Habari za Punde

Uongozi wa Wizara ya Ardhi Nyumba Maji na Nishati Zanzibar Yawailisha Taarifa ya Utekelezaji wa Mpango Kazi Kwa Mwezi Julai hadi Disemba 2019 /2020.

Waziri wa Ardhi,Nyumba,Maji na Nishati Salama Aboud Talib (katikati) akifafanua jambo katika Mkutano wa Utekelezaji Mpango kazi kwa Kipindi cha Julai-Disemba 2019, kwa Wizara hiyo uliofanyika leo katika ukumbi wa Ikulu Mjini Zanzibar,na kulia Naibu Waziri wa Ardhi,Nyumba,Maji na Nishati Juma Makungu Juma


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, ameeleza haja kwa uongozi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati kuendeleza uzalendo na uadilifu katika ufanyaji wa kazi zao.

Hayo aliyasema leo, Ikulu Jijini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati wakati ilipowasilisha utekelezaji wa Mpango Kazi  kwa kipindi cha Julai hadi Disemba 2019/2020.

Rais Dk. Shein aliwanasihi viongozi hao pamoja na wafanyakazi wote wa Wizara hiyo kuendelea kushirikiana sambamba na kuendeleza kasi ya kuwa wazalendo kwa kupenda vyao na kuithamini nchi yao sambamba na kuwa waadilifu katika kazi zao na maisha yao.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwashukuru na kuwapongeza wafanyakazi wote wa Wizara hiyo na kueleza kuwa yeye binafsi pamoja na Serikali wameridhika na utendaji wao wa kazi na kusisitiza haja ya kuendelea kumsaidia Waziri wao kutokana na uongozi wake madhubuti.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kufuata taratibu na sheria katika  kufanya maamuzi yao ili kuepuka sintofahamu kwa wananchi na kuwataka kutumia busara kubwa sana katika utendaji wao wa kazi hasa pale wanapoitukia jamii.

Alisisitiza umuhimu wa taarifa kwa viongozi wa mamlaka ya juu katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku  huku akiwataka viongozi hao pamoja na watendaji wa Wizara hiyo kuongeza kasi ya utendaji wa kazi zao ili kufikia malengo waliyokusudia.

Aidha, Rais Dk. Shein alisisitiza haja kwa Mamlaka ya Hifadhi na Uendelezaji Mji Mkongwe kuongeza kasi katika utoaji wa elimu kwa wananchi  juu ya uingiaji wa vyombo vya moto  kwa kushirikiana na taasisi nyenginezo ili zoezi hilo liende vyema.

Rais Dk. Shein pia, ameitaka Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) kuhakikisha ndani ya mwezi mmoja inaweka huduma ya umeme unaotumia nguvu za jua katika kisima kimoja wapo kwenye visima vinavyosimamiwa na Mamlaka hiyo.

Katika maelezo yake katika uwasilishaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo Rais Dk. Shein aliwataka viongozi na watendaji kuendelea kupendana na kushirikiana ili waweze kufanikisha shughuli zao ikiwa ni pamoja na kuwatumikia  vyema wananchi.

Rais Dk. Shein aliipongeza Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati (ZURA) kwa kuja na hoja Serikalini ya kujenga jengo jipya la Ofisi lililopo Maisara hatua itakayozidisha ufanisi na kuinua ari kwa wafanyakazi kufanya kazi ipasavyo.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliipongeza kazi nzuri ya uwasilishaji iliyofanywa na Wizara hiyo huku akisisitiza haja ya kuwepo kwa usimamazi mzuri kwa watendaji wa Wizara hiyo kutokana na sekta zake kuwagusa wananchi moja kwa moja.

Mapema Waziri wa Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati Salama Aboud Talib akisoma utangulizi wa Utekekezaji wa Wizara hiyo alisema kuwa Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati inatekeleza Malengo na Mikakati ya Serikali ya kuhakikisha kwamba Wananchi wa Visiwa vya Zanzibar kwa ujumla wao wanapata huduma stahiki.

Akizitaja huduma hizo alieleza kuwa ni pamoja na maji, nishati ya uhakika iliyo salama na endelevu, makaazi bora na matumizi mazuri ya ardhi yenye kukidhi mahitaji ya wananchi na shughuli nyengine za kiuchumi na kijamii.

Waziri huyo alieleza kuwa Wizara yake kupitia Mamlaka ya Maji (ZAWA) imeendelea kusimamia miradi na program za uhuishaji na upanuzi wa shughuli za maji Mijini na usambazaji wa maji Vijijini.

Alisema kuwa katika utekelezaji wa program hiyo, Mamlaka ya Maji kupitia mradi wa maji wa Mkoa wa Mjini Magharibi (ADF12) imekamilisha kazi ya utekelezaji wa mradi kwa uchimbaji wa visima vipya sita vyenye uwezo wa wastani wa lita 150,000 kwa saa kwa kila kisima.

Utekelezaji mwengine ni ukarabati wa visima vikongwe 23, ujenzi wa matangi 2 yenye ujazo wa lita milioni mbili Saateni na milioni moja la Mnara wa Mbao pamoja na ulazaji wa mabomba yenye urefu wa kilomita 75.7.

Aliongeza kuwa Wizara hiyo kupitia Shirika la Umeme katika kipindi cha mwaka wa fedha 2019/2020 imefanikiwa kutekeleza azma ya Serikali ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme katika maeneo yao kwa kufikisha umeme katika vijiji 26 (Unguja 16 na Pemba 10) ambapo jumla ya TZS Bilioni 1.96 zimetumika.

Alisema kuwa Wizara kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati (ZURA) inaendelea kutekeleza shughuli za ujenzi wa jengo la Ofisi hapo Maisara.

Alieleza kuwa ujenzi huo umefikia asilimia 96 na jengo litakamilika na kukabidhiwa mwezi wa Machi 2020. Aidha, matayarisho ya ujenzi wa Bandari mpya ya mafuta Mangapwani yanaendelea na hatua iliyofikiwa ni kukamilika ulipaji wa fidia kwa vipando na mali za wananchi wa eneo hilo.

Sambamba na hayo, Wizara kupitia Mamlaka ya Hifadhi na Uendelezaji Mji Mkongwe imekamilisha utayarishaji wa Mpango wa Uingiaji wa Vyombo vya Moto kwa kushirikiana na taasisi nyenginezo ikiwemo Baraza  la Manispaa, Usalama Barabarani, Shirika la Bandari pamoja na wadau wengine.

Pia, alieleza kuwa Serikali inaendelea na azma yake ya kuhakikisha Zanzibar inazalisha umeme kwa kutumia nishati mbadala ya jua baada ya Serikali kuridhia uzalishaji wa nishati hiyo kwa kutumia mfumo wa Mzalishaji wa Kujitegemea ambapo bado Serikali inahusika kwa njia moja au nyengine katika aina ya uwezekezaji huo.

Kwa maelezzo yake hadi hivi sasa jumla ya wawekezaji wasiopungua 47 wameonesha nia ya kuekeza katika miradi ya Nishati ya jua ambapo miongoni mwa wawekezaji hao ni Mirambo ya Tanzania na Green Energy ya Kenya.


Nao viongozi wa Wizara hiyo walimpongeza Rais Dk. Shein kwa maelekezo yake anayoyatoa kwao hatua ambayo inawarahisishia kutenda kazi zao kwa ufanisi huku wakimuhakikishia kuwa wanaendelea kutekeleza vyema kazi zao ili kuweza kutoa huduma bora kwa wananchi wote wa Zanzibar. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.