Habari za Punde

KAMISHNA WA OPERESHENI NA MAFUNZO CP SABAS, AMEAGIZA GODBLESS LEMA (MB) ATAFUTWE NA AKAMATWE POPOTE ALIPO KWA TUHUMA ZA KUTOA TAARIFA ZA UONGO


                                   JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
                                      WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI
                                                JESHI LA POLISI TANZANIA

   



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
KAMISHNA WA OPERESHENI NA MAFUNZO CP SABAS, AMEAGIZA GODBLESS LEMA (MB) ATAFUTWE NA AKAMATWE POPOTE ALIPO KWA TUHUMA ZA KUTOA TAARIFA ZA UONGO

Ndugu Wanahabari,
Kamishna wa Operesheni na Mafunzo CP Liberatus Sabas, mapema jana amewasili mkoani Singida na kutoa ufafanuzi wa matukio ya mauaji ya watu 14 yaliotokea mkoani humo wilayani Manyoni kuanzia mwaka jana mpaka kwaka huu mwezi wa pili.

Aidha katika kutoa ufafanuzi huo Kamishna  CP Sabas alisema taarifa hizo za uongo ambazo zilisambazwa na Mbunge wa Arusha, Godbless Lema huku akimtaka kujisalimisha katika kituo chochote cha Polisi, huku akitoa maagizo kwa Kamanda Polisi Mkoa wa Singida kumtafuta Mh Lema popote alipo na akamatwe.

Kamishna CP Sabas amesema Mnamo tarehe 29/2/mwaka huu huko katika Wilaya ya Manyoni wakati wa kutoa salamu kabla ya mazishi ya marehemu Alex Jonas ambaye alikutwa ameuawa kwa kukatwa na kitu chenye ncha kali sehemu mbalimbali za mwili wake katika Eneo la Mbugani, Godbless Leama ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini alionyesha orodha ya watu 14 ambayo pia aliiweka katika mitandao ya Kijamii akidai waliuawa kwa kuchinjwa Wilayani Manyoni bila ya kuwa na uhakika kama taarifa hizo ni sahihi huku akilituhumu Jeshi la Polisi Mkoa wa Singida kushindwa kutekeleza wajibu wake.

Cp sabas ameeleza ukweli wa matukio hayo ni kama ifuiatavyo;

1.    Sichelela Mosses, (22), Mkazi wa Sayuni, tukio lililotokea tarehe 13/8/2019 majira ya usiku huko maeneo ya Mnarani barabara ya kuelekea Itigi ambapo Binti huyo alikutwa ameuawa. Baada ya uchunguzi ilibainika kuwa mauaji hayo yametekelezwa na mume wake aitwaye Rashidi s/o Hamisi akishirikiana na Timoth s/o Leonard, sababu ikiwa ni wivu wa mapenzi kwa kumtuhumu mkewe kuwa na mahusiano ya kimapenzi watu wengine. Watuhumiwa wote wawili wamekamatwa pamoja na vielelezo vyote vilitumika kwenye mauja hayo.

2.    Abdallah Lyama, (38), Mkazi wa Kihanju, Itigi, alifariki dunia tarehe 26/8/2019 saa 2 usiku wakati akiendelea na matibabu katika Hospitali ya St. Gaspar Itigi, Wilayani Manyoni kutokana na shambulio la kupigwa kwa fimbo pamoja na mateke na ngumi sehemu mbalimbali za mwili wake na Rajabu s/o Juma, Msambaa, (42) akishirikiana na Haruna s/o Hamisi, kwa pamoja walikuwa wanamtuhumu marehemu kuwa na mahusiano ya kimapenzi na mtoto wa dada yake Rajabu s/o Juma, aitwaye Asha d/o Miraji, Msambaa, (19). Tukio hilo lilitokea tarehe 25/8/2019 huko maeneo ya Mji Mpya, Itigi walipomvizia marehemu akiongea na Binti huyo kichochoroni. Mtuhumiwa Rajabu s/o Juma amekamatwa na juhudi za kumtafuta mwenzake zinaendelea.

3.    Rajabu Abasi, (36), alifariki dunia tarehe 14/9/2019 usiku akiwa anapatiwa matibabu katika Hospitali ya St. Gaspar, Itigi kutokana na tukio la kuchomwa na kitu chenye ncha kali na mtuhumiwa aitwaye Mohammed Abdi, tukio lililotokea tarehe 13/9/2019 saa 3 usiku huko katika Kijiji cha Mwamagembe. Chanzo cha tukio hilo ni wivu wa kimapenzi ambapo mtuhumiwa alimfumania marehemu akiwa na mke wake nyumbani kwa mtuhumiwa. Mtuhumiwa amekamtwa na upelelezi umekamilika.

4.    Martini Motekwa, anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 30, ambaye inasadikiwa kuwa ana upungufu wa akili na akiwa hana makazi maalum, mwili wake ulikutwa kwenye kibanda alichokuwa akijihifadhi nyakati za usiku ukiwa umechomwa moto. Katika uchunguzi mwili huo pia ulibainika kuwa na jeraha kichwani ambalo linasadikiwa kusababishwa na kitu chenye ncha kali. Bado uchunguzi wa kuwatafuta watuhumiwa unaendelea

5.    Hamad Hussein, (37), mkazi wa Manyoni alifariki dunia baada ya kushambuliwa na wananchi wanaosadikiwa kujichukulia sheria mikononi kwa kutumia fimbo na mawe kutokana na tuhuma za wizi wa mifugo. Mtuhumiwa mmoja aitwaye Hussein s/o Mrisho amefikishwa mahakamani kuhusiana na tukio hilo.

6.    Emmanuel Meso, (50), Mkazi wa Kijiji cha Maweni, Tarafa ya Kintinku, alifariki dunia kwa kukatwa na kitu chenye ncha kali sehemu za siri. Mwili wake uligundulika tarehe 8/11/2019 alifajiri ukiwa umetupwa porini. Katika uchunguzi wa Polisi imebainika kuwa watu nane wanasadikiwa kuhusika katika kutenda kosa hilo linalohusishwa na imani za kishirikiana. Aidha katika tukio hilo yupo Mganga wa Jadi anayesadikiwa kuwatuma watuhumiwa kuchukua shemu hizo za siri. Watuhumiwa wote wamekamatwa na upelelezi umekamilika, waliokamatwa ni  Abdul Muhengwa, Henry Madinda, Stephano Ligoha, Juma Kassim, Makayola Gaudence, Regina d/o Jacob, Wami s/o Ngalya, na Anderson s/o Sabini.

7.    Mika Saimon, (38), alifariki dunia kwa kukatwa na vitu vyenye ncha kali katika sehemu mbalimbali za mwili katika tukio lililotokea tarehe 15/11/2019 saa 10 jioni huko Kitongoji cha Idodoma, Tarafa ya Nkonko, ambapo marehemu aliuawa na mtoto wake aitwaye Saimon s/o Mika kwa akishirikiana na mama yake mzazi aitwaye Mea d/o Mwarabu pamoja na rafiki wa mtoto wake aitwaye Robert Elia ambapo walikuwa wanataka kurithi shamba la baba yao. Watuhumiwa wote watatu wamekamatwa na upelelezi wa Polisi umekamilika.

8.    Mshoma Ngassa, (30), Mkazi wa Itigi alifariki dunia kwa kupigwa kwa fimbo kichwani na mume wake aitwaye Mariyambelele Senzo katika tukio lililotokea tarehe 21/11/2019 saa 2:30 asubuhi huko Majiweni, Kata ya Mitundu ambapo chanzo cha kifo ni wivu wa kimapenzi ambapo mtuhumiwa akimtuhumu mke wake kutembea na mwanaume ambaye bado hajafahamika. Mtuhumiwa amekamatwa na upelelezi wa Polisi umekamilika.

9.    John Logion, (60), Mkazi wa Mitundu alifariki dunia katika tukio lililotokea tarehe 22/11/2019 saa 11 jioni kwenye shamba la mihogo, lilnalomilikiwa na Anthony Lipiti huko Itigi. Uchunguzi wa awali wa Polisi umebaini kuwa chanzo cha tukio hilo ni wizi ambapo marehemu alikwenda kwenye shamba la mtuhumiwa kwa nia ya kuiba mihogo na mtuhumiwa kutumia mwanya huo kumshambulia kwa kumpiga na kitu kizito kichwani. Mara baada ya tukio mtuhumiwa alitoroka na juhudi za kumtafuta zinaendelea kwa kushirikiana na Viongozi wa Eeneo husika.

10. Michael Charles, (35), Mkazi wa Mwamagembe alifariki 1/1/2020 wakati anapatiwa matibabu katika Zahanati ya Mwamagembe, Itigi kutokana na taarifa za kujeruhiwa na Fatuma d/o Ramadhani tukio lililotokea tarehe 21/12/2019. Katika tukio hilo inasadikiwa kuwa Fatumaa d/o Ramadhani ambaye ni Mmiliki wa nyumba aliyokuwa anaishi marehemu alimpiga kwa jiwe kichwani na kisha kumvuta sehemu za siri kutokana na ugomvi wa uchafuzi wa mazingira katika eneo la nyumba wanayoishi. Hata hivyo tukio la kujeruhiwa halikuripotiwa Polisi hadi muathirika alipofariki. Baada ya tukio la kujeruhi mtuhumiwa alotoroka juhudi za kumtafuta zinaendelea.

11. Issa Abdallah (2), ambaye alikuwa mlemavu wa miguu alifariki dunia tarehe 24/1/2020 saa 12 jioni huko katika Kitongoji cha Ibonoa, Kata ya Sanjaranda – Itigi kutokana na kunyongwa na mama yake mzazi kwa kile kinachodaiwa kukosa mahitaji kutoka kwa baba wa mtoto aitwaye Abdallah s/o Muna, (56), Mnyaturu aliyemtelekeza bila matunzo. Mtuhumiwa amekamatwa na upelelezi wa Polisi umekamilika

12. Jumanne Ndelemo, (22), alifariki dunia baada ya kukatwa na kitu chenye ncha kali na kaka yake wake aitwaye  Hamisi s/o Ndelemo, kutokana na kumfumania akiwa na mke wake. Tukio lilitokea tarehe 5/2/2020 saa 3:30 usiku huko katika Kijiji cha Makasuku, huko Sasajila na mtuhumiwa amwekamatwa na upelelezi wa Polisi umekamilika.

13. Heri Mamba alifariki dunia baada ya kugongwa na pikipiki yenye namba za usasjili MC 273 CDK aina ya FEKON. Kutokana na uchunguzi wa awali wa Polisi imebainika kuwa marehemu alikuwa amelewa huku akikatiza barabarani bila kuchukua tahadhari. Mtuhumiwa Ombeni s/o Chanzi, Mgogo, (35), mkazi wa Chinyika amekasmatwa na amekiri kutenda kosa hilo na si kuchinjwa kama ilivyodaiwa kwenye malalamiko.

14. Alex Jonas, (40), dereva bodaboda, aligundulika kufariki dunia tarehe 26/2/2020 saa 1 asubuhi na Uchunguzi unaendelea ili kuweza kubaini chanzo cha kifo cha marehemu pamoja na wahusika wa tukio hilo.

Katika Taarifa ni za upotoshaji zenye lengo la kuleta taharuki kwa Jamii pamoja na kuwachonganisha Wananchi na Jeshi lao la Oilisi.

Mwisho Kamishna Sabas amesema kuwa hakuna Mwanasiasa au mtu yoyote atakaetumia Jeshi la Polisi kama kimvuli cha kujipatia umarufu, huku akiwaonya anasiasa wanaojifanya kuwa ni wasemaji wa Jeshi la Polisi amewaonya na kusema kuwa jeshi halitamvumilia mtu au kiongozi yoyote atakaeichafua serikali kwa namna moja au nyingine.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.