Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt.Harrison
Mwakyembe akisisitiza kuisimamia COSOTA kuandaa mikataba kati ya nchi na nchi
ili wasanii wamuziki waweze kunufaika na kazi zao zinazopigwa katika vyombo vya
habari nchi ya nje, kwa kupata gawio kwa
lengo la kulinda hakimiliki ya kazi zao, leo jijini Dodoma alipokuwa
akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya Mhe.Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania kusaini waraka wa kuhamishia ofisi hiyo ndani Wizara Habari,
Utamaduni, Sanaa na Michezo.
Na Shamimu Nyaki –WHUSM
Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo
Mhe.Dkt.Harrison Mwakyembe ameeleza kuwa lengo la kuihamisha Taasisi ya Hakimiliki
(COSOTA) kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara kuja katika Wizara anayoisisimamia
ni kuhakikisha wadau wa Sanaa wanapata huduma sehemu moja kwa sababu asilimia 86% ya wadau wake ni
Wasanii.
Dkt. Mwakyembe ameyasema hayo leo Jijini Dodoma
katika Mkutano na Waandishi wa habari ambapo amesema kuwa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli jana tarehe 13/07/2020 amesaini Waraka
unaogawa majukumu kwa wizara kuruhusu mabadiliko hayo muhimu ambayo yanawagusa
wabunifu,watunzi waandishi wa
vitabu,kazi za Sanaa na Sanaa na jadi.
“Namuagiza Katibu Mkuu wa Wizara hii ndani ya saa
ishirini na nne awe amekutana na Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara ili
waweze kukabidhiana nyaraka muhimu za uendeshaji wa COSOTA”alisema
Dkt.Mwakyembe.
Aidha Waziri huyo ameeleza kuwa ujio wa COSOTA
katika Wizara ya Habari,Utamaduni Sanaa na Michezo utarahisisha ushirikiano na
Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TCRA) katika kulinda na kusimamia maslahi ya wasanii
wa filamu na muziki pamoja na kupanua wigo wa malipo na stahili za wasanii kwa
kazi zao katika majukwaa mbalimbali ya Sanaa kielektroniki.
Mhe.Waziri amesisitiza kuwa lazima COSOTA ya sasa iingie
mikataba na nchi za nje ambazo vyombo vyake vya habari vimekua vikipiga muziki
wa wasanii wa Tanzania bila kuwapatia gawio au kufaidika kwa namna yoyote ile.
…MWISHO..
No comments:
Post a Comment