Habari za Punde

Suala la Utafiti Kwa Wizara ya Kilimo Maliasili Mifugo na Uvuvi Zanzibar Lina Umuhimu Mkubwa


Waziri wa Kilimo,Maliasili,Mifugo na Uvuvi (kushoto) akichangia katika mkutano wa Wizara hiyo wa   utekelezaji wa malengo ya mpango kazi kwa kipindi cha Julai  2018-Juni 2019 na mpango kazi wa mwaka 2019-2020 uliofanyika leo katika ukumbi wa Ikulu Mjini Zanzibar chini ya Mwenyekiti wake Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (katikati)
[Picha na Ikulu.] 26/08/2019.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza haja kwa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi kuongeza kasi katika kufanya utafiti kwani sekta zote za Wizara hiyo zinagusa chakula ambacho ndio maisha ya mwanaadamu.

Hayo aliyasema leo, Ikulu mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi wakati ilipowasilisha Mpango Kazi wa Julai  2018 hadi Juni 2019 sambamba na Mpango Kazi wa Utekelezaji kwa mwaka 2019/2020.


Rais Dk. Shein alieleza kuwa suala zima la utafiti lina umuhimu mkubwa kwani tayari hivi sasa Serikali ina taasisi tatu za utafiti ikiwemo, Taasisi ya Utafiti wa Afya, Taasisi ya Utafiti wa Mifugo na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo.

Alieleza haja ya kuendelea kuzitumia taasisi za kilimo kwani zina umuhimu mkubwa na ndio maana akafanya jitihada za kuzianzisha na kusisitiza haja ya kuendeleza tafiti kwani ndio nguzo na nyenzo kubwa ya Wizara hiyo.

Alieleza kuwa Chuo cha Kilimo cha Kizimbani (KATI), hivi sasa kimeiunganishwa na SUZA, hivyo ni vyema wakakiimarisha na kutokiwacha mkono kwani bado kinahitaji mchango kutoka kwa uongozi wa Wizara hiyo.

Alisisitiza kuwa bado kilimo kina nafasi katika Uchumi wa Bahari (Blue Economy) na kueleza kuwa Serikali ya Mpinduzi ya Zanzibar imo katika mpango wa kuandaa Idara itakayoratibu Uchumi wa Bahari hapa Zanzibar.

Alisema kuwa kwa mara ya kwanza Wizara hiyo imepata fedha nyingi katika Bajeti yake ambapo hizo zote ni jitiha za Serikali pamoja na jitihada za Wizara hiyo  akisisitiza Wizara hiyo ieleze mafanikio makubwa iliyoyapata yakiwemo mafunzo.

Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd ambaye alishirikia kikamilifu mkutano huo kwa upande wake alitoa pongezi zake kwa na kusisitiza suala zima la uzalishaji wa vifaranga vya samaki ili wananchi wengi walioamua kufanya kazi hiyo wafaidike.

Pia, alieleza haja ya kuwepo kwa mradi wa kuzalisha vifaranga vya kuku kwani hivi sasa vifaranga vya kuku vingi vinaagizwa kutoa nje ya nchi huku akisisitiza haja ya kuzalisha viungo vya chakula kwa vingi kwani masoko yapo sambamba na suala la ajira kwa vijana.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliipongeza kazi nzuri ya uwasilishaji iliyofanywa na Wizara hiyo huku akisisitiza haja kwa uongozi kuendeleza mafunzo kwa wafanyakazi pamoja na kuendeleza uadilifu.

Nae Mshauri wa Rais wa Zanzibar Pemba, Dk. Maua Abeid Daftari alipongeza azma ya Wizara hiyo kuliimarisha zao la halizeti ambalo alisema lina mapato mazuri na kusisitiza haja ya kuendelezwa utafiti katika maeneo ya Matangatuwani na Weni kisiwani Pemba.

Mapema Waziri wa  Kilimo, Maliasili,  Mifugo na Uuvi Mmanga Mjengo Mjawiri akisoma muhtasari wa Wizara  hiyo alisema kuwa Wizara imelenga kuendeleza mageuzi katika sekta ya kilimo kwa kukifanya kilimo kiwe cha kisasa, jumuishi na chenye ushindani.

Ambapo kwa maelezo ya Waziri Mjawiri sekta ya kilimo inachangia katika sekta ya viwanda na utalii ili kuleta tija na maisha bora ya wananchi wa Zanzibar na maendeleo ya uchumi kwa ujumla.

Alisema kuwa kilimo ikijumuisha mazao, mifugo, uvuvi, misitu na rasilimali zisizorejesheka bado ni mhimili mkuu wa uchumi  wa Zanzibar ambao asilimia 40 ya wananchi wamejiajiri kwenye sekta hii na inakadiriwa zaidi ya asilimia 70 ya wananchi wanategemea kilimo ambapo mwaka 2018 kimechangia pato la taifa la asilimia 21.3.  

Waziri Mjawiri alieleza malengo na mikakati elekezi ya Wizara hiyo kwa mwaka 2018/2019 ikiwa ni pamoja na kukamilisha utaratibu wa Chuo cha Kilimo Kizimbani (KATI) Zanzibar kujiunga na Chuo Kikuu cha Taifa (SUZA)  pamoja na ununuzi wa meli mbili.

Aidha, alieleza mafanikio yaliopatikana  mwaka 2018/2019 ikiwa ni pamoja na kuongeza uzalishaji wa mpunga, kuongeza uzalishaji wa miche ya mikarafuu, kuzindua kampeni ya kuendeleza zao la nazi, kuzalisha vifaranga 240,000 vya majongoo bahari pamoja na kuanza kwa mradi wa ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji maji.

Sambamba na hayo, Waziri Mjawiri alieleza kuwa kufuatia ziara ya Rais Dk. Shein nchini Indonesia aliyoifanya Agosti, mwaka 2018 uongozi ulipata kuona aina mpya ya mwani wenye thamani ambao Zanzibar unapatikana pamoja na kutayarishwa kwa Makubaliano mawili ya Masharikiriano katika sekta ya kilimo na uvuvi.

Nao viongozi hao walieleza jinsi walivyonufaika baada ya kuona ufugaji unaofanywa na Kampuni ya ufugaji ya Al Rawabi ya Dubai ambako walikwenda kujifunza uwekezaji katika uzalishaji wa maziwa ambapo pia, Rais Dk. Shein aliwahi kuitembelea Kampuni hiyo katika ziara yake ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) aliyoifanya Januri 2018.

Akisoma taarifa ya utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo, Katibu Mkuu wake Mariam Juma Abdalla Saadalla alieleza mikakati ya kuimarisha sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi sambamba na kuhifadhi rasilimali zisizorejesheka.

Katibu Maariam alieleza kuwa upatikanaji wa fedha nyingi ambazo zimetokana na msukumo wa Rais na muongozo wake umepeelekea uwezo na kuongeza ufanisi katika Wizara hiyo pamoja na kuwepo kwa miradi kadhaa ambayo wataweza kuitakeleza ikiwemo kujenga maghala, kununua meli inayosarifu samaki, kujenga Viwanda vya samaki Unguja na Pemba pamoja na kujengwa mabwawa ya kufugia samaki.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.