Taarifa
ya Tume ya Uchaguzi kwa Vyombo vya Habari Kuhusu Matayarisho ya Uchaguzi Mkuu
wa Mwaka 2020.
Ndugu Waandishi wa Habari,
Tume ya Uchaguzi inatarajia kuendesha Uchaguzi Mkuu mwaka 2020 ambapo wananchi
wa Zanzibar watapata fursa ya kumchagua Rais wa Zanzibar, Wajumbe wa Baraza la
Wawakilishi na Madiwani. Maandalizi ya uchaguzi huo yamegawika katika sehemu
tatu kubwa ambazo ni:
i)
Upatikanaji
wa Vifaa mbali mbali vya Uchaguzi,
ii)
Uandikishaji
wa Wapiga Kura Wapya na uhakiki wa taarifa za Wapiga Kura
iii)
Kazi ya kufanya Mapitio ya Idadi, Majina na
Mipaka ya Majimbo ya Uchaguzi
Ndugu Waandishi wa habari,
Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ipo katika hatua za mwisho za upatikanaji wa vifaa
vya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020. Nachukua nafasi hii kuwafahamisha kuwa Tume
imekamilisha uchapishaji wa nyaraka, uagiziaji na ununuzi wa vifaa na mbali
mbali vya uchaguzi na baadhi ya vifaa hivyo vimeshakabidhiwa Afisi ya Tume ya
Uchaguzi.
Ndugu Waandishi wa habari, Kazi
ya uandikishaji wa Wapiga Kura Wapya na Uhakiki wa taarifa za Wapiga Kura
waliokuwemo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ilianza tarehe 18/1/2020
katika Wilaya ya Micheweni kisiwani Pemba na kukamilika tarehe 15/3/2020 katika
Wilaya ya Mjini. Katika kazi hii Tume
iliandikisha wapiga kura wapya waliofikia umri wa kupiga kura. Aidha, ilifanya uhakiki wa wapiga kura waliokuwemo
katika Daftari la wapiga kura tangu
lilipoanzishwa mwaka 2005 na wapiga kura wengine ambao waliandikishwa
kwa nyakati mbalimbali kati ya mwaka 2010, 2013 na 2015. Lengo la uhakiki wa
wapiga kura ni kufahamu wapiga kura ambao wamepoteza sifa za kuwemo katika
Daftari na kuwafuta waliokosa sifa.
Ndugu Waandishi wa Habari. Kazi
ya uandikishaji na uhakiki wa taarifa za wapiga kura kwa ujumla ilikwenda
vizuri sana ingawa kulikuwepo na tatizo la baadhi ya Wananchi kukosa
kuandikishwa au kuhakikiwa taarifa zao kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo
kukosa Vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi.
Tume ya Uchaguzi ya
Zanzibar tayari imefanya tathmini ya kazi ya Uandikishaji ili kufahamu kwa
kiasi gani zoezi hilo limetekelezwa. Hivi
sasa Tume inaandaa utaratibu utakao wawezesha wananchi wenye sifa ambao
walikosa fursa ya kuandikisha na kuhakiki taarifa zao ili wapate nafasi ya kushiriki
kikamilifu katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Aidha, Afisi za Tume ya
Uchaguzi za Wilaya hivi sasa zinapokea maombi ya wapiga kura wanaotaka
kufanyiwa uhamisho wa taarifa zao kutoka vituo vya majimbo waliyopiga kura
katika uchaguzi uliopita kwenda katika vituo vya majimbo ambayo wanaishi hivi sasa
ambako watakuwa wametimiza sifa ya ukaazi katika vituo vya majimbo hayo.
Kazi hiyo itaendelea na itasita miezi mitatu
kabla ya upigaji wa kura. Tume inawaomba wale wote wanaotaka kufanya uhamisho
wa taarifa zao kufanya hivyo muda huu; vyenginevyo watalazimika kwenda kupiga
kura katika vituo vyao vya zamani.
Ndugu waandishi wa Habari, Katika
zoezi la awali la uandikishaji wa wapiga
kura wapya na uhakiki wa wapiga kura, Takwimu za awali zinaonesha kwamba jumla
ya wapiga kura 413,444 walipatiwa huduma hiyo vituoni na kati ya hao wanaume
walikuwa ni 199,327 na wanawake ni 214,117. (Inasisitizwa kuwa takwimu hizi ni za awali).
Ndugu Waandishi wa Habari, Kazi
nyengine ambayo Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar inawajibika kuifanya katika
kipindi hiki cha maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020 ni kupitia (review)
idadi, majina na mipaka ya majimbo ya Uchaguzi. Kazi hii itafanywa na Tume kwa
maelekezo ya kifungu cha 120(4) cha Katiba ya Zanzibar ambacho kimeipa uwezo
Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar katika kipindi cha miaka 8 hadi 10 au wakati
mwengine wowote, kuchunguza idadi ya mipaka na majina ya majimbo hayo kwa
kiwango kile ambacho Tume inahisi kuwa ni wajibu kuangaliwa upya na inaweza
kubadili idadi, mipaka na majina ya majimbo hayo kadiri itakavyoona inafaa.
Tume ya Uchaguzi ya
Zanzibar mara ya mwisho ilifanya mapitio kama haya ya majimbo mwaka 2015 kabla
ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2015, mapitio ambayo yalipelekea kuongezwa kwa
majimbo ya uchaguzi kutoka 50 yaliyokuwepo kabla na kuwa majimbo 54
yaliyotumiwa kwa uchaguzi wa wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Madiwani. Tume
inawajibika kufanyia tena mapitio ya majimbo haya miaka mitano baada ya zoezi
la mwaka 2015 kutokana na malalamiko katika baadhi ya majimbo ambako kuna wadi
ambazo Shehia zake zinahudumiwa na majimbo mawili tofauti kinyume na utaratibu.
Kwa kawaida kila jimbo linaundwa na wadi mbili mpaka tatu ambapo kila wadi
inaundwa na shehia mbali mbali zilizomo katika eneo la uchaguzi. Katika kazi ya
mapitio ya majimbo ya mwaka 2015, kuna mkanganyiko ulijitokeza katika wadi na
majimbo ya uchaguzi Unguja na Pemba.
Kutokana na hali hiyo, Tume imeamua kabla ya Uchaguzi Mkuu ujao wa mwaka 2020
ifanye mapitio ya majimbo na ikiwezekana kwa mamlaka iliyo nayo ifanye
marekebisho yanayostahiki kwa eneo ambalo linastahiki kufanyiwa marekebisho yanayofaa.
Ndugu Waandishi wa Habari, Mapitio
ya idadi na mipaka ya majimbo ya uchaguzi ni kazi shirikishi ingawaje mamlaka
ya kufanya kazi hiyo kisheria ni ya Tume ya Uchaguzi. Hata hivyo, Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar kwa
kuthamini uwepo mkubwa wa wadau wa uchaguzi vikiwemo vyama vya siasa, Asasi za
kiraia na mtu mmoja mmoja, inatoa nafasi kwa wadau wote kushiriki kikamilifu
kutoa maoni na maono yao kwa njia ya barua au mawasiliano yoyote kwa Tume ya
Uchaguzi ya Zanzibar juu ya hali ya majimbo kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka
2020. Maoni na maono hayo yatapokelewa katika Ofisi zote za Tume ya Uchaguzi ya
Zanzibar Unguja na Pemba wakati wowote baada ya kutoka kwa taarifa hii.
Tume ya Uchaguzi ya
Zanzibar ilipanga kuchukua maoni ya wadau juu ya suala hili kwa kufanya
mikutano mbali mbali na wadau. Hata hivyo, kutokana na maradhi ya homa ya
mapafu (COVID 19) yanayosababishwa na virusi vya CORONA yaliopo nchini na kutokana
na agizo lilitolewa na Serikali juu ya kujikinga na maradhi hayo kwa kuepuka
mikusanyiko ya watu, Tume haitoandaa mikutano ya maoni, badala yake itapokea
maoni na maono hayo kwa njia ya barua katika Afisi Kuu ya Tume ya Uchaguzi iliyopo
Maisara Unguja, Afisi ya Tume ya Uchaguzi Pemba iliyopo Chake Chake au katika
Afisi za Wilaya za Tume zilizopo katika Wilaya zote za Unguja na Pemba.
Ndugu Waandishi wa Habari, Baada
ya maelezo hayo ambayo yamegusa mambo matatu muhimu yanayofanywa na Tume ya
Uchaguzi ya Zanzibar katika kipindi hiki cha matayarisho ya Uchaguzi Mkuu wa
mwaka 2020, nachukua nafasi hii kuishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
kwa kutupa misaada mbalimbali iliyotuwezesha kufanikisha maandalizi ya Uchaguzi
Mkuu ujao. Ni imani yangu kubwa kuwa wakati mtakapokuwa mnatayarisha taarifa
zenu kwa umma mtakuwa makini kuyaeleza vyema yale yote ambayo nimeyasema katika
taarifa hii.
Nawashukuru nyote kwa
kunisikiliza.
Ahsante sana
JAJI MKUU (Mst) HAMID
MAHMOUD HAMID
MWENYEKITI
TUME YA UCHAGUZI YA
ZANZIBAR
ZANZIBAR
No comments:
Post a Comment