Habari za Punde

Maoni ya kamati ya Sheria, Utawala Bora na Idara Maalum kuhusu Makadirio na mapato ya TAMISEMI na Idara Maalum za SMZ



HOTUBA YA MAONI YA KAMATI YA SHERIA, UTAWALA BORA
NA IDARA MAALUM KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA
MATUMIZI YA OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA,
SERIKALI ZA MITAA NA IDARA MAALUM ZA SMZ KWA
MWAKA WA FEDHA 2020/2021

Mheshimiwa Spika, kila sifa njema ni za Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehma, Muumba wa Mbingu na Ardhi na vyote vilivyomo, kwa kutujaalia kukutana kwa mara nyengine tena katika Mkutano huu wa Kumi na Tisa wa Baraza laTisa kwa dhamira ya kujadili Bajeti kuu ya Serikali na taasisi zake katika Baraza lako Tukufu. Kwani hii ni rehma yake Muumba kwa kutupa pumzi na afya njema ambayo wenzetu wengine amewanyima fursa hii.

Mheshimiwa Spika, pia, napenda kutumia fursa hii adhimu kukushukuru na kukupongeza wewe binafsi kwa kunipa nafasi hii ya kusimama mbele ya Baraza lako Tukufu, kwa lengo la kuwasilisha maoni ya Kamati ya Kudumu ya Sheria, Utawala Bora na Idara Maalumkuhusina na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha kwa Wizara ya Nchi, (OR) Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ kwa mwaka wa fedha 2020/2021 kama Kanuni za Baraza hili zinavyoelekeza.

Mheshimiwa Spika, aidha, nawapongeza na kuwashukuru kwa dhati viongozi wa Wizara hii wakiongozwa na Waziri wao Mheshimiwa Haji Omar Kheri, Naibu Waziri, Mheshimiwa Shamata Shaame Khamis, Katibu Mkuu, Manaibu Katibu Mkuu, Wakuu wa Mikoa pamoja Afisa Mdhamini Pemba, na watendaji wote kwa mashirikiano yao makubwa waliyotuonesha katika Kamati yetu na kupelekea kutekeleza majukumu yetu ipasavyo. Vile vile, shukurani za pekee ziende kwa Wakuu, Maafisa na Wapiganaji wote wa Idara Maalum za SMZ kwa mashirikiano yao waliyotupatia kwa kipindi chote cha utekelezaji wa shughuli za Kamati.
Mheshimiwa Spika, sambamba na hayo, natumia nafasi hii kuishukuru Wizara ya Nchi (OR) Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ kwa kutumia na kutekeleza vyema ushauri na maagizo ya Kamati pamoja na kusimamia kwa ukamilifu na ufanisi utekelezaji wa Bajeti yao ya mwaka 2019/2020, jambo hili limewawezesha kujenga ari ya kuwasilisha mbele ya Kamati yetu, pamoja na Baraza lako Tukufu Makadirio mapya ya Mapato na Matumizi ya Fedha kwa mwaka wa fedha 2020/2021 ili yapate baraka za Wajumbe wako,na kwa mnasaba huo, tunaliomba Baraza lako tukufu liridhie na liipitishe Bajeti hii kwa maslahi ya wananchi na Serikali kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, aidha, naomba kutoa shukrani na pongezi za pekee kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi imara wa Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein katika uongozi wake na kuhakikisha maendeleo ya watu na ustawi wa jamii nchiniumeimarika pamoja na kusimamia maendeleo ya kiuchumi kufuatana na misingi na madhumuni yaliyowekwa katika Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, kwa kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora unafanikiwa kwa wananchi wote wa Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, ni matumaini ya Kamati yangu kuwa, mafanikio yanayopatikana katika uimarikaji wa uchumi wetu na huduma za kijamii yanatokana na utekelezaji mzuri wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015/2020.

Mheshimiwa Spika, Bajeti hii imekadiriwa kufanya kazi kwa kuzingatia malengo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na inaakisi hali halisi ya uchumi wetu na harakati za kupunguza umasikini lakini pia kwa kuzingatia malengo ya Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini Zanzibar (MKUZA III).

Mheshimiwa Spika, pia, nachukua nafasi hii kuwashukuru kwa kazi kubwa walioifanya Wajumbe wa Kamati yangu wakati tukiwa tunapitia bajeti hii, kwa kuonesha mashirikiano yao makubwa katika kutekeleza majukumu ya Kamati hii.


Hivyo, kwa ridhaa yako naomba sasa uwatambue Wajumbe wa Kamati hii kama ifuatavyo:
1.    
Mhe. Machano Othman Said
Mwenyekiti.
2.    
Mhe. Zulfa Mmaka Omar
Makamu Mwenyekiti.
3.    
Mhe. Dkt. Khalid Salum Mohamed
Mjumbe.
4.    
Mhe. Ali Khamis Bakar
Mjumbe.
5.    
Mhe. Salma Mussa Bilal
Mjumbe.
6.    
Mhe. Suleiman Makame Ali
Mjumbe.
7.    
Mhe. Maryam Thani Juma
Mjumbe.
8.    
Ndg. Haji Jecha Salim
Katibu.
9.    
Ndg. Ali Alawy Ali
Katibu.

Mheshimiwa Spika, Kamati ya Sheria, Utawala Bora na Iadara Maalum imetumia uweledi wake wa hali ya juu katika kupitia, kuchambua na kujiridhisha vyema naprogramu zote zilizokusudiwa kufanyiwa kazi kupitia Mafungu ya Bajeti ya Wizara hii kama ilivyoelezwa katika Kanuni za Baraza la Wawakilishi, Toleo la mwaka 2016.

Mheshimiwa Spika, ni imani ya Kamati hii kwamba kupatikana kwa fedha zilizopangwa katika Wizara hii kutasaidia kwa kiasi kikubwa utekelezaji na ukamilishaji wa malengo yaliyokusudiwa kutekelezwa ikiwa ni pamoja na kukamilisha miradi iliyotengwa kwa mwaka huu wa fedha 2019/2020 na vile vile kumalizia mradi mkubwa wa ujenzi wamahanga na nyumba za askari wa Idara Maalum kisiwani Pemba.

PROGRAMU ZA MAKAO MAKUU (FUNGU D 01)

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kazi zake kwa mwaka wa fedha 2019/2020, Kamati yangu imefanikiwa kutembelea na kujionea shughuli mbali mbali za kawaida na zile za miradi ya maendeleo ambazo zinasimamiwa na kuratibiwa na Wizara hii kupitia programu kuu tatu (3) zifuatazo:

(a)   Programu ya usimamizi na uendeshaji wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ;
(b)   Programu ya uratibu wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa;
(c)   Programu ya usimamizi wa utumishi na uratibu wa Idara Maalum za SMZ.

Mheshimiwa Spika, programu hizi pia ndani yake zimo programu ndogo ndogo ambazo zina lengo la kukamilisha utekelezaji wa programu kuu hizo katika maeneo tofauti ya kiutendaji. Aidha, utekelezaji wa programu hizi unakabiliwa na changamoto mbali mbali kama vile uhaba wa vitendea kazi, uhaba wa vyombo vya usafiri pamoja na ubovu wa barabara za ndani katika maeneo mengi ambako kunapelekea barabara hizo kutokupitika au kupitika kwa tabu hasa kwa wale wanaotumia vyombo vya moto pamoja na uchakavu na uhaba wa madarasa ya kusomea katika skuli za msingi, matundu ya vyoo, changamoto katika utoaji wa huduma za uji wa lishe katika skuli za maandalizi na ukosefu wa maji safi na salama katika baadhi ya vituo vya afya, skuli za msingi na maandalizi.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Kamati hii inaipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa juhudi zake za kusimamia vyema na kuzitatua baadhi ya changamoto hizi ambazo kwa kiasi kikubwa zimeshamiri katika skuli za msingi na maandalizi zilizopo vijijini.

Mheshimiwa Spika, vile vile, Kamati inatoa pongezi za dhati kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuhakikisha kuwa huduma za afya na elimu kwa wananchi zinakuwa bora kwa kusambaza dawa na vifaa tiba vinavyohitajika pamoja na kusambaza madaftari, vitabu na chaki katika skuli mbali mbali za Unguja na Pemba.

Mheshimiwa Spika, Kamati inashauri kwa mwaka wa fedha 2019/2020, idara zinazotekeleza miradi ya maendeleo, zipatiwe fedha za kutosha kwa miradi hiyo ambayo iliainishwa katika programu za fungu D01 ili kuweza kutatua changamoto zinazokwamisha utekelezaji wa shughuli zao kwa lengo la kuleta ufanisi na kuleta maendeleo katika Idara hizo.

Mheshimiwa Spika, Kamati imeridhishwa na kazi nzuri zinazofanywa na Ofisi kuu kwa kupitia na kuandaa miradi mbali mbali ya maendeleo ambayo msingi wake ni kuongeza kasi ya maendeleo ya kiuchumi kwa jamii. Aidha, Kamati imeelezwa kuwepo kwa fedha za mfuko wa barabara za ndani ambazo hazikutumika katika mwaka wa fedha unaomalizika mwezi Juni, 2020. Kamati inaishauri Serikali kuhusiana na fedha hizo zilizotengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara za ndani kuwekewa mpango maalum wa matumizi katika kila mwaka ili kunusuru fedha nyingi ambazo zinabakia bila matumizi yaliyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, Kamati inashauri barabara ambazo zilikusudiwa kujengwa na Halmashauri katika bajeti ya mwaka 2019/2020 na kushindwa kujengwa kutokana na kutokuwepo kwa mipango madhubuti ya matumizi ya fedha hizo zijengwe katika bajeti hii ya mwaka 2020/2021.

Mheshimiwa Spika, Kamati inaipongeza Wizara kwa kusimamia vyema zoezi la uwekaji wa mipaka ya kishehia na kuweza kufanikiwa kwa kiasi kikubwa na kuondoa changamoto katika maeneo yenye idadi kubwa ya wakaazi na hivyo kupelekea kutolewa kwa huduma za kijamii kwa ufanisi zaidi kwa mujibu wa ukubwa wa eneo na idadi ya wakaazi husika.

PROGRAMU ZA IDARA MAALUM ZA SMZ (FUNGU D 02 – D 06)

Mheshimiwa Spika, Kamati imeridhishwa na juhudi zinazofanywa na wapiganaji wetu wa vikosi kwa kazi nzito wanazozifanya za kulinda, kusimamia na kudumisha usalama wa raia na mali zao pamoja na kuhakikisha uwepo wa amani na utulivu katika nchi yetu. Sambamba na hayo, Kamati imeridhika na hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa Mahanga ya Kikosi cha Valantia Ndugukitu pamoja na Jengo la ghorofa mbili (2) la Kikosi cha Zimamoto na Uokozi cha Kijichame kisiwani Pemba. Ni dhahiri kabisa, juhudi hizo za Serikali zinaonekana kutia moyo na kuwajali sana vijana wetu na vile vile, Serikali kutekeleza kwa vitendo ahadi zake zilizotolewa katika Ripoti ya Kamati na Bajeti ya mwaka huu wa fedha 2019/2020.

Mheshimiwa Spika, Kamati inaishauri JKU kuweka utaratibu wa kuwa na programu za kuwafuatilia vijana ambao wamepata mafunzo kutoka katika Jeshi laKujenga Uchumi mara tu wanapomaliza mafunzo yao ili kuwafahamu mahali walipo na shughuli wanazozifanya kwa mujibu wa mafunzo waliyopatiwa. Programu hizi zitasaidia kufahamuni kwa kiasi gani mafunzo yanayotolewa yanasadifu mazingira na wakati tulionao.



PROGRAM KUUZA URATIBU WA TAWALA ZA MIKOA NA
SERIKALI ZA MITAA (Fungu D 07 – D 11)

Mheshimiwa Spika, katika programu kuu ya Uratibu wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kwa ujumla wake, Kamati ya Sheria, Utawala Bora na Idara Maalum imeridhishwa na utekelezaji wa programu zinazosimamiwa na Tawala za Mikoa pamoja Mamlaka ya Serikali za Mitaa zaidi katika ukusanyaji wa mapato kutokana na baadhi ya Halmashauri kuvuka malengo waliyokusudia.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa dhana ya Ugatuzi ni njema na inaleta ufanisi kwa watendaji, Kamati inapongeza sana juhudi za Serikali katika kusimamia vyema Ugatuzi katika taasisi zilizogatuliwa. Aidha, Kamati imeridhishwa na utendaji wa taasisi hizo katika kuwatumikia wananchi. Hata hivyo, ni vyema Halmashauri zetu zikajikita zaidi katika utafutaji wa vyanzo vipya vya mapato ambavyo havitawaumiza wananchi kwa kuyatumia maeneo waliyonayo na badala yake kuacha kufanyakazi kwa kutegemea ruzuku kutoka Serikali kuu kwani kutegemea ruzuku kutapelekea kushindwa kufikia malengo ya kuanzishwa kwa Halmashauri na kuizidishia mzigo Serikali kwa kuzingatia kipindi hiki ambacho uchumi wa Dunia umeshuka kutokana na athari za janga la ‘Corona’ (Covid – 19).

Mheshimiwa Spika, pamoja na maelezo mazuri ya Wizara juu ya utekelezaji wa Ugatuzi katika kipindi hiki, Kamati, wakati wa utekelezaji wa majukumu yake katika Halmashauri hizo, ilielezwa na kubaini kuwepo kwa changamoto katika baadhi ya sekta zilizogatuliwa hasa sekta ya kilimo na elimu, kwa kutokutekeleza ipasavyo suala hili la ugatuzi ambapo sekta hizo zimepeleka baadhi ya watendaji tu bila ya kupeleka fedha za matumizi katika uendeshaji wa programu zilizokusudiwa. Kwa mfano bajeti ya elimu ya msingi na maandalizi bado zipo Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, hivyo Halmashauri hulazimika kulipa maposho ya walimu pamoja na uji wa lishe kwa skuli za maandalizi na msingi. 

Mheshimiwa Spika, Kamati ilifanya ziara maalum Tanzania Bara kwa kutembelea Halmashauri ya Jiji la Mwanza na Jiji la Dar es Salaam kwa lengo la kujifunza namna ya uendeshaji wa Jiji, utekelezaji wa majukumu ya Taasisi hizo na namna gani wanaweza kukusanya mapato kupitia vyanzo walivyonavyo kisheria. Hivyo, Kamati inashauri katika utekelezaji mzuri wa majukumu ya Jiji la Zanzibar, kuainishiwa majukumu yake na vyanzo vya mapato ambavyo watavitumia ili kujikusanyia mapato kama zilivyo Halmashauri nyengine. Sambamba na hayo Kamati imeona ipo haja ya kufanywa marekebishho ya Sheria ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa, nambari 8 ya mwaka 2014 ili majukumu ya Jiji na vyanzo vya mapato viwekwe wazi katika Sheria hii.

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla, Serikali imejitahidi sana katika kunyanyua elimu ya msingi na afya, changamoto iliyopo ni idadi kubwa ya madarasa mabovu pamoja na uhaba wa matundu ya vyoo kwa skuli za maandalizi na msingi. Hivyo basi, Kamati inazishauri Halmashauri zetu kwa kupitia waheshimiwa Madiwani na Wawakilishi kuwashajihisha wananchi kujitolea kwa hali na mali katika kuongeza idadi ya matundu ya vyoo pamoja na madarasa ili kuweka mazingira rafiki kwa watoto wetu katika kujipatia elimu bora. Aidha, Serikali nayo itenge fungu maalum la fedha za kutatua tatizo hilo.

Mheshimiwa Spika, Kamati inaishauri Wizara kupitia Halmashauri, kuchukuwa hatua za makusudi kuhakikisha kuwa maeneo yote ya miji yanakuwa safi na salama kwa kuzipatia magari na vifaa vya kuzolea taka Halmashauri ambazo ndizo zenye jukumu hilo ili ziweze kudhibiti na kuandaa utaratibu wa kukusanya taka za majumbani na maeneo mengine au kuweka maeneo maalum ya kukusanyia taka ili wananchi waweze kuondokana na adha hii ya kukosa maeneo ya kutupia taka na kupelekea taka hizo kuzagaa mitaani.

WAKALA WA USAJILI WA MATUKIO YA KIJAMII (FUNGU D 12)
          
Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa, nachukuwa fursa hii kwa kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein kwa kumteua ndugu Idrissa Shaaban Zahran  kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala ambapo Kamati ina matumaini makubwa kwamba Mkurugenzi huyo atazimaliza changamoto zinazoukabili Wakala huo.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Wakala wa Usajili wa Matukio ya Kijamii umeendelea na usajili wa wazanzibari na kuwapatia vitambulisho vyao pamoja kusajili vizazi, vifo na talaka. Kamati inaishauri Ofisi hii kuwezeshwa kwa kupatiwa miundombinu ambayo itasaidia kuweza kusajili wazanzibari wote katika shehia zao pamoja na hospitali mara tu wanapozaliwa pamoja na kutoa vyeti vya kuzaliwa vyenye ubora zaidi.
HITIMISHO

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia, nachukua fursa hii kuiomba jamii katika kipindi hiki cha mvua za masika zinazoendelea kunyesha kuzidi kuweka usafi wa mazingira yetu kwa kuitunza michirizi ya maji ya mvua na kuepuka kutupa taka kiholela ndani ya miji yetu, kufanya hivyo kutasaidia kujikinga na maradhi ya mripuko na malaria ambayo ni hatari kwa nchi yetu pamoja na kuitunza misingi hiyo ambayo inajengwa kwa kutumia fedha nyingi za Serikali.

Mheshimiwa Spika, aidha, katika kukabiliana na mafuriko yanayotokea karibu kila mwaka katika maeneo mbali mbali ya Wilaya ya Magharib ‘A’ na ‘B’, Kamati inaishauri Serikali kujenga mitaro ya kupitishia maji katika maeneo hayo kama vile ilivyofanya katika maeneo ya Wilaya ya Mjini, Chake Chake, Wete na Mkoani.

Mheshimiwa Spika, pia, naomba niwashukuru Makamanda wa Idara Maalum za SMZ, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Makatibu Tawala wa Mikoa na Wilaya, Wakurugenzi, Madiwani, Masheha na watendaji wote wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ kwa utendaji, uzalendo wao na mashirikiano yao katika kutekeleza majukumu ya Kamati yetu katika kipindi chote cha maisha ya Kamati hii.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa, Kamati inawaomba Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako Tukufu wairidhie, waichangie na waipitishe Bajeti hii na hatimae waidhinishie makadirio ya fedha zilizopangwa kutumiwa kwa mwaka wa fedha 2020/2021 kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ.









Mheshimiwa Spika,          Naomba Kuunga Mkono Hoja.

Ahsante,


…………..…………………..
(Mhe. Maryam Thani Juma)
Mjumbe,
Kamati ya Sheria, Utawala Bora na Idara Maalum,
Baraza la Wawakilishi,
Zanzibar

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.