Mheshimiwa
Spika, Kwanza kabisa naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu
Mtukufu, Mjuzi wa yote, Muumba na mwenye kurehemu kwa kutujaalia Afya
njema iliyotuwezesha kukutana tena siku
ya leo katika Baraza hili Tukufu kwa lengo la kutekeleza majukumu yetu kwa
mustakabali ulio bora. Aidha, napenda pia, kukushukuru na kukupongeza wewe
binafsi kwa unavyoliongoza Baraza hili kwa hekma busara na upendo wa hali ya
juu, tunamuomba Allah (SW) azidi kukuongoza katika mambo ya kheri na In Shaa
Allah utaliongoza tena Baraza hili Tukufu kwa kipindi kinachokuja.
Mheshimiwa
Spika, Kwa moyo wa dhati napenda nitoe shukurani na
pongezi za pekee kwa Mheshimiwa Raisi wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Mheshimiwa Dkt. Ali Mohammed Shein kwa kipindi chote alichotumikia
nchi hii kwa utulivu na upendo wa hali ya juu na kuitekeleza vyema ilani ya
Chama cha Mapinduzi, ni dhahiri kwamba Mheshimiwa Rais amefanya mema mengi na
yamsingi ambayo daima wananchi wake tutayakumbuka. Tunamuomba mwenyezi mungu
amjaalie uzima, maarifa na nguvu kamili za kuweza kumaliza kipindi hichi kwa
salama na amani.
Mheshimiwa Spika,
Kwa heshima na taadhima nachukua nafasi hii kumpongeza na kumshukuru sana
Waziri wa Afya Mheshimiwa Hamad Rashid Mohamed, Naibu Waziri Mheshimiwa Harusi
Said Suleiman, Katibu Mkuu pamoja na Watendaji wake wote wa Wizara kwa jitihada
kubwa walizozichukua katika kuhakikisha wananchi wa Zanzibar wanapata huduma bora.
Mheshimiwa Spika,
Kwa kuwa hichi ni kipindi cha mwisho kukutana sote katika Baraza hili la Tisa
naomba niwashukuru wajumbe wa Baraza hili tukufu kwa muda wote ambao tulikuwa
pamoja katika kuhakikisha tunawakilisha vyema yale yote tuliagizwa na wananchi
wetu ambao walituamini huko majimboni na imani yangu kwa wale wote tutaokuwa
nania watatuchagua tena kuwatumikia katika kipindi kinachokuja.
Mheshimiwa Spika,
Kwa namna ya pekee napenda kuwashukuru Wajumbe wote wa Kamati ya Ustawi wa
Jamii kwa utekelezaji mzuri wa kazi zao, umakini na umahiri mkubwa na ndio
sababu kuu iliyopelekea kuijadili bajeti hii
pamoja na kuhoji mambo yote ambayo yalitupa mashaka kwa mantiki ya
kuhakikisha fedha wanazoidhinishiwa
Wizara hii na Baraza lako Tukufu zinatumika ipasavyo kama
zilivokusudiwa.
Mheshimiwa Spika,
Kabla sijaendelea na hotuba hii, kwa heshima kubwa naomba niwatambue Wajumbe wa
Kamati ya Ustawi wa Jamii ambao walifanya kazi na kushauri kwa namna moja au
nyengine wakati wakutekeleza kazi za Kamati hii kama ifuatavyo:
|
Mheshimiwa
Mwanaasha Khamis Juma
|
Mwenyekiti
|
|
Mheshimiwa
Nassor Salim Ali
|
M/Mwenyekiti
|
|
Mheshimiwa
Shehe Hamad Mattar
|
Mjumbe
|
|
Mheshimiwa
Tatu Mohammed Ussi
|
Mjumbe
|
|
Mheshimiwa
Yussuf Hassan Iddi
|
Mjumbe
|
|
Mheshimimwa
Amina Iddi Mabrouk
|
Mjumbe
|
|
Mheshimiwa
Ramadhan Hamza Chande
|
Mjumbe
|
Mheshimiwa
Spika, Kamati hii inafanyakazi na Makatibu wawili ambao
wamekuwa wakitusaidia kwa kiasi kikubwa na uweledi wa hali ya juu katika
kutekeleza majukumu yetu, msaada wa makatibu hao umekuwa ndio chanzo cha
mafanikio makubwa ya Kamati hii.
Makatibu hao ni:
1.
Ndg. Aziza Waziri Kheir Katibu
2.
Ndg. Mwanaisha Mohammed Kheir Katibu
Mheshimiwa Spika,
Kamati yetu ya Ustawi wa Jamii miongoni mwa majukumu yake ni kuchambua
mapendekezo ya Serikali, kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya kawaida na
miradi ya maendeleo ya Wizara ya kila mwaka, hivyo katika kutekeleza jukumu
hilo lililoelezwa katika Kanuni za Kudumu za Baraza la Wawakilishi (Toleo la
2020), Kamati yangu ilikaa na kujadili na hatimaye kupitisha Makadirio ya
Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2020/2021. Nasasa kwa
ruhusa yako na kwa niaba ya Kamati, napenda kuwasilisha maoni ya Kamati
kuhusiana na Bajeti hiyo.
Mheshimiwa Spika,
Kwa mwaka huu wa fedha Wizara ya Afya imepangiwa kutekeleza kazi zake kupitia
Programu Kuu Nne ambapo utekelezaji wake utasimamiwa na programu ndogo ndogo
ndani yake.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yetu inaipongeza Wizara ya Afya kwa kuweza kutekeleza kazi zake kwa
kiwango kikubwa kufuatia Bajeti iliyoidhinishiwa kwa mwaka uliopita 2019/2020. Aidha, imefurahishwa na ongezeko la bajeti kwa
mwaka wa fedha 2020/2021 ambayo imepangiwa kutumia jumla ya Tsh.
100,236,100,000/- kupitia (Fungu H01). Hata hivyo, Kamati inawapa tahadhari
Wizara kujipanga vizuri zaidi kwa mwaka
unaokuja kwa kuhakikisha
fedha watazoingiziwa hazipotei na matumizi yake yaende kwa usahihi ili kufikia
malengo yote yaliyokusudiwa.
PROGRAMU KUU YA KINGA NA ELIMU YA
AFYA
Mheshimiwa Spika, Programu
hii inajukumu la kuhakikisha jamii inapata elimu na huduma ya kujikinga na
maradhi mbalimbali yakiwemo ya kuambukiza na yasiyo yakuambukiza. Kwa mwaka huu wa fedha 2020/2021
programu ya Kinga na Elimu ya Afya imepangiwa kutumia jumla ya Tsh 28,664,931.000/-,
Kamati inaipongeza Wizara kwa ongezeko la bajeti hii ambapo kwa mwaka 2019/2020
Programu ya Kinga na Elimu ya Afya ilipangiwa kutumia jumla ya Tsh. 21,888,822.
Mheshimiwa Mwenyekiti,
Kupitia utekelezaji wa shughuli ya huduma za kumaliza Malaria Zanzibar Kamati
inaipongeza Wizara kwa kufanikiwa kuondosha maradhi haya kwa asilimia kubwa
kabisa kutokana na hatua mbali mbali walizozichukua za kuangamiza mazalio ya
mbu na kupiga dawa majumbani. Hata hivyo, Kamati inashauri Wizara kuongeza
jitihada za kuelimisha wananchi kufuatia ishara za ongezeko la homa ya malaria
siku zahivi karibuni. Hali hii imesababishwa na
mazalio ya mbu wa Malaria yanayotokana na mvua zinazoendelea, kuendelea
kugawa vyandarua vilivyotiwa dawa pamoja na jamii kuwa tayari kupuliziwa dawa
za kuangamiza maradhi hayo majumbani.
Hospitali ya Micheweni.
Mheshimiwa Spika,
Kamati katika mizunguko yake ya ufatiliaji wa utekelezaji wa Bajeti ilifika
Hospitali ya Micheweni na kutembelea wodi ya wazazi ambayo ilionekana wazi kuwa
na uhaba wa vyumba vya kujifungulia pamoja na uchache wa vitanda. hali hii imesababisha wazazi watatu kutumia
kitanda kimoja. Aidha, Kamati inasikitishwa na taarifa ya kusitishwa kwa ujenzi
wa banda moja la wodi ya wazazi kupitia wafadhili wa Milele Foundation ambao walijitolea kulijenga baada ya kukamilisha
taratibu zote za ujenzi. Kamati inaishauri Wizara kulifuatilia kwa undani suala
hili na baadae kukubiliana na Milele
Foundation kwa ajili ya ujenzi wa banda la Mama na Mtoto.
Mheshimiwa Spika,
Kamati pia inaishauri Wizara Kupitia bajeti hii ya 2020/2021 kurekebisha mfumo
wa upatikanaji wa kibali cha kusafirishia “Oxygen” kinatolewa kimoja tu kwa
Pemba nzima. Hali ambayo hupelekea utolewaji wa huduma kutokamilika kwa wakati
iwapo “oxygen” hiyo imemalizika. Aidha, hospitali ya Micheweni inakabiliwa na
upungufu wa seti za upasuaji kwa mama wajawazito pamoja na vifaa vya kumsaidia
hewa mgonjwa “Capnofraphy” ambapo kazi hufanyika kwa kusubiriana, pamoja na
kulishughulikia kwa upana wake tatizo la seti za upasuaji wa mama wanaotaka
kujifungua ili kuepusha hatari zinazoweza kutokea.
Mheshimiwa Spika,
Kufuatia muamko mdogo wa baadhi ya wananchi juu ya huduma za Kliniki Kamati
inatoa wito kwa Wizara juu ya umuhimu wa kuongeza bidii za kuwashajihisha
wanawake kuwahi kuhudhuria Kliniki pindi wanapojigundua wajawazito ili kama
kuna matatizo ambayo tiba yake inaweza kupatikana mapema kuweza kushughulikiwa
kuliko kwenda kwa ajili tu ya kupata gamba la kujifungulia.
Huduma za ufatiliaji wa Mienendo
ya Maradhi
Mheshimiwa Spika,
Kwa upande wa janga la maradhi ya homa kali ya mapafu inayosababishwa na virusi
vya Covid 19 Kamati inaipongeza
Wizara pamoja na Watendaji wake wote walijitolea na kuwa mstari wa mbele kwa
jitihada wanazozichukua kukabiliana na gonjwa hili licha ya changamoto ndogo
ndogo zinazojitokeza.
Mheshimiwa Spika,
Kamati inaiomba Wizara kuwapa motisha wauguzi wa Corona ili kuweza kufanya kazi
zaidi pamoja na kutoa elimu ya kutosha kwa wauguzi waliomo katika hospitali
zetu nyengine jinsi ambavyo wataweza kujikinga na kuwauguza washukiwa wa
maradhi ili kuepusha vifo vinavyoweza kutokea kwa kuhofia kuambukizwa na
maradhi hayo, kupitia bajeti hii ya 2020/2021 naiomba Serikali na Wizara kwa
ujumla kuhakikisha Madaktari na wauguzi wote wanaowahudumia wagonjwa wa Maradhi
ya Corona ambao wapo katika kambi zilizotengwa kuwarejeshea mfumo wa ulipaji
posho lililokuwa likitolewa kwa watendaji hao hapo awali ili kuondoa malalamiko
yanayojitokeza katika kipindi hichi.
PROGRAMU KUU YA HUDUMA ZA TIBA
Mheshimiwa Spika,
Dhumuni ya Programu Kuu ya Huduma za Tiba ni kutoa huduma za afya katika
Hospitali za ngazi za Vijiji hadi mkoa kupitia Mabaraza ya kitaaluma na Bodi,
kusimamia miradi mbali mbali ikiwemo Mradi wa Ujenzi wa Hospitali ya kisasa ya
Rufaa na kufundishia katika eneo la Binguni.
Hospitali ya Rufaa na Kufundishia
Binguni.
Mheshimiwa Spika,
Pamoja na kwamba eneo lililotengwa kwa ajili ya Hospitali ya Rufaa na
kufundishia huko Binguni limekuwa likitajwa kwa muda mrefu sasa bila ya
mafanikio. Kamati imefarijika na maelezo ya Wizara yaliyoelezea dhamira ya kuanza
ujenzi wa majengo matatu katika eneo hilo la Binguni likiwemo jengo la Dharura,
jengo la Upasuaji na jengo la Uchunguzi wa Maradhi.
Mheshimiwa Spika,
Ifahamike kwamba, Kamati ilifanya ziara mara kadhaa katika eneo hilo hata hivyo
haikubahatika kuona hatua za matayarisho ya ujenzi huo hata yale ya kuwalipa
fidia wakaazi wa eneo lile lililopimwa kwa ajili ya ujenzi zaidi ya
kuwekwa
viguzo vya kuzuia uvamizi wa eneo na kuelezwa kwamba michoro ya awamu ya kwanza
imeshakamilika baada ya kumalizika kwa hatua za upimaji wa ardhi
licha ya kuingiziwa fedha kwa vipindi tofauti
zisizopungua Tsh 10,472,592,000/- kwa ajili ya ujenzi huo na hadi kufikia mwisho wa mwezi Juni Mwaka huu kiasi
cha fedha zilizokua hazijatumika 6,000,000,000/- zitarudishwa Serikalini iwapo
hazijatumika.
Mhehimiwa Spika,
Kwa mwaka huu 2020/2021 Ujenzi wa Hospitali ya Binguni umepangiwa jumla ya Tsh
5,500,000,000/- Kamati inaiomba Wizara kutoa maelezo ya kutosha juu ya fedha zilizoidhinishwa
hapo kablalicha ya kueleza kuwa ujenzi huo utatumia kampuni ya Serikali ambayo
itawahusisha Wakandarasi wahandisi wa Vikosi vya Idara Maalumu za Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar.
Mheshimiwa Spika,
Kwa upande wa Hospitali ya Abdalla Mzee Kamati imekua haifurahishwi na majibu
ya Wizara kuhusiana na ujenzi wa nyumba za wafanyakazi katika Hospitali hiyo
kutokana na kwamba ujenzi wa nyumba hizo ni wa muda mrefu sasa na hakuna hatua
yoyote iliyofikiwa. Aidha, Kamati imechoka kuona hitilafu inayosababishwa na matumizi
ya umeme inayopelekea kuharibika kwa vifaa bado inaendelea. Naiomba Wizara
kutoa majibu ya kuridhisha kuhusiana na hatua walizofikia baada ya Kamati kutoa
maelekezo kwa Wizara kukaa pamoja na Shirika la umeme ZECO ili kujua kilio
hicho vipi kitamalizika.
Bohari Kuu ya Dawa Pemba.
Mheshimiwa Spika,
Kamati wakati ikiipitia Bajeti hii ilielezwa ujenzi wa Bohari kuu ya dawa Pemba
kwenye eneo la Hospitali ya Vitongoji umefikia katika hatua za kukamilika, na
ndani ya mwezi huu wa sita jengo hilo linategemewa kukabidhiwa rasmi kwa
Wizara. Kamati inaipongeza Wizara ya Afya kwa maendeleo hayo, hii itaifanya
Wizara kuondokana na ile shida ya usafirishaji wa dawa kila robo mwaka kisiwani
Pemba.
Hospitali ya Chake chake.
Mheshimiwa Spika,
Kamati wakati ikipitisha bajeti ya wizara hii ilielezwa kwamba hatua za
manunuzi kwa ajili ya ujenzi ya wodi ya mama na mtoto katika Hospitali ya
ChakeChake umekamilika. Niseme kwamba, taarifa hii imetushangaza kidogo kwa
kuwa hadi tunamaliza mzunguuko wa mwisho wa ufatiliaji wa utekelezaji wa kazi
za bajeti, Wizara haikua imepata muwafaka wa ujenzi huu kutokana na kampuni ya
RUNs ilishauri kutafuta eneo jengine kwa ajili ya ujenzi huo kwasababu ya ardhi
ya hapo haikubalini na ujenzi wa gorofa wanaoutaka na pia, gharama ya fedha walikusudia
kutumia kwa ajili ya kazi hiyo ambayo ni kiasi cha B. 1.4 hakitoshelezi, na
ikashauriwa kuongezwa kiasi chengine cha fedha kisichopungua Tsh. Bilioni moja.
Mheshimiwa Spika,
kwa upande mwengine Wizara iliwaomba Wakala wa Majengo nao kufanya utafiti wa
eneo hilo ambapo baada ya kukamilika kwa akazi waliyoagizwa ilitoa ripoti ya
kutaka ujenzi huo uendelee kwa misingi ya kusimamisha nguzo imara. Hivyo,
Kamati inashauri kwa Wizara kutafuta muwafaka wa ujenzi wa majengo ya Wodi ya
Mama na Mtoto yaliopo Hospitalini hapo kwa mujibu wa bajeti wanayoidhinishiwa
na kwa kufuata ushauri wa mjenzi ili kuepusha athari zinazoweza kutokea baada
ya ujenzi huo kukamilika.
Mheshimiwa Spika,
kupitia bajeti hii ya mwaka 2020/2021 Kamati inaiomba Wizara kutoa majibu ya
kina mbele ya Baraza hili tukufu kuhusiana na fedha ambazo zimekuwa zikiingizwa
katika bajeti zilizopita kwa ajili ya ujenzi huo ili iweze kuidhisha bajeti ya
mwaka huu bila ya matatizo yoyote.
PROGRAMU KUU YA UENDESHAJI NA
URATIBU WA WIZARA YA AFYA
Mheshimiwa Spika,
Kamati inaipongeza Wizara kufuatia ongezeko la bajeti kwa mwaka huu wa Fedha
2020/2021 kupitia programu ya Uendeshaji na Uratibu wa Wizara ya Afya ambayo imepangiwa
kutumia jumla ya Tsh. 20,312,959,000/- tofauti na mwaka wa fedha uliopita
2019/2020 ambayo programu hii iliidhinishiwa kutumia jumla ya Tsh.
17,428,825,000/- kwa ajili ya kazi zake za kawaida.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yetu kupitia programu hii
inaipongeza Wizara ya Afya kwa kupata Sheria mpya ya Utafiti na Wataalamu wa
Maabara za Tiba na Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Afya Zanzibar ambazo zote
kwa pamoja zimepitishwa katika kikao kilichopita na Tayari Mheshiwa Raisi wa
Zanzibar Dkt. Ali Mohamed Shein amezitia saini. Imani yetu kwamba Wizara kupitia
Taasisi husika zitafanya kazi kwa uweledi na uwadilifu wa hali ya juu kwa
misingi ya Sheria.
PROGRAMU KUU YA HOSPITALI YA MNAZI
MMOJA
Mheshimiwa Spika,
Kupitia (Fungu H02) la Hospitali ya Mnazi mmoja imepangiwa kutumia jumla ya
Tsh. 17,348,600,000/- kwa ajili ya kufundisha wanafunzi wa kada ya afya wa
ndani na nje ya Zanzibar na utoaji wa huduma za uchunguzi na matibabu kwa
wagonjwa wa rufaa.
Mheshimiwa Spika, Kamati
wakati ikifanya ziara katika hospitali ya Mnazi Mmoja iligundua kasoro kadhaa
ikiwemo ya Uchakavu wa Chumba cha Upasuaji, upungufu wa vifaa na ukosefu wa
mwanga wa kutosha katika chumba cha Upasuaji hali inayopelekea wakati mwengine
madaktari kushindwa kufanya kazi za upasuaji. Matatizo mengine ni pamoja na
kuharibika kwa AC mara kwa mara na ukosefu wa vyoo kwa ajili ya watu wenye
mahitaji maalumu. Kamati inaiomba Wizara katika bajeti hii ya 2020/2021 kupitia
changamoto hii ya uchakavu wa chombo cha upasuaji kuharakisha kupatikana kwa
Mkandarasi kwa ajili ya ukarabati wa chumba hicho.
Mheshimiwa Spika,
Baada ya maoni hayo ya Kamati, napenda kukushukuru kwa mara nyengine tena
Mheshimwa Spika, kwa kunipa nafasi ya kuwasilisha maoni ya Kamati yangu kwa
niaba ya Kamati pamoja na Wajumbe wa Baraza lako Tukufu kwa kunisikiliza kwa
umakini mkubwa, tunaimani Wizara hii inatekeleza majukumu yake kwa ufanisi
zaidi.
Mheshimiwa Spika,
mwisho kabisa, sasa niwaombe Wajumbe wa Baraza hili Tukufu, waichangie na
hatimae waiunge mkono bajeti hii, ili wamuwezeshe Mheshimiwa Waziri kufanikisha
na kutekeleza wa yale waliojipangia katika mwaka huu wa Fedha 2020/2021.
Mheshimiwa Spika,
Mimi mwenyewe na kwa niaba ya Kamati ya Ustawi wa Jamii, naunga mkono hoja kwa
asilimia 100%.
Naomba
kuwasilisha.
Ahsante,
……………………
Mhe. Mwanaasha Khamis Juma
Mwenyekiti,
Kamati ya Ustawi wa Jamii,
Baraza la Wawakilishi,
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment