HOTUBA YA MAKAMU WA PILI WA RAIS
WA ZANZIBAR ALIYOITOA
WAKATI AKIFUNGA MKUTANO WA 18 WA
BARAZA LA TISA LA WAWAKILISHI TAREHE 17 APRIL, 2020
Nianze
kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu mwingi wa Rehma kwa kutujaalia uhai,
akatupa na afya njema akatuwezesha kufanikisha Mkutano huu wa Kumi na nane wa
Baraza la Tisa ulioanza tarehe 01 April, 2020 hadi leo tarehe 17 April, 2020
tunapouakhirisha, baada ya shughuli zote zilizopangwa kukamilika.
Mheshimiwa
Spika,
Katika Mkutano huu, Baraza
lako Tukufu limepokea na limejadili Miswada 8 pamoja na Ripoti zipatazo 16
kutoka Wizara zetu. Miswada
iliyowasilishwa ni kama ifuatavyo:-
1.
Mswada wa Sheria ya Kufuta Sheria ya
mambo ya Rais Namba 5 ya mwaka 1993 na kutunga Sheria ya mambo ya kuweka
masharti bora zaidi kuhusiana na mambo mengine yanayohusiana na hayo.
2.
Mswada wa Sheria ya Kuanzisha Sheria ya
masuala ya Diaspora na mambo mengine yanayohusiana na hayo.
3.
Mswada wa Sheria ya kufuta na kuandikwa
upya Sheria ya vileo na kuweka Masharti ya kuzuia, kudhibiti na kusimamia
Uagizaji, kuhifadhi kwenye maghala, uuzaji, usambazaji na unywaji, vileo na
mambo mengine yanayohusiana na hayo.
4.
Mswada wa Sheria wa vipimo Nam. 4 ya
mwaka 1983 na kuanzisha Sheria ya Wakala wa viwango na mambo mengine yanayohusiana
na hayo.
5.
Mswada wa Sheria ya kuanzisha Taasisi ya
Utafiti wa Mifugo Zanzibar na mambo Mengine yanayohusiana na hayo.
6.
Mswada wa Sheria ya kufuta Sheria ya
Taasisi ya utafiti wa Kilimo Nam. 8 ya 2012 na kutunga Sheria ya Taasisi ya
utafiti wa Kilimo Zanzibar na mambo mengine yanayohusiana na hayo.
7.
Mswada wa Sheria wa Usajili na Usimamizi
wa Wataalamu wa maabara za Tiba na mambo mengine yanayohusiana na hayo, na
8.
Mswada wa Sheria ya kuanzisha Taasisi ya
utafiti wa Afya Zanzibar na mambo mengine yanayohusiana na hayo.
Mheshimiwa
Spika,
Baraza lako Tukufu
lilipata muda wa kutosha kuijadili Miswada yote hii minanekwa kina na
kuipitisha. Nawapongeza Wajumbe wote
waliopata nafasi ya kutoa michango yao ambayo bila shaka ilihitajika ili
kuiimarisha Miswada hiyo. Naamini
michango iliyotolewa na Wajumbe wa Baraza lako Tukufu imejitosheleza na hakuna
haja kwa upande wangu kuitolea maelezo mengine.
Mheshimiwa
Spika,
Baraza lako Tukufu pia
limepokea, limejadili na limepitisha Ripoti za Wizara za Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar, juu ya Utekelezaji wa maagizo ya Kamati za Kudumu za Baraza kwa
mwaka 2019/2020. Sina budi kuzipongeza
Kamati zote kwa utekelezaji makini wa majukumu yao. Napenda kuwashukuru Mawaziri wote kwa
uwasilishaji wa taarifa hizo; na pia Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako Tukufu
kwa michango yao ambayo itaendelea kuisadia Serikali katika utekelezaji wa
majukumu yake.
Mheshimiwa
Spika,
Kama tunavyojua Dunia
hivi sasa imekumbwa na janga kubwa la maradhi ya Corona yanayosababishwa na
kirusi kiitwacho COVID-19. Maradhi haya tayari yamesababisha na yanaendelea
kusababisha vifo vya watu wengi duniani kote.
Kwa hivi sasa Bara la Uropa, Asia na Marekani yameshapoteza watu
wengi. Duniani kote zaidi ya watu
milioni moja tayari wameshaambukizwa na Corona na zaidi ya watu 100,000
wameshapoteza maisha yao. Kwa mujibu wa Gazeti
la East Afrika la tarehe 5 mwezi huu, wanasayansi kutoka London School of
Hygiene and Tropical Medicine wanakadiria kuwa kwa kila nchi ya Afrika
Mashariki ikiwemo Tanzania watu wapatao 10,000 watakuwa wameambukizwa na
ugonjwa wa Corona ifikapo mwezi wa Mei.
Idadi hii itashuka endapo nchi zenyewe zitakuwa zimechukua tahadhari
kubwa ikiwemo watu kutokusanyika na kutokuchanganyika ovyo na kufuata masharti
ya wataalamu wa Afya. Ugonjwa huu hadi
sasa hauna dawa wala chanjo. Aidha,
uwezekano wa kupata chanjo ya kujikinga na maradhi haya hivi karibuni
haupo. Wataalamu wa afya wanasema kuwa
inaweza kuchukuwa zaidi ya miezi 6 kupatikana kwa chanjo ya Corona.
Mheshimiwa
Spika,
Maradhi ya Corona
hayana dawa lakini ikiwa tutafuata miongozo na maelekezo ya Viongozi na
Wataalamu wa Afya ikiwemo Shirika la Afya Duniani (WHO), tunaweza kabisa
kuutokomeza ugonjwa huu nje ya visiwa vyetu na nje ya Tanzania kwa jumla. Kwa mujibu wa miongozo ya viongozi wetu na
wataalamu wa Afya, ugonjwa wa Corona dawa yake kubwa ni kujikinga nao usikupate
kwa kufuata mambo yafuatayo:-
-
Kuosha mikono kwa sabuni na maji ya
kutiririka angalau sekunde 20;
-
Kuacha tabia ya kujigusa macho, pua na
mdomo kwa mikono ambayo haijaoshwa;
-
Kuvaa barkoa na kuweka Sanitizer;
-
Kuepuka mikusanyiko;
-
Kuepuka kuchanganyika na mgonjwa; kujitenga
na watu wengine hasa pale Corona ikiwa imeshaingia nchini kama hivi sasa hapa
kwetu. Kwa mujibu wa taarifa
zilizotolewa na wataalamu wetu wa afya maradhi haya siyo tena yanatoka nje ila
tunaambukizana wenyewe kwa wenyewe.
-
Kaa nyumbani (Stay at Home) kama huna
sababu maalum ya kutoka nje.
Mheshimiwa
Spika,
Napenda kuwajulisha
wananchi wenzangu kuwa hivi sasa tuko katika vita dhidi ya Corona; tunapambana
na adui ambaye haonekani, hachagui rangi, umri, jinsia, Taifa wala hadhi ya
mtu. Adui huyu anachojua ni kushambulia
tu mtu yeyote bila ya huruma. Ukipambana na adui wa aina hii ambaye haonekani;
anayeshambulia kila mtu, unatakiwa kuwa makini na kuchukua tahadhari kubwa
vyenginevyo utajishtukia umeshakuwa mateka.
Nchi ikishawekwa mateka na adui huyu shuhudia vifo vya watu wengi. Zipo nchi hivi sasa zinapoteza watu wapatao
800 hadi 1,000 kwa muda wa masaa 24.
Nchi hizi zina vifaa vya kisasa, wataalamu wa tiba waliobobea lakini zimezidiwa. Naomba tutafakari hali hii ili tupate kuelewa
ukubwa wa adui tunayepambana nae.
Mheshimiwa
Spika,
Hapa kwetu Serikali
zetu zote mbili zimechukuwa hatua za tahadhari mara tu ugonjwa huu ulipoanza
kuripotiwa nchini China mwezi wa Disemba, 2019 ili kuwakinga wananchi wake
wasiambukizwe. Viongozi wetu Wakuu Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli na Rais wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein,
wamechukuwa hatua mbali mbali za kupambana na ugonjwa wa Corona ikiwemo kuzuia
ndege kutua nchini kutoka nchi ambazo zimekumbwa na ugonjwa huu; kuanzisha
utaratibu wa kuweka watu kwenye karantini; kufunga Maskuli, Madrasa na Vyuo
mbali mbali, kuzuwia mikusanyiko isiyokuwa ya lazima. Vile vile, Serikali yetu ilizuia kufanyika
kwa Ijitimai ya Kimataifa, Mkutano wa Kimataifa wa Wawekezaji na Kongamano
kubwa la Kilimo. Hatua zote hizi
zilikuwa na lengo moja tu nalo ni kuwakinga wananchi wetu na maambukizi ya
maradhi ya Corona.
Aidha, Rais wetu wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, ametoa maagizo kujengwa maabara
ya kisasa ndani ya miezi mitatu katika eneo la Binguni ili kuchunguza na
kutafiti maradhi mbali mbali ikiwemo Corona.
Napenda kuchukua fursa
hii kuwapongeza kwa dhati Viongozi wetu hawa kwa juhudi zao za dhati
walizozichukua za kujikinga nchi yetu na janga la mripuko wa maradhi ya
Corona. Hatuna budi kuthamini juhudi zao
kwa kufuata malekezo yao na yale yanayotolewa mara kwa mara na wataalamu wetu
wa afya.
Mheshimiwa
Spika,
Tahadhari mbali mbali
za kujikinga na ugonjwa wa Corona zilizotangazwa kwa wananchi na Serikali yetu
zitafanikiwa tu ikiwa sote kwa umoja wetu bila kujali cheo, kabila wala wasifu
wa mtu tutazizingatia na kuzifuata bila ya muhali. Tahadhari hizi ni kwa wananchi wote kutoka
ngazi zote na wala hatutoruhusu majadiliano.
Kwa Lugha nyengine, ‘hakuna mbora
ambaye atakuwa juu ya tahadhari hii tulizojiwekea za kujikinga na maradhi haya
thakili’. Mtu yeyote atakayethubutu
kuzivunja tahadhari za kujikinga na maradi ya Corona atachukuliwa hatua kali
bila ya kumuangalia usoni. Napenda
kuwashukuru Mawaziri wetu wa Afya wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Ummy
Mwalimu na Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Hamadi
Rashid kwa kutupa taarifa za kila siku za hali ya ugonjwa inavyoendelea.
Mheshimiwa
Spika,
Nyote ni mashahidi kuwa
mara tu baada ya kutoka safarini nchini Cuba nilikuwa kwenye karantini na
ujumbe wangu wote kwa mujibu wa sheria zetu tulizoziweka. Nimetumikia kipindi cha zaidi ya siku 14 kwa
mujibu wa maelekezo ya wataalamu wa afya.
Nikaongeza na siku nyengine saba ili kujiridhisha kuwa tuko salama. Nawashukuru Wataalamu wa Afya waliokuwa
wakija kututembelea kila mara ili kujua tunavyoendelea. Hakuna anayependa kukaa karantini lakini ni
sheria na hakuna mtu ambaye yuko juu ya sheria.
Kama nilivyowahi kusema kukaa karantini si adhabu bali ni kitendo cha
kiungwana cha kujihakikishia usalama wako na waliokuzunguka, hasa kwa vile
maradhi haya ya Corona tayari yameshaingia nchini mwetu.
Nachukuwa nafasi hii
kuwataka Viongozi wa ngazi zote tushirikiane na wananchi katika kuzisimamia
taratibu tulizoziweka za kupambana na maradhi ya Corona. Afya
yetu ndio rasilimali yetu, Kinga ni Bora kuliko Tiba. Tuache ukaidi na
dharau wa kufuata maelekezo ya Viongozi wetu na wataalamu wetu wa afya. Sisi Wazanzibar tunasemwa sana kwa ukaidi na
dharau, lakini Wahenga wamesema mkaidi hafaidi mpaka siku ya Iddi, si hivyo
tutadhurika sisi wenyewe na familia zetu na jamii inayotuzunguka kwa ukaidi na
dharau zetu. Mheshimiwa Rais wetu Dk.
Ali Mohamed Shein ameteua viongozi mbali mbali kuanzia ngazi ya Shehia mpaka
Serikali Kuu kwa nia ya kumsaidia kazi, hivyo ni wajibu wetu kila mmoja wetu
katika eneo lake atimize wajibu wake kulisimamia suala la Corona.
Mheshimiwa
Spika,
Katika hotuba yangu ya
kuakhirisha Mkutano wa Kumi na Tano wa Baraza la Tisa nilieleza maamuzi ya
Serikali zetu mbili kuendeleza Mradi wa Kunusuru Kaya Maskini TASAF ambao bila
shaka ni mkombozi wa wanyonge.
Kwa furaha kubwa,
nachukua nafasi hii kuwaeleza Waheshimiwa Wajumbe na wananchi wote kwamba kama
mlivyoona na kusikia kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii tarehe 17
Februari, 2020 Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John
Pombe Magufuli amezindua rasmi Awamu ya Pili ya Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini
(TASAF III-II) unaotegemewa kutekelezwa kwa miaka minne.
Kufuatia uzinduzi huo
Serikali zetu zote mbili zimeanza hatua mbali mbali za matayarisho ya kitaalamu
ya utekelezaji wa awamu hiyo.
Utekelezaji huo unategemea kuvifikia vijiji vyote kwa Tanzania Bara na
Shehia zote kwa Tanzania Zanzibar.
Aidha, kwa upande wa Zanzibar jumla ya Shilingi Bilioni 21.5 zitatumika
kwa mwaka.
Mheshimiwa
Spika,
Nachukua nafasi hii kwa
mara nyengine tena kuwataka viongozi na wananchi kuendelea kushirikiana katika
utekelezaji wa awamu hii ya pili. Hatuna
budi kushiriki kikamilifu katika hatua zote za mradi kuanzia ukusanyaji wa
taarifa za walengwa katika ngazi za Shehia ili kuweza kupata takwimu sahihi
ambazo ndio kiini cha upatikanaji wa mlengwa aliyetimiza vigezo na masharti ya
mpango.
Nawaomba watendaji na
wahusika wote kufanya kazi kwa uadilifu, juhudi na uaminifu ili kuendeleza sifa
nzuri ambayo Zanzibar na Tanzania kwa ujumla imejipatia katika utekelezaji wa
Mradi huu wa TASAF iliyopelekea watu kutoka Mataifa mbali mbali kuja kujifunza
namna tunavyotekeleza Miradi ya TASAF Zanzibar.
Mheshimiwa
Spika,
Tupo katika kipindi cha
Masika na tayari mvua zimeshaanza nchini kote. Nawakumbusha wananchi umuhimu wa
kuzitumia vizuri mvua hizi kwa shughuli za kimaendeleo zikiwemo kilimo cha
mazao ya chakula na miti ya kudumu. Ni
wakati mzuri wa kupanda miche ya mikarafuu na minazi ambayo inatolewa bure na
Serikali. Aidha, nawataka wananchi
kuendelea kuchukua tahadhari za kujiepusha na maafa kwa kuhama katika maeneo
hatarishi, kufuatilia mienendo ya watoto wetu hasa kwa vile shule zimefungwa
kutokana na tatizo la Corona, kufuatana maelekezo ya wataalamu wa Mazingira,
wataalamu wa Afya na kuendelea kufuatilia taarifa za kitaalamu na elimu
zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa kanda ya Zanzibar.
Mheshimiwa
Spika,
Napenda kuwaasa
wananchi wote kuchukua tahadhari za kudumisha usafi ili kujikinga na maradhi ya
mripuko kama kipindupindu na maradhi ya matumbo. Mbali na juhudi za Serikali za kuondosha
maradhi hayo, wananchi kwa upande wao wana nafasi ya kujilinda kwa kudumisha
usafi hasa kipindi hiki cha mvua za masika.
Mheshimiwa
Spika,
Juhudi za Serikali za
uondoshaji wa maji ya mvua katika mitaa yetu zinaonekana na tayari misingi ya
Chumbuni, Jang’ombe, Mwanakwerekwe – Sebleni - Mikunguni hadi Mpiga Duri imekamilika. Ujenzi wa misingi hii umeigharimu Serikali
yetu fedha nyingi. Natoa wito kwa
wananchi kushirikiana na Serikali katika kuitunza ili iendelee kutumika kwa
madhumuni yaliyokusudiwa kwa muda mrefu.
Serikali haitamvumilia mwananchi ye yote atakaye unganisha misingi hii
na bomba lake la maji machafu kutoka nyumbani kwake. Hili ni kosa na lazima lichukuliwe hatua za
kisheria. Tuache tabia ya kuijaza taka
misingi hii ili isifanye kazi iliyokusudiwa ya kupitisha maji.
Mheshimiwa
Spika,
Katika kipindi hiki cha
mapambano dhidi ya Corona hatutakiwi kukaa pamoja kwa kipindi kirefu. Kwa hivyo, napenda kumalizia hotuba yangu kwa
kukushukuru wewe Mheshimiwa Spika pamoja na Naibu wako na Wenyeviti wote wa
Baraza kwa kuviendesha vyema vikao vyetu kwa hekima na busara. Nawashukuru pia Waheshimiwa Wawakilishi kwa
kutumia nafasi yao ya Kidemokrasia ya kuisimamia, kuishauri na kuihoji
Serikali, jambo ambalo limeonesha nia thabiti mliyokuwa nayo ya kuitaka
Serikali kuwajibika ipasavyo kwa wananchi wake.
Kadhalika, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Mawaziri
kwa kujibu maswali walioulizwa kwa ufasaha.
Namshukuru pia Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ufafanuzi
wake alioutoa katika mambo mbali mbali yaliyohitaji ufafanuzi wa kisheria, na hasa
wakati wa kujadili na kupitisha Miswaada mbali mbali. Pia namshukuru Katibu wa Baraza na Watendaji
wenzake wakiwemo wakalimali wa lugha ya alama, waandishi wa habari kwa kazi
nzuri wanayoifanya.
Mwisho, nawaomba
Wawakilishi wenzangu waendelee kuwaelimisha wananchi wetu kuhusu suala hili la
Ugonjwa wa Corona, sisi tunatakiwa tuwe mfano wa kuigwa ukiachia madaktari
wetu, sisi ndio tuwe askari wa mstari wa mbele katika kupambana na vita vya
maradhi ya Corona.
Kabla sijamaliza hotuba
yangu, napenda kuwapongeza watumishi wote wa Wizara ya Afya wa Unguja, Pemba na
Tanzania Bara ambao wanajitolea kupambana kwa hali na mali ili kuokoa maisha ya
wananchi wote. Watumishi wa Afya ndio
askari wetu, lazima tuwasaidie vita hivi kwa kufuata maelekezo yao ya kujikinga
na maradhi haya hatari ya Corona.
Tukifuata maelekezo yao idadi ya wagonjwa nchini itakuwa ndogo. Serikali kwa upande wake itahakikisha
inawapatia vifaa vinavyotakiwa vya kujikinga na maradhi ya Corona ili wafanye
kazi zao bila ya kuambukizwa. Nawashukuru
wote kwa uzalendo wao wanaouonyesha, Mwenyezi Mungu atawalipa kwa kujitolea
muhanga kuokoa maisha ya Watanzania.
Aidha, napenda
kuwashukuru kwa dhati wale wananchi wote
waliojitokeza kutoa misaada yao ya vifaa mbali mbali vya kinga kuisaidia
Serikali yetu katika mapambano haya dhidi ya ugonjwa huu hatari. Mwenyezi Mungu atawajazia maradufu pale
walipotoa.
Mwisho kabisa,
nawashukuru wananchi wote wa Zanzibar kwa kuitikia wito wa Serikali wa
kupambana na maradhi ya Corona kwa njia ya kufuata tahadhari zilizowekwa. Nawaomba tuzidi kushirikiana ili tushinde
vita hivi. Ni wakati huu ambapo sisi
Wazanzibari na Watanzania kwa jumla tunahitaji kuwa wamoja na kushikamana kuliko
wakati wote ule.
Mheshimiwa
Spika,
Baada ya maelezo hayo
sasa, kwa heshima na taadhima naomba kutoa hoja kwamba Baraza lako Tukufu
liahirishwe hadi siku ya Jumatano tarehe 6 Mei, 2020 saa 3.00 barabara za
asubuhi panapo majaaliwa.
Mheshimiwa
Spika, Naomba kutoa Hoja.
No comments:
Post a Comment