Habari za Punde

Zanzibar na Angola Kushirikiana Katika Sekta ya Utalii Chachu ya Maendeleo Kwa Pande Mbili Hizo.


Rais wa  Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Ali Mohamed Shein, akizungumza na  mgeni wake Balozi wa Angola Nchini Tanzania .Mhe.Sandro Agostinho De Oliveira , alipofika Ikulu Jijini Zanzibar kwa mazungumzo na kujitambulisha, leo Ikulu. 6-2-2020.(Picha na Ikulu) 

RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameupongeza uwamuzi wa busara na wenye tija wa Angola wa kutaka kushirikiana na Zanzibar kwenye sekta ya utalii hatua ambayo itaimarisha uhusiano wa kihistoria uliopo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo, Ikulu Jijini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Balozi wa  Angola katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  Sandro Agostinho de Oliveira aliyefika Ikulu kwa ajili ya kujitambulisha kwa Rais.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuusifu na kuupongeza uwamuzi huo wa Angola wa kutaka kushirikiana na Zanzibar katika sekta ya utalii na kusisitiza kuwa hatua hiyo ni chachu ya maendeleo kwa pande mbili hizo.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi Oliveira kuwa Zanzibar na Angola  zina mambo mengi ya kushirikiana kwa pamoja ambayo yanaweza kuleta mafanikio makubwa kwa pande zote mbili yakiwemo mashirikiano katika sekta ya utalii.

Dk. Shein alieleza kuwa  uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na Angola ni njia moja wapo kubwa itakayopelekea kuimarika zaidi kwa sekta ya utalii ambapo Zanzibar  imepiga hatua kubwa..

Aidha, Dk. Shein alimueleza Balozi Oliveira kuwa Zanzibar na Angola zote kwa pamoja zina mambo mengi ya kujifunza kwa kila upande ikiwa ni pamoja na namna ya kuendeleza na kuimarisha sekta ya utalii.

Alisema kuwa kwa upande wa  Zanzibar sekta ya utalii ni nguzo kubwa ya uchumi ambayo imekuwa ikichangia kiasi cha asilimia 20 ya Pato la Taifa na asilimia 80 ya fedha za kigeni.

Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa mashirikiano katika sekta ya utalii yatazidisha na kuimarisha uhusiano wa kihistoria ulioanzishwa na waasisi wa pande mbili hizo kupitia vyama vyao vya  (CCM) na MPLA.

Dk. Shein aliongeza kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ina mashirikiano makubwa na nchi za Kusini mwa Bara la Afrika kwani iliweza kushirikiana nazo bega kwa bega katika kupigania uhuru ikiwemo Angola, Msumbuji na Afrika Kusini kupitia vyama vyao vya ukombozi vya siasa.

Aliongeza kuwa, kutokana na Angola kupata mafanikio makubwa katika sekta ya mafuta na gesi asilia ipo haja kwa Zanzibar na nchi hiyo kushirikiana kwa pamoja katika kuhakikisha Zanzibar inapanua wigo kwa nchi hiyo ambayo ni ya pili kwa uzalishaji wa mafuta na gesi asilia barani Afrika ikitanguliwa na Nigeria.

Akieleza kuhusu mashirikiano katika sekta ya elimu, Rais Dk. Shein alieleza kuwa ipo haja kwa pande mbili hizo kushirikiana katika sekta ya elimu hasa kupitia vyuo vya nchi hizo kikiwemo Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) katika Kada ya lugha hasa lugha Kireno.

Aidha, Dk. Shein aliongeza kuwa mashirikiano yanaweza kuimarishwa katika sekta hiyo ya elimu, ikiwa ni pamoja na kubadilishana utaalamu na wataalamu hasa katika lugha ya Kireno ambayo itasaidia sana Zanzibar katika kuimarisha sekta ya utalii.

Rais Dk. Shein pia, alitumia fursa hiyo kumpongeza Rais wa Angola Joao Lourenco kwa kazi nzuri anayofanya ya kuiongoza nchi hiyo kwa mafanikio makubwa ambapo hivi sasa uchumi wake unakuwa kwa asilimia 8.4 na kueleza kuwa hayo ni miongoni mwa mambo yaliopelekea ushindi wa kishindo wa kiongozi huyo pamoja na chama chake cha (The People's Movement for the Liberation of Angola) MPLA.

Nae Balozi wa Angola nchini Tanzania Sandro Agostinho de Oliveira alimueleza Dk. Shein kuwa Angola iko tayari kushirikiana na Zanzibar katika sekta ya utalii  hasa ikizingatiwa kwamba Zanzibar imeanza kupata mafanikio na kutajika duniani kote katika sekta hiyo.

Balozi Oliveira alimueleza Rais Dk. Shein kuwa Angola ina mambo mengi ya kujifunza kutoka Zanzibar katika sekta ya utalii, hivyo iko tayari kushirikiana na Zanzibar katika kuimarisha sekta hiyo muhimu ya kukuza uchumi.

Katika maelezo yake Balozi Oliveira alimueleza Dk. Shein, kuwa Angola pia, iko tayari kutoa nafasi za masomo kwa Zanzibar katika Chuo chake kinachotoa mafunzo ya mafuta na gesi asilia ikiwa ni njia moja wapo ya kuendeleza ushirikiano wa kihistoria uliopo.

Alieleza kuwa kutokana na mafanikio makubwa yalioipata nchi yake katika sekta ya mafuta na gesi asilia, Angola iko tayari kushirikiana na Zanzibar katika sekta hiyo.

Sambamba na hayo, Balozi huyo alimueleza Rais Dk. Shein juhudi zinazochukuliwa na nchi yake katika kupambana na rushwa huku akisisitiza kuwa nchi yake itaharakisha mchakato wa  mashirikiano na Zanzibar katika kuendeleza sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo sekta ya utalii, elimu, mafuta na gesi asilia pamoja na kuendeleza utamaduni.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.