Habari za Punde

Sekta ya Uvuvi Zanzibar Inaimarika Katika Uvuvi wa Bahari Kuu.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akikata utepe kuashiria kuizindua Boti Mpya ya Kisasa ya Kampuni ya Uvuvi Zanzibar (ZAFICO) Sehewa 2, kushoto kwa Rais Naibu Waziri wa Kilimo Maliasili Mifugo na Uvuvi Zanzibar.Dkt. Makame Ali Ussi, hafla hiyo ya uzindizi imefanyika katika eneo la Hoteli ya Verde Mtoni Zanzibar leo, 2-12-2019.

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba kwa kuzingatia kuwa bado eneo la bahari la Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania halijatumika ipasavyo katika sekta ya uvuvi imeanza jitihada na mikakati ya kuhakikisha sekta hiyo inaimarika.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo zilizofanyika huko katika eneo la Hoteli ya Verde Mtoni, nje kidogo ya Mji wa Zanzibar katika uzinduzi wa boti mpya ya Uvuvi “Sehewa 02” inayomilikiwa na Kampuni ya Uvuvi Zanzibar (ZAFICO) hafla iliyokwenda sambamba na uzinduzi wa boti 3 za doria zinazomilikiwa na Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi, katika Idara ya Maendeleo ya Uvuvi.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alisema kwamba Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ina eneo la Ukanda Maalum wa Bahari wa Kiuchumi (EEZ) lenye ukubwa wa kilomita za mraba zipatazo 223,000 eneo ambalo litatoa fursa ya kuwekeza katika uvuvi wa Bahari Kuu ambapo samaki wakubwa wa aina ya jodari na jamii yake na wengine wa aina mbali mbali wanapatikana kwa wingi.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa bado kunalazimika kuziruhusu meli za kigeni kuendesha shughuli za uvuvi, kwa makubaliano maalumu ikiwa ni njia moja ya kunufaika na rasilimamali za baharini.

Alieleza kuwa uvuvi katika eneo la Bahari Kuu kwa sasa unafanyika kupitia meli kubwa za kigeni ambazo huwa zimepatiwa leseni za uvuvi kutoka Mamlaka ya Bahari Kuu ambapo hadi sasa wastani wa meli 100 za kigeni zinavua katika ukanda huo kwa mwaka.

Alisema kuwa jumla ya tani 12,276.2 za samaki wa aina ya Jodari na jamii zake zimevuliwa na meli kutoka nchi za Taiwan,Oman, Seychelles, Korea, Thailand, China, France, Spain na Mauritius ambazo zimepewa leseni ya uvuvi wa bahari kuu na Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu.

Hivyo, alieleza haja ya kuongeza bidii katika kuzitumia wenyewe rasilimali za bahari ili kuweza kufaidika moja kwa moja na matunda yake badala ya kusubiri kupokea faida kutoka mkono wa pili. “Hali hii inakwenda sambamba na methali isemayo “Kivuli cha mvumo, huwafunika walio mbali” alisisitiza Rais Dk. Shein.

Rais Dk. Shein aliongeza kuwa Serikali imeunda upya Kampuni ya Uvuvi ya Zanzibar, “Zanzibar Fisheries Company-ZAFICO” na imetafutiwa vifaa na nyenzo za kisasa za kuendeleza sekta ya uvuvi, ili kuweza kufanya matumizi bora ya bahari na hatimae kuleta tija.

Alieleza kwamba Shirika hilo lilikuwepo hapo kabla lililoanzishwa mwaka 1974 likijulikana kwa jina la “ZAFICO- Zanzibar Fisheries Coporation” ambalo ofisi zake zilikuwa eneo la Malindi ambalo lengo lake kuu la kuanzishwa kwake ilikuwa ni kukuza sekta ya uvuvi na kuongeza upatikanaji wa samaki kwa wananchi wa Zanzibar.

Hivyo, Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba, iliamua kuunda Kampuni ya Uvuvi Zanzibar (ZAFICO) kupitia Sheria Namb.15 mwaka 2013, ya usajili wa Makampuni Zanzibar kama ni hatua muhimu ya utekelezaji wa mipango na mikakati ya kuimarisha sekta ya uvuvi.

Alisisitiza kuwa hayo yote ni miongoni mwa utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 ambayo inasisitiza juu ya uimarishaji wa sekta ya uvuvi.

Aidha, Rais Dk. Shein alisema kwamba historia inaeleza kwamba wavuvi ndio wakaazi wa mwanzo waliohamia Zanzibar kutoka sehemu za Bara ambao waliishi katika eneo la Shangani, hivyo kuna kila sabahu ya kuiendeleza kazi hiyo ya uvuvi kwa kadri teknolojia inavyoimarika.

“Uvuvi kwetu ni kazi ya jadi, Wahenga walisema “Mkataa asili si mjasiri” kwa hivyo, na sisi ni lazima tuwe wajasiri katika kuziendeleza kazi za asili tulizozirithi kwa wazee wetu, ambazo ni za halali na zenye tija kwetu”,alisema  Dk. Shein.

Alieleza kuwa kwa muda mrefu wavuvi wamekuwa wakivua katika maeneo ya bahari yaliyo karibu ambayo tayari yameashiria upungufu wa upatikanaji wa samaki ambapo shughuli  za uvuvi za kila siku katika maeneo hayo zinapelekea kuwa tishio kubwa kwa mazingira ya bahari.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alisema kuwa mipango ya kuimarisha uchumi wa bahari inaendelea vizuri hapa nchini ikiwa ni pamoja na jitihada za kununua vyombo vipya vya baharini vilivyo na ubora pamoja na kuwashajiisha wawekezaji kuewekeza katika eneo hilo.

Alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inakusudia kuunda Idara itakayokuwa katika Wizara ya Fedha na Mipango (Tume ya Mipango), ili iweze kusimamia uchumi wa bahari huku akieleza kwamba tayari wameshajitokeza Washirika wa Maendeleo kuunga mkono eneo hilo.

Alieleza kuwa Serikali imepata ufadhili wa Dola za Kimarekani milioni 8.8 kutoka Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), ambazo zitatumika katika kuimarisha sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi ambapo pia, fedha hizo zitatumika kwa kujengea viwanda vidogo vidogo vya kusarifu samaki na mazao mengine ya baharini Unguja na Pemba.

Rais Dk. Shein alisema kuwa ili boti hizo zifanye kazi zake vizuri lazima kuhakikishwe kwamba wapo wataalamu wazuri wa kuziendesha na kuzishughulikia huku akitaka kutumiwa vizuri boti za doria kwa ajili ya kulinda maeneo ya bahari, fukwe na rasilimali za bahari ambazo baadhi yao ni muhimu kwa sekta ya utalii ambayo ni muhimu mkuu wa uchumi.

Alieleza kuwa ili sekta ya uvuvi pamoja na Kampuni ya (ZAFICO) iweze kupiga hatua na kupata maendeleo ya haraka, inahitaji ishirikiane na Taasisi mbali mbali za umma na binafsi huku akiwataka viongozi wa (ZAFICO) kuwa wabunifu na wajenga ari ya kujifunza zaidi.

Alisisitiza haja ya kujitathmini utendaji wa kazi zao kwa kufanya rejea za yale mambo ambayo yalipelekea (ZAFICO) ya mwanzo kuanguka. Pia alipongeza ujumbe wa sherehe hizo usemao “Tuimarishe uchumi wa bahari”.

Nae Waziri wa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Mmanga Mjengo Mjawiri alisema kwamba Serikali imegharimu fedha nyingi katika ununuzi wa boti hizo hatua ambayo ni miongoni mwa utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020.

Aliongeza kuwa mafanikio ya ununuzi wa boti hizo sambamba na kuifufua upya Kampuni ya ZAFICO yote hayo yanatokana na usimamizi imara wa Rais Dk. Shein katika kuhakikisha sekta ya utalii inaimarika.

Mapema Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Mariam  Juma Saadallah alisema kuwa Boti ya ZAFICO imetengenezwa nchini SriLanka na Kampuni ya Hairu Naval Craft Engineering Ltd ikiwa na urefu wa mita 18.5m na upana mita 5.1m kwa thamani ya TZS Bilioni 1,130.000.

Aidha, alisema kuwa katika kuimarisha ulizni wa bahari na kupambana na uvuvi haramu, Idara ya Maendeleo ya Uvuvi kupitia Mradi wa SWIOFish umenunua boti 3 za doria kutoka kampuni ya ‘TOM CAT BOAT BUILDINGS’ iliopo Afrika ya Kusini kupitia Kampuni ya Kizalendo ya hapa Zanzibar iitwayo Visiwani Traders ambapo boti hizo zilizogharimu jumla ya TZS 583,165,440.

Mapema Rais Dk. Shein aliizindua Boti hiyo na kupata maelezo kutoka kwa wafanyakazi pamoja na viongozi wa ZAFICO akiwemo Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni hiyo Zahor Kassin Mohammed ambapo pia, alipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Uvuvi Mussa Aboud Jumbe kuhusiana na Boti hizo 3 za doria.

Pia, Rais Dk. Shein alipata fursa ya kutembelea banda la Wajasiriamali walikuwa wakiuza bidhaa mbali mbali zikiwemo zile zinazotokana na rasilimali za bahari ambapo pia, wakati huo huo alikabidhi vifaa vya uvuvi zikiwemo mashine, nyavu na vihori kwa vikundi vya uvuvi kutoka Wilaya mbali mbali hapa nchini.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.