Habari za Punde

Kuazishwa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) Matokeo ya Kutafsiri Kwa Vitendo Dhamira na Fursa ya Elimu Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akihutubia wakati wa hafla ya kusherehekea mafanikio ya SUZA toka kuazishwa kwake Zanzibar mwaka 1999 -2019, hafla hiyo imefanyika katika ukumbi wa Dk. Ali Mohamed Shein, Tunguu Zanzibar Wilaya ya Kati Unguja.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa kuanzishwa kwa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) ni matokeo ya kutafsiri kwa vitendo dhamira ya kupanua fursa ya elimu hapa Zanzibar baada ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964.


Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hafla ya kusherehekea mafanikio ya  Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) iliyofanyika kwenye ukumbi wa Dk. Ali Mohamwd Shein uliopo katika Kampasi ya Chuo Kikuu hicho, Tunguu, Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alisema kuwa Chama cha Afro Shirazi Party (ASP), kilikuwa na dira na malengo ya muda mrefu ya kuandaa rasilimali watu ya kuitumikia nchi hii na kusukuma mbele maendeleo yake.

Aliongeza kuwa malengo hayo ya kizalendo yaliyotangazwa na Rais wa mwanzo wa Zanzibar Marehemu Mzee Abeid Amani Karume, tarehe 23, kwala 1964 yameweza kufanikiwa hatua kwa hatua kutokana na dhamira ya dhati ya viongozi waliopo ambao kwa pamoja wamechukua hatua madhubuti za kuimarisha maendekeo ya elimu nchini.

Alieleza kuwa hali hiyo imechochea kuwepo kwa hatua za kuimarisha sekta ya elimu kwa kuzifungua fursa za kuanzisha vyuo vikuu hapa Zanzibar kwani kabla ya mwaka 1998, Zanzibar haikuwa na Chuo Kikuu hata kimoja na vijana wachache waliobahatika walilazimika kuifuata fursa ya kusoma vyuo vikuu nje ya Zanzbar.

Alisema kuwa uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Tano wa Dk. Salmin Amour Juma ulifanya uamuzi wa kuanzishwa kwa Vyuo Vikuu nchini kwa kuruhusu kuanzishwa kwa vyuo vikuu viwili vya binafsi mwaka 1998.

Rais Dk. Shein alisema kuwa kwa lengo la kutimiza matakwa ya Kisheria na mamlaka aliyonayo, Rais Mstaafu wa Zanzibar wa Awamu ya Sita, Dk. Amani Abeid Karume alizindua rasmi Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar mwaka 2001 na kumpongeza kwa mchango wake mkubwa alioutoa kiongozi huyo akiwa Mkuu wa mwanzo wa Chuo hicho.

Rais Dk. Shein ambaye pia, ni Mkuu wa Chuo hicho alieleza kuwa ni dhahiri kwamba mafanikio yaliopatikana katika kipindi cha miaka 18 ni ya kupigiwa mfano na ni makubwa ambayo yakwenda sambamba na malengo yaliyowekwa na Serikali wakati kilipoanzishwa chuo hicho.

Aidha, Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba, ilipoingia madarakani baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 iliendeleza jitihada za kuimarisha elimu ya juu pamoja na kukiimarisha chuo hicho kwa kuzingatia mipango ya maendeleo ya Zanzibar ikiwemo Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM ya mwaka 2010-2015.

Rais Dk. Shein alitoa pongezi kwa Baraza la Mapinduzi kwa kutoa mwongozo wa Kisera wa kukiimarisha chuo hicho kwa kukiunganisha na Taasisi zilizokuwa zikitoa elimu ya juu katika fani mbali mbali hapa Zanzibar.

Miongoni mwa Taasisi hizo ni Chuo cha Afya na Sayansi za Tiba, Chuo cha Uongozi wa Fedha na Chuo cha Mandeleo ya Utalii kwa awamu ya kwanza na hivi karibuni tu katika awamu ya pili kimeunganishwa na SUZA, Chuo cha Kilimo cha Kizimbani.

Alieleza kuwa kati ya faida za muunganisho huo ni kwamba baada ya Chuo cha Afya na Sayansi za Tiba kuwa miongoni mwa Skuli za SUZA, Serikali iliamua kuanzisha masomo ya Shahada ya Udaktari, ili kuweza kumarisha upatikanaji mzuri wa wataalamu wa sekta ya afya.

“Mtakumbuka kuwa katika mahafali iliyopita, wahitimu wa mwanzo 25 walimaliza masomo yao ya Udaktari mwaka 2018, na hivi sasa vijana hao wameshaajiriwa na Wizara ya Adfya na wapo katika Hospitali ya Mnazimmoja”,alisema Dk. Shein.

Aidha, alieleza kuwa ni jambo la faraja kwamba kuanzia mwaka huu wa masomo, mafunzo ya Shahada ya Udaktari wa meno na Shahada ya Uuguzi na Ukunga yataanza kutoewa.

Alieleza kuwa kutokana na haja ya Zanzibar ya kutoa wataalamu wa ngazi ya juu wa lugha ya Kiswahli, Serikali iliamua kuanzisha mafunzo ya Shahada ya Uzamivu (PhD) ya Kiswahili ambapo tayari wahitimu 11 wameshamaliza Shahada hiyo ya juu ya lugha ya Kiswahili.

Dk. Shein alieleza kuwa kazi kubwa iliyo mbele hivi sasa ni kuhakikisha mafanikio yaliopatikana yanaendelezwa kwa vitendo, yanatangazwa kwa wananchi na wageni ikiwa ni hatua muhimu ya kutathmini jitihada za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Alieleza kufarajika kwake kwa kuona kwamba Chuo hicho kimepata Cheti cha Ithibati (Accreditation) kilichotolewa na Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), pamoja na Cheti cha Utambuzi wa kutoa masomo ya Afya na kuitumia Hospitali ya Mnazimmoja kuwa ni hospitali ya kufundishia kutoka Bodi ya Afrika Mashariki.

Pia, alipongeza jitihada za kuzinduliwa rasmi kwa skuli mpya ya Utibabu wa Meno, Skuli ya Kilimo na Taasisi ya Masomo ya Ubaharia za Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar ambayo hio ni sifa ya pekee kwa Chuo hicho.

Rais Dk. Shein aliwapongeza Makamo Wakuu wa Chuo na Manaibu wao wote waliotangulia kwa kazi nzuri waliyoifanya na kutoa pongezi maalum kwa Mwenyekiti wa Baraza la Chuo aliyepo hivi sasa Said Bakari Jecha na Wajumbe wote wa Baraza pamoja na aliyekuwa Mmakamo Mkuu wa Chuo Profesa Idris Rai ambaye amefanya kazi kubwa ya kuhakikisha SUZA inapiga hatua kufuatana na maelekezo ya Serikali.

Alieleza kuwa wakati SUZA ikianzishwa kulikuwa na Kampasi moja leo zipo Kamapasi 8, ilianza na Skuli moja na leo zipo skuli 8, kulikuwa na taasisi moja leo zipo mbili pamoja na vituo viwili maalum kwa ajili ya utafiti ambavyo mwanzoni havikuwepo.

Pia, kwa upande  wa programu, zilianza mbili zilizokuwa na idadi ya wanafunzi 71 ambapo hivi sasa Chuo kinaendesha programu 62 zenye idadi ya wanafunzi 4042.

Alieleza mipango ya kuansihwa kwa Skuli ya Kompyuta, mawasiliano na Habari, Skuli ya Uhandisi wa Mafuta na Gesi pamoja na Taasisi ya Uvuvi na Masomo ya Bahari ambazo zote zinakwenda sambamba na mipango ya maendeleo.

Dk. Shein aliuagiza uongozi wa Chuo hicho kuendelea kuwajengea uwezo wahadhiri na watumishi wake wa kada mbali mbali iki kukidhi mahitaji ya chuo hicho ili kiweze kutoa wahitimu weledi wanaokubalika katika ngazi ya Taifa na Kimataifa.

Nae Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Riziki Pembe Juma alimpongeza Rais Dk. Shein kwa juhudi zake za kuhakikisha kinapata mafanikio makubwa ambayo tayari hivi leo yameshaanza kupatikana na yanaonekana wazi.

Mapema Makamu Mkuu wa Chuo hicho Dk. Zakia Mohamed Abubakar alitumia fursa hiyo kueleza historia ya Chuo hicho na kueleza kuwa Kamati ya watu saba iliundwa na aliyekwua Rais wa Zaanzibar Dk. Salmin Amor Juma mwaka 1996 kufanyia kazi suala la kuanzishwa kwa SUZA ikiongozwa na Profesa Saleh Idrissa.

Alieleza kuwa Chuo hicho ni cha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kilichoanzishwa kwa Sheria Namba 8 ya mwaka 1999 na kuzinduliwa mwaka 2001 hatua iliyopelekea  kuzinduliwa rasmi na Dk. Amani Abeid Karume akiwa ni Mkuu wa Chuo wa Mwanzo.

Dk. Zakia alisema kuwa Chuo kilianza masomo kwa kuanza na Idara ya Sanaa mwaka 2001/2002 mwaka wa mwanzo wa masomo ikiwa na wanafunzi 71 Shahada 50 na Stashahada 21.

Nae Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), Professa Charles Kihampa alitoa pongezi kwa Serikali kwa kuanzisha Shahada ya Udaktari wa Meno ambacho SUZA kitakuwa cha pili kwa Tanzania pamoja na kuanziasha programu ya Kilimo ambayo kwa Tanzania inatolewa na Chuo cha Sokoine kiliopo Morogoro pekee.

Pia, alitumia fursa hiyo kueleza kuwa TCU itaendelea kuiunga Mkono SUZA katika kuhakikisha inapata mafanikio zaidi kwani tayari hivi sasa SUZA inatambulika Kitaifa na Kimataifa.

Mapema Rais Dk. Shein alitembelea  mabanda ya maonesho yaliomo ndani ya ukumbi huo ambayo yaliendeshwa na SUZA na kupata maelezo kutoka kwa wanafunzi wa chuo hicho juu ya shughuli na elimu inayotolewa na Skuli pamoja na Taasisi zote zilizomo katika Chuo Kikuu hicho.

Pia, Rais Dk. Shein akiwa Mkuu wa Chuo hicho cha SUZA, alitoa vyeti vya utambuzi kwa viongozi waliokitumikia Chuo hicho tokea kuanzishwa kwake pamoja na yeye kukabidhiwa vyeti vya Utambuzi na Ithibati wa Chuo Kikuu hicho cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).

Viongozi mbali mbali wa vyama vya siasa na Serikali pamoja na wakuu wa vyuo mbali vya ndani na nje ya Zanzibar walihudhuria pamoja na Mabalozi, Wawakilishi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa, Wakufunzi, wanafunzi, wazee na wageni mbali mbali.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.