Habari za Punde

Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolijia na Ubunifu Kufanyika Jijini Dodoma


Naibu  Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Mhe. William Tate Ole  Nasha akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma kuhusu mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU) mwaka 2020  yatakayofanyika kati ya Machi 16 hadi 20 mwaka huu Jijini Dodoma .


Mkurugenzi mkuu wa Idara ya wateja wakubwa Benki ya CRDB Bw. Prosper Nambaya akisisitiza kuhusu Benki hiyo kuendelea kushirikiana na Wizara ya Elimu , Sayansi na Teknolojia katikamashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU) mwaka 2020  yatakayofanyika kati ya Machi 16 hadi 20 mwaka huuJijini Dodoma .

 (Picha zote na  MAELEZO)

Na Mwandishi wetu- Dodoma                                                                                             Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU) mwaka 2020  kufanyika kati ya Machi 16 hadi 20 mwaka huu .                                                             

Akizungumza leo Februari  5, 2020, Jijini Dodoma, Naibu Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Mhe. William Tate Ole Nasha amesema kuwa lengo la MAKISATU ni kuibua, kutambua , kuendeleza Ubunifu na Ugunduzi unaofanywa na Watanzania ili kuchochea maendeleo  katika sekta mbalimbali.

“Mashindano haya yanatoa fursa kwa wabunifu na wagunduzi wa teknolojia mbalimbali kujitangaza na kutangaza bunifu zilizozalishwa ambapo  kaulimbiu ya mwaka huu ni ” Sayansi, Teknolojia na Ubunifu kwa Uchumi wa Viwanda”. alisisitiza Mhe Ole Nasha
Akizungumzia walengwa wa mashindano hayo Ole Nasha amesema kuwa ni Shule za Msingi; Shule za Sekondari; Vyuo vya Ufundi Stadi; Vyuo vya Ufundi wa Kati; Vyuo Vikuu, Taasisi za Utafiti na Maendeleo pamoja na mfumo usio rasmi.

Akifafanua amesema kuwa Serikali inatambua umuhimu wa mchango wa wabunifu na teknolojia katika kurahisisha na kuongeza ufanisi kwenye utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii na uzalishaji kupitia viwanda.

Akizungumzia mafanikio ya uendelezaji Sayansi na Teknolojia Mhe. Ole Nasha amesema kuwa hadi sasa Serikali imeweza kusimamia uanzishwaji wa vituo atamizi vipya 17 kwa ajili ya kukuza na kuendeleza ubunifu na hivyo kuanzishwa kwa  makampuni mapya 94 yanayotokana na ubunifu na kuzalisha ajira za moja kwa moja kwa vijana takribani 600 na ajira zisiszo za moja kwa moja zaidi ya vijana  elfu kumi na tano.

Mafanikio mengine ni pamoja na Serikali kuibua na kutambua wabunifu wachanga zaidi ya 415 na kati ya hao wabunifu 60 mahiri wanaendelezwa ili ubunifu wao uweze kufikia hatua ya kubiasharishwa.

Aidha, Usajili wa washiriki wa Mashindano haya ulianza tangu tarehe 2 Januari, 2020 na unaratibiwa na Wizara ya Elimu , Sayansi na Teknolojia ikishirikiana na Taasisi zake ambazo ni ; Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia ambayo inasajili wabunifu wa makundi ya Vyuo Vikuu na Taasisi za Utafiti na Maendeleo.

Taasisi nyingine ni pamoja na; Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) inayosajili wabunifu wa makundi ya Vyuo vya Ufundi Stadi na Mfumo usio Rasmi; Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) linalosajili wabunifu wa kundi la Vyuo vya Ufundi  wa Kati.

Mhe. Ole Nasha aliishukuru Benki ya CRDB kwa utayari wao wa kushirikiana na Wizara hiyo katika kukuza na kuimarisha ubunifu na teknolojia nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi mkuu wa Idara ya wateja wakubwa Benki ya CRDB Bw. Prosper Nambaya amesisitiza  kuwa  Benki hiyo itaendelea kushirikiana na Wizara ya Elimu , Sayansi na Teknolojia katika mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU) mwaka 2020  yatakayofanyika kati ya Machi 16 hadi 20 mwaka huu Jijini Dodoma .

Mwongozo na Fomu za maombi ya kushiriki zinapatikana katika tovuti za Wizara na Taasisi zake. sUsajili unafanyika pia kupitia tovuti ya MAKISATU, http//makisatu.costech.or.tz.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.