WAJASIRIAMALI kutoka
maeneo mbali mbali kisiwani Pemba, wakiwa kwenye mafunzo maalum ya utengenezaji
wa mikoba ya ukindu inayotumia vitambaa na kisha kushonwa kwa cherehani,
mafunzo hayo yaliyofayika mwaka 2017 Kiuyu wilaya ya Wete na kuendeshwa na
TAMWA, (Picha na Haji Nassor).
Na. HAJI NASSOR, PEMBA
TOKEA mwezi Disemba mwaka jana,
nchini China kulitangaazwa kuibuka kwa ugonjwa wa COVID 19, unaosababishwa na
virusi vya Corona.
Awali waliyowengi,
walidhani ugonjwa huo ni kama yale magonjwa mengine ya mafua ya ndege, pengine
na hata ebola ambayo huwa na kawaida ya kubakia katika nchi chache.
Ugonjwa huu,
ulianza kuingia barani Afrika kwenye nchi ya Misri mwezi Machi, na kisha
kusambaa kwa kasi kwenye nchi za Afrika Mashariki Tanzania, Uganda na Kenye
zikihusika.
Wataalamu
wanasema, ugonjwa huo ni wa aina ya pekee, katika kusambaa kwake, maana kwa
mfano UKIMWI ulihitaji nji kubwa mfano kubadilishana damu, tendo la kuingiliana
na mengine ndipo usambae.
Kwenye COVID
19, inasambaa kwa njia nyepesi mno, mfano mwenye ugonjwa hata chafya yake,
mafua, machozi, mate achia mbali damu au kulala nae.
Ndio maana
kila mmoja, hata baada ya kuingia kwa ugonjwa huo nchini Tanzania na hadi
kufikia Mei 7, kuwa na wagonjwa 509, kati ya hao Zanzibar ikiripoti 134,
alikuwa mwoga mara mbili.
Hapo tena
matamko ya viongozi wakishirikiana na watalamu wa afya, yalianza kuwataka
wafanyabiashara na wajasiriamali kama sio kufunga biashara zao kabisa, basi
wachukue kila aina ya tahadhari.
ATHARI YA CORONA KWA WAJASIRIAMALI
WANAWAKE
Kisiwa cha
Pemba kama kilivyo cha Unguja, kila penye wajasiriamali 10, basi nane kati yao
wamewezeshwa au kuoneshwa njia na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake
Tanzania ‘TAMWA’ ofisi ya Zanzibar.
Katibu wa
ushirika wa ‘Tupate sote wa Mavungwa shehia ya Mbuzini Wilaya ya Chake Chake
Meiye Hamad Juma, anasema kwao Corona imeathiri sana shughuli zao.
Kabla ya
ujio wa janga hilo, walikuwa wakiiuza bidhaa zao na kujipatia wastani wa
shilingi 250,000 hadi shilingi 300,000 kwa mwezi, kwa vile walikuwa na uhuru wa
kuzitembeza watakavyo.
Bidhaa zao
kama za mikoba ya kisasa ya ukili, inyoshonwa kwa cherehani, mafuta ya mti wa Mkaratusi,
jiki na sabuni ya maji walikuwa wakiwafuta wateja hadi majumbani mwao.
“Wateja wetu
ni wale wa nyumba kwa nyumba au mlango kwa mlango, ndio maana hapo ikifika
mwezi tukifanya hesabu tunajikuta mpaka na shilingi 300,000 lakini sasa Corona
imetupiga karantini ya kiuchumi,’’anasema.
Athari kubwa
ya Corona ndani ya kikundi hichi cha wanawake, Katibu anasema ni kushuka kwa
mauzo, hadi kujipatia shilingi 75,000 na zisizozidi shilingi 80,000 kwa mwezi.
Kwa hesabu za
darasa la saba, utagundua kila mwezi wanawake hawa sasa wanapoteza kati ya
shilingi 220,000 hadi shilingi 225,000 kutokana na kukosa kutembeza bidhaa zao.
Anasema
Corona ikiendelea kung’ang’ania Tanzania, safari ya kurejea kwenye umaskini,
ambao walishauwaga kwa miaka zaidi ya 10 sasa, itanukia.
Fatma Abdi wa
kikundi cha Nyota njema cha kijiji cha Kiungoni wilaya ya Wete, anasema kabla
ya Corona kwa mwaka 2019 pekee, walijipatia shilingi 1, 450,000 baada ya kuuza mikoba
45, sabuni ya maji dumu sita zenye ujazo wa lita tano tano, sabuni za miche 60
na vipochi 20 vya kisasa.
Anasema
Corona kwa vile wataalamu wa afya wanataka kujiepusha na mikusanyiko, ambayo ndio
waliyokuwa wakiitumia kutangaaza na kuuza bidhaa zao, sasa mambo ni magumu.
“Unajua sisi
tukisikia pahala panamikusanyiko tushafika na bidhaa zetu, maana ndio
tulivyofahamishwa na wawezeshaji kutoka TAMWA, lakini sasa Corona imeingilia
kati,’’anafafanua.
Kwa sasa
baada ya kukosa kutembeza bidhaa zo kutokana na uwepo wa Corona, wanazo bidhaa
za shilingi 279,500 ambazo zimo ndani zikisubiri wateja.
Miongoni mwa
bidhaa ambazo zimejiweka karantini kutokana na kuingia woga wa kuzitembeza kama
zamani, ni pamoja na sabuni ya maji dumu tatu zinazojumuisha lita 15, dawa maalum
ya kutolea madoa ‘Jik.
Lakini
athari hii ya Corona ambayo pia kwa Tanzania imeshasababisha vifo 16 hadi
Aprili 30 mwaka huu, imewakumba hata wajasiriamali wanawake mmoja mmoja,
akiwemo Nassr Salum Mohamed.
Anasema
katika eneo analoishi la Minungwini wilaya ya Wete, alikuwa na kawaida ya
kutembeza bidhaa vile karafuu mchanganyiko kwa ajili ya kutolea nongo za mwili
‘singo’.
Lakini
amekuwa akisambaaza kwa wateja wake pia bidhaa kama majani ya chai ya tiba,
mikoba ya kisasa ya ukili ambapo fursa hiyo ilikuwa ikimtanulia soko lake.
Kabla ya
Corona, alikuwa akipita kwenye vijiji vya Mchanga mdogo, Minungwini, Kwa
bikirembo, Kigongoni, Kojani, Kangangani na Ole ili kuwafuata wateja wake.
Hilo
analazimika kulifanya kutokana na uwepo wa wajasiriamali wengi zaidi sasa
kisiwani Pemba, na kama engeamua kuwasubiri, engechelewa kufikia lengo.
“Mimi hakuna
kijiji ambacho kwa wilaya ya Wete na Micheweni sijafika kuwafuta wateja tena
kwa mguu, na huingia kila nyumba kwanza kuwasomesha na kisha kuwauzia, na
narejea kwangu magharibi,’’anasema.
Anasema
ujasiriamali mzuri, lazima uwe na sifa ya kuitangaaza bidhaa na kisha kuwafuata
wateja walipo, ili kuwapunguzia usumbufu wa kukufuata ulipo.
Kazi hiyo za
kuviandama vijiji kimoja baada ya chengine, alikwisha izoea na alikuwa
akijipatia wastani wa shilingi 120,000 hadi shilingi 130,000 kwa mwezi
hutegemeana na msimu.
“’aaa…!!!... katika mjasiriamali mwanamke
aliyeathiriwa na Corona kiuchumi kwa hapa Tanzania basi ni mimi, maana sasa hakuna
tena mpango wa kuwafuata wateja majumbani, ukipiga hodi waangaliwa kwa
dirishani,’’anasema.
Anaeleza
kuwa, tokea kuanza kwa karantini ya kuacha mikusanyiko isiyo ya lazima kwa hofu
ya Corona, sasa biashara zake zinaelekea kupoteza mwelekeo.
“Sasa mimi
tokea kuanza kwa Corona kwa mwezi mapato yangu yameshuka kutoka shilingi
130,000 za kabla na sasa nauza shilingi 70,000 tu,’’anasema.
Hivyo
mjasiriamali huyo anasema, kama Corona ikiendelea kubakia Tanzania hadi
visiwani, hana hakika kuwa ujasiriamali wake ambao aliwezeshwa na mradi wa uwezeshaji
wa ‘WEZA II’ kuipitia TAMWA unaweza kuwa mkombozi.
Kadhia hii ya
Corona pia, imebisha hodi ndani ya kikundi cha ‘Nguvu yetu ni umoja’ cha Minunwgini kinachotengeneza majani ya chai
ya kileo na yenye tiba.
Kikundi
hicho chenye wanachama 11 wanawake waliyojikusanya na kuamua kuukimbia
umaskini, wanatengeneza mikoba ya kisasa ya ukili na pamoja na singo za
karafuu.
Kupitia
Mwenyekiti wake bibi Maulid Saleh Hamad, anasema walishajiandaa kwa bidhaa
zenye thamani ya shilingi milioni 1, 260,000 tayari kwa safari ya mkoani Tanga,
kwenye maonyesho waliyokwishaalikwa.
Wenyewe walikuwa
na mikoba ya kisasa 40 kwa bei ya mmoja shilingi 30,000 inayotengenezwa kwa
ukindu na kushonwa kwa cherehani na kutia kitambaa ndani, majani ya chai vikopo
100 sawa idadi kama hiyo ya vipochi.
“Lakini
safari yetu ya Tanga, iliota mbawa baada ya mdudu Corona kutia nanga Tanzania, na sasa bidhaa hizi
tumelazimika kuzisambaaza katika maeneo ambayo, hatuna uhakika wa
kununuliwa,’’analalamika.
Kikundi
hichi cha ‘Nguvu yetu ni umoja’ ambacho kilianzishwa mika tisa iliyopoita, kutokana
na dunia kutoingiliwa na ugonjwa huu wa Corona, mwaka 2018, waligawana faida na
kila mwanachama alijipatia shilingi 60,000.
Ingawa faida
hiyo ilipanda karibu mara mbili, maana mwaka 2019, waligawana kila mwanachama shilingi
110,000 baada ya kuzichana chana shilingi 1,210, 000 walizozipata kama faida
kupitiza uzalishaji wa bidhaa zao.
“Unaona
Corona ilivyotuvuruga, maana hata mwaka huu 2020 tunatarajia kugawa faida ndogo
sana, isiyozidi shilingi 50,000 kila mmoja, maana ndio imetuendesha mchomo kwa
kukosa kwenda kwenye maonyesho Tanga,’’anaeleza.
WATEJA WA WAJASIRIAMALI WAMEATHIRIWA
NA CORONA?
Ashura
Hassan Makame wa Mchanga mdogo, anasema ameshaacha kutumia sabuni ya maji na ya
kipande ‘miche’ aliyokuwa akipitishiwa na mjasiriamali kutoka wilaya ya Mkoani.
Anasema,
ilikuwa kila baada ya miezi miwili, alikuwa akigongewa mlango na mjasiriamali
huyo na kumkopesha sabuni hizo, ingawa kwa sasa mwezi mmoja na nusu hajampitia.
“Nilimpigia
simu siku moja akasema Corona imemzuia na hawezi kutoka, kiholela hivyo pesa
zake amtumie kwa simu na sabuni hana mtu wa kumpa ili zimfikie,’’anasema.
Omar Khamis
Haji wa Chake Chake, anasema alikuwa akiletewa majani ya chai ya asili kutoka
Wete na mwanamke mmoja ambae anamfahamu kwa jina la Rukia, ingawa sasa anasiku
30 zaidi hajamuona.
“Baada yeye
kutopita sasa nimerudia majani ya chai yale ya viwandani, ingawa moja hutumia
siku nne, maana ni makali sana, na sio mazuri kiafya,’’anasema.
Hasnuu Ussi
wa Mtambile anasema wiki moja ijayo atakuwa ameshamaliza majani ya chai na
sabuni za mjasiriamali Arafa Mohamed wa Kangani, na anasema kwa sasa ameshaacha
kutengeneza.
“Nilipomuuliza
anasema, kwa vile biashara yake ni ya kutembeza na sasa uwepo wa Corona, ana
hofu ikaganda ndani na kukosa wateja,’’anasema.
Mfanyabiashara
Mohamed Hamad ‘ustadhi’ wa mjini Chake Chake anasema hata yeye Corona
imemuathiri, maana alikuwa akipokea oda za sabuni ya maji kutoka kwa
mjasiriamali wa mji wa Konde na sasa amerudia zile za viwandani.
“Nikimpigia
simu anasema, kwanza ameamua kuacha maana baadhi ya malighafi huchukua mkoani
Tanga, lakini kutokana na janga la Corona, anahofu kwenda huko,’aliniaeleza.
SERIKALI KUU
Makamu wa
Pili wa Rais Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakati akiwasilisha bajeti ya ofisi
yake ya mwaka 2020/2021, Baraza la Wawakilishi, alisema uchumi wa Zanzibar
ulitarajiwa kukua kwa asiliamia 7 hadi 8 kwa mwaka 2020, lakini uwepo wa Corona
sasa unatarajiwa kukua kwa asilimia 3.
Alisema hilo
limesababishwa kutokana na kuyumba kwa sekta za uchumi ikiwemo utalii,
biashara, uwekezaji na kupungua kwa mapato ya serikali.
TAMWA KINASEMA JE?
Chama cha Waandishi
wa Habari Wanawake Tanzania ‘TAMWA’ ofisi ya Zanzibar, chenyewe kinakereketwa
na uwepo wa Corona, na hasa kuona ni adui wa uchumi kwa wajasiriamali wanawake.
Mkurugenzi
wa TAMWA Zanzibar dk. Mzuri Issa wakati akiwasilisha mada ya athari za Corona na
uhuru wa kujieleza hasa kwa wanawake, kupitia njia ya kielektroniki ya ‘zoom
cloud meeting’ ilioyoandaliwa na shirika la Internews, anasema Corana
ilisababisha serikali kufunga masoko kuanzia 10:00 jioni.
Anasema soko
kama la wazi la Darajani mjini Unguja, kabla ya uwepo wa Corona, lilikuwa
likianzia saa 11:00 jioni hadi saa 4:00 usiku, na kutoa fursa kwa wajasiriamali
wengi wao wanawake kuuza bidhaa zao mbali mbali.
“Wapo
wanawake, maskini na wajane wengi wanaofanyabiashara kama za mazao ya chakula
na biashara wakiyatumia masoko ya Mwanakwerekwe na Darajani, lakini hawafaidiki
nayo kiukamilifu na kuathiri uchumi wao,’’anasema.
Kwenye eneo
jengine Mratibu wa TAMWA Ofisi ya Pemba Fat-hiya Mussa Said, anasema ‘TAMWA’
imeshandaa mpango wa kisasa wa kuhakikisha inawaunganisha wajasiriamali wanawake
na wateja wao kwa njia ya kielektroniki.
Anasema,
ingawa wazo hilo lipo kwa muda mrefu, lakini sasa wameamua kulifungia kazi, ili
kuona Corona haiwi janga mara mbili, kwenye afya na uchumi wa wajasiriamalia
wao.
“Corona ipo
ulimwenguni kote na sasa hadi kisiwani Pemba, imeshaweka makaazi, na ni kweli
wajasiriamali wetu walitegemea sana mikusanyiko ili kuuza bidhaa zao, lakini sasa
ni marufuku,’’anafafanua.
Hivyo,
anaona njia moja ya kuhakikisha wanazalisha na kuuza bidhaa zao, ni
kuwatengenezea makundi ya ‘wasap’ kupitia simu zao na kisha kuwaunganisha na
makampuni kama ya ndege, meli, hoteli na taasisi za serikali, ili kuhakikisha
wanauza bidhaa zao,’’anafafanua.
Akawataka
wasikate tamaa nawendelee kuzalisha, kwani moja ya changamoto za ujasiriamali
ni uwepo wa magonjwa kama hayo, ambayo wakati mwengine hurejesha nyuma juhudi
zao.
MAPENDEKEZO
Wenyewe
wajasiriamali kisiwani Pemba, wamependekeza kuwa kama hali ya Corona itaendelea
kuwepo, basi masoko ya Jumapili yafunguliwe kwa utaratibu unaokubalika wa
wataalamu wa afya.
Mwisho
No comments:
Post a Comment