Habari za Punde

HOTUBA YA MWENYEKITI WA KAMATI YA MAENDELEO YA WANAWAKE HABARI NA UTALII YA BARAZA LA WAWAKILISHI KUHUSU MAKADIRIO YA BAJETI YA WIZARA YA KAZI, UWEZESHAJI, WAZEE , WANAWAKE NA WATOTO - 2020/2021



Mheshimiwa  Spika,  Awali ya yote napenda kuchukuwa nafasi hii  kumshukuru Mwenyezi Mungu , ambae ametuwezesha sisi kukutana hapa katika Baraza lako tukufu tukiwa katika hali ya uzima na afya njema.  Lakini pia, ningependa  kwa heshima na taadhima, nikushukuru wewe binafsi  kwa kunipa nafasi ya kusimama mbele ya chombo hiki muhimu cha wananchi  kueleza maoni ya Kamati ya Maendeleo ya Wanawake, Habari na Utalii kuhusiana na Bajeti ya Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee , Wanawake na Watoto kwa mwaka wa Fedha 2020/2021.
Mheshimiwa Spika, kazi hii ya kupitia bajeti ambayo inalenga kuleta maendeleo katika nchi yetu, isingewezekana kama tusingepata mashirikiano  yako ya dhati, pamoja na Wajumbe wangu  wa Kamati wakisaidiwa na Sekretariati ya Ofisi ya Baraza la Wawakilishi  ambao kwa heshima naomba niwatambue  kwa majina kama ifutavyo:-

1.  
Mhe.  Mwantatu Mbarak  Khamis
Mwenyekiti
2.  
Mhe.   Mussa  Foum  Mussa
M/Mwenyekiti
3.  
Mhe.  Makame  Said  Juma
Mjumbe
4.  
Mhe.  Saada  Ramadhan  Mwendwa
Mjumbe
5.  
Mhe.  Omar  Seif  Abeid
Mjumbe
6.  
Mhe.  Mwanaidi  Kassim  Mussa
Mjumbe
7.  
Mhe.  Zaina  Abdalla  Salum
Mjumbe
8.  
Ndg.  Himid   Haji  Choko
Katibu
9.  
Ndg.  Mussa  Issa   Mussa
Katibu
10.       
Ndg.  Amina  Abeid  Hemed
Msaidizi
11.       
Ndg. Azmina  Hamad  Khamis
Msaidizi

Mheshimiwa  Spika, Kamati ya Maendeleo ya Wanawake, Habari na Utalii  ya Baraza la Wawakilishi , ilipata fursa ya kulifikiria kwa kulifanyia uchambuzi  wa kina fungu la makadirio ya bajeti ya Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto ikiwa ni kutekeleza matakwa ya  Kanuni ya 96 (1) ya Kanuni za Baraza la Wawakilishi Toleo la 2016.
Mheshimiwa  Spika,  kwa mantiki hiyo nachukuwa nafasi hii kukuarifu kuwa kazi hiyo tuliifanya kwa umakini wa hali ya juu na leo hii tupo hapa kukuwasilishia kazi tuliyoifanya  kama ilivyoelezwa katika Kanuni ya 96 (1) ya Kanuni  za Baraza la Wawakilishi Toleo la 2016  kwamba:-
Mheshimiwa Spika , kuanzia na ufafanuzi  wa tathmini ya jumla iliyofanywa  na Kamati yangu kuwa makadirio ya Makusanyo ya Wizara  hii yamezidi kutoka  shilingi  1,039,464,000 kwa mwaka wa fedha unaomalizika hadi kufikia shilingi 2,108,555,000 kwa  mwaka ujao wa fedha wa 2020/2021.  Hii ni dalili kwamba Wizara imejipanga kuiongezea zaidi mapato Serikali,  hatua ambayo Kamati yangu inaipongeza.  Hata hivyo,  Kamati yetu inaishauri wizara kuongeza bidii zaidi ya utendaji ili kufikia malengo ya ukusanyaji wa mapato yaweze kufikiwa kwani hadi tunapitia bajeti hii wizara imeripoti kufanikiwa kwa asilimia 58% ya makusanyo kwa mwaka huu wa fedha unaomalizika.
Mheshimiwa Spika,  Wizara pia imeonekana kuongeza makadirio ya matumizi ya kazi za kawaida na kazi za Maendeleo , ingawa si kwa asilimia  kubwa sana,  ambapo kwa mwaka wa fedha 2019/2020 ilikuwa ni shilingi 17,299,600, 000   ukilinganisha na makadirio ya mwaka wa fedha 2020/2021 ambayo ni shilingi 18,510,451,000 .  Mheshimiwa  Spika, ni imani ya Kamati kwamba ongezeko hili la fedha  limelenga  kuleta ufanisi  katika kazi kwa Wizara hii na serikali yote kwa jumla.
PROGRAMU YA UWEZESHAJI WANANCHI KIUCHUMI
Mheshimiwa Spika , Kamati yangu inatoa pongezi za dhati kwa Wizara kwa kusimamia vyema utekelezaji wa programu ya Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi, kwani   sote tumekuwa tukishuhudia uimarishwaji wa  mipango ya upatikanaji wa mikopo nafuu ikiwa na lengo la kuimarisha kwa kuwajengea  uwezo  wajasiriamali  wetu.  Aidha , Kamati inaridhika  na juhudi za wizara za  kuimarisha na kukuza hadhi za kiuchumi kwa wazee, vijana, wanawake watoto na makundi mengine katika jamiii,  suala ambalo limepelekea matokeo mazuri ya viashiria vilivyowekwa katika utekelezaji wa programu hii.  
Mheshimiwa  Spika, Kamati yangu inaitakia Wizara kila la kheri na kufanikisha mipango iliyojiwekea katika mwaka ujao wa fedha ikiwa ni pamoja na kukusudia  kutoa mikopo  700 yenye thamani ya  shilingi Milioni Mia Nane na Hamsini El (850,000,000) kwa lengo lile lile la kuwawezesha wananchi wetu kiuchumi.
Mheshimiwa Spika,    Kamati yangu pia  inachukuwa nafasi hii kuipongeza  Wizara kwa kusimamia mradi kwa vijiji vilivyounganishwa kwa umeme wa jua ambapo tathmini ya mradi huo imebaini kwamba, Mradi huo umewasaidia wananchi kung’arisha vijiji vyao na kuweza kuwasaidia katika kuwawezesha watoto kudurusu masomo yao wakati wa usiku na kujiongezea kipato kwa ‘Solar Mama’.   Hata hivyo, Kamati inaishauri Wizara katika malengo yake  ya mwaka ujao wa fedha, kuongeza idadi ya kinamama  watakaowapatia  mafunzo ya utengenezaji wa vifaa vya umeme wa jua pamoja na idadi ya watakaowezeshwa  kujikwamua kimaisha kupitia kituo cha Barefoot Kinyasini Kibokwa, kutokana na umuhimu wa viashiria hivyo na mafanikio yanayopatikana hasa vijijini.
PROGRAMU YA HIFADHI YA JAMII NA MAENDELEO YA WANAWAKE NA WATOTO.
 Mhesimiwa Spika, Kamati pia imeguswa na kilio cha Wizara hii na jamii kwa ujumla,  kwa kukerwa  na kuchukizwa sana na vitendo vya baadhi ya akinamama kwa  kuwatupa watoto wao baada ya kujifungua.  Tunaendelea  kuungana na Wizara kutoa wito kwa jamii kuendeleza  zaidi mshikamano wa kijamii  pamoja na  kuendeleza mshikamano wa kifamilia na kuwasaidia kwa kila hali na kuwa karibu na wanawake wanapokuwa wajawazito, ili kuepusha msongo wa mawazo unaopelekea kufanyika kwa vitendo vya ukatili kwa watoto.
Mheshimiwa  Spika,  Kamati yetu pia imepata faraja kutokana na azma ya Wizara ya  kufuatilia uwezekano wa kuanzisha Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi hapa Zanzibar.  Kamati inaamini kwamba, uanzishaji wa mfumo huo  unaweza ukawa ni  suluhisho la malipo ya Fidia kwa wafanyakazi watakaoumia au kuuguwa  wakiwa  kazini.  Mheshimiwa Spika, Kamati yetu iliwahi kutembelea Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi wa Tanzania Bara na kubaini kwamba, umekuwa ukiwasaidia sana wafanyakazi  kwa kugharamiwa matibabu kwa wanaoumia au kupata maradhi wakiwa kazini pamoja na malipo kwa msaidizi wa mgonjwa.
Mheshimiwa Spika, Wizara  imeainisha viashiria kadhaa  vinavyolenga matokeo mazuri ya  Huduma za kuratibu masuala ya Kijinsia na Uendelezaji wa Wanawake, ikiwa ni pamoja na kuendelea kuwapatia wanawake mafunzo ya kuelewa haki zao,  pamoja na kuwahamasisha kugombea nafasi mbali mbali za uongozi na ngazi za maamuzi.  Hili ni jambo zuri ukizingatia ya kwamba,  hivi sasa tupo katika vuguvugu la kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwezi Oktoba mwaka huu ambapo tutakuwa na chaguzi mbali mbali ikiwemo Uwakilishi, Ubunge na Madiwani. Hapa tunachukuwa fursa hii kuiomba sana wizara kuifanya shughuli hii haraka mara tu watakavyoingiziwa fedha, ili kuimarisha maendeleo ya wanawake na kukuza muitikio wa kuelewa haki za mwanamke, ushirikishwaji na uongozi. Tunawaomba waheshimiwa wajumbe sote tukubaliane na maombi ya Wizara kwa kuidhinisha jumla ya shilingi 1,009,759,061 kwa ajili ya Programu ya  Maendeleo ya Wanawake na Kupinga Udhailishaji.
PROGRAMU YA USIMAMIZI WA SHERIA ZA KAZI UKAGUZI
NA KAZI ZA STAHA KWA WOTE

 Mheshimiwa   Spika,  Kamati ya Maendeleo ya Wanawake , Habari na Utalii  imeshangazwa na uamuzi wa Wizara  wa  kushusha makadirio ya matumizi  kwa ajili ya utekelezaji wa Programu ya Usimamizi wa Sheria za Kazi, Ukaguzi Kazi na Kazi za Staha kwa  Wote kutoka shilingi 1,688,300,000 kwa mwaka wa fedha  unaomalizika hadi shilingi 1,484,900,000  kwa  mwaka ujao.  Kamati inadhani kuipunguzia fedha programu hii wakati huo huo ikizidishiwa kazi ya kukusanya zaidi ni kuibebesha mzigo mkubwa Kamisheni ya Kazi.  Tunaishauri Wizara iangalie tena mgawanyo wa fedha kwa taasisi zake ukizingatia ya kwamba Wizara inategemea sana vianzio vya mapato vilivyochini ya Kamisheni ya kazi kwa ajili ya mapato yake.
Mheshimiwa  Spika,  mwisho napenda  nichukuwe fursa hii , kuipongeza Wizara , akiwemo Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na Watendaji  wake wote wa ngazi za juu, pamoja na wa ngazi ya chini, kwa mashirikiano yao waliyotupa katika Muda wa wote wa kazi za Kamati . Ni imani yangu kwamba mashirikiano haya yataimarishwa,  ili kuleta ufanisi na kuweza kufikia lengo la kuleta maendeleo katika jamii na Taifa  kwa ujumla.
Nawashukuru sana wajumbe wa Kamati yangu kwa kuniamini na mashirikiano makubwa waliyonipa wakati wote nilipokuwa naongoza Kamati hii. Namuomba Mwenyezi Mungu awajaalie mafanikio mema Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi, ili kutimiza malengo yao waliyokusudia na pia nawatakia kila la kheri wale wote tutakaojaaliwa kuendelea kukitumikia chombo hiki muhimu cha wananchi.
Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa nakushukuru wewe binafsi kwa kuniruhusu nitumie muda wako  adhimu ili kuwasilisha hotuba hii. Naamini haya yote yanafanyika ili kuisaidia  serikali  kufikia malengo iliyojiwekea ya kuleta maendeleo kwa wananchi wake.
Mheshiwa Spika, naomba kuwasilisha.
                                             Ahsante.
(Mhe. Mussa Foum Mussa)
Makamu Mwenyekiti
Kamati ya Maendeleo ya Wanawake Habari na Utalii,
Baraza la Wawakilishi.
Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.