkakati madhubuti wa kuhakikisha sheria zinazowekwa zinapunguza masuala ya ukatili kwa watoto kama sio kwisha kabisa.

Serikali na wadau wanaitakia nchi yetu mafanikio wafungue macho dhidi ya ukatili huu kwani watoto wengi wanakutwa na majanga ya kubakwa na kulawitiwa  wawapo njiani wanapoelekea shuleni , wanapocheza na wenzao au wanapoelekea dukani kufata mahitaji wanayoagizwa na wazazi wao

Kwa bahati mbaya sana wahusika wengi wanaowafanyia watoto ukatili ni sehemu ya familia ya watoto husika. Mara nyingi unakuta ni aidha, wazazi, baba wadogo , wajomba, mama wa kambo, jirani, rafiki wa familia na jamii ya karibu na anapoishi mtoto.

Baba wa kambo mkazi wa buguruni amlawiti mtoto wa umri wa miaka 4 , Baada ya kuachiwa na mkewe amuamshe iliaweze kumuandaa kwenda shule na muhusika alikamatwa  baaada ya mtoto kusema kitendo anachofanyiwa na baba huyo, baadae muhusika alipewa dhamana na kutoka kwa dhamana.

Aidha kutokana na jamii kutokuwa na ufahamu wa kutosha kuhusu sheria na taratibu za kufuata mara baada ya mtoto kufanyiwa ukatili wa aina yeyote ile. Suala la utamaduni au desturi na mila ya kuamua kumaliza kimyakimya masuala hayo ya  ukatili kwa kisingizio cha kulinda heshima  ya mkosaji na kumlindia hadhi katika jamii ndio chanzo cha kuongezeka kwa masuala hayo.

Changamoto hizi zinawafanya wazazi kushindwa kuwatoa watoto wao kwenye mambo tofauti ya kijamii kutokana na kuogopa kutokea kwa matatizo kama hayo. Aidha kesi zikipelekwa katika sehemu husika, wenye ushahidi kutokwenda mahakamani au mara nyingine mhusika kutoroka na  baadae kesi hufutwa bila kujua hatma ya mtoto aliyepata madhara.

Mpaka sasa kuna idadi kubwa ya watoto waliobakwa na kulawitiwa ambapo mwaka 2015/2016 watoto aliobakwa na kulawitiwa walikuwa 394 na mwaka 2016/2017  kufikia 2,984 ,Tafiti zinaonyesha idadi ya watoto waliobakwa itazidi kuongezeka kwa mwaka 2018 na 2019 na  kuwa kubwa zaidi.

Suala hili sio la Serikali peke yake ushirikiano unahitajika kutoka kwa jamii yote kwa ujumla ili kushiriki katika kutokomeza uhalifu huu ambao unatupelekea kuwa na Taifa lisilofaa hapo baadaye.  Pia, nguvu za ziada zinahitajika kuhakikisha watoto wanaokumbwa na majanga haya kusaidiwa kisaikolojia ili kurudi katika hali yao ya kawaida itakayowafanya kuwa Rais wema na wazazi hapo baadaye.

Mmoja wa wazazi wa mtoto aliye fanyiwa ukatili wa kijinsia  mkazi wa  singida  alisema hatutakiwi kuwa na imani juu ya watu ambao wanatuzunguka kwani wengi wanatufanyia mambo haya ni miongoni mwa hawa tunaoishi nao na hii hutokana na matamanio yao ya kimwili.

Jamii kwa ujumla inatakiwa iwemacho kupinga vikali ukatili huu unaowakumba watoto  wadogo kwani wao ndio taifa la kesho na ndio tegemeo kubwa la taifa kwa mwaka ujao hivyo tunapofumbia macho matukio kama haya na  kutokukaa kimya pale tunapogundua kama mtoto amefanyiwa ukatili basi lazima tuchukue hatua ya kupeleka mashtaka ya kitendo hicho mbele ya sheria .

“Tunatakiwa tufungue macho juu ya haya matukio yanayowakuta watoto wetu na pia tuwe makini na jamii inayotuzunguka kwa ujumla kwani wengi wao ndio wanaohusika na vitendo hivi kwa watoto na badae kutoka hivyo serikali tunaiomba iwe macho  juu ya matukio kama haya “.

Mapendekezo yangu kama raia mwema wa Tanzania viongozi mbalimbali wakiwemo wa dini na viongozi wa serikali wanajitahidi kupiga vita juu ya ukatili wa namna hii kwa jamii lakini hali bado ni tete kwani watuhumiwa wengi wa matukio haya wamekuwa hawajui wala kuelewa juu ya vita vinavyoendelea  dhidi ya ukatili  kwa watoto .

Ushauri wangu Sheria zitakazotungwa ziwe kali kwa kuweka amani na utulivu, pia serikali ingetoa elimu juu ya matukio ya ulawiti na hasara zake kwa jamii pia kuwajulisha juu ya sheria zinazotumika kuwaadhibu watendaji wa matukio ya ulawiti na ubakaji ili kuweza kupunguza utokeaji wa matukio kama haya kwa asilimia kubwa .

Jamii ikiwa macho dhidi ya matukio haya basi watoto wengi watakuwa salama dhidi ya matukio ya ukatili pia kuwapeleka wahusika wa matukio haya polisi ili sheria ifate mkondo wake basi yaweza pelekea nchi ikawa huru na amani .
05. Julai 2019

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.