Habari za Punde

HOTUBA YA MAONI YA KAMATI YA MAENDELEO YA WANAWAKE, HABARI NA UTALII YA BARAZA LA WAWAKILISHI KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMUZI YA FEDHA KWA MWAKA 2020/2021 - WIZARA YA HABARI, UTALII NA MAMBO YA KALE



Mheshimiwa Spika,  Awali ya yote, naomba nichukuwe nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu sub-hanahu wataalah  kwa kutujaalia afya njema na uwezo wa kutekeleza majukumu yetu kwa lengo la kuwatumikia wananchi wetu, na mafanikio yake ni kuijenga nchi yetu ya Zanzibar itakayowanufaisha wananchi wetu wa sasa na vizazi vijavyo.
Mheshimiwa Spika,  Naomba sasa niziwasilishe shukurani zangu za dhati kwako wewe,  kwa kunipa fursa hii kusimama mbele ya Baraza lako tukufu kwa lengo la kuzungumzia machache na ya muhimu, yanayohusu bajeti ya Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale kwa mwaka wa Fedha 2020/2021.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa maelekezo ya  Kanuni ya 96 (1) ya Kanuni za Kudumu za Baraza la Wawakilishi Toleo la 2016, naomba kulijuilisha Baraza lako tukufu kwamba, Kamati ya Maendeleo ya Wanawake, Habari na Utalii ya Baraza la Wawakilishi imepitia Makadirio ya Mapato na Matumizi  ya kazi za kawaida na kazi za maendeleo  kwa  Mwaka 2020/2021  kwa Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale. 
Mheshimiwa Spika, Kamati ya Maendeleo ya Wanawake,  Habari na Utalii ya Baraza la Wawakilishi inaipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kukipandisha hadhi Chuo cha Uandishi wa  Habari na Mawasiliano ya Umma Zanzibar na kukihamishia Chuo Kikuu cha Zanzibar, ili kiweze  kutoa Shahada ya Kwanza ya Uandishi  wa Habari hapa nchini. Tunaamini kwamba kitendo hiki  ni miongoni mwa hatua muhimu ya kukuza na kuinua tasnia ya Habari hapa Zanzibar ikiwa ni miongoni mwa mafanikio ya utekelezaji wa ilani ya Chama cha Mapinduzi ya 2015- 2020.
MAPATO
Mheshimiwa Spika, Kamati yetu inaipongeza Wizara kwa kusimamia vyema makusanyo hasa kwa Kamisheni ya Utalii iliyofikia asilimia 71%.  Hata hivyo, juhudi zaidi  bado zinahitajika kwa taasisi nyengine za wizara hiyo zinazopeleka mapato yake katika mfuko mkuu wa Hazina ikiwemo Idara ya Habari Maelezo, Tume ya Utangazaji, Idara ya Makumbusho na Mambo ya Kale, Taasisi ya Nyaraka na Kumbukumbu pamoja na Ofisi kuu Pemba, ili nazo ziweze kufikia malengo ya makusanyo waliyopangiwa. Kwenye eneo la Makusanyo ya taasisi zilizoruhusiwa kutumia  hali haiko vizuri, kwani kwa tathmini ya jumla taasisi hizo zimekusanya asilimia 42% tu, ambapo Wakala wa Uchapaji alikusanya asilimia 27% na Shirika la Utangazaji Zanzibar  lilifikia  asilimia 30% tu ya ukusanyaji.  Ni mategemeo ya Kamati kuwa taasisi hizi zilizoruhusiwa kutumia zingefanya juhudi za ukusanyaji ili zipate fungu kubwa zaidi la matumizi na hivyo kufanikisha utendaji wa taasisi hizo.
PROGRAMU YA MAENDELEO YA HABARI, UTANGAZAJI NA UPIGAJI CHAPA
Mheshimiwa Spika, Kamati yetu imefurahishwa na inaunga mkono uamuzi wa serikali wa kuendelea  kukuza misingi ya Demokrasia na Utawala Bora hapa nchini  na hatimae kuwa na jamii iliyoimarika katika maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kisiasa kupitia habari. Kamati Inazihimiza  Shirika la Ungazaji Zanzibar (ZBC), Idara ya Habari Maelezo na Shirika la Magazeti la Serikali kuimarisha huduma za Urushaji wa Vipindi na matangazo pamoja na utoaji wa taarifa, picha na sinema kwa ufanisi mzuri ili  kufanikisha viashiria na shabaha zilizokusudiwa katika Programu  ya Maendeleo ya Habari, Utangazaji na Upigaji Chapa.
Mheshimiwa Spika, Kamati yetu inazidi kutoa wito kwa vyombo vyetu vya habari vya umma kuzidi kujitambua kwamba ni mdomo wa Serikali na hivyo vinabeba dhima kubwa na nzito katika jamii, napia  vitambue kwamba bado  vinaendelea kuaminiwa na kupendwa na wanajamii walio wengi, hivyo havina budi kuwa mstari wa mbele katika kukuza mila, silka na utamaduni wetu ikiwemo matumizi fasaha ya lugha ya Kiswahili. Mheshimiwa Spika , tumekuwa tukishuhudia baadhi ya watangazaji wa shirika letu la ZBC wamekuwa na mbwembwe nyingi tena katika vipindi muhimu kama vile taarifa za habari na vipindi maalum suala ambalo wakati mwengine linaishushia hadhi Shirika hilo. Tunawaomba wale wote waliopewa dhamana ya kuwasimamia sekta ya utangazaji watimize wajibu wao, ili watangazaji wa ZBC wasiwakwaze wasikilizaji na watazamaji wao kwa kuwa na uteuzi na matamshi mazuri ya maneno wanayoyatumia.
Katika hatua nyengine, Kamati yetu inaipongeza sana Kampuni ya Uunganishaji wa Maudhui (ZMUX), kwa kuweza kuvuka lengo la kukusanya asilimia hadi 184% ya mapato yake na kufikia hatua ya kuhudumia wateja 14,485 kutoka na ufanisi mzuri wa utendaji na ubora ya king”amuzi cha ZMUX.
PROGRAMU YA MAENDELEO YA UTALII , MAKUMBUSHO, MAMBO YA KALE NA UTUNZAJI WA NYARAKA NA KUMBUKUMBU

Mheshimiwa Spika, Katika eneo ambalo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inapaswa kujivunia ni uendelezaji wa Maeneo ya kihistoria na Mambo ya Kale kwa jitihada zake za kuyalinda na kuyahifadhi. Kamati imetembelea takriban  maeneo yote yaliyofanyiwa ukarabati katika miaka ya hivi karibuni  Unguja na Pemba na inaridhika na kazi iliyofanyika na inayoendelea kufanyika katika maeneo hayo,  na kupelekea kuongezeka kwa watalii wa nje na ndani ya nchi katika maeneo hayo.  
Kamati imepokea kwa nia njema hatua ya ufungaji wa boya katika mji wa Kale uliozama wa Mkumbuu uliopo Ndagoni Pemba. Hata hivyo, kwa kuwa “Mkono mmoja hauchinji Ng’ombe ”; tunaziomba Mamlaka zote zinahuzosika kushirikiana kufufua miundombinu yote ya kulifikia eneo hilo na kulitangaza zaidi kwa lengo la kuongeza idadi ya wageni watakaotembelea mji huo.  


Mheshimiwa Spika, Kamati  pia imefarajika na uamuzi wa wizara kwa kuanza kufikiria kubuni vianzio vipya vya Mapato, ambapo kwa mwaka ujao wa fedha  Idara ya Nyaraka na Kumbukumbu inakusudia kuanza kutoza ujira wa Kutengeneza Nyaraka. Huu ni mwanzo mzuri, na tunaishauri wizara isichoke na kutumia wataalamu wake wa mipango na uchumi kufikiria njia mbali mbali za kutunisha mifuko ya wizara hiyo na serikali kwa ujumla.
PROGRAMU ZA UTANGAZAJI NA UHAMASISHAJI WA UTALII
Mheshimiwa Spika, Kabla sijamaliza hotuba hii naomba tuiangalie Sekta ya Utalii,   Sekta ambayo  ndio tegemeo kuu la Mapato ya Wizara hii na serikali kwa ujumla pamoja na Ajira kwa vijana wetu. Tunapata matumaini kusikia kwamba Kamisheni ya Utalii kwa Kipindi hiki imeweza kusimamia uanzishwaji wa Miradi ya wazalendo 100 na kutengeneza ajira za moja kwa moja zipatazo 980.  Hii ni hatua nzuri na tunaiomba Kamisheni ya Utalii kuongeza juhudi na bidii ya kazi, ili kupiga hatua kubwa zaidi katika sekta hii ya utalii. Tunawaomba waheshimiwa Wajumbe kuridhia maombi ya Kamisheni na kuwaidhinishia shilingi 4,115,300,000 kwa ajili ya shughuli mbali mbali walizojipangia mwaka ujao wa Fedha,  ikiwa ni pamoja na kuyaimarisha mashamba ya viungo yanayotoa huduma kwa watalii na kuandaa vielelezo vya kutangaza utalii kwa kushirikiana ipasavyo na Ofisi za Ubalozi za Tanzania zilioko nje ya nchi.
Mheshimiwa Spika, Mwisho  naomba kuchukua fursa hii kwa  kuwashukuru Wajumbe wa Kamati kwa mashirikiano yao waliyoyaonesha kuanzia mwanzo hadi mwisho wa tukipitia bajeti hii, kwa ruhusa yako naomba niwatambue kwa majina kama ifuatavyo:
1.   Mhe. Mwantatu Mbarak Khamis                    -  Mwenyekiti
2.   Mhe. Mussa Foum Mussa                     -  Makamu Mwenyekiti
3.   Mhe. Omar Seif Abedi                         -  Mjumbe
4.   Mhe. Zaina Abdalla Salum                    -  Mjumbe
5.   Mhe. Saada Ramadha Mwendwa          -  Mjumbe
6.   Mhe. Mwanaidi Kassim Mussa              -  Mjumbe
7.   Mhe. Makame Saidi Juma                     -  Mjumbe
8.   Ndg. Himid Haji Choko                                -  Katibu
9.   Ndg. Mussa Issa Mussa                      -  Katibu
10.                Ndg. Amina  Abeid                        - Msaidizi
11.                Ndg. Azmina  Hamad                    - Msaidizi
Nimalizie kwa kuwashukuru Wajumbe wote wa Baraza la Wawakilishi kwa kunisikiliza kwa umakini na kwa utulivu mkubwa.
 Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.

Ahsante.
(Mhe. Omar Seif Abeid)
Mjumbe,
Kamati ya Maendeleo ya Wanawake Habari na Utalii,
Baraza la Wawakilishi,
Zanzibar.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.