Mdhibiti wa Magonjwa ya
Kuambukiza wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Dkt.
George Ndaki (anayetazama komputa), leo akikagua abiria (hawapo pichani)
waliowasili leo wakitokea nchi mbalimbali ili kubaini waliopata maambukizi ya
homa ya Corona iliyoanzia nchini China hivi karibuni.
Na Bahati Mollel, TAA
KITENGO cha Kudhibiti Magonjwa ya Kuambukiza, kilichopo chini ya
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwenye Kiwanja cha
Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), kimejipanga kukabiliana na
wagonjwa watakaobainika kuwa na virusi vya homa ya Corona, vilivyoanzia nchini China.
Daktari George Ndaki, ambaye ni Mdhibiti wa Magonjwa ya Kuambukiza
wa JNIA, leo amesema Wizara ya Afya imekabiliana na ugonjwa huo na tayari imefunga
mashine tano zinazotumia komputa zinazopima joto la mwili la abiria bila
kujitambua, na mashine sita za mkononi, ambazo abiria anapimwa endapo
ataonekana kuwa na joto kali zaidi.
Amesema mashine moja imefungwa kwenye Jengo la Watu Mashuhuri
(VIP) , nyingine imefungwa Jengo la Pili la abiria na tatu zipo jengo la Tatu
la abiria; wakati za mkono zimeganywa kwenye majengo hayo.
Dkt Ndaki amesema wataalam wa afya wanaokuwa kwenye mashine
zinazotumia komputa wanamtambua abiria mwenye jotokali mara anapopita mbele ya
kamera, na endapo litabainika ni zaidi ya nyuzijoto 37.4 anahakikiwa zaidi kwa
kutumia mashine ya mkono, huku akihojiwa zaidi juu ya afya yake na nchi
aliyotoka, ili kubaini endapo anavirusi hivyo.
“Hadi sasa hakuna abiria aliyebainika kuwa na ugonjwa huu, lakini
tunaendelea kwani hapa Kiwanja cha ndege ni moja ya njia kuu au lango Kuu la
abiria hususan wa nje ya nchi wanapotumia kuingia nchini, na ndio maana
tunawakagua na tunashukuru Serikali yetu kupitia Wizara ya Afya kwa kuwa na
mashine hizi mbili, ambazo zinafanyakazi mara mbili na kwa uhakika zaidi ili kubaini
abiria mwenye virusi, ambaye atapelekwa eneo maalum kwa ajili ya uchunguzi
zaidi,” amesema Dkt Ndaki.
Dkt Ndaki amesema pamoja na kukaguliwa kwa abiria wote wanaowasili
kutoka nje ya nchi, pia wanaweka mkazo zaidi kwa abiria wanaotoka nchi
zilizoathiriwa na ugonjwa huom, ambapo abiria wake mbali na kupimwa joto la
mwili, pia wanaandikwa majina yao na maeneo wanayokwenda baada ya kutoka JNIA.
“Ukiangalia kuna ndege ambazo zinakuja na abiria waliotoka China
baada ya kuunganisha ndege kama Kenya Airways, Qatar, South Africa, Fly
Emirates na na Shirika la ndege la
Tanzania (ATCL), zinakuwa aidha zimebeba abiria waliounganisha ndege kutoka
nchi zilizoshambuliwa na homa ya Corona”. Amesema Dkt Ndaki.
Hata hivyo, amesema siku zote wamekuwa wakijiweka tayari kwa ajili
ya kukabiliana magonjwa mbalimbali ya mlipuko na kuambukiza, ili yasiweze
kuingia nchini kupitia mipaka mbalimbali, pamoja na viwanja vya ndege.
Mbali na China nchi nyingine zilizoathirika na homa hii ni pamoja
na Thailand, Australia, Marekani, Singapore, Malaysia, Japan, Korea Kusini,
Ufaransa, Canada, Vietnam, Ujerumani, Nepal, Sri-lanka na Cambodia. Hata hivyo,
kasi ya maambukizi ya virusi vya Corona sasa ni tishio hadi Barani Ulaya.
Corona ni kundi kubwa la aina ya virusi, ambavyo huweza kumuathiri
binadamu na wanyama, ukubwa wa maambukizi unahusisha homa za kawaida pamoja na
homa kali na wakati mwingine matatizo katika mfumo wa upumuaji.
Dalili za kuathiriwa na virusi vya Corona ni pamoja na kukohoa,
homa kali, nimonia, kupumua kwa tabu, kutapika na kuharisha; na hali ikiwa
mbaya dalili hizi hujidhihirisha matatizo kwenye mapafu na figo kushindwa
kufanya kazi.
Namna mtu anavyoambukizwa homa hii ni pamoja na kugusana moja kwa
moja bila kinga na muathirika; kushika kwa mkono vifaa vya muathirika na baadaye
kushika mdomoni au puani, ambapo virusi husambaa kwa kasi.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Profesa
Palamagamba Kabudi, hivi karibuni amesema hakuna Mtanzania yeyote anayeishi
nchini China, aliyekumbwa na maambukizi ya virusi vya homa ya Corona,
vilivyozuka katika Mataifa ya Marekani, China, Thailand, Korea Kusini na Japan.
Waziri Kabudi ameyasema hayo wakati akitoa ufafanuzi juu ya hali
ya Watanzania waishio nchini China na kusema kuwa Tanzania ina wanafunzi
takribani 4000, ambapo katika mji wa Wuhan kuna wanafunzi 400 na kwamba kwa
mujibu wa Balozi wa Tanzania Nchini China, Balozi Mbelwa Kairuki,
ameihakikishia Serikali kuwa mpaka sasa hakuna mtanzania yeyote aliyeathiriwa
ama kukumbwa na maradhi hayo.
Ameongeza kuwa Tanzania inaendelea kufuatilia kwa ukaribu kujua
maendeleo na hali za Watanzania wanaoishi jimboni Wuhan na China kwa ujumla na
kuwataka Watanzania kuwa makini na suala la kutoa taarifa zisizo rasmi ama
uvumi, kwani kwa kufanya hivyo ni kinyume cha sheria za Tanzania na kuwataka
kuwa na subira ili kupata taarifa rasmi kutoka serikalini.
Kutokana na maradhi haya kuwa mapya hadi sasa hakuna chanjo ya
homa hii , na badala yake wagonjwa wamekuwa wakipewa dawa za kutuliza maumivu
pekee.
Wataalam wa Kitengo cha Kudhibiti Magonjwa ya Kuambukiza wa
Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), leo wakijiandaa
kabla ya kutua kwa ndege zinazofanya safari zake kutoka nchi mbalimbali kwenye
Jengo la Tatu la abiria (TB3).
Moja ya eneo la ukaguzi wa afya kwa abiria wanaowasili kupitia Kiwanja
cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), wakitokea nchi mbalimbali.
Abiria waliowasili kwa ndege ya Qatar wakikaguliwa kwa mashine
maalum za kupima joto la mwili, ili kubaini walioingia nchini na virusi vya
Homa ya Corona iliyoanzia nchini China hivi karibuni, na kuua watu kadhaa.
Afisa Afya Mkuu Mazingira, Onesmo Kitange (mwenye mashine ya
mkono), leo akimpima Maitrick Dave, raia wa India, aliyewasili kwa ndege ya
Kenya Airways alipowasili leo kwenye
Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA).
No comments:
Post a Comment