Habari za Punde

Taasisi za Utawala Bora Zashauriwa Kushirikiana

Mwenyekiti wa THBUB, Jaji (Mst) Mathew Mwaimu (kulia) akiongea na Kamishna wa Sekretarieti ya Maadili ya Utumishi wa Umma, Jaji (Mst) Harold Nsekela (Kushoto) alipomtembelea ofisini kwake jijini Dodoma jana. Lengo la ziara hiyo ya THBUB ni kuimarisha ushirikiano na Sekretarieti ya Maadili.

Na  Mbaraka Kambona,
Kamishna wa Sekretarieti ya Maadili ya Utumishi wa Umma, Jaji (Mst) Harold Nsekela amezishauri taasisi zinazosimamia utawala bora kushirikiana kwa karibu ili waweze kutekeleza majukumu yao vizuri.

Jaji Nsekela alitoa rai hiyo katika ofisi yake jijini Dodoma jana alipokutana na Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), Jaji (Mst) Mathew Mwaimu.

Alisema kuwa taasisi hizo zimekuwa na mazoea ya kushirikiana kwa ukaribu wakati wa sherehe za maadhimisho ya siku ya maadili na haki za binadamu, jambo ambalo alisema kuwa haipaswi kuwa hivyo na badala yake taasisi hizo ziimarishe ushirikiano huo wakati wote.

Aliongeza kuwa kufanya kazi kwa ukaribu na kubadilishana taarifa wakati wa kutekeleza majukumu yao kutasaidia taasisi hizo kuainisha mipaka yao ya kiutendaji ambapo itawawezesha kujiepusha na muingiliano wa shughuli zao.

“Kuna umuhimu wa kuwa na ushirikiano wa karibu kati yetu, hii itatusaidia kubadilishana taarifa ambazo zitatusaidia kutoa huduma kwa wananchi ipasavyo”, Jaji Nsekela alieleza.

Aliendelea kusema kuwa kimsingi majukumu ya taasisi hizo yanafanana, kwani zote ni taasisi za uchunguzi, tofauti iliyopo ni kwamba THBUB inashughulikia masuala ya haki za binadamu, Sekretarieti ya Maadili inasimamia maadili ya utumishi wa umma, TAKUKURU wao wanachunguza masuala ya rushwa na  ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa hesabu za serikali inasimamia  matumizi ya fedha za umma.

Aliongeza kuwa kuna haja ya taasisi hizi kubadilishana uzoefu wa mara kwa mara ili kila mmoja aelewe mipaka ya mwenzake jambo ambalo  litawasaidia kuepuka muingiliano wa majukumu yao.

Aidha,  Jaji Nsekela aliishauri THBUB kuendelea na utekelezaji wa majukumu yake kwa kuzingatia maadili kwa sababu hiyo ndio njia pekee itakayowawezesha kutoa huduma kwa wananchi bila malalamiko.

“Katiba imewapa mamlaka ya kulinda na kuhamasisha haki za binadamu na misingi ya utawala bora nchini, tumieni mamlaka hayo kwa kutoa huduma bora kwa Wananchi huku mkizingatia maadili”, Jaji Nsekela alisisitiza

Akiongea mapema, Jaji Mwaimu alieleza kuwa lengo la ziara yake ni kuimarisha ushirikiano na Sekretarieti ya Maadili, lakini pia kuwakumbusha wananchi kuwa THBUB ipo kwa ajili ya kuwasaidia.

Jaji Mwaimu aliendelea kueleza kuwa katika kipindi cha miaka miwili iliyopita THBUB imekuwa ikitekeleza majukumu yake bila ya uongozi kwa maana ya Makamishna jambo ambalo liliathiri utendaji wa taasisi hiyo.


“THBUB ni huru, hatupaswi kuchukua upande tunaposhughulikia masuala ya uvunjifu wa haki za binadamu na misingi ya utawala bora, jukumu letu la msingi ni kusaidia wananchi kupata haki zao”, Jaji Mwaimu ilifafanua
Mwenyekiti wa THBUB, Jaji (Mst) Mathew Mwaimu (kulia) akimkabidhi Kamishna wa Sekretarieti ya Maadili ya Utumishi wa Umma, Jaji (Mst) Harold Nsekela (Kushoto) barua ili kuimarisha ushirikiano baina ya THBUB na Sekretarieti ya Maadili. 
Kamishna wa Sekretarieti ya Maadili ya Utumishi wa Umma, Jaji (Mst) Harold Nsekela (Kulia) akimsindikiza Mwenyekiti wa THBUB, Jaji (Mst) Mathew Mwaimu (kushoto) mara baada ya kumaliza mazungumzo yao.
Kamishna wa Sekretarieti ya Maadili ya Utumishi wa Umma, Jaji (Mst) Harold Nsekela (Kushoto) akiteta jambo na Kaimu Katibu Mtendaji wa THBUB, Hajjat Fatuma Muya (Kulia) muda mfupi mara baada ya kumaliza kikao.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.