Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akihutubia na kuufungua Mkutano Mkuu wa Jumuiya ya Majaji na Mahakimu wa Nchi za Afrika Mashariki (EAMJA) uliofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Madinat Al Bahri Mbweni Zanzibar.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein
amesema kwamba matumizi mazuri ya ardhi na usimamizi bora wa mazingira ni
misingi muhimu katika maendeleo ya Taifa lolote duniani.
Rais Dk. Shein
aliyasema hayo leo katika Mkutano wa mwaka wa Jumuiya ya Majaji na Mahakimu wa
Nchi za Afika Mashariki unaofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Madinat Al Bahr,
Mbweni mjini Zanzibar.
Katika maelezo yake
Rais Dk. Shein alisema kuwa mkutano huo umekuja wakati muwafaka ambapo changamoto
kadhaa zinazohusiana na ardhi pamoja na mazingira zimekuwa zikiibuka katika
nchi za Afrika Mashariki.
Alisema kuwa
kuongezeka kwa idadi ya watu sambamba na kukua kwa uchumi kumeleta changamoto nyingi
katika sekta ya ardhi na mazingira katika nchi hizo na kutolea mfano migogoro
ya ardhi ambayo imeikumba miji na vijiji ambayo baadhi ya wakati hujumuisha
wananchi na wawekezaji walioekeza katika
nchi za Afrika Mashariki.
Aliongeza kuwa iwapo
hali hiyo itaendelea itakuwa ni tishio kwa maendeleo ya kiuchumi na usalama kwa
nchi za Afrika Mashariki huku akieleza jinsi alivyovutiwa na maudhui ya mwaka
huu yasemayo ‘’Ardhi na Mazingira kwa Maendeleo Endelevu ya Afrika Mashariki”.
Rais Dk. Shein
alieleza kuvutiwa na maudhui hayo ambayo yamekuja wakati muwafaka ambapo nchi nyingi za
Afrika Mashariki zimeweka mikakati ya makusudi katika kuimarisha mazingira na matumizi mazuri ya ardhi.
Alieleza kuwa kutokana
na mada zitakazojadiliwa katika mkutano huo wa siku nne ana matumaini makubwa
kuwa hatimae mkutano huo utakuja na mbinu pamoja na njia mbadala za kutatua
changamoto zilizopo.
Kwa upande wa
Zanzibar, Rais Dk. Shein alieleza hatua zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika
kutatua migogoro ya ardhi huku akisisitiza kuwa Zanzibar ardhi yote ni mali ya
Serikali kama ilivyoelezwa katika sheria namba 12 ya mwaka 1992.
Kwa upande wa
mazingira, Rais Dk. Shein alieleza changamoto mbali mbali za mazingira
zinazosababishwa na shughuli za kibinaadamu pamoja na athari za kimaumbile hasa
suala zima la mabadiliko ya tabianchi.
Rais Dk. Shein
alieleza haja kwa Jumuiya hiyo ikashirikiana na taasisi mbali mbali za serikali katika masuala ya kimazingira
hasa ikizingatiwa kwamba uchumi wa nchi za Afrika Mashariki unaendelea kukua
katika sekta nyengine mpya ikiwemo sekta ya mafuta na gesi ambayo imethibikika
kwamba imekuwa ikileta changamoto nyingi za mazingira katika nchi za Afrika pamoja
na zile nchi za Mashariki ya Kati.
Pia, alisisitiza
kwamba taaluma ya Sheria inahitajika katika kusimamia sekta hizo mpya ili
kwenda sambamba na ukuaji wa sekta hizo mpya.
Vile vile aliwahimiza
Majaji na Mahakimu kushirikiana na
Mihimili ya utungaji sheria ili kuweza kuja na sheria madhubuti katika kuja na
sheria ya utalii ambayo vuile vue inaendelea kukua kwa kasi katika nchi
wananchama.
Dk. Shein alieleza
changamoto ya mazingira Zanzibar hasa katika tatizo la mchanga na athari zake
huku akieleza haja ya kuimarisha sheria katika sekta ya utalii.
Katika hotuba yake
hiyo, Rais Dk. Shein alifahamisha juhudi zinazochukuliwa na Serikali katika
kuimarisha matumizi bora ya ardhi na uhifadhi wa mazingira kwa kutoa mfano semina
na viongozi iliyofanywa tarehe 16 mwezi Machi mwaka 2019 iiyowashirikisha
Majaji, Mahakimu, Wanasheria pamoja na watendaji wengine wa Serikali ili kupata
rai kwa kutafuta mwelekeo na njia mbadala juu ya matumizi bora ya ardhi na
mazingira na hatimae kuja na maazimio 28.
Aidha, Rais Dk. Shein
alieleza mwelekeo wa Zanzibar katika hatua za ufukiaji wa bahari kwa lengo la
kupunguza changamoto zilizopo.
Aliwafahamisha
wanasemina hao kwamba Zanzibar suala la ufukiaji wa bahari sio geni na
kufahamisha kwamba baadhi ya maeneo ya Mjai Mkongwe yamejenwga katika ardhi iliyofukiwa karibu karne moja na
nusu iliyopita yakiwemo maeneo ya Mji Mkongwe wa Zanzibar hasa katika eneo la
Darajani.
Anaamini wkamba jambo
hilo linawezekana hivi sasa, alifahamisha kwamba tayari mafanikio yameshaanza
kuonekana katika suala la ufukiajai wa ardhi wka kutoa mfano mradi uliofanywa na mwekezaji wa ndani Sheikh
Said Salim Bakhresa kupitia Kampuni yake ya SSB ya kufukia bahari na kufanya
shughuli za maendeleo katika eneo la Mtoni kwa kujenga hoteli ya kisasa,
viwanja vya watoto, michezo ya maji na mambo mengineyo.
Alikipongeza kitendo
hicho kilichofanywa na mwekezaji huyo kwa kuonesha matumizi mazuri ya
ardhi hapa Zanzibar inayoenda sambamba
na maudhui ya mkutano huo.
Sambamba na hayo, Rais
Dk. Shein aliitaka Jumuiya hiyo kufanya bidii katika kuhakikisha kunafanywa
tafsiri ya Sheria kutoka lugha ya Kiingereza na kwenda lugha ya Kiswahili jambo
ambalo litawasaidia na kuwarahisishia wananchi katika kupata haki zao za kisheria katika kuzifahamu
sheria jambo ambalo ni muhimu katika kutafuta haki zao za kisheria na kuwafanya
kuwa raia bora wenye kutii sheria.
Alieleza kuwa ufahamu
wa Sheria ni jambo muhimu katika kupata haki kwa wananchi hivyo, Majaji na
Mahakimu wana dhima ya kushirikiana na taasisi nyengine za nchi za Afrika
Mashariki katika kuiendeleza lugha ya Kiswahili ili lugha hiyo iendelee kukua
kwa kasi zaidi na na kutumika katika mikutano
mikubwa ya Kimataifa.
Aliwataka Majaji hao
wahakikishe kwamba lugha hiyo ina msamiati wa kutoka katika masual ya sheria
pamoja na masuala mengine ya kiuchumi, teknolojia na kijamii.
Alisisitiza na
kupendekeza kuwa katika mikutano ijayo kukatumika
lugha ya Kiswahili huku akieleza haja ya kutumia lugha hiyo na kuhakikisha
Kiswahili inakuwa na msamiati wa kutosha katika sheria na masuala mengineyo na kimaendeleo.
Rais Dk. Shein
aliipongeza Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania kwa juhudi zake inazozichukua
katika kutafsiri Sheria kutoka lugha ya Kiingereza kwenda lugha ya Kiswahili.
Nae Jaji Mkuu wa Zanzibar
Omar Othman Makungu alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa
juhudi zake alizozichukua katika kuhakikisha watendaji katika kada ya Sheria
wakiwemo Majaji, Mahakimu na Wanasheria wanatizamwa vizuri ikiwa ni pamoja na
kuwaongezea mishahara.
Aidha, Jaji Makungu
alimpongeza Rais Dk. Shein kwa kuipa ardhi Mahakama Kuu kwa ajili ya Ujenzi wa
Mahakama Kuu huko Tunguu, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja ambapo hapo
jana Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilitiliana saini na Kampuni ya “ADVET
Constraction Limited kwa ajili ya kuanza ujenzi.
Nao viongozi wengine
wa Jumuiya hiyo kutoka nchi za Afrika ya Mashariki akiwemo Rais wa Jumuiya hiyo
Jaji Anjeline Rutazama walieleza hatua mbali mbali zinazochukuliwa na Jumuiya
hiyo katika kuhakikisha suala zima la sheria linapewa kipaumbele katika sekta
zote muhimu ndani ya nchi za Afrika Mashariki.
Aidha, waliipongeza
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuufadhili mkutano huo kwa asilimia 90 za
bajeti ya mkutano huo pamoja na kutoa shukurani kwa Taasisi nyengine ambazo
zimewaunga mkono katikia kufanikisha mkutano huo.
Viongozi kadhaa
walihudhuria katika Mkutano huo akiwemo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
Balozi Seif Ali Idd, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid, Jaji
Mkuu wa Zanzibar Omar Othman Makungu, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Profesa Ibrahim Juma, Majaji, Wanasheria, Majaji Wastaafu, Mahakimu
kutoka nchi za Afrika Mashariki , Mawaziri na viongozi wengine.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment