Habari za Punde

Kamati ya BLW Yaitaka SMZ Kujipanga Kukabiliana za Athari za Mripuko wa Corona Kiuchumi


Na Himid Choko, BLW

KAMATI ya  Bajeti ya Baraza la Wawakilishi  imeishauri Serikali kutengeneza mpango madhubuti wa  kukabiliana na athari za kiuchumi zinazosababishwa na kuenea kwa virusi vya CORONA.
Akichangia Ripoti ya Utekelezaji wa Maagizo ya Kamati  ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi ya Mwaka 2019/2020  kwa Wizara ya Fedha  na Mipango, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Dkt. Mohammed Said Dimwa  amesema  janga la maradhi ya COVID 19 lililoikumba Dunia hivi sasa ikiwemo Zanzibar  linaleta  tishio kubwa la kiuchumi.
Amesema uchumi wa dunia upo katika hatari ya kuporomoka kutokana na Serikali za nchi mbali mbali kupiga marufuku mikusanyiko, kuzuia wageni kuingia, na hata  wananchi wake kutoka majumbani mwao ili kujaribu kudhibiti kuenea kwa maambukizi ya virusi vya CORONA.
Hivyo amesema Kamati yake  inashauri Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar  ishirikiane na SMT kupitia Kamati ya Kitaifa ya Mawaziri ili kuweka mikakati ya kitaifa ya pamoja ya kukabilina na janga hili la ugonjwa katika kuenea kwa maambukizi na pia kunusuru uchumi  wa taifa.
Aidha Kamati hiyo ya Bajeti  wameiomba SMZ ishirikiane na SMT kutafuta usaidizi wa kiuchumi kwa taasisi za kimataifa kama vile Benki ya Dunia (WB) na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) kwani taasisi hizi  huweka bajeti kwa ajili ya kukabiliana na changamoto za kiuchumi kwa nchi wanachama.
Kamati hiyo pia, imeishauri Serikali kuomba kupewa tahfifu ya madeni yake (debt relief) kwa kuondolewa au kupunguzwa riba katika kipindi hichi ambacho nchi yetu inapambana na kuenea kwa maambukizi ya virusi hivi hatari.
Nae Mwakilishi wa Jimbo la Uzini Mheshimiwa Mohammed Raza Dharamsy  ameishauri Wizara ya Fedha na Mipango  kuhakikisha bidhaa na mahitaji muhimu ya mwanadamu hasa chakula vinapatikana kwa wingi kipindi hiki pamoja na kudhibiti njia zisizorasmi za kuingiza bidhaa na mfumko wa bei.
Akitoa ufafanuzi wa Hoja za Wajumbe waliochangia hoja hiyo, Waziri wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Balozi Mohammed Ramia amesema Serikali ya SMZ na SMT kwa sasa wanalishughulikia Suala la CORONA  kitaifa na kwa pamoja na wanaendelea kushirikiana vizuri.
Amesema kwa sasa Serikali imeelekeza kuliangalia suala la ugonjwa huu kiafya zaidi na baadae watakaa kwa pamoja kulitafakari suala hili na athari zake kiuchumi.
Haina maana hivi sasa hatujui kama kuna huu ugonjwa, tunajua vizuri lakini tukifanya hivi sasa matokeo yatakuwa madogo zaidi halafu tutakuja pata tabu ya kurekebisha wakati huo…………… Sasa wakati tunakwenda hivi sijui tutafanya tathmini gani yakua leo sita, kesho nane na kesho kutwa Kumi. Mheshimiwa Mungu atusaidie.” Alisema Waziri wa Fedha na Mipango.

Mwisho
Himid Choko, BLW
Alhamis, April 16, 2020

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.