Habari za Punde

BODIYA UTALII YATAJA MIKAKATI ENDELEVU 10 KUINUA UTALII KATIKA MLIPUKO WA CORONA

Mwenyekiti wa Bodi ya Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Jaji Mstaafu Thomas Mihayo akizungumza na Waandishi wa Habari katika  Mkutano wa  Bodi uliofanyika Jijini Dar es Salaam
Wajumbe wa Bodi wakifuatilia Mkutano wa Waandishi wa Habari na Mwenyekiti wa Bodi ya Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Jaji Mstaafu Thomas uliofanyika Jijini Dar es Salaam
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Utalii (TTB), Bi. Devotha Mdachi akifafanua jambo kwa waandishi wa habari wakati wa Mkutano wa Waandishi wa Habari na Mwenyekiti wa Bodi ya Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Jaji Mstaafu Thomas uliofanyika Jijini Dar es Salaam Aprili, 29, 2020, ukihusisha Bodi ya Taasisi hiyo.
 Picha na Idara ya Habari-MAELEZO.

Na Mwandishi Wetu, MAELEZO DAR ES SALAAM 29.4.2020
BODI ya Utalii Tanzania (TTB) imeainisha mikakati 10 ya muda mrefu inayolenga kuinua soko la utalii nchini ambalo kwa sasa limeathirika na mlipuko wa ugonjwa wa homa kali ya mapafu (CORONA) unaosababishwa na kirusi cha (COVID-19) na kuenea katika nchi mbalimbali duniani.

Hayo yamesemwa leo Jumatano (Aprili 29, 2020) Jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Bodi ya (TTB) Jaji Mstaafu Thomas Mihayo wakati wa mkutano na Waandishi wa vyombo vya habari kuelezea athari za mlipuko ugonjwa wa CORONA na tathimini ya sekta ya Utalii nchini.

Alisema kuwa kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Shirika la Utalii Duniani (UNWTO), inaonesha kuwa mlipuko wa ugonjwa wa CORONA utasababisha kushuka kwa kiwango cha kati ya asilimia 20-30 ya idadi ya watalii kwa mwaka 2020 pamoja na kusababisha ukosefu wa mapato kiasi cha Dola za Marekani 300-450 Bilioni duniani.

Akifafanua zaidi Jaji Mihayo alisema pia utabiri wa awali uliofanywa na Shirika lisilo la kiserikali linaloshauri nchi na taasisi za kimataifa la DEFC unaonesha kuwa mwenendo wa uchumi duniani umebadilika na utaendelea kubadilika ambapo sekta za utalii na usafiri wa anga ziilizokuwa zimeshamiri, kwa sasa zitakuwa za mwisho kwenye uchangiaji wa ukuaji wa uchumi duniani.

‘’Sekta ya Utalii nchini Tanzania inachangia takribani asilimia 17-17.5 ya mapato ya Serikali (GDP) ambapo kwa mwaka 2018 Tanzania ilitembelewa na watalii wapatao 1,505,702 kutoka watalii 1,327,143 wa mwaka 2017, hivyo  janga la virusi vya CORONA limeleta athari kwenye soko la utalii duniani na hapa nchini pia kwenye sekta zinazowezesha sekta ya utalii’’ alisema Jaji Mihayo.

Aidha Jaji Mihayo aliitaja mikakati endelevu iliyowekwa na TTB katika kuendeleza na kukuza sekta ya utalii nchini ni pamoja na kushirikiana na wadau wa utalii kuandaa mkakati wa pamoja wa kukabiliana na janga la COVID-19 kwenye sekta ya utalii, kuandaa mkakati mpya wa mauzo wa kimataifa kupitia ufadhili wa Shirika la Misaada la Marekani (USAID) na kushirikisha watu mashuhuri na mabalozi wa utalii Tanzania kwa ajili ya kutangaza utalii.

Aliitaja mikakati mingine ni pamoja na kuimarisha timu ya mauzo kubuni mbinu za kisasa na kitaalamu zenye ubunifu wa kuandaa mikakati ya mauzo ya  mtandao, kutangaza utalii wa ndani kupitia programu maalum za mashule na vyuo vya elimu pamoja na kushirikiana na Balozi za Tanzania nje ya nchi kuweka mikakati bayana ya kuwapata mabalozi wa TTB.

Kwa mujibu wa Jaji Mihajo alisema mara baada ya kutokea kwa mlipuko wa ugonjwa wa CORONA, TTB ilianza kuchukua tahadhari mbalimbali ikiwemo kuandaa na kurusha makala fupi ya dakika 1.5 iliyosambaa duniani kuhamasisha watalii kujikinga na COVID-19 na kuwakumbusha wasifute safari zao za utalii nchini Tanzania.

‘’Makala hiyo fupi imezunguka kwenye masoko yetu yote makubwa duniani na imevuka matarajio ya awali ya kiwango cha watu waliyoiona na pia makala hiyo imeoneshwa kwenye vituo vyetu vya Televisheni na kuwekewa lugha za kiarabu, kifaransa, kijerumani na kidachi’’ alisema Jaji Mihayo.

Jaji Mihayo alisema TTB, Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Mamlaka ya Uhifadhi Ngorongoro (NCAA) wameingia ubia na kampuni ya Great Migration Camp kwa pamoja wamebuni kipindi maalum kinachoitwa ‘’Serengeti Live Show’’, kinachorushwa mubashara na vingine kurekodiwa na kurushwa kwa awamu kwenye mitandao ya TTB na washirika wake nchini na nje ya nchi kuonesha utalii wa Tanzania.

Aliongeza kuwa madhumuni ya vipindi hivyo ni kukonga mioyo ya watalii ambao wameahirisha safari zao za kuja Tanzania kwa kipindi hiki cha mlipuko wa ugonjwa wa CORONA, ambapo kupitia vipindi hivyo Tanzania itahakikisha kuwa Jina maalum la kutangaza utalii wa Tanzania la Tanzania Unforgettable linaendelea kutumia ili kuhamasisha sekta ya utalii nchini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TTB, Devotha Mdhachi alisema mwezi Mei mwaka huu Ofisi yake inatarajia kufanya kikao na wadau wa sekta ya utalii nchini ili kujadili mikakati ya pamoja inayolenga kuimarisha soko la utalii nchini katika kipindi hiki ambacho dunia inakabiriwa na mlipuko wa ugonjwa wa CORONA.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.