Habari za Punde

HOTUBA YA WIZARA YA KAZI UWEZESHAJI WAZEE WANAWAKE NA WATOTO


UTANGULIZI

1.     Mheshimiwa Spika; Naomba kutoa hoja kwa Baraza lako Tukufu likae kama Kamati ya Matumizi ili liweze kupokea, kujadili na kuidhinisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto kwa mwaka wa fedha 2020/2021.
2.     Mheshimiwa Spika; Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uhai na afya njema na kuweza kukutana tena kujadili Bajeti ya Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto. Kwa niaba ya Wafanyakazi wa Wizara, Napenda kukupongeza Mheshimiwa Spika wa Baraza la Wawakilishi kwa namna unavyoliongoza Baraza lako na kusimamia kwa dhati utekelezaji wa Mipango ya Maendeleo na Bajeti za Serikali kufikia malengo yaliyokusudiwa ya kuondosha umaskini kwa wananchi. Nachukua fursa hii pia kuwashukuru Naibu Spika,  Waheshimiwa Wenyeviti, Waheshimiwa Wajumbe na Watendaji wote wa Baraza kwa namna wanavyotekeleza majukumu yao kwa ufanisi.
3.     Mheshimiwa Spika; Napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein kwa Busara, Hekima, Maarifa, Weledi na Miongozo anayotupa katika kufanikisha utekelezaji wa Shughuli za Wizara pamoja na kusimamia imara utekelezaji wa Dira 2020 na Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi kwa vitendo ikiwemo kudumisha Amani na utulivu. Sote ni mashuhuda wa namna Serikali ya Awamu ya Saba ilivyopiga hatua ya Maendeleo katika kila nyanja.
4.     Mheshimiwa Spika; Kwa namna ya pekee napenda kumshukuru Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo ya Wanawake, Habari na Utalii ya Baraza la Wawakilishi; Mheshimiwa Mwantatu Mbaraka Khamis; Mwanamke Jasiri na Shupavu katika utekelezaji wa Majukumu yake pamoja na Wajumbe wake wote, Makatibu wa Kamati na Wasaidizi wake kwa walivyofanya kazi na Wizara bega kwa bega bila ya kuchoka ili kuleta ufanisi wa kiutendaji. Michango na miongozo waliyotupa ililenga katika kuimarisha ufanisi wa utekelezaji wa Programu zetu ili kuimarisha ustawi na hifadhi ya jamii kwa wananchi na maendeleo yao.
5.     Mheshimiwa Spika; Aidha, Nampongeza kwa dhati Mheshimiwa Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi na Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi kwa jinsi wanavyozisimamia kwa ufanisi na umahiri mkubwa shughuli za Serikali ikiwemo kumsaidia Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kutekeleza Dira 2020 na Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi pamoja na kutupa maelekezo ya kitaalam katika kuimarisha ufanisi wa utekelezaji wa kazi zetu. Maendeleo haya tunayojivunia ni kutokana na uongozi wao imara, thabiti na mahiri. Namuomba Mwenyezi mungu awape umri mrefu Viongozi wetu hawa Baraka, Busara na Maarifa ya kuendelea kutuongoza. Amin.
6.     Mheshimiwa Spika; Kwa niaba ya Watendaji wote wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto napenda kutoa tahadhari kwa wananchi wote ya kuendelea kujikinga na maradhi ya mlipuko ya Corona yaliyoingia hapa nchini na duniani kwa ujumla. Nawasisistiza wananchi kufuata maelekezo yote yanayotolewa na Serikali na Wizara ya Afya ya kujikinga na maradhi haya ikiwemo kunawa mikono kwa sabuni kwa maji yanayotiririka kila wakati, kutumia visafisha mikono (hand sanitizer) na kudumisha usafi wa miili na mazingira yanayotuzunguka na kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima. Pia, napenda kuwasisitiza wazazi na walezi kuwa karibu na watoto wao kwa kipindi hiki na kutowaacha kuzurura ovyo mitaani kwani wanaweza kuathirika na maradhi haya. Vile vile, Kuwasimamia kudurusu masomo yao.
7.     Mheshimiwa Spika; Mbali na Corona nawaomba wananchi waendelee na jitihada za kupambana na vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa wanawake na watoto nchini. Jitihada zetu kwa pamoja zitatupelekea katika kuvitokomeza kabisa vitendo hivi nchini. Tuendelee kushirikiana katika kuelimishana, kuvipiga vita na kila mmoja atekeleze wajibu wake kwa nafasi aliyonayo. Namuomba Mwenyezi Mungu atuondoshee mabalaa yote yaliyopo nchini. “Tushikamane! Kwa Pamoja Tutaweza”. Aidha nawaomba wananchi tuzidi kuchukuwa tahadhari za kujikinga na maradhi ya miripuko ikiwemo kipindupindu na matumbo ya kuharisha wakati huu wa mvua za masika zikiendelea kunyesha.
8.     Mheshimiwa Spika; Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto inaendelea kusimamia utekelezaji wa Sheria na Miongozo ya Kazi, kuratibu upatikanaji wa ajira za staha hasa kwa Vijana, kuimarisha programu za kuwawezesha wananchi kiuchumi na kuimarisha haki, ustawi, hifadhi na maendeleo ya wanawake, watoto, wazee na watu wanaoishi katika mazingira magumu zaidi.  Pia, Wizara inasimamia na kuratibu utekelezaji wa shughuli za hifadhi ya jamii na uzingatiaji wa masuala ya jinsia katika Sera, Sheria, Mipango na Bajeti za Kitaifa, Kikanda na Kisekta.

VIPAUMBELE VYA WIZARA


9.      Mheshimiwa Spika; Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto kwa mwaka wa fedha 2020/2021 imejipangia kutekeleza vipaumbele vifuatavyo:-
       i.          Kusimamia utekelezaji wa Sheria za Kazi na Kuratibu upatikanaji wa Ajira za Staha ndani na nje ya nchi;
     ii.          Kuimarisha masuala ya Usalama na Afya Kazini katika Sekta Binafsi na za Umma.
    iii.          Kukamilisha Uandaaji wa Mfumo wa Taarifa za masuala ya Kazi.
   iv.          Kukuza Usawa wa Kijinsia, Kumwezesha Mwanamke na Kuendeleza Mapambano ya Kumaliza Vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji wa Wanawake na Watoto;
     v.          Kusimamia Ujenzi wa Kituo cha Kulea Wajasiriamali Pemba na kuimarisha uendeshaji kwa Unguja.
   vi.          Kuimarisha Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi kwa kutoa mikopo yenye thamani ya hadi Shilingi Milioni Kumi.
  vii.          Kuanzisha Mfuko wa Fidia Zanzibar.
viii.          Kujenga Ukuta wa Nyumba ya Wazee Welezo.
   ix.          Kuimarisha uratibu wa Programu za Hifadhi ya Jamii na Hifadhi ya Mtoto.
     x.           Kuimarisha Uendeshaji wa Kituo cha Kuzalisha Vifaa vya Umeme wa Jua (Barefoot).
   xi.           Kuimarisha uandaaji na utekelezaji wa Sera, Sheria, Mipango, Uratibu na ufuatiliaji na tathmini wa shughuli za Wizara.
  xii.           Kujenga Uwezo wa Wizara kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.

MUHTASARI WA MATUMIZI KWA MWAKA 2019/2020


10. Mheshimiwa Spika; Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto kwa mwaka wa fedha 2019/2020 iliidhinishiwa jumla ya Shilingi Bilioni Kumi na Saba, Milioni Mia Mbili na Tisini na Tisa, Laki Sita (Tshs. 17,299,600,000) ambapo Shilingi Bilioni Kumi na Tano, Milioni Mia Moja Thamanini na Tatu, Laki Tisa (Tshs. 15,183,900,000) ziliidhinishwa kwa kazi za kawaida na Shilingi Bilioni Mbili, Milioni Mia Moja na Kumi na Tano, Laki Saba (Tshs. 2,115,700,000) kwa kazi za Maendeleo. Kati ya hizo, Shilingi Bilioni Moja, Milioni Mia Nane Arobaini na Tisa, Laki Tatu Tisiini na Tisa Elfu, Mia Mbili na Thamanini (Tshs.1,849,399,280) ni kwa ajili ya kutekeleza Programu ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi; Shilingi Bilioni Kumi, Milioni Mia Nane na Thalathini na Saba, Laki Mbili na Thalathini Elfu, Mia Nne na Arobaini (Tshs. 10,837,230,440) kwa ajili ya kutekeleza Programu ya Hifadhi ya Jamii na Maendeleo ya Wanawake na Watoto. Shilingi Bilioni Tatu, Milioni Sabiini na Nne, Laki Sita na Sabini Elfu, Mia Mbili na Thamanini (Tshs. 3,074,670,280) kwa ajili ya kutekeleza Programu ya Uendeshaji na Uratibu wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto na Shilingi Bilioni Moja, Milioni Mia Sita Thamanini na Nane, Laki Tatu (Tshs.1,688,300,000) ni kwa ajili ya utekelezaji wa Programu ya Usimamizi wa Sheria za Kazi, Ukaguzi Kazi na Kazi za Staha kwa wote.

11. Mheshimiwa Spika; Hadi kufikia Mwezi Machi 2020, Wizara iliidhinishwa matumizi ya jumla ya Shilingi Bilioni Kumi na Moja, Milioni Mia Nne Hamsini na Saba, Laki Mbili na Thalathini Elfu, Mia Mbili Hamsini na Sita (Tshs. 11,457,230,256) sawa na asilimia Sitini na Sita (66%) ya fedha zote. Kati ya hizo Shilingi Bilioni Kumi, Milioni Mia Sita na Sitini, Laki Nane Sabini na Mbili Elfu, Arobaini na Sita (Tshs. 10,660,872,046) sawa na asilimia Sabini (70%) ya fedha zilizoidhinishwa zilitumika kwa Kazi za Kawaida na Shilingi Milioni Mia Saba Tisini na Sita, Laki Tatu Hamsini na Nane Elfu, Mia Mbili na Kumi  (Tshs. 796,358,210) sawa na asilimia Thalathini na Nane (38%) ya fedha zilizoidhinishwa zimetumika kwa kazi za Maendeleo.

Mheshimiwa Spika; Kati ya hizo, Shilingi Milioni Mia Nane na Sabini na Mbili, Laki Nane Kumi na Nane Elfu, Mia Saba Sitini na Nne (Tsh.  872,818,764) zilitumika kwa ajili ya kutekeleza Programu ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ambayo ni sawa na asilimia Arobaini na Saba (47%)  ya fedha kwa programu hiyo. Shilingi Bilioni Saba, Milioni Mia Tano Tisini na Tatu, Laki Mbili Ishirini na Tisa Elfu, Mia Tisa na Thamanini na Tatu (Tshs. 7,593,229,983) zilitumika kwa kutekeleza Programu ya Hifadhi ya Jamii na Maendeleo ya Wanawake na Watoto ambayo ni sawa na asilimia Sabini na Moja (71%). Jumla ya Shilingi Bilioni Mbili, Milioni Ishirini na Mbili, Laki Tano Ishirini na Tano Elfu, Mia Nne na Thalathini na Nane (Tshs. 2,022,525,438) zilitumika kwa kutekeleza Programu ya Uendeshaji na Uratibu wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto sawa na asilimia  Sitini na Sita (66%) ya fedha za Programu hiyo. Jumla ya Shilingi Milioni Mia Tisa Sitini na Nane, Laki Sita Hamsini na Sita Elfu na Sabini na Moja (Tshs. 968,656,071) zilitumika katika kutekeleza Programu ya Usimamizi wa Sheria za Kazi, Ukaguzi Kazi na Kazi za Staha kwa wote sawa na asilimia Hamsini na Saba (57%) ya fedha kwa programu hiyo. (Kiambatanisho namba 1 kinahusika).

MUHTASARI WA MAPATO KWA MWAKA WA FEDHA 2019/2020


12. Mheshimiwa Spika; Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 ilitarajiwa kukusanya mapato ya Shilingi Bilioni Moja, Milioni Thalathini na Tisa, Laki Nne Sitini na Nne Elfu (Tshs. 1,039,464,000) kutokana na Ada za Usajili na Ukaguzi wa Vyama vya Ushirika, Ada ya Ukaguzi wa Mikataba ya Ajira za Nje ya Nchi, Ada ya Ukaguzi wa Maeneo ya Kazi na Vibali vya Kazi.

13. Mheshimiwa Spika; Hadi kufikia Mwezi Machi 2020, Wizara kupitia Kamisheni ya Kazi, Idara ya Ajira, Idara ya Usalama na Afya Kazini na Idara ya Ushirika ilikusanya jumla ya Shilingi Milioni Mia Sita na Sita, Laki Nne, Sabini na Tisa Elfu, Mia Nane na Saba (Tshs. 606,479,807) kutokana na Ada za Usajili, Ada ya Ukaguzi wa Vyama vya Ushirika na Vibali vya Kazi ambayo ni sawa na asilimia Hamsini na Nane (58%) ya Makadirio ya Makusanyo (Kiambatanisho namba 2 kinahusika).

UTEKELEZAJI WA PROGRAMU ZA WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA 2019/2020


14. Mheshimiwa Spika; Kwa mwaka wa fedha 2019/2020, Wizara imetekeleza Programu Kuu na Ndogo zifuatazo:-

PROGRAMU KUU PQ 0101: UWEZESHAJI WANANCHI KIUCHUMI.


Matokeo ya muda mrefu: Kila Mzanzibari anafanya shughuli za kiuchumi za kumuwezesha kumudu mahitaji yake ya msingi.

Programu ndogo SQ010101: Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi


Lengo Kuu: Kuimarisha upatikanaji wa Mikopo nafuu kwa Wananchi.

15. Mheshimiwa Spika; Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi unaendelea kufanya shughuli zake za kutoa mikopo kwa Wananchi. Madhumuni ya Mfuko ni Kuwawezesha Wananchi wenye kipato kidogo kupata mitaji ya kufanya shughuli za uzalishaji ili kujiajiri na kuinua vipato vyao. Walengwa wakuu wa Mfuko ni Vijana, Wanawake, Wanafunzi waliomaliza elimu ya vyuo vikuu, Vyuo vya Amali na Sekondari, Wastaafu na Watu walio katika makundi maalum. Mfuko kwa mwaka wa Fedha 2019/2020 imetekeleza yafuatayo:-

·       Umetoa mikopo 811 Unguja na Pemba yenye thamani ya jumla ya Shilingi Milioni Mia Saba Thamanini na Tisa, Laki Tatu na Arubaini na Nane Elfu (Tshs. 789,348,000).  Wilaya Nne za Pemba zimepata mikopo 330 yenye thamani ya Shilingi Milioni Mia Mbili na Thalathini na Laki Nne (Tshs. 230,400,000) na Wilaya Saba za Unguja zimepata mikopo 481 yenye thamani ya Shilingi Milioni Mia Tano na Hamsini na Nane, Laki Tisa na Arubaini na Nane Elfu (Tshs. 558,948,000). (Kiambatanisho namba 3 kinahusika).

·       Kati ya  mikopo 811 iliyotolewa; Mikopo 461 yenye thamani ya Shilingi Milioni Mia Tano na Kumi na Moja, Arubaini na Nane Elfu (Tshs. 511,048,000) imetolewa kuendesha shughuli mbalimbali za kiuchumi kama vile biashara za jumla na rejareja, utoaji huduma za kutuma na kupokea fedha, uuzaji wa vinywaji baridi, uvuvi, viwanda vidogo vidogo, ufugaji, uchongaji na kazi za mikono na Mradi wa kilimo cha Matunda na Mboga mboga umetoa mikopo 350 yenye  thamani ya Shilingi Milioni Mia Mbili na Sabini na Nane na Laki Tatu (Tshs. 278,300,000).

·       Kati ya Mikopo hiyo, Mikopo ya vikundi ni 223, na ya mtu mmoja mmoja ni 588. Kati ya vikundi 223 vilivyopatiwa mikopo; vikundi 42 ni vya makundi maalum ya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu na vikundi vilivyobaki 181 ni vya mchanganyiko. Jumla ya wajasiriamali 5,092 walinufaika na mikopo hiyo, Wanawake ni asilimia 53% na Wanaume ni asilimia 47%. (Kiambatanisho namba 4 na 5 kinahusika).


·       Mfuko umefanikiwa kupata Shilingi Milioni Mia Moja na Sitini na Moja (Tshs. 161,000,000) kutoka Mradi wa FEED THE FUTURE wa Mboga Mboga na Matunda ikiwa ni moja ya mikakati ya kutunisha fedha zake. Mikakati mingine ambayo imeuwezesha Mfuko kupata  fedha za ziada ni uwekezaji wa sehemu ya fedha zake katika Benki ya Biashara PBZ Ltd ambapo Mfuko ulipata faida ya  Shilingi Milioni Arobaini (Tshs. 40,000,000) na mkakati wa tatu ni kutoa mikopo midogo midogo na ya muda mfupi wa miezi sita hadi tisa; hivyo kuwezesha kutoa mikopo mingi kwa muda mfupi kutokana na  kasi ya mzunguko wa fedha za mikopo.

·       Kwa ajili hiyo Mfuko umefanikiwa kuongeza kasi ya utoaji mikopo  kufikia 811 yenye thamani ya Shilingi Milioni Mia Saba Thamanini na Tisa, Laki Tatu na Arobaini na Nane Elfu (Tshs. 789,348,000) badala ya mikopo 650 yenye thamani ya Shilingi Milioni Mia Saba (Tshs. 700,000,000) iliyojipangia. Kwa kawaida Mfuko hutoa mikopo ya kuanzia 500,000 hadi Milioni 5,000,000 na hutoa Mkopo kwa mujibu wa matakwa ya Muombaji baada ya kufanyiwa tathmini ya biashara yake na uwezo wa kulipa Mkopo aliouomba.

·       Jumla ya Shilingi Milioni Mia Nne Kumi na Tatu, Laki Sita na Ishirini na Tisa Elfu (Tshs. 413,629,000) zimekusanywa Unguja na Pemba katika kipindi cha Miezi Tisa kuanzia Julai, 2019 hadi Machi, 2020. Pemba imekusanya Shilingi Milioni Mia Moja na Arobaini na Tisa, Laki Mbili Sabini na Sita Elfu na Mia Tano (Tshs. 149,276,500) na Unguja imekusanya Shilingi Milioni Mia Mbili na Sitini na Nne, Laki Tatu Hamsini na Mbili Elfu na Mia Tano (Tshs. 264,352,500). Marejesho ni mazuri kwani kwa kila mwezi Mfuko umeweza kukusanya  wastani wa Shilingi Milioni Arubaini na Sita (Tshs. 46,000,000) zaidi ya Milioni Sita kila mwezi ya makisio ya kukusanya Shilingi Milioni Arubaini (Tshs. 40,000,000).


·       Unaendelea kuwajengea uwezo wakopaji wote wanaopewa mikopo ili kuleta ufanisi wa biashara zao. Pia, Mfuko umeandaa na kufanikisha ziara tatu za wajasiriamali kujifunza (2 Unguja na 1 Pemba) ambapo wajasiriamali walipata wasaa wa kuwatembelea wenzao waliofanikiwa katika shughuli zao za uzalishaji kwa nia ya kujifunza kwa vitendo na kwa nadharia. Kwa upande wa Unguja wajasiriamali 30 (Wanawake 19 na Wanaume 11) walitembelea wenzao wa Mkoa wa Kaskazini kujifunza shughuli za kilimo cha viazi vidogo na kabichi na wengine 30 (Wanawake 17 na Wanaume 13) walienda Kibwegere Makunduchi Mkoa wa Kusini Unguja kujifunza ulimaji wa tungule na matikiti maji.

·       Vile vile, ziara nyengine zilifanyika Kisiwani Pemba ambapo wakulima na wasarifu wa mazao ya kilimo 31 (Wanaume 22 na wanawake 9) walitembelea wakulima wa Shehia ya Chimba huko Micheweni. Wakulima walijifunza jinsi ya kutengeneza hodhi la kuhifadhia maji kwa kutumia turubali na namna ya kuchagua mbegu kulingana na hali ya hewa. Pia, walipata fursa ya kuiona mashine ya umwagiliaji maji inayoitwa MWANAMEKA ambayo iliwavutia sana wakulima kwa kuwa haitumii umeme na ina uwezo mkubwa wa kuvuta maji na kurahisisha shughuli za umwagiliaji.

·       Kwa upande wa mafunzo ya nadharia, Mfuko umetoa mafunzo ya kilimo bora (Good Agricultural Practices) na masuala ya usimamizi wa Fedha, uwekaji wa Akiba, uimarishaji wa bidhaa na elimu ya Masoko kwa wajasiriamali 1,061 (Unguja 446 na Pemba 615) kati ya hao Wanawake 573 na Wanaume 488) kutoka katika Wilaya zote 11 za Unguja na Pemba. Mafunzo yamewawezesha wajasiriamali kuzalisha bidhaa kwa wingi na zenye ubora, hali iliyopelekea kuongeza mauzo na kurahisisha urudishaji wa mikopo yao.

·       Imewezesha kikundi kimoja cha NURU TAILORING kilichopo Jumbi Wilaya ya Kati Unguja kuibuka mshindi wa vikundi vinavyozalisha bidhaa za ushoni nchini yaliyoandaliwa na Jumuiya ya Taasisi zinazotoa mikopo midogo midogoTanzania (TAMFI) na kupatiwa zawadi ya US$1,000.

16. Mheshimiwa Spika; Kwa mwaka wa fedha 2020/2021; Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi umejipangia Kutoa mikopo 700 yenye thamani ya Shilingi Milioni Mia Nane na Hamsini Elfu (Tshs. 850,000,000) kwa vikundi vya kiuchumi na mjasiriamali mmoja mmoja katika sekta zote za kiuchumi; Kuangalia fursa mpya za kiuchumi ambazo zinaweza kutekelezwa na wananchi katika sekta mbali mbali; Kuhakikisha kuwa mikopo inayotolewa inatumiwa ipasavyo na inarudishwa kwa wakati uliopangwa; Kuimarisha uwekaji wa kumbukumbu za wateja wa mikopo; Kuendelea na juhudi za kutunisha fedha ili Mfuko uendelee kuwasaidia wajasiriamali wengi zaidi; Kuimarisha mashirikiano na uratibu wa shughuli za mikopo nafuu hapa nchini; Kuimarisha mashirikiano na taasisi zinazotoa mikopo nafuu; Kuimarisha uwezo wa watendaji ili kuongeza ufanisi wa kazi na Kuufanyia mabadiliko madogo Muongozo wa Usimamizi wa Mikopo ili uende sambamba na mabadiliko na mahitaji ya walengwa katika kipindi kilichopo. Kushirikiana na Wizara ya Biashara na Viwanda (Kupitia SMIDA) na Benki ya Watu wa Zanzibar  - PBZ Ltd kufanikisha  uendeshaji wa Mpango wa Maendeleo ya Wajasiriamali Wadogo wadogo na wa Kati utakaopata ufadhili wa Mfuko wa Khalifa.

17. Mheshimiwa Spika; Ili Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi uweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi kwa Mwaka wa fedha 2020/2021 naliomba Baraza lao kuidhinisha Ruzuku ya Shilingi Milioni Mia Mbili Thamanini, Laki Nne Arobaini na Sita Elfu, Mia Saba Ishirini na Nne (Tsh. 280,446,724).

Programu Ndogo:  SQ010102: Usimamizi na Uimarishaji wa Vyama vya Ushirika.


Lengo kuu: Kusimamia mageuzi ya Mfumo wa Ushirika ili kuviwezesha Vyama vya Ushirika kuchangia katika kukuza Ajira na Uchumi wa Nchi

18. Mheshimiwa Spika; Programu hii ina lengo la kusimamia Mageuzi ya Mfumo wa Vyama vya Ushirika ili viwe imara, endelevu, vinavyoendeshwa kiujasiriamali na vinavyokidhi mahitaji ya wanachama kiuchumi na kijamii. Pia, inachangia kukuza ajira na pato la Taifa. Programu ilitekeleza shughuli zifuatazo:

·       Imesajili vyama vya ushirika 860 (Unguja 100; Pemba 760). Kati ya hivyo SACCOS 2 na vyama vya Uzalishaji na utoaji wa huduma ni 858. Idadi ya vyama vyote vya ushirika vilivyosajiliwa hadi mwezi Machi 2020 ni 4,534 (Unguja 2,521 na Pemba 2,013). 

·       Imekagua hesabu za vyama vya ushirika 186 (Pemba 104 na Unguja 82). Lengo ni kukagua hesabu za vyama vya ushirika 170 (Pemba 70; Unguja 100).

·       Imefuatilia uendeshaji wa shughuli za vyama, utunzaji wa vitabu na kutoa ushauri wa kitaalamu kwa vyama 671 (246 Pemba na Unguja 425). Lengo ni kufuatilia vyama 840. Ufuatiliaji katika SACCOS umeonesha kuwa mitaji imeongezeka kufikia Shilingi Bilioni Kumi na Tano, Milioni Mia Tisa na Ishirini (Tshs. 15,920,000,000) kati ya hizo Unguja ni Shilingi Bilioni Kumi na Tatu, Milioni Mia Moja na Kumi (Tshs 13,110,000,000) na Pemba ni Shilingi Bilioni Mbili, Milioni Mia Nane na Kumi (Tshs. 2,810,000,000)

·       Imetoa leseni kwa SACCOS 22 kati ya 227 zilizopo. lengo ni  kuhakikisha kuwa SACCOS zote zinaimarishwa na zinaendeshwa kwa kufuata masharti kama yalivyoelekezwa katika Sheria ya Vyama vya Ushirika Nambari 15 ya Mwaka 2018. Pia, imetoa leseni kwa taasisi 3 kutoa Huduma za Ukaguzi kwa vyama vya ushirika Unguja na Pemba.

·       Imeimarisha uwezo wa watendaji, viongozi na wanachama kwa kutoa mafunzo. Washiriki 2,410 (Wanawake: 1,608: Wanaume: 802) kutoka vyama vya ushirika 168. Kati ya washiriki hao, viongozi walikua 284 na wanachama ni 2,126.


·       Pia mafunzo kwa waandishi wa habari 40 kutoka vyombo vya Habari 20 (Pemba 8; Unguja 12) yalitolewa. Mafunzo hayo yaliwajengea uelewa juu ya kuundwa kwa FARAJA Union Ltd. Matokeo ni kuwa vipindi 80 na Makala zilizosaidia kuelimisha jamii viliandaliwa na kurushwa hewani kupitia vyombo vyao na Gazeti la Zanzibar leo. 

·       Imeimarisha matumizi ya mfumo wa kielektroniki wa kukusanya, kuchambua na kutoa taarifa za vyama vya ushirika. Taarifa za vyama 2,258 kati ya vyama 4,534 vilivyomo katika Daftari la Usajili zimeingizwa. Kati ya hivyo, vyama 1,141 vipo Unguja na 1,117 vipo Pemba. Pia, ipo katika hatua ya kukamilisha zoezi la  kuviingiza vyama vyote vya Ushirika katika Mfumo wa Uwekaji wa Kumbukumbu za Vyama vya Ushirika.
   
·       Imeadhimisha Siku ya Ushirika Duniani katika Uwanja wa Gombani Pemba tarehe 6/7/2019. Maadhimisho yalijumuisha shughuli za kuwaelimisha wanaushirika juu ya  uanzishwaji wa FARAJA Union Ltd, kufanya usafi katika hospitali kuu tano za Pemba na kuchangia Damu, Ujumbe ulikuwa “Ushirika kwa Kazi za Staha

·       Imeendesha mikutano 53 (Pemba 25 na Unguja 28) kwa ajili ya kuitangaza Sheria mpya ya Vyama vya Ushirika Nambari 15 ya mwaka 2018. Jumla ya vyama 783 (Unguja 598 na Pemba 185) vimefikiwa. Washiriki walikua 2,708 (Wanawake 1,735 na Wanaume 973) kutoka Wilaya zote za Unguja na Pemba.


·       Imekamilisha uundaji wa Taasisi ya fedha ya kitaifa FARAJA UNION Ltd. Pia imejeijengea uwezo wa taasisi hiyo kwa kuipatia ofisi na vitendea kazi vikiwemo, kompyuta, printa, meza,viti, mtandao wa kielektroniki wa uendeshaji wa shughuli za fedha. FARAJA UNION Ltd inaendesha shughuli zake kupitia ofisi zake zilizopo katika Shehia za Kisiwandui kwa Unguja na Tibirinzi Pemba.

·       Imefanya ziara ya mafunzo iliyowajumuisha Maafisa wa Wizara, viongozi na watendaji 16 wa FARAJA UNION LTD, kwenye Mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma na Iringa. Lengo la ziara hiyo ni kujifunza mbinu za uendeshaji na uongozi wa taasisi za fedha za kitaifa.


19. Mheshimiwa Spika; Kwa mwaka wa fedha 2020/2021 Programu ya Usimamizi na Uimarishaji wa vyama vya Ushirika imepanga kusajili Vyama Vya Ushirika 400 (Unguja 250 na Pemba 150); Kusimamia uundwaji wa chama kimoja cha kisekta; Kukagua hesabu za Vyama vya Ushirika 200 Unguja (120) na Pemba (80); Kufuatilia na kufanya uchunguzi kwa vyama vya ushirika 800 Unguja (480) na Pemba (320) na Kuimarisha matumizi ya mfumo wa kielektroniki wa ukusanyaji Taarifa za Vyama Vya Ushirika.

20. Mheshimiwa Spika; Ili Programu ndogo ya Usimamizi na Uimarishaji wa Vyama vya Ushirika iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi kwa mwaka wa fedha 2020/2021 naliomba Baraza lako Kuidhinisha jumla ya Shilingi Milioni Mia Tatu Sabini na Tisa, Laki Tisa Sitini na Saba Elfu, Mia Moja na Kumi na Mbili (Tshs. 379,967,112).

Programu Ndogo SQ 010103: Uratibu na Uendelezaji wa Programu za Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi.


Lengo Kuu: Kukuza Hadhi ya kiuchumi kwa Vijana, Wanawake, Wazee, Watoto, Watu wazima na Makundi maalum katika jamii.


21. Mheshimiwa Spika; Programu hii inaongozwa na Idara ya Uratibu wa Programu za Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi na ina jukumu la kubuni na kuratibu programu za uwezeshaji wananchi kiuchumi ili kuwawezesha Wananchi kujiajiri na kuwa na kipato endelevu cha kuweza kumudu maisha yao. Msingi wa malengo haya ni kuwawezesha Wananchi kumiliki uchumi wao na kuchangia katika kuleta maendeleo ya nchi. Programu inasimamia uendeshaji wa vituo viwili; Kituo cha Kulea na kukuza Wajasiriamali kilichopo Mbweni na Kituo cha Wanawake cha kutengeneza Umeme wa Jua kilichopo Kinyasini. Programu kwa mwaka wa fedha 2019/2020 imetekeleza shughuli kuu zifuatazo:-
·     Imeanzisha vituo vya ushauri wa kibiashara Pemba katika Wilaya ya Mkoani, Wete na Chake Chake na Unguja katika Wilaya ya Kusini. Pia, imeviimarisha Vituo vilivyopo Unguja na Pemba katika Wilaya za Kaskazini A, Kaskazini B, Kati na Micheweni ilikufanya kazi kwa ufanisi ikiwemo kununua vifaa mbali mbali na mafunzo kwa ajili ya uendeshaji wa vituo hivyo.

·     Imeandaa mafunzo ya huduma za ushauri wa kibiashara kwa Maafisa watakaotoa huduma katika vituo hivyo pamoja na wajasiriamali. Kwa Unguja, Jumla ya wajasiriamali 110 wamepatiwa mafunzo ya kuendeleza biashara zao kupitia Wilaya zao Kaskazini “A” 35, “B” 35, Kusini 25 na Kati 25. Kwa Pemba, Maafisa na Wajasiriamali 99 wamepatiwa mafunzo katika Wilaya za Chake Chake, Micheweni, Wete na Mkoani.

·     Imeandaa ziara za kuwatembelea Wajasiriamali Unguja na Pemba na jumla ya vikundi 70 (Unguja 40 na 30 Pemba) vinavyojishughulisha na kazi za mikono, ufugaji wa nyuki, ng’ombe, umeme wa jua, ushonaji, ufinyanzi, kilimo, salon ya kike na usarifu wa mazao, ambapo ziara hiyo kwa upande wa Unguja zilihusisha vikundi vya watu wanaoishi katika mazingira magumu, baadhi ya vikundi hivyo Unguja ni Sogea, Afraa Kijichi, Refasha, Sab Spice Kijichi, Bau Business Group, Mtundani Metaring Work na kwa Pemba ni Makoongwe, Kisiwa Panza, Zoyina Partnership na kikundi cha watu wenye mahitaji maalum. Vikundi hivyo viliweza kupatiwa ushauri unaofaa juu ya kuviendeleza vikundi vyao.


·     Imeandaa vikao vya tathmini ya maendeleo ya Idara na kuandaa Maonesho ya kutimia miaka 20 ya kuanzishwa tena kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki yaliyofanyika Fumba Mji Mpya kuanzia tarehe 16/11/2019 hadi tarehe 24/11/2019 ambapo yaliwashirikisha jumla ya wajasiriamali 183 kutoka Zanzibar, Tanzania Bara na Taasisi 17. Wajasiriamali waliweza kutangaza na kuuza bidhaa zao.
·     Imesimamia uendeshaji wa Kituo cha Wanawake cha Utengenezaji wa Vifaa vya Umeme wa Jua (Barefoot College) na imetowa mafunzo ya ufugaji wa nyuki kwa wanawake 20 huko Pemba. Pia, Kituo kimeajiri vijana watatu katika masuala ya ushonaji.


·     Imefanya ufuatiliaji na tathmini ya Maendeleo ya mradi kwa vijiji vilivyounganishwa umeme wa jua pamoja na kutembelea vijiji tofauti Unguja na Pemba kwa ajili ya kubaini changamoto na mafanikio ya mradi. Tathmini imebaini kwamba Mradi unawasaidia wananchi kwa kunga’risha vijiji vyao, watoto kuweza kudurusu masomo yao nyakati za usiku na kuongeza kipato kwa sola mama.

·     Imefanya upembuzi yakinifu ili kuchagua kinamama ambao watapatiwa mafunzo ya nishati ya umeme wa jua kwa muhula wa 3 wa masomo. Jumla ya vijiji 6 (Kigongoni, Ukongoroni, Kendwa Unguja na Kukuu, Msuka na Matale Pemba) vimeweza kuchaguliwa na wanawake 12 wameweza kupata nafasi ya kujifunza masomo ya nishati ya umeme wa jua kwa Unguja na Pemba.

·     Kituo kimenunua vifaa kutoka nchini India kwa ajili ya kufundishia wanawake ambao watajifunza nishati ya umeme wa jua  kwa muhula wa 3 wa masomo vifaa vilivyopelekwa ni pamoja na dayoda, tranzista na daiva.

·     Kituo kimeweza kuadhimisha siku ya Wanawake Duniani kwa kutoa misaada ya vitu mbalimbali katika hospitali ya Kivunge, vifaa hivyo ni pamoja na mito ya kulalia, mashuka, sabuni za kukogea na kufulia.

·     Katika kipindi hichi kituo kimeweza kutangazwa kupitia njia mbalimbali zikiwemo, Makala katika Gazeti la Zanzibar Leo, semina, warsha na mikutano ambapo kituo hupata fursa ya kualikwa pamoja na kutangaza na kuuza bidhaa zinazozalishwa kituoni hapo ikiwepo taulo za wanawake, nguo na asali.   

·     Imesimamia uendeshaji wa Kituo cha Kulea na Kukuza Wajasiriamali (ZTBI) ambapo mashine za maziwa zimefanyiwa matengenezo. Pia, kituo kimeweza kufanya ukarabati wa vifaa mbali mbali vya ofisi. Pia Vipindi mbali mbali vya kukitangaza kituo na huduma zinazotolewa vimerushwa kupitia redio za KISS FM, Bahari FM, Hits FM na ZBC.


·     Vijana 40 wamepatiwa mafunzo juu ya usarifu wa mazao ya kilimo kituoni kupitia mradi wa FAO, pamoja na kupewa tunzo kwa washindi watatu (3) wa mpango wa biashara. Vile vile, Kituo kimefanya mafunzo ya bekari kwa vijana 12.


22. Mheshimiwa Spika; Kwa mwaka wa fedha 2020/2021, Programu ya Uratibu na Uendelezaji wa Program za Wananchi Kiuchumi imepanga kuendelea kutoa mafunzo ya ujasiriamali kwa Vijana 300, Wanawake na Makundi maalum, itatekeleza Miradi ya kuwawezesha Wajasiriamali na Vijana ili kutoa huduma na bidhaa zenye ubora; itawawezesha Wajasiriamali 25 kushiriki katika maonyesho ya Afrika Mashariki (Jua Kali); itaendelea kuwawezesha Vijana kujiajiri kupitia Kituo cha Kulea na Kukuza Wajasiriamali (INCUBATION CENTRE) pamoja na kuwawezesha Wanawake kiuchumi kupitia Kituo cha Wanawake cha utengenezaji wa vifaa vya umeme wa jua (BAREFOOT) Kibokwa.
23. Mheshimiwa Spika; Ili Programu ndogo ya Uratibu na Uendelezaji wa Program za Wananchi Kiuchumi iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi kwa mwaka wa fedha 2020/2021, naiomba Kamati yako kuidhinishia jumla ya Shilingi Bilioni Moja, Milioni Mia Sita Ishirini na Nne, Laki Saba Ishirini na Mbili Elfu, Mia Saba na Kumi na Mbili (Tshs.1,624,722,712/-).
24. Mheshimiwa Spika; Ili Programu Kuu ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi kwa mwaka wa fedha 2020/2021, naliomba Baraza lako Tukufu Kuidhinisha jumla ya Shilingi Bilioni Mbili, Milioni Mia Mbili na Thamanini na Tano, Laki Moja Thalathini na Saba Elfu, Mia Tano na Arobaini na Nane (2,285,137,548/-).

PROGRAMU KUU PQ0103: HIFADHI YA JAMII NA MAENDELEO YA WANAWAKE NA WATOTO


Mtokeo ya Muda Mrefu: Kuimarisha Ustawi na Hifadhi ya Jamii na kupunguza kiwango cha umaskini kwa wanawake wa Zanzibar.

Programu ndogo SQ010301: Uratibu wa Huduma za Uhifadhi wa Jamii.

Lengo kuu: Kuimarisha mifumo ya hifadhi ya jamii na huduma kwa wazee na watoto wanaoishi katika mazingira magumu.

25. Mheshimiwa Spika; Programu hii inatekelezwa na Idara ya Wazee na Ustawi wa Jamii ambayo ina jukumu la kuratibu na kusimamia upatikanaji wa haki kwa makundi yanayoishi katika mazingira magumu zaidi. Pia, programu ina lengo la kuimarisha Mfumo wa Hifadhi ya Mtoto, Kuimarisha hifadhi ya wazee, Kusimamia ulipwaji wa fidia kwa wafanyakazi waliopatwa na ajali kazini na Kusimamia malipo ya Pensheni kwa Wazee wenye umri wa miaka 70 na kuendelea. Pamoja na Mikakati ya Kitaifa na Mpango Mkakati wa Wizara, Utekelezaji wa shughuli za Programu unaongozwa na Sheria ya Watoto Na. 6 ya 2011 na Sera ya Hifadhi ya Jamii ya Mwaka 2014. Programu imetekeleza yafuatayo:-

·       Imeendelea kupokea na kuyafanyia kazi malalamiko yanayohusu ukiukwaji wa haki za watoto kupitia Kitengo cha Hifadhi ya Mtoto cha Taifa  ambapo jumla ya malalamiko 390 yalipokelewa na kufanyiwa kazi kwa Unguja ambapo Malalamiko 255 yalihusu kunyimwa matunzo na  135 yalihusu mvutano wa malezi. Kwa upande wa Pemba jumla ya malalamiko 289 yalipokelewa na kufanyiwa kazi ambapo Malalamiko 194 yalihusu kunyimwa matunzo na 95 yalihusu mvutano wa malezi. Takwimu zinaonyesha kuwa malalamiko ya matunzo na mvutano wa malezi yanaendelea kuongezeka kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo. Hii ni aina mbaya sana ya ukatili dhidi ya watoto ambayo inatokea ndani ya familia na kuwaweka idadi kubwa ya watoto katika hatari ya kupata aina nyengine za udhalilishaji na ukatili. Sababu kuu ya kuongezeka aina hii ya ukatili dhidi ya watoto ni talaka. (Kiambatanisho namba 6a na 6b kinahusika).


·       Imeendelea kufuatilia kesi za jinai na madai 230 (72 Madai na 158 Jinai) katika Mahakama za Watoto za Mahonda, Vuga na Mahakama ya Mkoa wa Kaskazini na Kusini Pemba. Jumla ya kesi 158 za jinai zilizofuatiliwa zilihusisha makosa ya kubaka, kutorosha, kujaribu kulawiti, kulawiti, shambulio la hatari, shambulio la kuumiza mwili, kukashifu na unyanga’nyi Unguja na Pemba. Kesi 108 (Unguja 58 na Pemba 50) bado zinaendelea na kesi 24 zimepewa rufaa kituo cha Marekebisho ya tabia. Aidha, kesi za madai 72 (Vuga 65 na Mahonda 7) zilifunguliwa Unguja ambapo zinazohusisha kunyimwa matunzo na mvutano wa malezi. Kesi 59 zinaendelea; Kesi 11 zimemalizika na 2 zimepatiwa rufaa (Kiambatanisho namba 7(7a na 7b) na 8 (8a, 8b, 8c, 8d) Vinahusika).

·       Imeendelea kusimamia uendeshaji wa Kituo cha Marekebisho ya Tabia kwa Watoto Wanaokinzana na Sheria na Walio katika Hatari ya Kukinzana na Sheria. Hadi kufikia Mwezi Machi, 2020 Kituo kimepokea watoto 21 (Wanawake 8 na Wanaume 13) ambao wamefanya makosa mbali mbali ikiwemo; wizi, kukashifu na kuondoka nyumbani.  Watoto hao hupatiwa taaluma ya mambo mbalimbali ikiwemo; stadi za maisha, ushauri nasaha, ufundi, ushoni, uchoraji, kompyuta, sarakasi na maigizo. Aidha, jumla ya watoto 13 (7 wanawake na 6 wanaume) wamemaliza muda wao wa mafunzo na kuondoka kituoni katika kipindi hiki.

·       Watoto wote hao wanaendelea vizuri ambapo 6 wamerudi Skuli kuendelea na masomo yao, 5 wanaendelea na Mafunzo ya Ufundi  katika  Taasisi ya Sayansi na Teknolojia Karume  na 2 wamejiunga na Mafunzo ya ufundi wa  uchomaji na uunganishaji wa Vyuma katika chuo cha Mafunzo. Ziara katika familia za watoto hawa zinafanywa mara kwa mara na Maafisa wa Kitengo ili kuhakikisha uendelevu wa marekebisho ya tabia zao.

·       Imefuatilia na kusimamia uendeshaji wa vituo 6 vya kulelea watoto yatima vya binafsi Unguja na Pemba. Mpaka kufikia Mwezi Machi, 2020; jumla ya watoto 235 (wanaume 172 na wanawake 63) wanaendelea kutunzwa kwa kupatiwa huduma mbali mbali katika vituo hivyo. Wamiliki wa vituo hivyo wameendelea kupatiwa maelekezo ya namna bora ya uendeshaji wa vituo na kuimarisha malezi ya watoto wanaolelewa katika vituo hivyo.

  • Inaendelea kuhakikisha kwamba msisitizo unawekwa kwa familia kuzingatia jukumu la msingi la malezi na ulinzi wa mtoto kwa ukuaji mzuri wa kimwili na kiakili na kwamba watoto kuwekwa kwenye vituo ni suluhisho la mwisho baada ya mibadala yote ya malezi kushindikana. Wizara imekuwa ikichukua juhudi kadhaa za kuhakikisha inadhibiti ongezeko la watoto wanaolelewa katika vituo hivyo ikiwemo; kukamilisha kanuni za Makaazi yaliyokubaliwa na hivyo kuanzisha utaratibu wa kuvipatia leseni vituo vyenye sifa tu, kuhakikisha watoto wanaoingizwa katika vituo wanapata ridhaa ya Wizara kupitia Idara ya Wazee na Ustawi wa Jamii. Jitihada hizo zimepelekea kupungua kwa kiasi kikubwa idadi ya Vituo pamoja na wimbi la watoto wanaolelewa katika vituo hivyo kutoka watoto 551 mwaka 2015 na kufikia watoto 270 mwaka 2020. (Kiambatanisho namba 9 kinahusika).

·       Imewajengea uwezo Wakuu wa Vituo na Walezi 22 wa vituo vya binafsi vya Unguja na Nyumba ya Watoto Mazizini juu ya Kanuni za Makaazi, viwango na mahitaji katika uendeshaji wa Vituo hivyo pamoja na ulinzi na usalama wa watoto.

·       Wizara ipo katika hatua ya kuanzisha Programu ya Malezi itayohusisha kuwepo kwa Walezi maalum wa kujitolea, watakaofanyiwa tathmini ya kina juu ya malezi, kupatiwa mafunzo na kusajiliwa. Walezi hao wataishi na Watoto wanaohitaji matunzo baada ya kufikwa na kadhia mbali mbali ikiwemo ukatili na udhalilishaji. Pia, imeandaa Kitini cha mafunzo, nyenzo za ufuatiliaji na tathmini pamoja na vipeperushi.

·       Imeendelea kuwatunza Watoto 37 (wanaume 19 na wanawake 18) wa Nyumba ya watoto Mazizini kwa kupatiwa huduma zote muhimu. Aidha, Nyumba ya Watoto Mazizini imekuwa ikitoa hifadhi ya muda kwa watoto wanaofanyiwa udhalilishaji na wanaopata matatizo mbali mbali ya malezi; ikiwemo mvutano wa malezi au kukosa wazazi. Kwa mwaka wa fedha 2019/2020 jumla ya watoto 18 (wanawake 14 na wanaume 4).


·       Kituo cha Mazizini kimepokea Watoto watatu wote wa kike, baada ya kutupwa katika maeneo tofauti Unguja na Pemba. Watoto hao wanaendelea vizuri na malezi. Napenda kuchukua fursa hii kukemea vikali vitendo hivi vya kinyama ambavyo vinaendelea kushamiri katika nchi yetu. Aidha, tunatoa wito kwa jamii kuendeleza mshikamano wa kifamilia pamoja na kuwasaidia kwa kila hali na kuwa karibu na wanawake wanapokuwa wajawazito ili kuwaepusha na msongo wa mawazo unaopelekea kufanya vitendo vya kikatili.

·       Imeendelea kuwahifadhi wahanga 26 (wanawake 22 na wanaume 4) wa ukatili na udhalilishaji katika nyumba salama ili kuzuia kupotea kwa ushahidi na usalama wao.

·       Imeendelea kuratibu utekelezaji wa Sera ya Hifadhi ya Jamii ya mwaka 2014 na imesimamia kufanya tathmini ya Sera hiyo kufuatia kufikia nusu ya utekelezaji wa Mpango kazi wake ili kuangalia mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika utekelezaji huo. Tathmini ya awali imeonyesha kuwa Sera imefanikiwa katika uanzishaji na uendeshaji wa zoezi la Pensheni Jamii kwa Wazee wote lakini kumeonekana changamoto katika masuala ya uratibu. Tathmini hii itakapokamilika itaota muongozo wa namna bora ya utekelezaji wa sera hiyo kwa kipindi kijacho.


·       Imeendelea kuwapatia huduma muhimu ikiwemo Afya, Chakula, Malazi na Mavazi wazee 80 wanaotunzwa katika Makao ya Wazee Welezo, Sebleni na Limbani, Pemba ambapo katika Makao ya Welezo kuna wazee;  42 (wanaume 32 na wanawake 10) Sebleni Wazee 30 (wanaume 9 na wanawake  21) na  Limbani Pemba  Wazee 8 ( wanaume 5 na wanawake 3). Aidha, waathirika wa maradhi ya ukoma wa Makundeni 52 (wanaume 25 na wanawake 27) wanaendelea kupatiwa posho maalum.

·       Kwa kushirikiana na Jumuiya za Wazee nchini imeadhimisha Siku ya Wazee Duniani tarehe 1 Oktoba iliyofanyika kitaifa katika Hoteli ya Zanzibar Beach Resort, Mazizini ambapo Mh. Waziri wa Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto alikuwa Mgeni rasmi. Kauli mbiu ya mwaka huu ilikuwa ni “Tuimrishe Usawa Kuelekea Maisha Ya Uzeeni”. Maadhimisho yaliambatana na shughuli mbali mbali za kuwaenzi na kuwathamini Wazee.

·       Imeendelea kutoa misaada ya kiustawi kwa familia zenye watoto wanaoishi katika mazingira magumu zaidi ambapo familia 152 (Unguja 86 na Pemba 66) zimesaidiwa. Aidha, imewapatia msaada wa posho la maziwa kwa familia zenye mapacha zaidi ya wawili; 14 (9 Unguja na Pemba 5).

·        Imeendelea kulipa na kusimamia malipo ya fidia kwa Wafanyakazi walioumia wakiwa kazini. Jumla ya wafanyakazi 20 wamelipwa fidia katika kipindi hiki, kati ya hao Unguja 11 na Pemba 9. Jumla ya Shilingi Milioni Ishirini na Moja, Laki Mbili Thamanini na Tisa Elfu, Mia Nane na Tisini na Moja (Tshs. 21,289,891) zilitumika kufanya malipo hayo. Aidha, madai 33 (Unguja Madai 21 na Pemba Madai 12) ya malipo ya fidia yenye thamani ya Shilingi Milioni Arobaini na Saba, Laki Nne na Sitini Elfu, Mia Sita na Kumi na Moja (Tshs. 47,460,611) yameshafanyiwa tathmini na yanasubiri malipo. Aidha, Wizara inaendelea na hatua za kuanzisha Mfuko wa Fidia nchini.


·       Hadi kufika mwezi Machi, 2020; jumla ya Wazee 28,516 (16,565 wanawake na 11,951 wanaume) wamesajiliwa katika Programu ya Pensheni Jamii; kati ya hao; Unguja ni 17,660 na Pemba ni 10,856. Jumla ya wazee wapya 2,380 (Unguja 1,434 na Pemba 946) wamesajiliwa na Wazee 1,437 (Unguja 991 na Pemba 446) walifariki na kuondolewa katika Programu katika kipindi hichi. (Kiambatisho namba 10a na 10b Kinahusika)

·       Pia, Mfumo wa kuhifadhi taarifa za Wazee wanaopokea Pensheni unaendelea kuboreshwa na taarifa za wazee zinaendelea kuchukuliwa kwa kufanyiwa usajili wa alama za vidole na picha zao kwa kupitia ving’amuzi kila mwezi. Malipo ya kutumia ving’amuzi kwa upande wa Unguja yameanza rasmi mwezi wa April, 2020 na kwa upande wa Pemba malipo ya ving’amuzi yanaendelea.  Mfumo huo utarahisisha pamoja na mambo mengine utaratibu wa kupokea Pencheni za Wazee kwa njia ya kielekitroniki.

·       Mpango unaendelea vizuri kwa mashirikiano makubwa tunayoyapata kutoka kwa Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya na Masheha wa Unguja na Pemba yanayopelekea ufanisi wa utekelezaji wa program hii. Aidha, tunaendelea kutoa wito kwa Taasisi na jamii kuhakikisha kwamba wazee wote wenye sifa wanasajiliwa kwa wakati ili waweze kupokea Malipo yao ya pensheni kwa wakati na kutoa taarifa kwa wakati kwa wazee waliofariki ambao tayari wamesajiliwa katika Mpango huu.

26. Mheshimiwa Spika; Kwa mwaka wa fedha 2020/2021, Programu ya Uratibu wa Huduma za Uhifadhi wa Jamii imepanga Kuendelea kuimarisha Hifadhi ya  Watoto kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto namba 6/2011; Kuratibu uendeshaji wa Kituo cha kurekebisha tabia za Watoto; Kulipa fidia kwa Wafanyakazi wanaopatwa na ajali kazini; Kufuatili uanzishaji wa Mfuko wa Fidia; Kusimamia uendeshaji wa Makao ya Wazee Unguja na Pemba; Kusimamia uendeshaji wa nyumba ya watoto Mazizini; Kuendelea kutoa misaada ya Kiustawi kwa familia zenye Mazingira magumu zaidi; Kusimamia utekelezaji wa Mpango wa Pensheni Jamii; kuratibu utekelezaji wa Sera ya Hifadhi ya Jamii na Kuzika maiti zisizokuwa na wenyewe na Kuandaa Kanuni na kuratibu utekelezaji wa Sheria ya Wazee
27. Mheshimiwa Spika; Ili Programu ndogo ya Uratibu Uratibu wa Huduma za Uhifadhi wa Jamii iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi kwa mwaka wa fedha 2020/2021; naliomba Baraza lako kuidhinisha jumla ya Shilingi Bilioni Kumi, Milioni Mia Tano Arobaini na Nne, Thalathini na Tano Elfu na Thalathini (Tshs.10,544,035,030).

Programu ndogo SQ010303: Maendeleo ya Wanawake na Kupinga Udhalilishaji.


Lengo kuu: Kuimarisha maendekeo ya wanawake na kuratibu mwitiko wa mapambano dhidi ya udhalilishaji wa Wanawake na Watoto.

28. Mheshimiwa Spika;  Programu hii inatekelezwa na Idara ya Maendeleo ya Wanawake na Watoto ina jukumu la kuratibu na kusimamia utekelezaji wa haki za wanawake na watoto ikiwa ni pamoja na kusimamia utekelezaji wa sera na sheria zinazohusu maendeleo ya wanawake na watoto. Programu inatekeleza majukumu yake ya kuwaendeleza wanawake kwa kuzingatia Sera na Mipango ya Kitaifa, Mikataba ya Kimataifa na Kikanda. Programu kwa mwaka wa fedha 2019/2020 imetekeleza shughuli zake kama ifuatavyo:

·       Imefanya Kikao cha Kamati ya Viongozi wa juu na kujadili taarifa za utekelezaji wa Mpango Kazi wa Kitaifa wa Kupambana na Vitendo vya ukatili na Udhalilishaji kwa taasisi zinazosimamia utekelezaji wa Mpango huo. Pia, imeratibu vikao vitatu vya Kamati ya Kitaalamu ya kupambana na vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa wanawake na watoto na kupata taarifa ya utekelezaji ambayo iliunganishwa na kupatikana taarifa iliyowasilishwa katika Kamati ya Viongozi wa Juu.
·       Imefanya mkutano wa kutathmini na kujadili utekelezaji  wa  mikakati ya kupambana na vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji iliyopendekezwa na wananchi  kupitia programu ya uhamasishaji jamii kupitia sanaa shirikishi. Wananchi walichukua hatua mbali mbali za kujikinga ikiwemo kufyeka vichaka, kuondosha baadhi ya vigenge viovu, kuwaelimisha na kuwapa mbinu watoto/ wanafunzi juu ya namna ya kujikinga na vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji, maboma kuwatafuta wenyewe kwa ajili ya kuyamaliza au kuyasafisha ili kuweka udhibiti wa matukio ya ukatili na udhalilishaji yasitokee. Kudhibiti uzururaji wa wanafunzi kwa mfano skuli ya Nungwi imejengwa ukuta, kuanzisha na kuimarisha ulinzi shirikishi na doria katika Shehia, kudhibiti utizamaji wa TV za nje (maskani) kwa watoto, kulifukia shimo liliopo eneo la Skuli ya Kibeni ambalo linatumiwa na wanafunzi kufanyiana vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji, kuondoshwa kwa baadhi ya magesti na mabaa kwa mfano Donge Mchangani.
·       Imefanya  mkutano wa Robo Mwaka kwa Timu ya Viongozi wa Dini  zinazojumuisha Viongozi wa Dini 88 za Wilaya kwa ajili ya kutathmini utekelezaji wa shughuli wanazofanya katika kupambana na vitendo vya ukatili na udhalilishaji dhidi ya wanawake na watoto pamoja na kutayarisha na kujadili mipango kazi yao kwa robo mwaka unaokuja. Miongoni mwa shughuli walizozifanya ni pamoja na kufanya mikutano ya hadhara, kutayarisha na kusambaza hotuba katika misikiti mbali mbali ya Ijumaa, kuandaa vipindi kupitia redio ya ZBC, Annur na redio jamii (Mkoani na Micheweni) na wamefanya uhamasishaji kupitia Skuli na Madrasa. Jumla ya watu waliofikiwa ni 49,438 (wanaume 27,454 na wanawake ni 21,984).
·       Imeziwezesha Timu za Viongozi wa dini za Wilaya kwa kuwapa nauli na vitendea kazi kama karatasi na kalamu ili waweze kutekeleza  shughuli zao za kutoa elimu na kuihamasisha jamii juu ya kupambana na vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji dhidi ya Wanawake na Watoto.
·       Imetoa Mafunzo ya wasimamizi wa utoaji wa haki Unguja na Pemba na kujadili Uwajibikaji wa Vyombo vya Sheria na Changamoto wanazokabiliana nazo katika utoaji wa huduma. Mkutano huo uliwashirikisha Polisi, DPP, Mahkama, Kituo cha huduma ya Mkono kwa Mkono. Washiriki hao walipendekeza kufanya mikutano endelevu itakayoimarisha mahusiano kati ya vyombo vinavyosimamia masuala ya Haki na kuanzisha mfumo wa uratibu katika masuala ya Sheria ikiwemo chuo cha mafunzo.

·       Imeelimisha na kuhamasisha jamii juu ya kupambana na vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji dhidi Wanawake na Watoto katika Shehia 37 (22 Unguja na 15 Pemba) kwa kupitia mbinu ya sanaa shirikishi. Baada ya maigizo, wananchi walipata fursa ya kuibua na kujadili sababu hatarishi za vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa Wanawake na Watoto katika shehia zao na hatimae kupendekeza mikakati kwa ajili ya kuzitatua sababu hizo. 
·       Imehamasisha viongozi wa Kamati za Kudumu za Baraza la Wawakilishi, Watendaji wa Wizara, Viongozi wa Dini na Wandishi wa Habari kuhusu vuguvugu la malezi kwa watoto ambapo jumla ya watu 120 wamefikiwa ili kuimarisha uwajibikaji wa malezi ya pamoja na kuondoa vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa watoto. Wajumbe wa Wawakilishi wanatarajiwa kutoa elimu hiyo katika majimbo yao ili kuimarisha malezi bora ya watoto nchini. Aidha, imeandaa vipindi vitano (5) vya uhamasishaji kuhusu vuguvugu la malezi kwa watoto kupitia vipindi vya redio na Tv ikiwemo ZBC TV na Redio, Asalam FM, Chuchu Fm, na Zanzibar Cable TV.  
·       Imekiimarisha Kitengo cha Ushauri Nasaha kwa kupatiwa vitendea kazi muhimu ikiwemo mafuta ili waweze kutoa huduma madhubuti na msaada wa kisaikolojia kwa Wahanga wa vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji dhidi ya Wanawake na Watoto. Msaada huo ulisaidia kitengo kufanya ufuatiliaji kwa wahanga wa ukatili na udhalilishaji  pamoja na familia zao na kutoa ushauri unaofaa.
·       Imeandaa na kurusha hewani vipindi 12 (8 Unguja na 4 Pemba) vya kuhamasisha jamii kupinga vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji na majukumu ya waratibu wa Wanawake na Watoto katika Shehia. kupitia ZBC TV, Redio na redio jamii Pemba. Kupitia vipindi hivyo wanananchi wamepata fursa ya kuzijua Sheria mpya zinazohusiana na kupambana na vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa Wanawake na Watoto pamoja na kujua utaratibu wa kutoa taarifa ya vitendo hivyo kupitia ngazi mbali mbali. Aidha, Makala moja ilichapishwa na  gazeti la Zanzibar leo inayohusu masuala ya Udhalilishaji wa Wanawake na Watoto na vipeperushi vilichapishwa na kusambazwa kwa wananchi kwenye maonesho ya chakula huko Chamanangwe.

·       Imefanya mikutano mitatu (3) ya kujenga uelewa juu ya Kuhamasisha malezi bora na Matunzo kwa Familia kwa Watendaji kutoka taasisi za Serikali na Binafsi zinazoshughulikia masuala ya Watoto, Waandishi wa Habari na Kamati ya Maendeleo ya Wanawake, Habari na Utalii ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar.

·       Imeratibu Mkutano wa Kimataifa na Kikanda wa Huduma za Simu kwa Watoto ambao ulizishirikisha Nchi 86 kutoka Afrika Mashariki ya Kati na Ulaya uliojadili juu ya kuwekeza katika teknolojia ya kuwalinda Watoto dhidi ya vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji wa kingono. Aidha, Wajumbe walikubaliana kutumia Mfumo wa pamoja wa Kielektroniki wa ukusanyaji wa taarifa za Udhalilishaji katika Nchi wanachama wanaoendesha huduma za simu kwa Mtoto ili kukinga na kuripoti vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji. Pia, imeandaa kikundi kazi cha kusimamia huduma za simu na masuala ya rufaa kwa watoto waliofanyiwa masuala ya ukatili na udhalilishaji kwa kuwaunganisha na mifumo ya utoaji wa huduma za hifadhi ya mtoto.
·        Imewajengea Uwezo  Waratibu wa Wanawake na Watoto 209 (105 Unguja na 104 Pemba) kwa kupatiwa  mafunzo juu uelewa wa Sheria dhidi ya Ukatili na Udhililishaji wa Kijinsia, Sheria ya Mtoto, Mambo muhimu ya kuzingatia katika kuwasaidia wahanga wa ukatili wa kijinsia, kuelimisha jamii juu ya hifadhi ya mtoto na Kampeni ya kitaifa ya kupambana na Udhalilishaji ambayo ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango kazi wa Kitaifa wa Kupambana na Vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa kijinsia.
Pia, Waratibu 319 walipatiwa posho la usafiri wa kufuatilia (190  Unguja kwa Wilaya za Mjini, Magharibi “A na B” na Kusini na Kati Unguja na 129 kwa Shehia zote za Pemba).

·       Imefanya maadhimisho ya siku 16 za wanaharakati wa kupinga Vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji Unguja na Pemba ambayo huadhimishwa kila mwaka Ifikapo tarehe 25 Novemba – 10 Disemba. Ujumbe wa mwaka huu ni “Imarisha Usawa Pambana na Udhalilishaji, Pinga Ubakaji. Wizara ilitoa zawadi maalum kwa waratibu wa Shehia wa Wanawake na Watoto  pamoja na Shehia zinazofanya vizuri zaidi katika harakati za kupambana na vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa Wanawake na Watoto ambapo jumla ya Waratibu 11 na Shehia  11 zilipatiwa zawadi hizo ili kuchochea ari ya uwajibikaji kwa Shehia na Waratibu wengine katika Mapambano hayo.
·       Imeadhimisha siku ya Mtoto wa Kike tarehe 11/10/2019 katika Ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdul Wakil Wilaya ya Mjini ambapo ujumbe wa mwaka huu ni “Utekelezaji wa Sheria ni Jukumu Letu Sote! Tuwajibike. Pia, Imetoa mafunzo ya Watoto wa Kike ya kuandika Makala ya Udhalilishaji wa kijinsia ambazo zitachapishwa katika Jarida la SEMA ambalo linalenga kuhamasisha uzuiaji wa ukatili wa Kijinsia kwa Watoto na Kuimarisha Malezi Bora.
·       Imeadhimisha siku ya wanawake Duniani tarehe 8/3/2020 Ujumbe wa mwaka huu ni “Endeleza Vuguvugu la Usawa: zingatia Haki na Maendeleo ya wanawake”.  Kilele cha Maadhimisho hayo kilifanyika katika Ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdul Wakil Kikwajuni Zanzibar kwa kufanya Kongamano la Kitaifa. Lengo  la Kongamano hilo ni kutathmini mafanikio na changamoto za utekelezaji wa Azimio la Beijing kwa miaka 25 iliyopita.
·       Imefanya ufuatiliaji wa  vikundi vya wanawake 74 (14 Unguja na 60 Pemba) Vikundi hivyo vimepatiwa ushauri na maelekezo pamoja na kuwaunganisha na fursa za ujasiriamali, mikopo na ushirika ili kuinua kiwango cha uzalishaji.
·       Imepokea, kuyasikiliza na kuyafanyia kazi malalamiko ya Wanawake 105  (41 Unguja na 64 Pemba) kwa kupatiwa maelekezo na Ushauri nasaha, Malalamiko hayo yalihusu  kutelekezwa na mume, madai ya mali,madai ya mahari, dai la talaka, migogoro ya ndoa, shambulio la matusi kwa njia ya simu, madai ya makaazi, kupigwa, huduma za ujauzito, kudhalilishwa na madai ya mafao.
·       Imepokea jumla ya simu 17 zilizorasmi za waathirika wa vitendo vya udhalilishaji kati ya hizo, 1 kutelekezwa, 5 kubakwa, 2 kupigwa, 1 kutishiwa amani, 1 kukatishwa masomo, 1 kulawitiwa, 1 kushikwa makalio, 1 kutumikishwa kazi za majumbani.1 kutukanwa, 1 mvutano wa malezi na 2 adhabu mbadala ya kutoleshwa pesa na mwalimu. Malalamiko hayo  yamefikishwa sehemu husika kwa kuchukuliwa hatua za Kisheria kwa mujibu wa lalamiko.
29. Mheshimiwa Spika; kwa mwaka wa fedha 2020/2021, Wizara kupitia Programu ya Maendeleo ya Wanawake na Kupinga Udhalilishaji inatarajia kufanya ufuatiliaji wa vikundi na kuviunganisha na fursa mbalimbali zilizopo za kiuchumi pamoja na kuhamasisha wanawake kugombea nafasi mbalimbali za uongozi; itaendelea kuwajengea uwezo wadau katika kupinga vitendo vya ukatili na udhalilishaji dhidi ya wanawake na watoto pamoja na kuratibu utekelezaji wa Mpango Kazi wa Miaka Mitano wa Kupambana na Vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji dhidi ya Wanawake na Watoto (2017/2022) na Kuimarisha uhamasishaji na utekelezaji wa Vuguvugu la malezi ya familia  na ushiriki wa watoto katika kupambana na mimba za umri mdogo kupitia mabaraza na vilabu vya watoto.

30. Mheshimiwa Spika; Ili Programu ya Maendeleo ya Wanawake na Kupinga Udhalilishaji itekeleze majukumu yake kwa ufanisi kwa mwaka wa fedha 2020/2021; naliomba Baraza lako Kuidhinisha jumla ya Shilingi Bilioni Moja, Milioni Tisa, Laki Saba Hamsini na Tisa Elfu na Kumi na Sita (Tshs. 1,009,759,016).

31. Mheshimiwa Spika; Ili Progaramu Kuu ya Hifadhi ya Jamii na Maendeleo ya Wanawake iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi kwa mwaka wa fedha 2020/2021; naliomba Baraza lako Kuidhinisha jumla ya Shilingi Bilioni Kumi na Moja, Milioni Mia Tano Hamsini na Tatu, Laki Saba Tisini na Nne, Arubaini na Sita (11,553,794,046).

PROGRAMU KUU PQ0104: UENDESHAJI NA URATIBU WA WIZARA YA KAZI UWEZESHAJI WAZEE WANAWAKE NA WATOTO


Matokeo ya muda Mrefu: Kuwa na Mipango endelevu na Sera sahihi zitakazoimarisha upatikanaji wa ajira zenye staha na ustawi wa vijana, wanawake, watoto, wazee na makundi mengine yanayoishi katika mazingira magumu zaidi.

Programu ndogo SQ010401: Uratibu wa Mipango, Sera na Tafiti za Wizara.


Lengo Kuu:          Kusimamia uandaaji na utekelezaji wa Sera, Mipango, Programu na Tafiti za Wizara itakayosaidia kukuza uchumi endelevu nchini.

32. Mheshimiwa Spika;  Programu ya Uratibu wa Mipango, Sera na Tafiti za Wizara inalenga Kusimamia uandaaji na utekelezaji wa Sera, Mipango, Programu na Tafiti za Wizara ili  Kuwa na Mipango endelevu na Sera sahihi zitakazoimarisha upatikanaji wa ajira zenye staha na ustawi wa vijana, wanawake, watoto, wazee na makundi mengine yanayoishi katika mazingira magumu zaidi. Programu hii iko chini ya Idara ya Mipango, Sera na Utafiti na kwa mwaka wa fedha 2019/2020 imetekeleza shughuli zifuatazo:


·        Imekamilisha uandaaji wa Mswada wa Sheria ya Masuala ya Wazee 2020 na tayari umepitishwa na Baraza la Wawakilishi. Sheria pamoja na mambo mengine inatoa muongozo wa Uendeshaji wa Programu ya Pensheni Jamii kwa Wazee wote na kutoa Muongozo kwa Jamii kusimamia malezi bora ya Wazee.

·        Imekamilisha tafsiri ya Kiswahili ya Sera ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya mwaka 2019 pamoja na nakala nyepesi ya Sera hiyo kwa lugha ya Kiswahili na vikatuni kwa ajili ya urahisi wa kueleweka kwa wananchi. Jumla ya nakala 50 za nakala nyepesi zimetolewa. Pia, imekamilisha Mpango Mkakati wa Wizara na kuchapisha nakala 300 za Mpango mkakati huo na tayari zimeshanza kufanyiwa kazi.

·        Inaendelea na hatua ya kutayarisha Rasimu ya Sera ya Mafunzo Kazi (Apprenticeship Policy) ambapo imefanya vikao na Watendaji wa taasisi mbali mbali Unguja na Pemba juu ya kuimarisha rasimu ya Sera ya hiyo na hivisasa iko katika hatua ya kujadiliwa na Kamati ya Uongozi ya Wizara.

·        Imekamilisha kutoa matokeo ya Utafiti wa ukatili na Udhalilishaji katika maeneo ya kazi katika sekta binafsi ambapo matokeo yameonyesha kuwa waajiri wanaume wanafanya ukatili na udhalilishaji kwa asilimia 44.2 ukilinganisha na waajiri wanawake ambao wanafanya kwa asilimia 18.2. Vile vile, tatizo la kutoleana maneno mabaya limeripotiwa na karibu asilimia 90 ya waliohojiwa. Pia, Asilimia 72.5 ya wahojiwa wamesema kuwa mwenendo mzima wa kuzisimamia kesi za ukatili na udhalilishaji wa kijinsia katika vyombo vya sheria hauridhishi na hakuna kitengo maalum ndani ya taasisi binafsi zilizohojiwa, kinachoshughulikia malalamiko ya ukatili na udhalilishaji wa kijinsia. Vile vile, sababu zilizotajwa zinazopelekea ukatili na udhalilishaji ni pamoja na kupungua kwa mashirikiano baina ya wakuu wa taasisi na waajiriwa, kuwepo kwa watumiaji wa ulevi, mazingira yasiyo salama, kiwango kidogo cha mshahara na kutopata mshahara kwa wakati. Hivyo, imebainika kuwa mfumo maalum wa kushughulikia tatizo la ukatili na udhalilishaji wa kijinsia katika sekta binafsi unahitajika.

·        Kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mjini magharibi imekamilisha zoezi la kufanya tathmini ya tatizo la Omba omba kwa Mkoa wa Mjini Magharibi. Jumla ya omba omba 24 kati ya 42 walifanyiwa tathmini ya kina kwa kutambuliwa wanapotoka, sababu za kujiingiza katika kuomba na hatua gani zichukuliwe. Tathmini imeonyesha kwamba asilimia 87 ya Omba omba ni wanawake na walifanyiwa tathmini ya kina kwa kutambuliwa Shehia wanazotoka ambazo ni Chumbuni, Kilimahewa juu, Mtopepo, Kwaalinato, Mkele, Rahaleo, Mwembe makumbi, Mtoni Kidatu, Nyerere, Amani, Fuoni Uzi, Tomondo na Kisauni. Pia, iliangalia sababu za kujiingiza katika kuomba na hatua gani zichukuliwe. Imegundulika kuwa asilimia 17 (4) ya Omba omba wanafanya shughuli ya kuomba kutokana na matatizo ya kimaisha na asilimia 83 walionyesha kuomba ni tabia yao lakini sishida za kimaisha. Wengine wanaomba kwa kuiga watu na kutafuta njia rahisi za kujipatia kipato.



·        Kwa kushirikiana na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali imeimarisha uaptikanaji wa takwimu za matukio ya ukatili na udhalilishaji wa wanawake na watoto na imeanza kutoa taarifa za takwimu za matukio ya makosa ya jinai ya ukatili na udhalilishaji wa wanawake na watoto za mwaka 2017/2018 na 2018/2019 katika vyombo vya habari mbali mbali ikiwemo ZBC redio na TV, Chuchu FM, Daily News, Nipashe, The Guardian, Bahari FM. Zenj FM, Hits FM, Zanzibar leo, Majira, Island, Mwenge, Uhuru, Mwananchi, Habari leo, Zanzibbar Cable, On line TV, TBC redio na TV pamoja na ITV. Pia, imefanya kipindi maalum Mubashara na ZBC redio kutoa takwimu hizo kwa wananchi.

·        Imeshiriki katika Kikao cha Maandalizi ya Utafiti wa Taasisi za Kijamii na Jinsia Dodoma ambapo utafiti huu utafanywa kuangalia ni namna gani taasisi za kijamii kama familia, skuli, madrasa, mila, desturi n.k zinavyochangia au kupunguza masuala ya ukatili na udhalilishaji wa wanawake na watoto nchini. Tayari nyenzo za kufanyia utafiti huo za ngazi ya Kaya na Binafsi zimeshatayarishwa na kupitiwa na wadau kwa kuimarishwa. Mafunzo kwa wakusanya data yatafanyika muda wowote na zoezi la utafiti litaanza mara baada ya mafunzo Tanzania Bara na Visiwani.

·        Imetayarisha vipindi 75 vya redio na televisheni ambapo vipindi 55 vimerushwa kupitia ZBC, Hits FM pamoja na CHUCHU FM na Vipindi 20 vilirushwa kupitia ZBC TV na ZCTV. Pia imetayarisha Makala 10 katika Magazeti mbali mbali na habari 103 zinazohusu shuguli za Wizara ziliziandikwa na kurushwa hewani kupitia vyombo mbali mbali vya habari. Documentary 2 zinazohusu masuala ya Wazee na Wanawake zilitayarishwa pamoja na kipindi maalum cha utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi kwa miaka 4 na utekelezaji wa miaka 9 wa kipindi cha awamu ya 7 ya Dkt. Ali Mohamed Shein. Pia, imetayarisha tangazo maalum la Wazazi kufanya jitihada ya kuwalinda watoto kuepukana na maradhi ya Corona kwa kutowaachia kuzurura ovyo na kufuata maelekezo ya kinga yanayotolewa na kulirusha kwenye vyombo vya habari.

·        Imekamilisha zoezi la kuandaa taarifa ya utekelezaji wa Maazimio ya Ulingo wa Beijing kwa upande wa Zanzibar na taarifa hiyo imewasilishwa Tanzania Bara na kutayarishwa taarifa moja ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Taarifa hii imeshawasilisha Umoja wa Afrika na pia imeshawasilishwa Umoja wa Mataifa. Pia, imemalizia kuratibu uandaaji wa taarifa ya Zanzibar ya utekelezaji wa Mkataba wa Kimataifa wa Kupinga aina zote za ubaguzi dhidi ya Wanawake (CEDAW) na taarifa imeshawasilishwa Tanzania Bara na imeshatayarishwa Taarifa ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

·        Imefanya ufuatiliaji kwa maeneo tofauti ikiwemo Makao ya Wazee Welezo na Sebleni na Nyumba ya Watoto Yatima Mazizini, Chuo cha Kulea na Kukuza Wajasiriamali na Chuo cha Barefoot cha kinamama pamoja na kuwapitia wanufaika waliofungiwa umeme wa jua. Aidha, imefanya ufuatiliaji katika shuguli mbali mbali za Wizara ikiwa ni pamoja na vikundi vilivyopatiwa mikopo na Mfuko wa Uwezeshaji katika maeneo ya Kaskazini Unguja ili kuona mafanikio yaliyofikiwa na changamoto zilizopo. Changamoto zilizopatikana zimewasilishwa sehemu husika kwa kufanyiwa kazi.

·        Inaendelea na hatua ya kuandaa Mpango Mkakati wa Takwimu wa Wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali. Imeshandaa viashiria vya Wizara ambavyo vitatumika kuandaa nyenzo za kukusanya takwimu za Wizara. Mpango Mkakati umeshakamilika na uko tayari kwa kutumika. Pia, imeandaa Mpango kazi (Roadmap) ya Kuimarisha Takwimu za Wizara ambayo utekelezaji wake utaenda sambamba na Mpango Mkakati wa Takwimu wa Wizara.

·        Imeratibu Kikao cha Mashirikiano baina ya Mfuko wa Uwezeshaji Kiuchumi Zanzibar na Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (National Economic Empowerment Council (NEEC) na kukubaliana kushirikiana katika kubadilishana taarifa, kutafuta rasilimali kwa pamoja, maonyesho ya biashara na mafunzo kwa Watendaji wa pande zote mbili. Pia, Kikao cha mashirikiano ya utendaji baina ya Wizara ya afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ya Tanzania bara na Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto kilifanyika Dodoma ambapo Wizara zimekubaliana kuimarisha mashirikiano katika masuala ya Ustawi wa Jamii, Wazee, Wanawake, Jinsia na Watoto.

·        Kwa kushirikiana na Watendaji wa Wizara ya Fedha na Mipango imeshiriki katika uandaaji na Uwasilishaji wa Taarifa ya Hiari ya Nchi juu ya Utekelezaji wa Malengo Endelevu ya Ulimwengu katika kipengele cha Usawa wa Kijinsia, Ajira na Uwezeshaji wa Wanawake. Ambapo tumejifunza kuwa mbali ya Mafanikio tuliyonayo lakini bado tunahitaji kulisimamia imara suala la kuimarisha Bajeti inayozingatia jinsia; suala la uwezeshaji Wanawake kiuchumi; kuwahamisha Wanawake kushika nafasi mbali mbali za maamuzi; kupambana na mimba za utotoni; ndoa za umri mdogo na ukatili na udhalilishaji hasa katika sehemu za kazi, ajira hasa kwa vijana na suala la ukatili wa wafanyakazi wa majumbani.





33. Mheshimiwa Spika;; Katika mwaka wa fedha 2020/2021 Wizara kupitia Programu ya Uratibu wa Mipango Sera na Tafiti za Wizara itafanya tathmini ya kuangalia mchango wa Mfuko wa Uwezeshaji katika Kuzalisha Ajira na kuongeza kipato kwa wanachama wake; Itafanya tathmini ya Kuangalia namna ya Kuanzisha Mfuko wa Fidia Zanzibar; Itafanya tathmini ya Mapitio ya Utekelezaji wa Mpangokazi wa Kupinga Vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji Wanawake na Watoto kwa muda wa Kati; Itakamilisha na kuchapisha Sera ya Mafunzo Kazi; Itaandaa taarifa ya mwaka 2019/2020 ya utekelezaji wa Mpango wa kitaifa wa kupambana na vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa wanawake na watoto; Itafanya Ufuatiliaji wa Shughuli za Wizara; Itaratibu utekelezaji wa Programu na miradi ya Wizara; Itaimarisha mawasiliano ya Wizara na Itaimarisha Mashirikiano ya Kitaifa, Kikanda na Kimataifa kwa shughuli za Wizara.

34. Mheshimiwa Spika;; ili Programu ya Uratibu wa Mipango Sera na Tafiti za Wizara iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi kwa mwaka wa fedha 2020/2021, naliomba Baraza lako liidhinishe jumla ya Shilingi Milioni Mia Tatu Thamanini na Nane, Sitini na Moja Elfu, Mia Mbili na kumi na Sita (Tshs. 388,061,216). 

Programu ndogo SQ010402: Utawala na Uendeshaji


Lengo Kuu:  Kuweka Mazingira bora ya kazi kwa Wafanyakazi.

35. Mheshimiwa Spika; Programu ndogo hii ina jukumu la kuratibu na kusimamia utekelezaji wa shughuli za uendeshaji na utumishi za Wizara Unguja. Programu ilijipangia kutekeleza yafuatayo:
·        Imekamilisha ujenzi wa ghorofa ya pili ya jengo la Wizara lililopo Mwanakwerekwe na kwa sasa inatumiwa na Kamisheni ya Kazi jambo ambalo kwa kiasi kikubwa limerahisisha upatikanaji wa huduma zinazotolewa na Wizara.

·        Kwa kushirikiana na Tume ya Utumishi Serikalini imekamilisha taratibu za uajiri wa Wafanyakazi wapya 73 kwa Unguja na Pemba, 35 wakiwa ni wanaume na 38 wanawake ili kuongeza ufanisi katika Idara ya Uendeshaji na Utumishi, Idara ya Maendeleo ya Ushirika, Idara ya Wazee na Ustawi wa Jamii. Kati yao 2 ni watu wenye ulemavu.

·        Imefanya malipo ya bima kwa gari zote za Wizara kama agizo la Serikali linavyoelekeza, pamoja na kuzifanyia ukaguzi wa kawaida wa kiufundi gari 8, likiwemo Basi linalotumika kusafirisha watendaji wa kitengo cha Pencheni jamii kipindi cha uhakiki na ulipaji wa pencheni hiyo. Aidha, imeendelea kulipia gharama za umeme, maji, vifaa vya usafi, pamoja na kuimarisha kitengo cha TEHAMA kwa kununua CCTV Cameras za kisasa ambazo kwa kiasi kikubwa zitasaidia kuimarisha usalama na kurahisisha mawasiliano katika ofisi yetu.

·        Imesimamia ulipaji wa posho la likizo kwa wafanyakazi 63 ( 40 kwa Unguja na 23 kwa Pemba), malipo ya muda wa ziada kwa wafanyakazi 15 na imefuatilia malipo ya kiinua mgongo kwa wastaafu 10 kwa Unguja na Pemba.

·        Imeendesha mafunzo ya ndani yanayohusu kupiga vita vitendo vya rushwa, utawala bora, maadili ya kazi na kanuni za utumishi wa umma.

·        Imelipia ada ya mafunzo ya awali “Induction Course” kwa wafanyakazi kumi na mbili (12). Aidha, inaendelea kuwasaidia ada za masomo wafanyakazi watano (5) ambapo kwa ngazi za shahada ya pili ni wawili (2) na wafanyakazi watatu (3) katika mafunzo ya udereva.

·        Programu imeendelea kukiimarisha kitengo cha Habari na Uenezi na kwa kushirikiana na vyombo mbali mbali vya habari kimeweza kurusha habari zinazohusu shughuli za Wizara na kwa mwaka 2019/2020 kimetoa jumla ya vipindi vya Redio 65, Televisheni 20, makala 23.

·        Kupitia Mkataba wa Utoaji wa huduma kwa Mteja Wizara imeendelea kutoa elimu kwa wanananchi ili kuwapa uelewa juu ya fursa na huduma zinazopatikana katika Wizara.


·        Imekamilisha upembuzi yakinifu kwa wafanyakazi wa idara zote zilizomo ndani ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2019/2020 kwa lengo la kwenda sambamba na mpango mkakati wa rasilimali watu (2017/2021) wa Wizara na Taasisi zilizopo chini yake.

·        Imeendelea kugharamia safari za ndani na nje ya nchi kwa Viongozi na Maafisa wa Wizara ili kuweza kushiriki Mikutano ya kikanda, Kitaifa na Kimataifa kwa manufaa ya Wizara na Taifa kwa ujumla.

36. Mheshimiwa Spika; Katika mwaka wa fedha 2020/2021 Wizara kupitia Programu ya Utawala na Uendeshaji itasimamia ulipaji wa mishahara, posho la likizo, malipo ya muda wa ziada na kufuatilia malipo ya viinua mgongo kwa wastaafu wetu, tukiwa na lengo la kuhakikisha wafanyakazi wanapatiwa stahiki zao bila kuchelewa. Katika kuwajengea uwezo wafanyakazi wetu, Wizara itaendelea kusimamia mafunzo ya awali (Induction Course) kwa wafanyakazi wapya walioajiriwa. Programu itaandaa mafunzo yatakayolenga kuhamasisha uwajibikaji ikiwemo kujiweka mbali na vitendo vya rushwa, pamoja na kuratibu mafunzo ya muda mfupi na ya muda mrefu kwa wafanyakazi wake. Pia Wizara itasimamia ununuzi wa jenereta la akiba ili kujihakikishia huduma zinazotolewa na Wizara zinaendelea kupatikana kwa urahisi pale umeme wa gridi ya Taifa unapokosekana.

37. Mheshimiwa Spika; Ili Programu ya Utawala na Utumishi iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi kwa mwaka wa fedha 2020/2021; Naliomba Baraza lako Kuidhinisha jumla ya Shilingi Bilioni Moja, Milioni Mia Tisa Thalathini na Nane, Thalathini na Tano Elfu, Mia Nne na Thamanini (Tshs.1,938,035,480).

Programu ndogo SQ010403: Uratibu na Utekelezaji wa shughuli za Wizara Pemba.


Lengo kuuu: Kuratibu na Kusimamia Mipango na Uendeshaji wa shughuli za Wizara Pemba.

38. Mheshimiwa Spika; Programu ndogo hii ina jukumu la kuratibu na kusimamia utekelezaji wa shughuli za Wizara Pemba na inahusisha Idara ya Utumishi na Uendeshaji pamoja na Idara ya Mipango, Sera na Utafiti. Programu kwa mwaka wa fedha 2019/2020 imetekeleza yafuatayo:-
·       Imeendelea kuwasaidia wafanyakazi watano (5) kwa mafunzo ya ndani. Kati ya hao Wafanyakazi wawili (2) (mwanamme 1 na mwanamke 1) katika mafunzo ya muda mrefu wa ngazi ya shahada ya pili katika fani ya Teknolojia ya habari na ngazi cheti katika fani ya utunzaji wa kumbukumbu na Wafanyakazi watatu (3) (mwanamme 1 na wanawake 2) wa Mafunzo ya muda mfupi katika fani ya Ununuzi na ugavi na uandishi wa miradi.

·       Imelipa fedha za likizo kwa wafanyakazi 24 na wafanyakazi 12 wamelipwa posho la masaa ya ziada. Pia, imelipia gharama za safari za ndani ya nchi ili kushiriki katika vikao na shughuli mbali mbali za wizara Unguja.

·       Imefanya manunuzi ya magazeti pamoja na kulipia gharama za umeme, maji, mafuta, na huduma za mtandao. Pia, imefanya matengenezo vyombo vya moto (5) pamoja na kulipa bima gari (1) na vespa (6).

·       Imefanya ziara 4 za ufuatiliaji na tathmini kwa madhumuni ya kuboresha utendaji wa shughuli mbali mbali za Wizara ikiwemo Wanufaika wa Mikopo, maendeleo ya Vikundi vya Ushirika, Nyumba ya Wazee Limbani, zoezi la pencheni jamii, mabaraza ya watoto ya Shehia, Kamati za Shehia za kupinga Udhalilishaji na utekelezaji wa Sheria za Kazi na usimamiaji wa Sheria ya Usalama na Afya Kazini katika sekta binafsi. Changamoto mbalimbali zilzobainika katika maeneo haya zimeweza kufanyiwa kazi. Aidha imewajengea uwezo watendaji 30 (wanawake 13 na wanaume 17) wa Wizara katika masuala ya Ufuatiliaji na tathmini wa shughuli za Wizara.

·       Programu imefanya vikao viwili (2) kwa watendaji 30 (wanaume 11 na wanawake 19) wa Wizara juu ya maswala Mtambuka kama Udhalilishaji, UKIMWI na umuhimu wa lishe kwa jamii.

·       Imeratibu uandaaji wa ripoti mbali mbali za utekelezaji ikiwemo ripoti ya utekelezaji ya Bango kitita, ripoti za utekelezaji za Ilani za Uchanguzi ya mwaka 2015/2020, pamoja na utayarishaji wa mpango wa Bajeti wa muda wa kati wa Wizara (MTEF) ya mwaka 2020-2023.

39. Mheshimiwa Spika; Kwa mwaka wa fedha 2020/2021, Wizara kupitia program ya Uratibu na Utekelezaji wa Shughuli za Wizara Pemba itasimamia upatikanaji wa maslahi na mafao ya wafanyakazi yakiwamo mishahara, posho la likizo, malipo ya viinua mgongo, malipo ya muda wa ziada, itawaendeleza wafanyakazi, itafanya ununuzi wa Pikipiki 1, na kufanya matengenezo ya vifaa na pamoja na kusimamia upatikanaji wa huduma muhimu za uendeshaji wa ofisi; itasimamia shughuli za ufuatiliaji na tathmini, itawajengea uwezo watendaji katika masuala ya takwimu, utayarishaji wa ripoti za utekelezaji wa kazi za Wizara pamoja na kuratibu masuala mtambuka na kusimamia utekelezaji wa sera na mpango mkakati wa Wizara.

40. Mheshimiwa Spika; Ili Programu ya Uratibu na Utekelezaji wa Shughuli za Wizara Pemba iweze kutekeleza majukumu yake kwa mwaka wa fedha 2020/2021; Naliomba Baraza lako Kuidhinisha jumla ya Shilingi Milioni Mia Nane Sitini na Sita, Laki Tano Ishirini na Tatu, Mia Sita na Sitini (Tshs. 866,523,660).

41. Mheshimiwa Spika; Ili Programu Kuu ya Uendeshaji na Uratibu wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto itekeleze majukumu yake kwa ufanisi kwa mwaka wa fedha 2020/2021; naliomba Baraza lako Tukufu Kuidhinisha jumla ya Shilingi Bilioni Tatu, Milioni Mia Moja Tisini na Mbili, Laki Sita Ishirini Elfu, Mia Tatu Hamsini na Sita (3,192,620,356).



PROGRAMU KUU PQ 0105: USIMAMIZI WA SHERIA ZA KAZI, UKAGUZI KAZI NA KAZI ZA STAHA KWA WOTE


Matokeo ya Muda Mrefu: Upatikanaji wa Kazi za Staha kwa Vijana na Kufuata Kanuni na Sheria za Kazi

Programu ndogo: SQ010501: Uratibu wa Upatikanaji wa Ajira za Staha


Lengo kuu: Kuongeza kiwango cha Ajira zenye Staha na kupunguza kiwango cha ukosefu wa Ajira kwa Vijana


42. Mheshimiwa Spika; katika kutekeleza majukumu yake ya uratibu na usimamizi wa Sera ya Ajira ya Zanzibar ya mwaka 2009. Kwa mwaka wa fedha 2019/2020, Programu ilitekeleza yafuatayo.
·       Imeweza kuratibu upatikanaji wa ajira 659 (421 Wanaume na Wanawake 238) katika Sekta Binafsi nchini na Ajira 909 (Wanaume 83 na Wanawake 826) nje ya nchi, na kwa sasa imo katika kuboresha mfumo wa soko la Ajira ili uweze kukusanya na kuchambua mwenendo wa fursa za ajira kwa ufanisi kwa lengo la kubainisha maeneo muhimu yenye fursa na mafunzo yanaohitajika.

·       Kwa kushirikiana na Ofisi ya Ubalozi nchini Qatar imeweza kuratibu upatikanaji wa fursa za mafunzo kazi kwa vijana wa kike nchini Qatar, vijana 16 wamefaidika na fursa hio na kuanza masomo katika chuo cha malezi ya watoto nchini Qatar, chuo kinachojulikana kwa jina la Qatar Nanny Training Academy (QNTA). Fursa hizo zinatarajiwa kuongezeka zaidi katika kipindi kijacho ambapo wahitimu wa mafunzo hayo wataunganishwa na ajira mara tu baada ya kumaliza masomo yao.

·       Imeendelea kuratibu vyema Taasisi zote za Wakala Binafsi wa Ajira ambapo kwa sasa zimefikia taasisi 15 zilizopatiwa leseni ya wakala wa Ajira Binafsi.

·       Imefanya mikutano na Kamati za Kisekta za Uzalishaji na Ukuzaji wa Ajira za Wilaya kwa Unguja na Pemba ili kuibua fursa mpya za ajira zinazoweza kupatikana katika wilaya zetu kupitia sekta za Kilimo, Utalii, Mazingira, Ujenzi, Sanaa na Michezo.

·       Imefanya mikutano miwili na wadau wakuu wa sekta ya usafiri wa nchi kavu (Magari ya Abiria) ili kujadili hatua ya urasimishaji wa sekta ya Usafiri wa Umma hususani wa Daladala kwa lengo la kufikia ajira za staha kwa wote.

·       Inaendelea na uratibu wa programu ya majaribio awamu ya pili ya Mafunzo Kazi ambapo jumla ya mikutano minne ya uratibu huo imefanyika na jumla ya vijana 120 wamejiunga na mafunzo hayo kutoka wilaya zote za Unguja na Pemba, aidha Sera ya Mafunzo Kazi inategemewa kukamilika.

·       Imeendelea na maandalizi ya Mafunzo Kazi kwa vijana ambao hawatambuliwi na mfumo wa elimu, hawana ajira na hawaajiriki (NEET) ili kufikia lengo la kutomuacha  mtu yeyote nyuma kwenye upatikanaji wa fursa za Ajira

·       Imetoa mafunzo kwa Vijana 40 wanaotafuta ajira ili waweze kukabiliana na mbinu mbali mbali zinazotumika katika usaili wa kutafuta Ajira.

·       Imeandaa programu tatu za Ajira ili ziweze kuongeza fursa za ajira na hatimae vijana waweze kuzitumia kwa kuajiriwa na kujiajiri wenyewe.

43. Mheshimiwa Spika; Programu ya Uratibu wa Upatikananji wa Ajira za Staha kwa mwaka wa fedha 2020/2021, imepanga kuwawezesha na kuelimisha jamii juu ya upatikanaji wa ajira za staha kwa kutangaza nafasi za fursa za ajira zitakazopatikana kupitia Mfumo wa Taarifa za Soko la Ajira na vyombo vya habari; itaimarisha mashirikiano na wadau wa nje na ndani katika kutafuta fursa za ajira kwa vijana; itatoa mafunzo kwa watafuta kazi juu ya kujiajiri na kuajirika; itaendelea kusimamia program ya mafunzo kazi kwa wanagenzi.
44. Mheshimiwa Spika; Ili Programu ya Upatikanaji wa Ajira za Staha iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi kwa mwaka wa fedha 2020/2021; naliomba Baraza lako kuidhinisha ruzuku ya Shilingi Milioni Mia Mbili Ishirini na Nne, Laki Nne Hamsini na Mbili Elfu, Mia Tatu na Thamanini (Tshs 224,452,380).

 




Programu Ndogo SQ010502: Usimamizi wa Usalama na Afya Kazini.


Lengo Kuu: Kuimarisha masuala ya Usalama na Afya katika sehemu za kazi

45. Mheshimiwa Spika;  Programu hii inatekelezwa na Idara ya Usalama na Afya Kazini na inasimamia utekelezaji wa Sheria Namba 8 ya Mwaka 2005 ya Usalama na Afya Kazini. Kwa mwaka wa fedha 2019/2020; Programu imetekeleza yafuatayo:-

·       Imefanya usajili wa sehemu za kazi 78 (57 Unguja na 21 Pemba) ili kuzitambua na kuweka taarifa zao kwenye daftari la usajili wa sehemu za kazi. Hii itarahisisha shughuli za ukaguzi kwa kutambua mapema mazingira ya kazi zao, hatari zinazoweza kutokea katika sehemu hizo na hivyo kutoa ushauri na maelekezo yanayofaa, kabla ya  kutokea tatizo.

·       Imefanya ukaguzi wa sehemu za kazi 137 (84 Unguja na 53 Pemba) ili kuangalia hali ya usalama na afya katika maeneo hayo. Ushauri ulitolewa juu ya kurekebisha kasoro zilizobainika. Ufuatiliaji uliofanywa baada ya ukaguzi, umeonesha kuwa kasoro nyingi zimerekebishwa baada ya kufuatwa ushauri uliotolewa.

·       Imefanya uchunguzi wa matukio ya ajali na maradhi yatokanayo na kazi  katika sehemu  (5) za  kazi ambazo ziliripotiwa kutokea kwa ajali hizo wakati wafanyakazi wakiendelea na kazi. Wafanyakazi 2 walifariki kwa kufukiwa na udongo katika ujenzi wa mtaro wa kupitishia maji ya mvua   na mfanyakazi 1 wa kampuni ya CCE alifariki baada ya kukanyagwa na gari wakati wa ujenzi wa barabara.

·       Katika kukuza uelewa wa masuala ya usalama na afya kazini, Idara imeandaa na kurusha hewani vipindi vitatu (3) vya radio na vipindi vinne (4) vya televisheni kupitia Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC).  Vile vile Idara imetoa mafunzo kwa wawakilishi 80 (50 Unguja na 30 Pemba) wa masuala ya usalama na afya kazini kutoka kwenye Wizara na taasisi za umma ili waweze kufahamu majukumu yao na wajibu wao wakiwa kwenye maeneo yao ya kazi kwa mujibu wa Sheria ya Usalama na Afya Kazini.
 
·       Ili kukuza mashirikiano na uratibu wa masuala ya usalama na afya kazini, imewajengea uwezo watendaji wake kwa kuweza kuhudhuria mikutano na makongamano mbali mbali ya mashirikiano Kitaifa, Kikanda na Kimataifa juu ya Masuala ya Usalama na Afya Kazini katika sekta ya Mafuta na Gesi Asilia na Virusi vya Ukimwi na Ukimwi na TB sehemu za kazi. Pamoja na hayo, Uratibu wa shughuli za usalama na afya kazini unaendelea kufanyika ili kupata mashirikiano kwa taasisi zote zinazotakiwa kufanya kazi kwa pamoja.

46. Mheshimiwa Spika; Katika mwaka wa fedha 2020/2021, Programu imejipangia kuendelea Kuimarisha utekelezaji wa Sheria Nambari 8 ya mwaka 2005 ya Usalama na Afya Kazini; Itafanya ukaguzi wa sehemu za Kazi 300; Itafanya usajili wa sehemu za kazi 120; Itatoa elimu kwa waajiri na wafanyakazi 170 (Sekta ya Umma 90 na Sekta Binafsi 80); Itaimarisha mashirikiano na uratibu wa masuala ya usalama na afya kazini na itakuza uelewa wa jamii kupitia vyombo vya habari.

47. Mheshimiwa Spika; Ili Programu ya Usimamizi na Usalama wa Afya Kazini iweze kutekeleza majukumu yake kwa mwaka wa fedha 2020/2021; naliomba Baraza lako kuidhinisha jumla ya Shilingi Milioni Mia Mbili na Sita, Laki Tatu na Saba na Mia Tatu na Ishirini (Tshs 206,307,320) kwa ajili ya matumizi ya kazi za kawaida.

Programu Ndogo: Q010503: Usimamizi wa Viwango vya Kazi vya Kitaifa na Majadiliano ya Pamoja Kazini


Lengo Kuu: Kuhakikisha Kunakuwepo Utekelezaji Mzuri wa Sheria za Kazi.

48. Mheshimiwa Spika; Kamisheni ya Kazi ina jukumu la kusimamia utekelezaji wa Sheria za kazi katika sekta za binafsi kwa hapa Zanzibar. Pia, Kamisheni ya Kazi inajukumu la kufanya ukaguzi kazi kwa taasisi hizo, kusimamia ajira za wafanyakazi wa kigeni, kuthibitisha Mikataba ya Wafanyakazi wazalendo na wageni na kuimarisha mahusiano mema kati ya waajiri na waajiriwa sehemu za kazi.  Kwa mwaka wa fedha 2019/2020, Programu imetekeleza shughuli kuu zifuatazo:-

·       Imefanya ukaguzi kazi kwa Taasisi 380 (Unguja ni 314 na Pemba ni 66). Ukaguzi huo unafanyika ili kusimamia ipasavyo utekelezaji wa Sheria za Kazi kwa taasisi zote.
·        Pia, imefanya ukaguzi maalumu kwa Taasisi 403 kati ya hizo (Unguja ni 324 na Pemba ni 79) ili kuona utekelezaji wa ulipaji wa kima cha chini cha mishahara tokea kilipotangazwa mwezi Julai 2017.
·       Imethibitisha mikataba ya kazi 2,329  (Unguja ni 2,082 na Pemba ni 247) kwa wafanyakazi ili kuhakikisha inaendana na Sheria za Kazi ikiwa ni miongoni mwa haki yao ya msingi kwa mujibu wa Sheria za Kazi. Wakati wa uthibitishwaji wa Mikataba hiyo wafanyakazi husika husomewa Mikataba hiyo na Maafisa Kazi ili kupata uelewa mzuri juu ya haki zao.
·       Imepokea migogoro ya kazi 288 iliyowasilishwa (Unguja 236 na Pemba 52). Migogoro 52 ilitatuliwa kwa njia ya upatanishi (mediation) (Unguja 50 na Pemba 2), Migogoro 84 ilitatuliwa kwa njia ya usuluhishi (arbitration) (Unguja 61 na Pemba 23), Migogoro 67 imepelekwa Mahkama ya kazi kwa taratibu nyengine za kisheria. Migogoro 6 iliamuliwa nje ya kitengo.  Aidha, Migogoro 24 imefutwa kutokana na sababu za kutokufika kwa pande zote mbili pamoja na kuchelewa kufungua shauri na Migogoro 55 inaendelea katika ngazi ya usuluhishi na uamuzi. Migogoro yote hiyo iliyowasilishwa inahusu kukatishwa Mikataba ya Kazi kwa wafanyakazi, kutokulipwa kwa kiwango cha mshahara stahiki kwa mujibu wa sheria, na kufukuzwa kazi.
·       Imewapatia Vibali vya Kazi jumla ya wafanyakazi wa kigeni 1,441 kutoka Mataifa mbali mbali (Italy, India, China, Uingereza na Nchi za Afrika ya Mashariki) kufanya kazi nchini. Idadi kubwa ya wafanyakazi waliopatiwa vibali hivyo ni kutoka Sekta Binafsi (hoteli na Vyuo) na Sekta za Umma (Afya, Ujenzi na Utalii).
·       Imeanza hatua ya kuandaa database ya Kamisheni ya Kazi ambapo Hadidu Rejea ya utayarishaji wa Database imekamilika na hatua inayoendelea ni kutangazwa kwa wakandarasi ili kupata wataalamu wa kuitengeneza.
·       Imefanya Ukaguzi wa Vyama vya Wafanyakazi kwa matawi 5; matawi mawili (2) Mkoa wa Kaskazini Unguja, Matawi mawili (2) Mkoa wa Kusini Unguja, na Tawi moja Mkoa wa Kusini Pemba.
·       Imetoa elimu ya Sheria za Kazi kwa Taasisi 26 (Unguja 17 na Pemba 9). Pia, imerusha vipindi tisa (9) kuhusu elimu hiyo kupitia vyombo vya habari. Kati ya vipindi hivyo 4 vilirushwa ZBC TV, ZBC Redio 3 na 2 Chuchu FM. Lengo hasa la kutoa taaluma hiyo ni kujenga uelewa kwa Waajiri, Wafanyakazi na jamii kwa jumla juu ya Sheria za Kazi.

49. Mheshimiwa Spika; kwa mwaka wa fedha 2020/2021 Kamisheni ya Kazi kupitia programu ya Usimamizi wa Viwango vya Kazi vya Kimataifa na Majadiliano ya Pamoja mbali na majukumu mengine Itafanya ukaguzi kazi kwa Taasisi 700; Itathibitisha mikataba ya kazi kwa wazalendo 6,000; Itakagua vyama vya waajiri na wafanyakazi 16; itatoa elimu ya Sheria za Kazi kwa taasisi 45 na itarusha vipindi 25 kupitia vyombo vya habari.

50. Mheshimiwa Spika; Ili Programu ya Usimamizi wa Viwango vya Kazi vya Kimataifa na Majadiliano ya Pamoja iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi kwa mwaka wa fedha 2020/2021; naliomba Baraza lako Kuidhinisha Ruzuku ya jumla ya Shilingi Bilioni Moja, Milioni Arobaini na Nane, Laki Moja Arobaini Elfu na Mia Tatu (Tshs.1,048,140,300)

51. Mheshimiwa Spika; Ili Programu Kuu ya Usimamizi wa Sheria za Kazi, Ukaguzi Kazi na Kazi za Staha kwa wote itekeleze majukumu yake kwa ufanisi kwa mwaka wa fedha 2020/2021; naliomba Baraza lako Tukufu Kuidhinisha jumla ya Ruzuku ya Shilingi Bilioni Moja, Milioni Mia Nne Sabini na Nane, Laki Tisa (1,478,900,000).

MAOMBI YA FEDHA KWA PROGRAMU ZILIZOPANGWA KUTEKELEZWA MWAKA WA FEDHA 2020/2021


52. Mheshimiwa Spika; Ili Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto iweze kutekeleza Programu zake kwa ufanisi kwa mwaka wa fedha 2020/2021, naliomba Baraza lako Tukufu iidhinishe jumla ya Shilingi Bilioni Kumi na Nane, Milioni Mia Tano na Kumi, Laki Nne na Hamsini na Moja Elfu, (Tshs.18,510,451,000/-). Kati ya hizo, Shilingi Bilioni Kumi na Tano, Milioni Mia Mbili Hamsini na Moja, Laki Tatu (15,251,300,000/-) ni kwa ajili ya Kazi za Kawaida ambapo Shilingi Bilioni Kumi, Milioni Tisini na Tano, Laki Mbili  (10,095,200,000/-) ni matumizi ya Uendeshaji wa Ofisi; Shilingi Bilioni Tatu, Milioni Mia Tano Thalathini na Tatu, Laki Tatu (3,533,300,000) ni kwa ajili ya Mishahara na Shilingi Bilioni Moja, Milioni Mia Sita Ishirini na Mbili, Laki Nane (1,622,800,000) Ruzuku. Pia, Shilingi Bilioni Tatu, Milioni Mia Mbili Hamsini na Tisa, Laki Moja Hamsini na Moja Elfu (3,259,151,000/-) ni fedha za maendeleo
53. Mheshimiwa Spika; Kati ya Fedha hizo, Shilingi Bilioni Mbili, Milioni Mia Mbili na Thamanini na Tano, Laki Moja Thalathini na Sita Elfu, Mia Tano na Arobaini na Nane (Tshs. 2,285,137,548) ni kwa ajili ya kutekeleza Programu ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi. Shilingi Bilioni Kumi na Moja, Milioni Mia Tano Hamsini na Tatu, Laki Saba Tisini na Nne Elfu, Arobaini na Sita (Tshs.11,553,794,046) kwa ajili ya kutekeleza Programu ya Hifadhi ya Jamii na Maendeleo ya Wanawake na Watoto. Shilingi Bilioni Tatu, Milioni Mia Moja na Tisini na Mbili, Laki Sita Ishirini Elfu, Mia Tatu Hamsini na Sita (Tshs. 3,192,620,356) zimetengwa kwa ajili ya kutekeleza Programu ya Uendeshaji na Uratibu wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto na Shilingi Bilioni Moja, Milioni Mia Nne Sabini na Nane na Laki Tisa (Tsh.1,478,900,000) ni kwa ajili ya utekelezaji wa Programu ya Usimamizi wa Sheria za Kazi, Ukaguzi Kazi na Kazi za Staha kwa wote (Kiambatanisho namba 11 kinahusika).
54. Mheshimiwa Spika; Wizara katika kipindi cha mwaka wa fedha 2020/2021 inatarajiwa kukusanya mapato ya Shilingi Bilioni Mbili, Milioni Mia Moja na Nane, Laki Tano Hamsini na Tano Elfu (Tshs. 2,108,555,000) kutokana na Ada  za Usajili na Ukaguzi wa Vyama vya Ushirika, Ada ya Ukaguzi wa Mikataba ya Ajira Nje ya Nchi, Ada ya Ukaguzi wa Maeneo ya Kazi na Vibali vya Kazi (Kiambatanisho namba 12 kinahusika).

          

HITIMISHO


55. Mheshimiwa Spika; Wizara inatekeleza majukumu yake kwa  kushirikiana na Watendaji mbali mbali ikiwemo taasisi za Serikali, taasisi za kiraia na Washirika wa Maendeleo zikiwemo UNICEF, UN WOMEN, UNDP, UNIDO, UNFPA, ILO, SAVE THE CHILDREN, FHI, MIVARF, HELP AGE INTERNATIONAL, CSEMA, Milele Foundation, COSTECH, na Jumuiya ya Afrika Mashariki.
56. Mheshimiwa Spika; Pia, Wizara inafanya kazi na Taasisi za Kiraia nazo ni ZAFELA, ZLSC, UWAWAZA, UWT, ACTION AID, TAMWA, CUZA, Madrasa Resource Centre, JUMAZA, ZANEMA, ZATUC, Male Network na Pathfinder. Pia, nazishukuru Taasisi zote za kifedha, ikiwemo PBZ kwa mashirikiano yao mazuri kwa Wizara.
57. Mheshimiwa Spika; Napenda kuvishukuru vyombo vya habari vya Serikali na binafsi kwa jitihada kubwa wanayoichukua ya kuelimisha jamii juu ya shughuli zinazofanywa na Wizara ikiwemo kupiga vita suala la ukatili na udhalilishaji wa Wanawake na Watoto na mapambano dhidi ya ugonjwa wa Corona ambao kwa njia moja au nyengine umeathiri wanawake, watoto na sekta ya kazi nchini.  Vyombo hivyo ni pamoja na ZBC redio na televisheni, Gazeti la Zanzibar Leo, Zanzibar Cable televisheni, TBC, AZAM TV, Zenj FM, Island TV na Hits FM, Redio Jamii za Mtegani, Micheweni, Mkoani na Tumbatu. Ni vigumu kuvitaja vyote lakini napenda kuvishukuru vyombo vyote vya habari vilivyoshirikiana nasi.

58. Mheshimiwa Spika; Mwisho kabisa napenda kuwashukuru watendaji wote wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto kuanzia Naibu Waziri Mheshimiwa Shadya Mohammed Suleiman, Katibu Mkuu Ndugu Fatma Gharib Bilal, Manaibu Makatibu Wakuu Ndugu Maua Makame Rajab na Ndugu Mwanajuma Majid Abdallah, Kamishna wa Kazi, Ofisa Mdhamini Pemba, Wakurugenzi na Watendaji wa ngazi zote kwa mashirikiano makubwa ya kiutendaji wanayonipa katika kutekeleza majukumu yetu Wizara. Wamekuwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa tunatekeleza majukumu ya Wizara kwa ufanisi ili kuleta maendeleo endelevu kwa walengwa wetu wote. Yote niliyoyaeleza katika kitabu hiki ni mafanikio tunayoyapata kutokana na utendaji wao mahiri na thabiti. Nawaomba waendeleze mashirikiano haya na kuendelea kuwatumikia wananchi wetu. Namuomba Mwenyezi Mungu adumishe mapenzi na mashirikiano baina yetu katika kutekeleza majukumu yetu.

59. Mheshimiwa Spika; Naomba kutoa hoja.
  Ahsanteni.
  
MHE. DKT. MAUDLINE CYRUS CASTICO (MBM)
WAZIRI WA KAZI, UWEZESHAJI, WAZEE, WANAWAKE NA WATOTO
ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.