SERIKALI
YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR
MUKHTASARI
WA HOTUBA YA WAZIRI WA NCHI,
OFISI
YA RAIS TAWALA ZA MIKOA, SERIKALI ZA
MITAA NA
IDARA MAALUM ZA SMZ
MHE. HAJI
OMAR KHERI (MBM)
KUHUSU
MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA
MWAKA
WA FEDHA 2020/2021
KATIKA
BARAZA LA WAWAKILISHI LA ZANZIBAR
MEI, 2020
1
Yaliyomo
i
MUKHTASARI WA HOTUBA YA
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA, SERIKALI ZA MITAA NA IDARA
MAALUM ZA SMZ, MHE. HAJI OMAR KHERI KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA
MWAKA WA FEDHA 2020/2021
UTANGULIZI
1.
Mheshimiwa Spika, naomba
kutoa hoja kwamba Baraza lako Tukufu likae kama Kamati kwa madhumuni ya
kupokea, kujadili na hatimaye kuidhinisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya
Fedha kwa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za
SMZ kwa mwaka wa fedha 2020/2021.
2.
Mheshimiwa Spika, awali ya
yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu Muumba Mbingu na Ardhi kwa
kutujaalia uhai na uzima na kutuwezesha kukutana hapa leo katika Baraza hili
Tukufu tukiwa salama katika hali ya amani na utulivu. Tunamuomba Mwenyezi Mungu
atuzidishie neema zake za uhai, atuzidishie amani na utulivu na atuondoshee
janga la maradhi ya corona.
3.
Mheshimiwa Spika, baada ya
kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu, naomba kutumia nafasi hii adhimu kupitia
Baraza lako Tukufu kumshukuru na kumpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dk. Ali Mohamed Shein kwa uadilifu na uongozi
wake wenye busara na hekima ambao umeiwezesha nchi yetu kuwa katika hali ya
amani na utulivu. Uongozi wake mahiri umekuwa dira sahihi katika kuleta mabadiliko
ya kweli ambayo Wazanzibari sote tunayashuhudia katika nyanja mbali mbali
ikiwemo Elimu, Afya, Kilimo, Miundombinu na kuongezeka kwa pato la Taifa na
maslahi ya Watumishi.
4.
Mheshimiwa Spika, pongezi
maalum kwa Mheshimiwa Rais kwa jinsi alivyoweza kutoa maelekezo na kufanya
maamuzi magumu katika kupambana na janga la maradhi ya corona kwa faida na
maslahi ya Taifa. Napenda kumuahidi Mimi Binafsi na Viongozi wenzangu katika
Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum tutaendelea
kumuunga mkono na kufuata maelekezo yake
katika kuhakikisha ugonjwa huu hauenei na
unaondoka kwenye Mikoa, Wilaya na
Shehia. Aidha, nawasisitiza wananchi kufuata maelekezo ya Serikali na Wataalamu
wa afya ili kuyashinda maradhi haya.
5.
Mheshimiwa Spika, nachukua
nafasi hii pia kumpongeza Makamu wa Pili wa Rais, Mheshimiwa Balozi Seif Ali
Iddi kwa kuendelea kumshauri vyema Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi sambamba na kuendelea kuongoza vyema shughuli za Serikali
katika Baraza la Wawakilishi na kusimamia vyema utekelezaji wake. Nichukue
fursa hii kukupongeza wewe Mheshimiwa Spika kwa jinsi ulivyo mahiri kuliongoza
Baraza hili Tukufu kwa hekima, busara na uweledi mkubwa. Uongozi wako
umeliwezesha Baraza hili kutimiza kikamilifu jukumu lake la kusimamia na
kuishauri Serikali. Nimpongeze pia Mheshimiwa Naibu Spika na Wenyeviti wa
Baraza kwa kukusaidia kuliongoza vyema Baraza la Wawakilishi. Aidha, natoa pongezi maalum kwa Kamati ya Sheria,
Utawala Bora na Idara Maalum chini ya Mwenyekiti wake Mheshimiwa Machano Othman
Said Mwakilishi wa Wananchi Jimbo la Mfenesini.
6.
Mheshimiwa Spika, wakati
nchi yetu ikiwa katika taharuki ya kupambana na kujikinga na maambukizi ya
virusi vya corona (COVID 19), naomba nichukue fursa hii kuwanasihi wananchi
wote wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla kuendelea kuchukua tahadhari dhidi ya
ugonjwa huu, naomba tuendelee kufuata maelekezo yanayotolewa na Serikali ili
kujikinga na madhara yatokanayo na ugonjwa huu. Aidha, naomba kutoa salamu
zangu za pole kwa wananchi wote ambao wamepoteza jamaa zao kwa madhara ya
maradhi
ya corona, sote kwa umoja
wetu tumuombe Mwenyezi Mungu kwa rehema zake atuondoshee maradhi haya ili
tuendelee kuijenga nchi yetu.
7.
Mheshimiwa Spika, baada ya
utangulizi huo, sasa naomba uniruhusu niwasilishe utekelezaji wa Programu za
Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ kwa
kipindi cha Julai hadi Machi 2019/2020.
MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA BAJETI
KWA MWAKA WA
FEDHA 2019/2020
8.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2019/2020,
Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ kwa
ujumla imetekeleza mambo yafuatayo;
A. TAWALA ZA MIKOA NA
SERIKALI ZA MITAA
9.
Mheshimiwa Spika, katika
kusimamia utekelezaji wa Mpango wa Upelekaji Madaraka kwa wananchi (Ugatuzi),
Ofisi imefanikiwa kukamilisha muundo wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa,
muundo huo unajumuisha uanzishaji wa Idara tano zinazounda Sekreterieti za
Mikoa, Idara sita za Mamlaka za Serikali za Mitaa na Mabaraza ya Wadi na Kamati
za Mashauriano za Shehia. Kwa upande wa Rasilimali watu Ofisi imeweza kuongeza
watumishi wapya 932 wakiwemo walimu 673, wahudumu wa afya 93 na Mabwana shamba
na Mabibi shamba 166. Aidha, uteuzi wa Wasaidizi Makatibu Tawala Mikoa 25 na Wasaidizi Wakurugenzi 66
umefanyika na wameanza kutekeleza majukumu yao katika Tawala za Mikoa na
Serikali za Mitaa. Kwa upande wa fedha, Serikali kuu imeongeza kiwango cha
ruzuku kwa matumizi mengineyo katika Serikali za Mitaa kutoka shilingi
8,702,800,000 kwa mwaka 2018/2019 na kufikia shilingi 11,014,260,000 kwa mwaka
2019/2020 sawa na ongezeko la asilimia 27.
10.
Mheshimiwa Spika, mafanikio
ya ugatuzi kwa wananchi yamezidi kuimarika ambapo Serikali za Mitaa
zimetekeleza miradi 61 ya maendeleo yenye thamani ya shilingi 1,697,359,323 katika maeneo ya wadi mbali mbali. Miradi
hiyo imehusisha ujenzi wa madarasa mapya 72, matengenezo ya skuli 43 na ujenzi
wa matundu ya vyoo 133. Kwa upande wa huduma za Afya, Ofisi imesimamia
matengenezo ya vituo 29 vya afya, matengenezo hayo yanajumuisha uwekaji wa
maji, umeme na mapaa. Huduma za mama na mtoto zimeimarishwa ambapo kinamama
wanaojifungulia katika vituo vya Afya wameongezeka na kupunguza idadi ya vifo
vinavyotokana na uzazi kutoka asilimia 55 hadi asilimia 41. Aidha, katika
kuimarisha huduma za ugani jumla ya wananchi 19,912 wamepatiwa mafunzo ya
kisasa ya kilimo, mifugo na uvuvi.
11.
Mheshimiwa Spika, katika
kuendeleza matengenezo ya barabara za ndani, Ofisi imewasilisha Serikalini
Mpango wa miaka mitano wa matengenezo ya barabara za ndani pamoja na makisio
yake ya bajeti ambapo Serikali imeridhia asilimia 40 ya bajeti ya Mfuko wa
barabara kutumika katika matengenezo ya barabara za ndani na utekelezaji wake
unatarajiwa kuanza katika mwaka wa fedha 2020/2021. Mpango huu utasaidia
kutatua changamoto za matengenezo ya barabara za ndani na kuiwezesha Ofisi
kuongeza idadi ya kilomita za barabara za ndani zitazojengwa katika Wilaya.
Vilevile, Ofisi imeajiri Mshauri Elekezi kwa ajili ya kuzifanyia tathmini
barabara zote za ndani za Zanzibar na kuzigawa kwa mujibu wa madaraja ya Wilaya
na Vijiji.
12.
Mheshimiwa Spika, Hadi
kufikia Machi, 2020 Ofisi imekamilisha matengenezo ya barabara ya Tume ya
Uchaguzi yenye urefu wa kilomita 0.22 na barabara ya Skuli ya Kinuni yenye
urefu wa kilomita 0.95. Kwa upande wa Pemba, ujenzi ya Barabara ya Gombani –
Pagali yenye urefu wa kilomita 1.8 unaendelea katika hatua ya mwisho ya
kuwekewa lami.
Aidha, Ofisi inakamilisha
matengenezo ya Barabara ya Fuoni Mambosasa hadi Mwera Wilayani yenye urefu wa
kilomita 3.4 kwa kiwango cha lami. Barabara hizo zinapitia katika maeneo ambayo
yanaishi idadi kubwa ya watu, hivyo kukamilika kwa ujenzi huo wa barabara
utarahisisha upatikanaji wa huduma za kijamii na kiuchumi, kupunguza msongamano
wa gari katika barabara kuu, kuongeza haiba ya mji na kupunguza masafa kutoka
sehemu moja kwenda sehemu nyengine.
13.
Mheshimiwa Spika, Tawala
za Mikoa zimeratibu utoaji na usimamizi wa huduma za ustawi wa jamii kwa
makundi maalum ya watu wakiwemo wazee wasiojiweza 5,492 ambapo jumla ya shilingi 319,670,000 zimetumika katika
kuwasaidia wazee. Aidha, kupitia kifungu maalum cha bajeti cha Waheshimiwa
Wakuu wa Mikoa, watu wenye ulemavu, wenye kuishi mazingira magumu na waliofikwa
na matatizo mbali mbali ya kifamilia wameweza kupatiwa misaada mbalimbali ya
matibabu, vifaa vya skuli, vifaa vya ujenzi na kujikimu kimaisha.
14.
Mheshimiwa Spika, Mikoa
imeendelea kudhibiti na kusuluhisha migogoro ya ardhi kwa kuhakikisha kuwa
masuala yanayohusiana na migogoro ya ardhi yanashughulikiwa na kupatiwa
ufumbuzi kwa mujibu wa Sheria, Kanuni na taratibu zilizopo. Kwa kipindi cha
Julai hadi Machi 2019/2020, jumla ya migogoro 196 ya ardhi iliyohusisha umiliki
wa mashamba, viwanja na mipaka imeripotiwa katika Ofisi za Mikoa na Wilaya
Unguja na Pemba. Kati ya migogoro hiyo, migogoro 105 imepatiwa ufumbuzi katika
ngazi ya Wilaya na Mikoa, 14 imepelekwa Mahakama ya Ardhi na 77 inaendelea
kupatiwa ufumbuzi kwa kushirikiana na Kamisheni ya Ardhi, Wizara ya Kilimo,
Maliasili, Mifugo na Uvuvi na Kamisheni ya Wakf na Mali ya Amana.
15.
Mheshimiwa Spika, suala la
kupambana na udhalilishaji wa kijinsia limeendelea kupewa umuhimu mkubwa katika
utekelezaji wa majukumu ya Tawala za Mikoa. Jitihada mbali mbali zimeendelea
kufanyika katika ngazi za Mikoa, Wilaya na Shehia ili kuhakikisha matukio hayo
yanapungua na hatimae yanaondoshwa kabisa. Miongoni mwa jitihada zinazofanyika
ni pamoja na kutoa elimu kwa jamii na kufuatilia matukio yaliyoripotiwa katika
ngazi mbali mbali za kisheria. Kwa kipindi cha Julai hadi Machi 2019/2020,
jumla ya matukio 1,060 ya udhalilishaji yameripotiwa ndani ya Mikoa. Kati ya
hayo, matukio 501 yapo katika hatua ya upelelezi wa Polisi, 119 yamepelekwa
Mahakamani ambapo 45 yameshatolewa hukumu, matatu yamefutwa na matukio 71
yanaendelea kusikilizwa. Aidha, matukio 29 yamepelekwa Ofisi ya Mkurugenzi wa
Mashtaka (DPP), 343 yamepatiwa ufumbuzi katika ngazi za Wilaya na 23
yanaendelea na ufumbuzi Wilayani.
B. IDARA MAALUM ZA SMZ
16.
Mheshimiwa Spika, Maofisa
187 wa Idara Maalum wamejengewa uwezo kwa kupatiwa mafunzo ya msingi kwa mujibu
wa vyeo vyao na nafasi zao kazini pamoja na mafunzo maalum (msasa). Kati yao,
Maofisa 49 (32 KVZ na 17 JKU) walipewa mafunzo ya ‘Platoon Commander’ ambapo
maafisa wanne hawakufaulu mafunzo hayo; Maofisa 53 (28 KZU na 25 MF) walipatiwa
mafunzo ya ‘Special Course’; Maofisa 35 (22 KZU na 13 MF) walipatiwa mafunzo ya
‘Advanced Course’ na Maofisa 50 wa KMKM walipatiwa mafunzo ya ‘Specialization’
ambapo Afisa mmoja hakufaulu mafunzo hayo. Mafunzo yaliyotolewa yamewawezesha
Maofisa kuwa na uwezo wa kutekeleza vyema majukumu yao kama ilivyokusudiwa
kuanzishwa kwa mpango huu maalum wa mafunzo katika Idara Maalum za SMZ. Aidha,
mafunzo hayo yameimarisha utayari wa Idara Maalum katika kusimamia majukumu ya
ulinzi na usalama nchini.
17.
MheshimiwaMwenyekiti,Ofisi imeratibu uajiri wa askari wapya 3,000 wakiwemo wataalamu wa
fani mbali mbali 600 na kupatiwa mafunzo ya awali ya uaskari kwa muda wa miezi
sita katika vyuo vya Idara Maalum za SMZ. Askari 2,990 waliweza kumaliza
mafunzo yao ya awali na kugaiwa katika kila Idara Maalum. Hatua inayofuata ni
kupata mafunzo ya miezi mitatu kulingana na majukumu na utendaji kazi wa Idara
Maalum husika. Uajiri huu utaziwezesha Idara Maalum za SMZ kutekeleza majukumu
yake kwa ufanisi na kuongeza wataalam wapya kwenye Idara na Vitengo vya Idara
Maalum za SMZ. Aidha, uajiri huo umesaidia kupunguza changamoto za ajira kwa
vijana na kuwawezesha vijana hao kutumika katika kuimarisha shughuli za ulinzi
na usalama katika
Taifa.
18.
Mheshimiwa Spika, katika
utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika
Idara Maalum za SMZ, Ofisi imesimamia ujenzi wa Mahanga, nyumba na Ofisi uliotekelezwa
kwa kila kikosi. Kwa upande wa
KMKM imefanya ujenzi wa Kambi ya KMKM Micheweni ambapo ujenzi huu upo katika
hatua ya kuezeka paa. KVZ imejenga hanga
moja na nyumba ya Mkuu wa Zoni Pemba katika kambi ya Ndugukitu ambapo ujenzi
upo hatua ya kuezeka paa. Majengo manne
katika Kambi ya Chuo cha Mafunzo Kangagani yameezekwa upya na kazi za uwekaji
wa milango, madirisha pamoja na miundombinu ya maji zinaendelea. Ujenzi wa
Majengo ya Kambi za JKU Msaani upo katika hatua ya kuezeka kwa mahanga mawili
na bwalo moja la chakula. Aidha, ujenzi wa jengo la Kituo cha Zimamoto
Kijichame umekamilika ghorofa ya kwanza na kazi ya uwekaji wa mfumo wa maji na
umeme inaendelea. Kukamilika kwa ujenzi wa mradi wa mahanga, nyumba na Ofisi
katika kambi za Idara Maalum utasaidia kuimarisha mazingira bora ya kazi na
makaazi ya Maofisa na Wapiganaji wa Idara Maalum za SMZ.
C. MAMBO
MAALUM YALIYORATIBIWA
19.
Mheshimiwa Spika, katika
kuanzisha Jiji la Zanzibar, mnamo tarehe 6 Agosti, 2019 Mheshimiwa Rais wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi alimteua Mkurugenzi wa Jiji na
hivyo kuanzisha rasmi Jiji la Zanzibar kwa mujibu wa kifungu cha 18 (1) cha
Sheria Namba 7/2014 ya Mamlaka za Serikali za Mitaa. Zanzibar kwa mara ya
kwanza baada ya Mapinduzi Matukufu ya Januari 1964 imeanzisha Jiji lake ambalo
litaipandisha hadhi Zanzibar katika nyanja tofauti hususan utalii. Zanzibar
ilikosa uwakilishi mzuri kwenye sura ya Kimataifa ya Majiji na hivyo kupoteza
nafasi ya uwakilishi mpana kwenye mambo mengi ya kimaendeleo yanayofanywa
kwenye Mataifa duniani. Hongera kwa Mheshimiwa Rais Dkt Ali Mohammed Shein kwa
kuliona jambo hili na hivyo kuanzisha Jiji la Zanzibar. Hii ni hatua muhimu ya
kuiweka Zanzibar katika ramani ya dunia yenye mnasaba wa kutatua changamoto za
maendeleo ya nchi na wananchi wake. Uwepo wa Jiji ni kiashiria cha ukuaji wa
uchumi, upatikanaji wa huduma muhimu za kijamii, upanuzi wa huduma na
miundombinu ya kiuchumi na utayari wa Serikali kuendeleza mipango mipana na
miradi mikubwa zaidi ya maendeleo kwa wananchi wake.
20.
Mheshimiwa Spika, katika
utekelezaji wa miradi ya maendeleo, Ofisi imeendelea kufanya malipo ya kila
mwezi ya Mradi wa Mji Salama kwa mujibu wa masharti ya mkataba. Kupitia mradi
huu jumla ya matukio ya kihalifu 214 yalibainika na kuchukuliwa hatua za
kisheria. Matukio 80 yalihusu wizi, matukio 122 ajali za barabarani, saba
utapeli wa mali na matano yalihusu matumizi haramu ya dawa za kulevya. Aidha,
shughuli za uendelezaji wa Mradi wa Mji Salama kwa Miji ya Mkoani, Chake Chake
na Wete zimekamilika kwa kuchimba mashimo na ujenzi wa kangriti kwa ajili ya
uwekaji wa nguzo za kamera za usalama. Kazi inayoendelea kwa sasa ni matayarisho
ya uwekaji wa waya na kusimamisha nguzo za kamera.
21.
Ofisi
imeendelea kuviimarisha vituo vya uokozi viliopo Kibweni, Nungwi na Mkoani.
Vituo hivyo vimefungwa vifaa maalum vya mawasiliano na kuweza kuwa na mifumo
mitatu ijulikanayo kwa majina ya VMS, Sea Vision na Find Ship. Mifumo hii
imekuwa na faida nyingi zikiwemo upatikanaji wa taarifa kwa urahisi kutoka
kwenye vyombo vya baharini na wananchi
na kuimarisha mashirikiano baina ya KMKM na ZMA, MRCC pamoja na vyombo vya
ulinzi vya Jamuhuri ya Muungano Tanzania hususan Jeshi la Wananchi Tanzania na
Uhamiaji. Hivyo uwepo wa vituo vya uokozi kunahakikisha upatikanaji wa huduma
za uokozi, uzamiaji na ulinzi wa nchi na kuepusha majanga ya uzamaji wa vyombo
vya baharini na athari za maisha ya wananchi.
22.
Mheshimiwa Spika, Ofisi
imesimamia utaratibu ulioanzishwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wa
kusimamia upatikanaji wa rasilimali ya mchanga kwa wananchi. Utaratibu huo
unawataka wananchi wanaohitaji mchanga kujaza fomu maalum za maombi ambazo
zinapatikana kwenye ngazi ya Shehia wakielezea malengo, mahala, na kiwango cha
mchanga. Lengo la utaratibu huo ni kupunguza uharibifu wa kimazingira, kuweka
usimamizi bora wa upatikanaji wa mchanga na kusimamia matumizi bora ya mchanga
nchini. Mkoa kwa kushirikiana na Idara ya Misitu na Maliasili zisizorejesheka
umeendelea kusimamia mpango wa Serikali katika kudhibiti rasilimali ya mchanga
kwa kufanya operesheni maalum na kukagua magari yanayobeba mchanga kwa lengo la
kuhakikisha taratibu zinafuatwa.
23.
Mheshimiwa Spika, Ofisi ya
Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ imeshiriki
kikamilifu katika kupambana na maradhi ya Corona (COVID19) kwa kushirikiana na
Wizara ya Afya na Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar. Ofisi
imetekeleza mikakati ya kupambana na COVID19 ikiwemo kuanzisha kambi za
karantini katika kila Wilaya ambapo jumla ya wananchi 715 walioingia kupitia
bandari zisizo rasmi waliwekwa karantini na vyombo saba vilivyobeba abiria
kinyume na utaratibu vimekamatwa. Aidha, Ofisi kupitia Tawala za Mikoa
imesimamia wafanyabiashara kuweka vitakasa mikono katika maeneo yao ya
biashara, kupunguza misongomano katika masoko na shughuli za kijamii ikiwemo
maziko na harusi, kuwafuatilia wageni wote wanaoingia na kutoka katika Shehia
na kuelimisha wananchi juu ya kujikinga na maradhi kupitia njia za radio,
televisheni, vipeperushi na matangazo.
D. UPATIKANAJI WA FEDHA
24.
Mheshimiwa Spika, kwa
mwaka wa fedha 2019/2020, Ofisi iliidhinishiwa kiasi cha shilingi 208,218,000,000. Kati ya fedha hizo, shilingi 80,113,100,000 mishahara, shilingi 26,919,660,000 matumizi mengineyo, shilingi 77,390,000,000 ruzuku kwa Tume ya Utumishi ya Idara Maalum
za SMZ, Wakala wa Ulinzi JKU na Mamlaka za Serikali za Mitaa na shilingi 23,795,240,000 kwa kazi za
maendeleo ikijumuisha shilingi
785,240,000 mchango kutoka kwa Washirika wa Maendeleo. Hadi kufikia Machi
2020, Ofisi iliingiziwa shilingi
161,172,240,898 sawa na asilimia 77 ya makadirio ya mwaka. Kati ya fedha
hizo, shilingi 65,346,633,845 sawa
na asilimia 82 ni mishahara, shilingi
19,351,608,936 sawa na asilimia 72 matumizi mengineyo, shilingi 59,166,932,761 sawa na asilimia 76 ni ruzuku kwa Tume ya
Utumishi ya Idara Maalum, Wakala wa Ulinzi JKU na Mamlaka za Serikali za Mitaa
na shilingi 17,471,441,356 sawa na
asilimia 73 kwa kazi za maendeleo.
25.
Mheshimiwa Spika, kwa
upande wa mapato, Ofisi iliidhinishiwa kukusanya shilingi 1,867,667,000 kwa ajili ya kuchangia Mfuko Mkuu wa
Serikali na kukusanya shilingi
1,018,557,468 sawa na asilimia 55 ya makadirio ya mwaka. Kwa upande wa
Mamlaka za Serikali za Mitaa zilikadiriwa kukusanya shilingi 13,260,003,546 na kukusanya shilingi
9,781,317,531 sawa na asilimia 74 ya
makadirio ya mwaka.
26.
baada
ya utekelezaji wa ujumla wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa
na Idara Maalum za SMZ, nawaomba Waheshimiwa Wajumbe waangalie ukurasa wa 12
hadi wa 87 katika kitabu cha Hotuba ya Bajeti kwa utekelezaji mahsusi wa
programu za Fungu D01 hadi Fungu D12.
MWELEKEO KWA MWAKA WA FEDHA
2020/2021
27. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2020/2021, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa,
Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ imepanga kutekeleza vipaumbele
vifuatavyo;
A. TAWALA ZA MIKOA NA
MAMLAKA ZA SERIKALI ZA MITAA
i.
Kuimarisha
Amani, Utulivu na Usalama katika Mikoa, Wilaya na Shehia hasa ikizingatiwa
Taifa linaelekea kwenye uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020.
ii.
Kuimarisha
mfumo wa ukusanyaji wa mapato ya Serikali za Mitaa kwa kuhakikisha kila
Halmashauri inakuwa na “electronic database” ya vyanzo vyote vya mapato na
Walipa Kodi.
iii.
Kusimamia
utekelezaji wa majukumu ya Jiji la Zanzibar ili kuufanya mji wa Zanzibar kuwa
mji wa kisasa na kivutio cha utalii.
iv.
Kuondosha
msongamano na vurumai kwenye masoko ya Mwanakwerekwe, Mombasa na Darajani na
kuwahamishia baadhi ya wafanyabiashara katika Soko la Saateni na maeneo
mengine.
v.
Kuhamisha
daladala Michenzani na kuzipeleka katika Kituo cha daladala Kijangwani kwa
kushirikiana na Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji.
vi.
Kuajiri
Makatibu wa Wadi na Shehia ili kuwezesha Mabaraza ya Wadi na Kamati za
Mashauriano za Shehia kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria.
vii.
Kuendeleza
uwekaji wa anuani za mitaa (postcode) katika maeneo ya Miji.
B. IDARA MAALUM ZA SMZ
i.
Kuimarisha
Kambi na Makaazi ya Idara Maalum za SMZ kwa kuendeleza ujenzi wa majengo ya
Ofisi, nyumba za Maafisa na Mahanga ya Wapiganaji.
ii.
Kuimarisha
Vyuo vya mafunzo vya Idara Maalum za SMZ ili kuviwezesha kutoa mafunzo kwa
Maafisa na Wapiganaji wa ngazi zote.
iii.
Kuimarisha
Kiwanda cha kushona sare na viatu cha Idara Maalum KVZ – Mtoni kuanza kazi na
uzalishaji.
iv.
Kuanza
ujenzi wa Kituo cha Mafunzo ya Uzamiaji KMKM Kama.
v.
Kuendelea
na utekelezaji wa mradi wa Mji Salama kwa upande wa Pemba katika Miji ya Chake
Chake, Wete na Mkoani na maeneo mengine ya Unguja.
vi.
Kuimarisha
huduma za zimamoto na uokozi kwa kununua gari za zimamoto pamoja na kufanya
upembuzi yakinifu wa uanzishaji wa Chuo cha kisasa cha Zimamoto na Uokozi.
vii.
Kuimarisha
uzalishaji wa chakula na kuanzisha mashamba ya mifugo kwa Chuo cha Mafunzo na
Jeshi la Kujenga Uchumi-JKU
C. MAMBO MAALUM KWA
OFISI
viii. Kuandaa rasimu ya sera mpya ya Serikali za
Mitaa yenye kuzingatia kiukamilifu dhana ya ugatuzi na ushirikishwaji wa
wananchi katika Serikali za Mitaa.
ix.
Kuandaa
Mpango Maalum wa Utafiti wa Ofisi kwa kushirikiana na Taasisi za Utafiti za SMZ
na COSTECH.
x.
Kuimarisha
Mfumo wa Usajili na Uratibu wa Jumuiya zisizo za Kiserikali (NGOs) kwa lengo la
kuwa na NGOs zenye tija na maslahi ya Nchi na Wananchi.
xi.
Kuimarisha
mfumo wa usajili wa matukio ya kijamii kwa kuhakikisha huduma ya usajili wa
vizazi, vifo, ndoa na talaka vyeti vyake vinapatikana katika Ofisi ndogo za
kila Wilaya.
xii.
Kuendeleza
ujenzi wa barabara za ndani kwa kiwango cha
lami pamoja na kuandaa
andiko la mradi litalochambua na kuainisha barabara zote za ndani Zanzibar.
28.
Mheshimiwa Spika, baada ya
mukhtasari huo wa mwelekeo wa vipaombele vya Ofisi, naomba kuwasilisha mwelekeo
wa bajeti ya Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum
za SMZ kwa mwaka wa fedha 2020/2021 kwa kila fungu.
29.
Mheshimiwa Spika, kwa
mwaka wa fedha 2020/2021, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na
Idara Maalum za SMZ itaendelea kutekeleza Programu Kuu 18 kupitia Mafungu 12
yaliyoanzia D01-D12. Fungu D01 limepangiwa kuetekeleza programu kuu tatu;
Mafungu (D02–D06) yamepangiwa kutekeleza programu kuu mbili kwa kila mmoja;
Mafungu (D07-D11) yamepangiwa kutekeleza programu kuu tatu kwa kila mmoja na
Fungu (D12) limepangiwa kutekeleza programu kuu mbili.
PROGRAMU ZA OFISI KUU FUNGU-D01
30.
Mheshimiwa Spika, kwa
mwaka wa fedha 2020/2021, Fungu D01 litatekeleza Programu Kuu tatu ambazo ni
Programu ya Usimamizi na Uendeshaji wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali
za Mitaa na Idara Maalum za SMZ, Programu ya Uratibu wa Tawala za Mikoa na
Serikali za Mitaa na Programu ya Usimamizi wa Utumishi na Uratibu wa Idara
Maalum za SMZ.
31.
Mheshimiwa Spika, kwa
maelezo zaidi ya mwelekeo wa Programu za Fungu D01, nawaomba Waheshimiwa
Wajumbe waangalie ukurasa wa 90 hadi wa 93 katika kitabu cha Hotuba ya Bajeti.
32.
Mheshimiwa Spika, ili
programu zilizo chini ya Fungu D01 ziweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi,
kwa mwaka wa fedha 2020/2021, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya shilingi 28,451,630,000. Kati ya fedha
hizo, shilingi 1,740,900,000 kwa
ajili ya mishahara, shilingi
11,025,800,000 kwa matumizi mengineyo ikijumuisha shilingi 261,100,000 mchango kutoka kwa Washirika wa Maendeleo, shilingi 1,288,700,000 kwa ajili ya
ruzuku ya Tume ya Utumishi ya Idara
Maalum na Wakala wa Ulinzi JKU na shilingi 14,396,230,000 kwa kazi za maendeleo.
Aidha, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe makusanyo ya shilingi 832,800,000 kuchangia Mfuko
Mkuu wa Serikali.
PROGRAMU ZA IDARA MAALUM ZA SMZ - FUNGU
(D02-D06)
33.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2020/2021,
Idara Maalum za SMZ zitaendelea kutekeleza majukumu yake kupitia Programu Kuu
mbili zitakazotekelezwa kwa kila Fungu kuanzia Fungu D02 hadi D06 na kufanya
jumla ya Programu zitakazotekelezwa na
Idara Maalum zote kuwa 10. Maelezo yafuatayo yanahusu mwelekeo wa utekelezaji
wa Programu za Idara Maalum za SMZ kwa kila Fungu.
JESHI LA KUJENGA UCHUMI (JKU)- FUNGU D02
34.
Mheshimiwa Spika, kwa
mwaka wa fedha 2020/2021, Jeshi la kujenga Uchumi litatekeleza Programu kuu
mbili ambazo ni Programu ya Mafunzo kwa Vijana na Uzalishajimali na Programu ya
Utawala na Uendeshaji wa JKU.
35.
Mheshimiwa Spika, kwa
maelezo zaidi ya mwelekeo wa Programu za Fungu D02, nawaomba Waheshimiwa
Wajumbe waangalie ukurasa wa 94 katika kitabu cha Hotuba ya Bajeti.
36.
Mheshimiwa Spika, ili
Jeshi la Kujenga Uchumi kwa mwaka wa fedha 2020/2021 liweze kutekeleza Programu
zake kwa ufanisi, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya shilingi 31,557,600,000. Kati ya fedha
hizo, Shilingi 24,066,000,000 kwa
ajili ya mishahara, shilingi
2,991,600,000 kwa matumizi mengineyo na shilingi 4,500,000,000 kwa kazi za maendeleo. Aidha, naliomba
Baraza lako Tukufu liidhinishe makusanyo ya Shilingi 87,224,000 kuchangia Mfuko Mkuu wa Serikali.
CHUO CHA MAFUNZO-FUNGU D03
37.
Mheshimiwa Spika, kwa
mwaka 2020/2021, Chuo cha Mafunzo kitatekeleza Programu kuu mbili ambazo ni
Programu ya Urekebishaji Tabia kwa Wanafunzi na Programu ya Utawala na
Uendeshaji wa Chuo cha Mafunzo.
38.
Mheshimiwa Spika, kwa
maelezo zaidi ya mwelekeo wa Programu za Fungu D03, nawaomba Waheshimiwa
Wajumbe waangalie ukurasa wa 95 katika kitabu cha Hotuba ya Bajeti.
39.
Mheshimiwa Spika, ili Chuo
cha Mafunzo kwa mwaka wa fedha 2020/2021 kiweze kutekeleza programu zake kwa
ufanisi, naliomba Baraza lako tukufu liidhinishe jumla ya shilingi 21,865,600,000. Kati ya fedha hizo shilingi 17,276,200,000 ni mishahara, shilingi 3,089,400,000 matumizi mengineyo na shilingi 1,500,000,000 kwa kazi za Maendeleo. Aidha, naliomba
Baraza lako tukufu liidhinishe makusanyo ya shilingi 75,720,000 ili kuchangia Mfuko Mkuu wa Serikali.
KIKOSI MAALUM CHA KUZUIA MAGENDO (KMKM)-FUNGU D04
40.
Mheshimiwa Spika, kwa
mwaka wa fedha 2020/2021, Kikosi Maalum cha Kuzuia Magendo (KMKM) kitatekeleza
Programu kuu mbili ambazo ni Programu ya Ulinzi na Uzuiaji wa Magendo na Programu
ya Utawala na Uendeshaji wa KMKM.
41.
Mheshimiwa Spika, kwa
maelezo zaidi ya mwelekeo wa Programu za Fungu D04, nawaomba Waheshimiwa
Wajumbe waangalie ukurasa wa 95 hadi wa 96 katika kitabu cha Hotuba ya Bajeti.
42.
Mheshimiwa Spika, ili
Kikosi Maalum cha Kuzuia Magendo kwa mwaka wa fedha 2020/2021 kiweze kutekeleza
Programu zake kwa ufanisi, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya shilingi 35,630,700,000. Kati ya fedha
hizo shilingi 24,543,900,000 kwa ajili ya mishahara, shilingi 5,586,800,000 kwa matumizi mengineyo na shilingi 5,500,000,000 kwa kazi za
Maendeleo. Aidha, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe makusanyo ya shilingi 60,542,000 ili kuchangia Mfuko
Mkuu wa Serikali.
KIKOSI
CHA ZIMAMOTO NA UOKOZI (KZU)-FUNGU D05
43.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka
wa fedha 2020/2021, Kikosi cha Zimamoto na Uokozi kitatekeleza Programu Kuu
mbili ambazo ni Programu ya Uzimaji moto na Uokozi na Programu ya Utawala na
Uendeshaji wa KZU.
44.
Mheshimiwa Spika, kwa
maelezo zaidi ya mwelekeo wa Programu za Fungu D05, nawaomba Waheshimiwa
Wajumbe waangalie ukurasa wa 96 hadi wa 97 katika kitabu cha Hotuba ya Bajeti.
45.
Mheshimiwa Spika, ili
Kikosi cha Zimamoto na Uokozi kwa mwaka wa fedha 2020/2021 kiweze kutekeleza
Programu zake kwa ufanisi, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya shilingi 16,795,900,000. Kati ya fedha
hizo, shilingi 11,852,000,000 kwa
ajili ya mishahara, shilingi
2,443,900,000 kwa matumizi mengineyo na shilingi 2,500,000,000 kwa kazi za maendeleo. Aidha, naliomba
Baraza lako Tukufu liidhinishe makusanyo ya shilingi 45,700,000 na kuchangia Mfuko Mkuu wa Serikali.
KIKOSI
CHA VALANTIA ZANZIBAR (KVZ) – FUNGU D06
46.
Mheshimiwa Spika, kwa
mwaka wa fedha 2020/2021, Kikosi cha Valantia Zanzibar kitatekeleza Programu
Kuu mbili ambazo ni Programu ya Ulinzi wa Nchi, Raia na Mali zao na Programu ya
Utawala na Uendeshaji.
47.
Mheshimiwa Spika, kwa
maelezo zaidi ya mwelekeo wa Programu za Fungu D06, nawaomba Waheshimiwa
Wajumbe waangalie ukurasa wa 97 hadi wa 98 katika kitabu cha Hotuba ya Bajeti.
48.
Mheshimiwa Spika, ili
Kikosi cha Valantia kwa mwaka wa fedha 2020/2021 kiweze kutekeleza Programu
zake kwa ufanisi, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya shilingi 20,135,000,000. Kati ya fedha
hizo, shilingi 15,975,100,000 kwa
ajili ya mshahara, shilingi
2,659,900,000 matumizi mengineyo na shilingi
1,500,000,000 kwa kazi za maendeleo.
PROGRAMU ZA TAWALA ZA MIKOA NA
SERIKALI ZA
MITAA - FUNGU (D07-D11)
49.
Mheshimiwa Spika, kutokana na kufanana kwa majukumu
ya Mikoa, Wilaya na Mamlaka za Serikali za Mitaa, Mikoa yote imepanga
kutekeleza shughuli zake chini ya Programu Kuu tatu ambazo ni Programu ya
Kusimamia Shughuli za Serikali katika Mkoa; Programu ya Uratibu na Uendeshaji
wa Tawala za Mikoa; na Programu ya Usimamizi na Uendeshaji wa Mamlaka za
Serikali za Mitaa. Maelezo yafuatayo yanahusu mwelekeo wa utekelezaji wa
Programu za Tawala za Mkoa kwa kila Fungu kuanzia fungu D07-D11.
MKOA WA MJINI MAGHARIBI– FUNGU D07
50.
Mheshimiwa Spika, kwa
maelezo zaidi ya mwelekeo wa Programu zitazotekelezwa na Fungu D07 la Mkoa wa
Mjini Magharibi pamoja na Jiji la Zanzibar, Baraza la Manispaa Mjini, Baraza la
Manispaa Magharibi ‘A’ na Baraza la Manispaa Magharibi ‘B’ nawaomba Waheshimiwa
Wajumbe waangalie ukurasa wa 98 hadi wa 101 katika kitabu cha Hotuba ya Bajeti.
51.
Mheshimiwa Spika, ili Mkoa
wa Mjini Magharibi kwa mwaka wa fedha 2020/2021 uweze kutekeleza Programu zake
kwa ufanisi, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya shilingi
35,826,000,000. Kati ya fedha hizo, shilingi
1,653,600,000 ni mishahara, shilingi
1,749,650,000 matumizi mengineyo na shilingi
32,422,750,000 ni ruzuku kwa Jiji la Zanzibar, Baraza la Manispaa Mjini,
Baraza la Manispaa Magharibi ‘A’ na Baraza la Manispaa Magharibi ‘B’. Aidha,
naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe makusanyo ya shilingi 125,000,000 ili kuchangia Mfuko Mkuu wa
Serikali.
MKOA WA KUSINI UNGUJA – FUNGU D08
52.
Mheshimiwa Spika, kwa
maelezo zaidi ya mwelekeo wa Programu za Fungu D08 la Mkoa wa Kusini Unguja
pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Kusini na Halmashauri ya Wilaya ya Kati
nawaomba Waheshimiwa Wajumbe waangalie ukurasa wa 101 hadi wa 103 katika kitabu
cha Hotuba ya Bajeti.
53.
Mheshimiwa Spika, ili Mkoa
wa Kusini Unguja kwa mwaka wa fedha 2020/2021, uweze kutekeleza programu zake
kwa ufanisi, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya shilingi 14,068,800,000. Kati ya fedha
hizo shilingi 1,369,900,000 ni
mishahara, shilingi 758,630,000 kwa
matumizi mengineyo na shilingi
11,940,270,000 ni Ruzuku za Halmashauri ya Wilaya ya Kusini na Halmashauri
ya Wilaya ya Kati. Aidha, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe makusanyo ya shilingi 50,750,000 na kuchangia Mfuko
Mkuu wa Serikali.
MKOA WA KASKAZINI UNGUJA – FUNGU D09
54.
Mheshimiwa Spika, kwa
maelezo zaidi ya mwelekeo wa Programu za Fungu D09 la Mkoa wa Kaskazini Unguja
pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini ‘A’ na Halmashauri ya Wilaya ya
Kaskazini ‘B’ nawaomba Waheshimiwa Wajumbe waangalie ukurasa wa 103 hadi wa 105
katika kitabu cha Hotuba ya Bajeti.
55.
Mheshimiwa Spika, ili Mkoa
wa Kaskazini Unguja kwa mwaka wa fedha 2020/2021, uweze kutekeleza Programu
zake kwa ufanisi, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya Shilingi 15,365,100,000. Kati ya fedha
hizo, shilingi 1,397,700,000 kwa
ajili ya mishahara, shilingi 770,500,000
kwa matumizi mengineyo na shilingi
13,196,900,000 kwa ajili ya Ruzuku ya Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini
‘A’ na Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini ‘B’. Aidha, naliomba Baraza lako
Tukufu liidhinishe makusanyo ya shilingi
27,500,000 ili kuchangia Mfuko Mkuu wa Serikali.
MKOA WA KUSINI PEMBA – FUNGU D10
56.
Mheshimiwa Spika, kwa
maelezo zaidi ya mwelekeo wa Programu za Fungu D10 la Mkoa wa Kusini Pemba
pamoja na Baraza la Mji Chake Chake na Baraza la Mji Mkoani, nawaomba
Waheshimiwa Wajumbe waangalie ukurasa wa 105 hadi wa 107 katika kitabu cha
Hotuba ya Bajeti.
57.
Mheshimiwa Spika, ili Mkoa
wa Kusini Pemba kwa mwaka wa fedha
2020/2021, uweze kutekeleza
Programu zake kwa ufanisi, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya shilingi
14,682,500,000. Kati ya fedha hizo, shilingi
1,124,200,000 ni mishahara, shilingi
994,690,000 matumizi mengineyo na shilingi
12,563,610,000 ni ruzuku kwa Baraza la Mji Chake Chake na Baraza la Mji
Mkoani. Aidha, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe makusanyo
ya shilingi 25,700,000 na kuchangia Mfuko Mkuu wa
Serikali.
MKOA WA KASKAZINI PEMBA – FUNGU D11
58.
Mheshimiwa Spika, kwa
maelezo zaidi ya mwelekeo wa Programu za Fungu D11 la Mkoa wa Kaskazini Pemba
pamoja na Baraza la Mji Wete na Halmashauri ya Wilaya ya Micheweni, nawaomba
Waheshimiwa Wajumbe waangalie ukurasa wa 107 hadi wa 108 katika kitabu cha
Hotuba ya Bajeti.
59.
Mheshimiwa Spika, ili Mkoa
wa Kaskazini Pemba kwa mwaka wa fedha 2020/2021 uweze kutekeleza Programu zake
kwa ufanisi, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya shilingi 13,408,940,000. Kati ya fedha
hizo, shilingi 1,226,400,000 kwa
ajili ya mishahara, shilingi
1,078,340,000 ni matumizi mengineyo na shilingi
11,104,200,000 ni ruzuku kwa Baraza la Mji Wete na Halmashauri ya Wilaya ya
Micheweni. Aidha, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe makusanyo ya shilingi
25,476,000 na kuchangia Mfuko Mkuu wa Serikali.
WAKALA WA USAJILI WA MATUKIO YA
KIJAMII –FUNGU D12
60.
Mheshimiwa Spika, kwa
mwaka wa fedha 2020/2021,
Ofisi ya Wakala wa Usajili
wa Matukio ya Kijamii itatekeleza Programu kuu mbili ambazo ni Programu ya
Usajili wa Matukio ya Kijamii na Programu ya Utumishi na Uendeshaji.
61.
Mheshimiwa Spika, kwa
maelezo zaidi ya mwelekeo wa Programu za Fungu D12, nawaomba Waheshimiwa
Wajumbe waangalie ukurasa wa 108 hadi wa 109 katika kitabu cha Hotuba ya
Bajeti.
62.
Mheshimiwa Spika, ili
Ofisi ya Wakala wa Usajili wa Matukio ya Kijamii iweze kutekeleza Programu zake
kwa ufanisi, naliomba Baraza lako tukufu kuidhinisha jumla ya shilingi 4,909,600,000. Kati ya fedha
hizo shilingi 1,475,000,000 kwa
ajili ya mishahara, shilingi
2,434,600,000 kwa matumizi mengineyo na shilingi 1,000,000,000 kwa kazi za maendeleo. Aidha, naliomba
Baraza lako Tukufu liidhinishe makusanyo ya shilingi 626,512,000 na kuchangia Mfuko Mkuu wa Serikali.
SHUKURANI
63.
Mheshimiwa Spika,
namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia kuwasilisha hotuba hii mbele ya
Baraza lako Tukufu kwa hekima na utulivu.
64.
Mheshimiwa Spika, napenda
kutoa Shukrani zangu za dhati kwa Waheshimiwa Mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar, Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Watumishi wa
Baraza la Wawakilishi kwa mashirikiano yao ya dhati waliyoyaonyesha katika
kipindi chote cha Baraza la Tisa la Wawakilishi. Mashirikiano na utendaji wao
umepelekea kufanikisha kwa uweledi utekelezaji wa majukumu ya Serikali na Ilani
ya Chama ya Mapinduzi.
65.
Mheshimiwa Spika, kwa
umuhimu wa kipekee naomba niwashukuru Wananchi wa Jimbo la Tumbatu kwa
kuniamini na kushirikiana nami katika kuliletea maendeleo Jimbo la Tumbatu.
Nawaahidi nitaendelea kwa moyo wangu wote kuzidi kushirikiana nao kwa hali na
mali kuwaletea maendeleo. Aidha, natumia fursa hii kuwapa pole waathirika wa
mvua za masika zinazoendelea kunyesha na kupelekea watu kupoteza maisha, mali
na makaazi. Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum
za SMZ iko pamoja nao katika kipindi hiki kigumu. Nachukua fursa hii kutoa wito
kwa wananchi kuchukua kila tahadhari
ili kuepukana na athari
zaidi zinazoweza kutokea ikiwemo maradhi ya mripuko.
HITIMISHO
66. Mheshimiwa Spika, naomba Waheshimiwa
Wajumbe wa Baraza lako Tukufu waipokee
na kuichangia hotuba hii na hatimae waidhinishe kwa Ofisi ya Rais, Tawala za
Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ kwa mwaka wa fedha 2020/2021
makadirio ya shilingi 252,697,370,000. Kati ya fedha hizo, shilingi 103,700,900,000 kwa ajili ya mishahara na maposho, shilingi 35,583,810,000 kwa matumizi
mengineyo, shilingi 82,516,430,000
ni ruzuku kwa Tume ya Utumishi ya Idara Maalum, Wakala wa Ulinzi wa JKU na
Mamlaka za Serikali za Mitaa, shilingi
30,896,230,000 kwa matumizi ya kazi za maendeleo. Aidha, nawaomba
Waheshimiwa Wajumbe waidhinishe mchango wa shilingi
1,982,924,000 ikiwa ni mapato yatakayoingizwa katika kuchangia Mfuko Mkuu
wa Serikali. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.
No comments:
Post a Comment