Habari za Punde

Hotuba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Al Hajj Dk. Ali Mohameed Shein, Katika Baraza la Idd El Hajj - Julai 31, 2020, Sawa na Mwezi 10, Mfungo Tatu 1441, HIJRIA


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Alhajj Dk. Ali Mohamed Shein, akihutubia katika hafla ya Baraza la Eid Alhajj katika Ukumbi wa Mitihani Skuli ya Sekondari Bumbwini Wilaya ya Kaskazini "B" Unguja kwa mwaka huu limefanyika Kitaifa katika Wilaya hiyo.



BISMILLAH RAHMAN RAHIM

Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan;
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,

Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi;
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar,

Mama Fatma Karume,

Mheshimiwa Shamsi Vuai Nahodha;
Waziri Kiongozi Mstaafu,

Mheshimiwa Khamis Juma Maalim;
Waziri wa Katiba na Sheria,

Mheshimiwa Sheikh Saleh Omar Kabi;
Mufti wa Zanzibar,

Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid;
Spika wa Baraza la Wawakilishi,

Mheshimiwa Omar Othman Makungu;
Jaji Mkuu wa Zanzibar,

Sheikh Khamis Haji Khamis;
Kadhi Mkuu wa Zanzibar,

Waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Mawaziri,

Mheshimiwa Hussein Ali Hassan Mwinyi;
Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, ambaye pia, ni Mgombea Urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM),

Abdalla Juma Mabodi;
Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar,

Dkt. Abdulhamid Yahya Mzee;
Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi,

Waheshimiwa Wabunge na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Wastaafu,

Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya,
Wheshimiwa Washauri wa Rais,

Masheikh wote mliohudhuria,

Makatibu Wakuu na Manaibu Makatibu Wakuu wa Wizara mbali mbali,

Waheshimiwa Mabalozi,

Viongozi mbali mbali wa Serikali,

Viongozi wa Vyama vya Siasa,

Wageni Waalikwa,

Ndugu Wananchi,

Mabibi na Mabwana.


Assalamu Aleikum Warahmatullahi Wabarakatuh

IDD MUBARAK

Namshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu, Azza Wa Jalla, Mwenye Hekima, Ujuzi na Muweza wa kila jambo, ambaye kwa kudra zake, ametujaaliya uhai na afya njema; ambayo ndio yaliyotuwezesha kujumuika hapa leo, katika Baraza hili la Idd kwa kusherehekea Sikukuu hii ya  ya Idd el Hajj. Tunamuomba Yeye amshushie Rehema na Amani Mtukufu wa daraja, Mtume wetu Muhammad (S.A.W), Aali na Sahaba zake pamoja na waumini wote waliofuata mwendo wake mwema.  Allah, Subhanahu Wa Taala atujaalie na sisi uwezo wa kuyafanya mambo ya kheri na atuepushe  na shari na maovu, ili tufanikiwe hapa duniani na kesho mbele ya haki. 

Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uhai na afya njema na tukaweza kuishuhudia na kuisherehekea sikukuu ya Idd el Hajj ya mwaka huu kwa furaha kubwa, kwani kuna baadhi ya waumini wenzetu ambao tulishereheka nao katika Sikukuu kama hii mwaka jana, lakini kwa mapenzi yake Allah, ameshawaita mbele ya haki. Tunamuomba Allah, Subhanahu Wa Taala, awarehemu wote na awasamehe makosa yao wenzetu hao,  sisi tulioko nyuma yao atupe khatima njema.

Ndugu Wananchi,
Sherehe hizi za Idd el Hajj za mwaka huu, zimetufikia sisi Watanzania  tukiwa bado tumo katika hali ya msiba mkubwa wa kuondokewa na kiongozi wetu Mpendwa wa Kitaifa, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa Awamu ya Tatu, Marehemu Mheshimiwa Benjamin William Mkapa, ambaye kifo chake kilichotokea usiku wa tarehe 23 Julai, 2020, kuamkia Ijumaa iliyopita huko Dar es Salaam.  Wananchi wa Zanzibar tuliungana na Watanzania wenzetu katika wiki ya maombolezo ya Kitaifa kama ilivyotangazwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli baada ya kutokea kifo hicho.  Marehemu Rais Mstaaafu alizikwa nyumbani kwao Lupaso, Masasi juzi tarehe 29 Julai, 2020 na maombolezo ya Kitaifa yamemalizika jana.

Marehemu Mzee Benjamin Mkapa ataendelea kukumbukwa nchini mwetu, Barani Afrika na duniani kote, kwa uongozi wake uliojaa busara, hekima na upendo.  Tutamkumbuka kwa tabia yake ya ucheshi na uzalendo, ufanyaji kazi kwa bidii na nidhamu kubwa, ukweli na uwazi, sifa ambazo zimeweza kuendeleza umoja na mshikamano wa Watanzania wote kwa kipindi chote cha uongozi wake Serikalini, kwenye Chama cha Mapinduzi (CCM) na kwenye nyadhifa mbali mbali alizoshika nje ya nchi yetu.

Hata wananchi katika mataifa mbali mbali duniani walifaidika na busara na hekima zake pale ambapo alishughulikia masuala muhimu ya upatanishi na usuluhishi wa mizozo, migogoro na changamoto nyengine ilizokuwa zikitishia hali ya amani ulimwenguni.  Kutokana na thamani kubwa aliyonayo Mheshimiwa Benjamin Mkapa kwetu sote Watanzania, tunamuomba Mwenyezi Mungu amuweke mahali pema, na awape subira na ustahamilivu wafiwa na Watanzania wote katika kipindi hiki kigumu.  Ninakuombeni tusimame kwa muda wa dakika moja, kwa ajili ya kumkumbuka kiongozi wetu huyu mpendwa.

Ndugu Wananchi,
Natanguliza shukurani zangu za dhati kwa Mufti wa Zanzibar na watendaji wa  Ofisi yake, kwa kushirikiana vizuri na Kamati  ya Kitaifa ya Sala na Baraza la Idd pamoja na Uongozi wa Mkoa wa  Kaskazini Unguja na Wilaya zake kwa maandalizi mazuri ya shughuli hii. Nimefurahi kuona kwamba katika  Baraza hili wamehudhuria viongozi na baadhi ya wananchi wengine wakiwawakilisha wenzao kutoka kwenye Wilaya zote za Unguja na Pemba.  Ndugu zetu hao wamekuja kwa ajili ya kuifanikisha  hafla hii ya Baraza la Idd el Hajj, ambalo litakuwa la mwisho katika  uongozi wangu mwaka huu.  Nimefurahi sana kwa mahudhurio haya makubwa na maandalizi ya aina yake. Nakupongezeni sana. Vile vile,  natoa shukurani zangu za dhati kwa wageni waalikwa wote kwa kuhudhuria kwa wingi katika shughuli hii.  Kadhalika, nawapongeza Makamanda na Viongozi wa Vikosi vyetu vya Ulinzi na Usalama,  wapiganaji wote, Vyombo vya Habari na wananchi wote wanaotusikiliza kupitia vyombo mbali mbali kwa kuwa pamoja nasi katika shughuli hii.   Kwenu nyote nasema, ahsanteni sana. 

Leo tupo hapa Bumbwini  katika Wilaya ya Kaskazini B,  Mkoa wa Kaskazini Unguja, kwa ajili ya shughuli hii muhimu ya Baraza la Idd.  Leo asubuhi, tulijumuika pamoja na wananchi wa Mkoa huu katika Sala ya Idd- el- Hajj ambayo imesaliwa katika kiwanja cha Misuka, kilichopo eneo la Mahonda, na sasa tuko hapa kwa ajili ya Baraza la Idd. Tunaendelea na utekelezaji wa utaratibu maalum tulioupanga wa kusherehekea Sikukuu ya Idd- el- Hajj katika kila Wilaya kwa ratiba maalum iliyoandaliwa.  Utaratibu huu ulitekelezwa katika Wilaya zote kumi na mwaka huu tunaukamilisha katika Wilaya hii ya Kaskazini “B”.

Utaratibu huu umeanzishwa, ili kutoa fursa kwa wananchi katika maeneo mbali mbali waweze kuisherehekea siku hii muhimu pamoja na viongozi wao. Hapana shaka kwamba utaratibu huu umeweza kuimarisha mapenzi  miongoni mwetu na umeongeza imani ya umoja na mshikamano wetu.  Kwa hivyo, mafanikio haya tuliyoyapta ni makubwa na tunayo kila sababu ya jambo hili zuri tuliendeleze.

Ndugu Wananchi, 
Leo ni siku ya furaha, Waislamu na wananchi wote wa Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa jumla, tunaungana na Waislamu wenzetu waliopo katika nchi mbali mbali  kwa ajili ya kuisherekea siku hii ya Idd el Hajj.  Kama tunavyofahamu kwamba, ibada hii ambayo ni nguzo ya tano ya Kiislamu, huwa inatekelezwa na maelfu ya mahujaji wa rangi, wasifu na hadhi tafauti kutoka kwenye mataifa mbali mbali duniani, ambao wote hukusanyika katika nyumba tukufu ya Al-Kaaba, huko Makka kwa lengo moja tu, la kuitikia wito wa Mwenyezi Mungu Subahanahu Wa Taala.

Ibada hii ina uzito maalum katika Dini ya Kiislamu na Mwenyezi Mungu, Subhaanahu Wa Taala ametueleza uzito huo katika sehemu ya mwisho ya Aya ya 97 ya Surat Al-Imran, yenye tafsiri isemayo:
“….Na Mwenyezi Mungu, amewawajibishia watu  wafanye Hijja katika Nyumba hiyo; yule awezaye kufunga safari kwenda huko. Na atakayekanusha (asiende, na hali ya kuwa anaweza) basi Mwenyezi Mungu si muhitaji kwa kuwahitajia walimwengu”.

Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwawezesha Waislamu wenzetu walioko Saudi Arabia kuitikia wito wake wa kuitekeleza ibada hii muhimu, kwa mwaka huu na leo tunaungana nao baada ya kuikamilisha. Tunamuomba Mwenyezi Mungu Subhanahu Wataala azikubali Hijja zao na ibada zao zote walizozifanya katika Mji Mtukufu wa Makka na Madina na sehemu mbali mbali kabla na baada  ya Hijja. 

Ndugu Wananchi, 
Sote tunafahamu kwamba, hapa Zanzibar na Tanzania nzima kwa jumla, walikuwepo waumini wenzetu ambao mwaka huu walidhamiria kwenda kuitekeleza ibada hii, kama ilivyo kawaida. Hata hivyo, kwa bahati mbaya, safari ya kwenda huko kwa ajili ya kuitekeleza ibada hii haikuwezekana kutokana na kuzuka kwa janga la maradhi ya COVID-19, yanayosababishwa na virusi vya Korona.  Maradhi ya COVID-19 yaliyoleta, athari katika nchi nyingi duniani pamoja na Saudi Arabia.

Habari tunazoendelea kuzipata kutoka nchi nyengine kupitia katika vyombo vya habari na kutoka kwa baadhi ya wanaosafiri, kwamba, hadi sasa maradhi ya COVID-19, yanaendelea kuwepo katika mataifa mbali mbali. Kwa hivyo, kutokana na kuwepo maradhi hayo, Serikali ya Saudi Arabia kupitia Wizara yake ya Hijja na Umra, ndipo ilipoamua kuendelea kuchukua tahadhari, kwa kuwazuia mahujaji kutoka nje ya nchi hio wasiingie nchini humo katika msimu huu wa ibada.

Naamini kwamba Umoja wa Taasisi zinazoshughulikia masuala ya Hijja, kwa mashirikiano na Taasisi za Serikali zinazosimamia  Hijja, hapa Zanzibar (UTAHIZA), na Taasisi zote zinazosafirisha mahujaji zimeshaandaa utaratibu mzuri wa namna ya kuwahudumia wale mahujaji ambao wamekosa kwenda Hijja mwaka huu.

Ndugu  Wananchi,
Natoa shukurani zangu za  dhati kwa  wananchi wote  wa Zanzibar na Tanzania nzima kwa jumla kwa kuendelea kushirikiana na Serikali zetu zote mbili, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar  katika mapambano dhidi ya Maradhi ya COVID 19. Natoa pongezi kwa Kamati mbali mbali zilizoundwa katika ngazi ya Taifa, Mikoa, Wilaya na maeneo mengine yote, kwa ajili ya kupambana na maradhi haya. Umoja na mashirikiano tuliyoonesha na tuliyonayo katika kutii sheria, kufuata miongozo ya madaktari na wataalamu wa afya pamoja na viongozi, vimetuwezesha kupata mafanikio katika kuyadhibiti maradhi haya.

Ujasiri wetu wa  kuondosha hofu zisizo na msingi juu ya maradhi haya, uzalendo wetu na  kutokana na dua tunazoziomba tumeweza kupata mafanikio makubwa tunayoyashuhudia katika kupambana na maradhi haya. Mwenyezi Mungu amezipokea dua zetu. Sote tumefurahi kwa taarifa tulizopewa kwamba hadi kufikia tarehe 10 Juni, 2020, vituo vyetu vyote vilivyofunguliwa maalum kwa wagonjwa wa maradhi haya havikuwa na mgonjwa hata mmoja hadi hivi leo. Kutokana na matokeo hayo, Serikali ililazimika iregeze masharti tuliyoyaweka dhidi ya COVID- 19, hatua kwa hatua na hivi sasa hali yetu imekuwa bora zaidi, na ndipo Serikali ikaamua kuziruhusu huduma zote zinazohitajika katika maisha ya kawaida ziendelee; huku sote tunatakiwa tuendelee kuchukua tahadhari za kujikinga.

Tunapaswa tujifunze kutokana na athari na madhara tuliyoyapata wakati maradhi haya yalipoingia nchini na hatua madhubuti tulizozichukua. Tulilazimika tujinyime na tuyakose mambo muhimu tunayoyahitaji katika maisha yetu ya siku zote.  Lakini tulifanya hivyo, ili kuyanusuru maisha yetu kwa kujikinga na COVID-19.  Tuliendelea kumuomba Mwenyezi Mungu wakati wote, ili atuondoshee maradhi haya na atuzidishie afya njema, baraka na atujaalie kila la kheri hapa duniani na kesho akhera.

Kwa hivyo, tutaendelea kuomba dua kwa wingi na tutashikamana na subira kila tunapokutana na mitihani ya maisha, kama Mwenyezi Mungu alivyotuelekeza katika Aya ya 153 ya Surat Al Baqarah  yenye tafsiri isemayo:
“Enyi mlioamini! (Jisaidieni katika   mambo yenu)  kwa subira na sala,   bila ya shaka Mwenyezi Mungu yu  pamoja na wanaosubiri”.

Taarifa za maradhi ya COVID 19 bado zinaendelea kutolewa kila siku katika vyombo vya habari. Bila ya shaka, kuna mambo mengi ya kujifunza kutokana na taarifa hizo, na  tuendelee kuchukua tahadhari kwa kuzingatia  elimu ya kinga tuliyoipata, lakini tusisitishe shughuli za ujenzi wa Taifa na nyengine muhimu ikiwemo za kutafuta riziki kwa ajili ya familia zetu. Vile vile, tushikamane na mafundisho ya Kuran Tukufu, ili tuweze kumtanguliza Mwenyezi Mungu kwa kila jambo letu na kuondoa khofu, kwani Mola wetu Mtukufu, anatukataza kutanguliza khofu  kwa mambo tunayotaka kuyafanya, kama alivyotufahamisha hivyo  katika Aya ya 51 ya Surat Tawba yenye tafsiri isemayo:
          “Halitatusibu, ila alilotuandikia Mwenyezi Mungu. Yeye ni Mola wetu”

Ndugu Wananchi,
Uislamu unatufundisha kuwa kwa kila ibada tunayoifanya, tuzingatie mafundisho yake na tujitahidi kuyatekeleza katika maisha yetu ya kila siku.  Miongoni mwa mafunzo makubwa yanayopatikana katika utekelezaji wa ibada ya Hijja, ni utii wa sheria pamoja na kuimarisha umoja na mshikamano katika hali ya amani na utulivu. Ni vyema sote tuuone umuhimu wa kufungamana na mambo haya katika kuiletea nchi yetu maendeleo, kwani mambo haya ndio msingi mkubwa wa mafanikio.

Sikukuu hii inaambatana na kisa cha Nabii Ibrahim (AS) kilichoelezwa katika Kuran Tukufu, pale  alipooteshwa usingizini na Mola wake Muumba kuwa anamchinja mwanawe wa pekee, ambaye ni Ismail (AS). Kwa vile, ndoto za Mitume zilikuwa ni maamrisho kutoka kwa Allah, Nabii Ibrahim (AS) ilimlazimu ayatekeleze maamrisho hayo, na akamjuilisha mwanawe kuhusu utekelezaji wa amri ile. Naye Ismail (AS), aliridhia bila ya usumbufu. Haya yanathibitika katika Aya ya 102 ya Surat Saaffaat yenye tafsiri isemayo:
Basi alipofika makamo ya kwenda na kurudi pamoja  naye, alimwambia: “Ee mwanangu! Hakika nimeona katika ndoto ya kwamba ninakuchinja. Basi fikiri waonaje? ”Akasema: “Ee baba yangu! Fanya  unayoamrishwa, utanikuta Insha Allah miongoni mwa wanaosubiri”.



Ndugu Wananchi,
Kuanzia Aya hii ya 102 mpaka Aya ya 110 ya Surat Saaffaat, Mwenyezi Mungu Mtukufu anatuelezea tukio hili la Nabii Ibrahim (AS) na mwanawe Ismail, ambapo anatuonesha jinsi alivyowapa waja wake hao mtihani huo mzito, ili kuwapima imani yao juu Yake; na alipohakikisha kwamba wao walikuwa ni watu wenye imani thabiti Kwake, aliigeuza amri hio na alimpa Nabii Ibrahim mnyama amchinje, badala ya kumchinja mwanawe Ismail.

Mwenyezi Mungu Mtukufu anatufundisha kwamba kipimo cha imani na utu wa mtu ni miongoni mwa mambo muhimu katika uongozi. Kadhalika, anatufundisha umuhimu wa kutii sheria, pamoja na kushirikiana na kushauriana katika kupitisha maamuzi mazito. Vile vile, tunajifunza utii wa mtoto kwa mzazi wake na umuhimu wa kiongozi kuwa muadilifu.  Ni wajibu wetu viongozi na wazazi tuzitii na tuzifuate sheria pamoja  na kuwashirikisha tunaowaongoza  katika mambo muhimu ya maisha yanayotuhusu sote moja kwa moja. Bila ya shaka, kuna fadhila kubwa kutoka kwa Mola wetu kwa kuzitii amri zake na hutupa yale mambo yaliyo mepesi, tunapokua na imani ya kweli ya kufuata maamrisho yake.

Jambo jengine, kubwa tunalojifunza katika ibada ya Hijja ni usawa wa binaadamu mbele ya sheria na mbele  ya Mwenyezi Mungu. Waislamu wa  makabila mbali mbali  na  wenye vyeo na  uwezo wa fedha na mali uliotofautiana,  hukusanyika pamoja wakiongozwa na sheria zisitofautisha  vyeo, hadhi na mali zao katika kukamilisha ibada ya Hijja. Kwa hivyo, katika ibada hii ya Hijja tunajifunza  mengi kuhusu usawa mbele ya sheria na umuhimu wake katika kutekeleza na kufanikisha mambo mbali mbali katika maisha ya mwanaadamu.

Ndugu Wananchi,
Hivi sasa tunaelekea kwenye Uchaguzi Mkuu utakaofanyika katika mwezi wa Oktoba mwaka huu, kwa hivyo, tunapaswa  tukumbuke wakati wote kwamba msingi wa mafanikio yote tuliyoyapata katika awamu zote ni juhudi zetu za pamoja katika kufanya kazi, kuilinda hali ya amani na utulivu; pamoja na kudumisha umoja na mshikamano.  Kwa hivyo, tuendelee kushirikiana, ili tuhakikishe kwamba, Uchaguzi Mkuu  utakaofanyika katika mwezi Oktoba mwaka huu unafanyika kwa amani na utulivu,  ili Serikali ya Awamu ya Nane itakapoingia madarakani, iweze kuyashughulikia maendeleo ya nchi yetu kwa ufanisi zaidi.  Lazima tuhakikishe kwamba hatokei mtu, au kundi lolote likajaribu kuharibu amani ya nchi yetu, kupandikiza chuki, uhasama na fitina miongoni mwetu na ndani ya jamii yetu. Nawanasihi viongozi wa vyama vyote vya siasa na wagombea wao, wakati ukifika, wajinadi kwa wapiga kura  kwa kutangaza Ilani, sera na mipango ya vyama vyao.  Ni lazima wahubiri amani, umoja na mshikamano kwa maneno na vitendo,  wakijuwa kwamba, lengo lao ni kujinadi, ili wachaguliwe kwa ajili ya kuiletea maendeleo nchi yetu na kutoa huduma bora kwa wananchi. Ni wajibu wetu tuzingatie, tuziheshimu na tuzitii sheria na miongozo ya Uchaguzi inayotolewa na Tume zetu mbili za Uchaguzi (ZEC na NEC).

Ni jukumu letu tushikamane kwa kuishi kwa mapenzi baina yetu na tufanyekazi kwa pamoja.  Suala la kudumisha umoja ndani ya jamii, ikiwa ni msingi wa mafanikio  limehimizwa sana katika Uislamu. Mwenyezi Mungu Mtukufu anatwambia katika Quran Tukufu, sehemu ya Aya ya 103 ya Surat Aali- Imran kwa tafsiri isemayo:
“Na shikamaneni kwa kamba (dini) ya Mwenyezi Mungu nyote, wala msifarikiane”.   

Ili tuweze kuudumisha na kuuendeleza umoja ni lazima tujiepushe na tabia mbaya kama kudharauliana, kusengenyana, kuhusudiana, kuhasimiana na kushawishiana katika kufanya hujuma dhidi ya wananchi wenzetu na Serikali yetu, na badala yake tuhimizane katika kufanya mambo mema.  Vile vile, Allah, Subhanahu Wa Taala, anatuhimiza tuishi kwa kupendana na kusaidiana  katika Quran Tukufu, sehemu ya mwisho ya Aya ya 2 ya Surat Al- Maidah, kwa tafsiri isemayo:
“…Na saidianeni katika wema na taqwa, wala msisaidiane katika dhambi na uadui….”

Nawapongeza wananchi wote kwa kuendelea kuishi pamoja, na huku tunajiandaa kuzikaribisha shughuli za uchaguzi katika hali ya utulivu, umoja na maelewano mazuri. Hadi sasa, nchi yetu iko shwari,  harakati za kisiasa, kiuchumi na kijamii zinaendelea vizuri. Ni mategemeo yangu  kwamba  hali hii itadumu  hadi siku ya uchaguzi na baada ya uchaguzi.  Tukifanya hivyo, tutatoa  fursa nzuri kwa Serikali ya Mapanduzi ya Zanzibar ya  Awamu ya Nane ya kuanza utekelezaji wa mipango yake ya maendeleo kwa wepesi, hamasa zaidi na ari kubwa, ili hatimae  iweze  kupata mafanikio makubwa zaidi. Hii ndio dhamira na matakwa ya watu wa Zanzibar.  Wazanzibari wanataka maendeleo na kamwe hawataki fujo wala watu wagombane.

Ndugu Wananchi,
Ni dhahiri kwamba, licha ya mafanikio tuliyoyapata katika kipindi cha miaka kumi, iliyopita, lakini bado tunahitaji kuongeza kasi ya kuzifanyia kazi  changamoto tunazoendelea kukabiliana nazo, ambazo baadhi yake, zinaonekana huenda  zikahatarisha hali ya amani.  Kwa mfano, bado hatujafanikiwa kulitatua tatizo la vitendo vya ukatili na udhalilishaji dhidi ya wanawake na watoto. Ingawa tulizindua  Mpango Kazi wa Zanzibar wa Miaka Mitano wa Kupambana na Vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji dhidi ya Wanawake na Watoto hapo Agosti, 2017 na utekelezaji wake utaendelea hadi mwaka 2022. Kadhalika,  tulikuwa nao mpango uliofanana nao kabla ya hapo, lakini, bado tatizo la udhalilishaji wa watoto na kijinsia linaendelea kujitokeza katika sehemu mbali mbali za Unguja na Pemba. Tunaendelea kusikia matukio ya unyanyasaji na udhalilishaji  katika vipindi vya mawio vya ZBC Redio. Vile vile, matukio kama hayo yanaripotiwa  mara kwa mara katika vituo vya polisi. Kadhalika, wamejitokeza vijana wanaowasumbua wananchi, hasa wanawake kwa kuwavamia, kuwapiga na kuwanyang’anya vitu vyao. 

Kadhalika,  zipo taarifa za kuongezeka kwa vitendo vya wizi wa mifugo na mazao pamoja  na uchimbaji ovyo wa mchanga katika maeneo yasiyoruhusiwa.  Kwa hakika wananchi wamechoshwa na vitendo hivi na vyenginevyo na inaonekana kama wanaanza kukata tamaa.  Kwa hivyo, ni jukumu la vyombo vya ulinzi na usalama kwa kushirikiana na jamii, vikundi vya ulinzi shirikishi, tuwachukulie hatua za kisheria vijana hao na watu wengine wanaotenda uovu huo, ili tuhakikishe kwamba vitendo  hivyo tunavikomesha na wananchi wanaendelea kuishi kwa amani.  Tumesema sana kwa muda mrefu sana ni lazima kazi hii ifanywe na iwe endelevu.  Watu wanasikitika kwenye jamii yetu na wengine wanadiriki hata kuilamu Serikali kuhusu vitendo hivi.  Tutekelezeni wajibu wetu, kwani huruma hailei mwana. Sote tuwe tayari, kujitokeza mahakamani kila inapohitajika kwa ajili ya kutoa ushahidi kwa wale watakaoshuhudia vitendo vibaya  vikitendwa ndani ya jamii yetu. 

Malezi bora ndio msingi wa kumuandaa mtoto na maisha ya baadae. Tuendelee kushirikiana katika kuwasomesha na kuwapa malezi bora watoto wetu. Tuhakikishe wanatumia vizuri fursa za elimu zilizoandaliwa na Serikali yao kwa ajili yao.   Wazazi na  walezi  tufanye juhudi za makusudi  katika kuwasomesha watoto wote, hasa wale wanaojiandaa na mitihani mwaka huu, tukizingatia kwamba mfumo na mtiririko wa masomo yao umeathiriwa  kutokana na kufungwa skuli na madrasa kwa kipindi kirefu  kwasababu ya  maradhi ya  COVID 19.  Wazee wanatuhimiza kwamba “Udongo upate ulimaji na Kambare Mkunje angali mbichi”.

Ndugu Wananchi,
Utaratibu huu wa kusali sala ya Idd na shughuli za Baraza la Idd unanipa fursa nyengine ya kuyaona maendeleo na kuzifahamu changamoto za ndani zinazojitokeza katika Wilaya zetu na Mikoa yetu.  Nimefurahi kupata fursa ya kuona ukumbi huu mpya na wa kisasa uliojengwa ndani ya Wilaya hii.  Natoa pongezi kwa viongozi na wananchi wa Jimbo la Bumbwini kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini “B” pamoja na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali  kwa ujenzi wa ukumbi huu mzuri na wa kisasa wenye nafasi na uwezo wa kukidhi mahitaji ya shughuli mbali mbali za kiserikali na  kijamii. Haya ndio maendeleo tunayoyataka.  Hongereni sana.

Nimepata habari kwamba, Wazee wa Bumbwini, mmeunda Kamati maalum iliyojumuisha vijana kwa ajili ya kufuatilia kero na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika Jimbo hili na hata katika ngazi ya Wilaya. Ninafahamu kwamba, Kamati mliyoiunda  inaendelea kushirikiana vizuri  na uongozi wa Wilaya na Mkoa katika kutafuta uwezekano wa kujenga  skuli mpya ya Sekondari ya Bumbwini katika eneo la Bumbwini Gongoni,  kwenye kijiji kipya, kwa ajili ya kutatua changamoto ya msongamano wa wanafunzi uliopo katika Skuli ya Bumbwini, Sekondari na Msingi.  Naziunga mkono jitihada hizi na nakupongezeni kwa juhudi zenu hizo. Nauagiza Uongozi wa Wizara ya Elimu, ushirikiane na uongozi wa  Wilaya ya Kaskazini “B” na Mkoa huu wa Kaskazini  kwa ajili ya kulikagua eneo hilo, na baadae iwasilishwe taarifa itakayotoa mapendekezo na mpango wa kuufanikisha ujenzi wa  skuli hiyo.  Napenda nikumbushe kwamba, dhamira ya Serikali hivi sasa ni kujenga Skuli za ghorofa, ili tuwe na matumizi bora ya ardhi. Ni vyema suala hili nalo likazingatiwa katika ujenzi wa skuli hio. Ni kweli skuli mpya katika eneo jipya inahitajika, tukiangalia nje tunaona jinsi, msikiti na  makazi ya watu yalivyokaribiana  na majengo ya skuli.

Kadhalika, nimesikia kilio cha wananchi wa Wilaya ya Kaskazini “B” cha kutaka kuwa na Hospitali yenu ya Wilaya kama ilivyo katika Wilaya nyengine hivi sasa. Huu ni wivu ambao wengi tunaupenda yaani wivu wa maendeleo, ambao wananchi sote tunapaswa tuwe nao. Ni dhamira ya Serikali ya kuwa na Hospitali za Wilaya, Skuli za Wilaya, Viwanja vya Michezo vya Wilaya na mambo mengine. Haya ni masuala muhimu katika utekelezaji wa Mpango wa Ugatuzi na kwa maendeleo yetu ya baadae.

Nina taarifa kwamba, tayari mmeanza kulifikiria eneo kubwa  la wazi lilioko karibu na Skuli ya  Pangatupu  kwa ajili  ya ujenzi wa Hospitali hio. Kwa hivyo, uongozi wa Mkoa wenu na Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini “B” uanze mazungumzo na Wizara ya Afya na Wizara ya Nchi,  Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ, kuhusu ujenzi wa Hosptali hio katika eneo la Pangatupu mnalillofikiria. Ikithibitika kwamba eneo hilo linafaa kwa kuzingatia mipango miji na vijiji iliyopo na maendeleo ya muda mrefu ya Mkoa huu, basi nauagiza uongozi wa Mkoa uanze mradi huo japo kwa kujenga  jengo moja dogo kama ni kielelezo cha utekelezaji wa dhamira hio, na muweze kupata ardhi itakayohitajika kwa kazi hio. Mkifanya hivyo, bila ya shaka, Serikali ya Awamu ya Nane, itaweza kuuandaa mpango huu katika mipango yake baadae.  

Maendeleo ya Taifa lolote hupatikana kwa utaratibu wa hatua kwa hatua. Ndiyo maana,  kumekuwa na  usemi maarufu wa Warumi  uliotafsiriwa kwa  Kiingereza, usemao  Rome wasn't built in a day”, kwa maana ya kwamba “Jiji la  Roma (nchini Italia) halikujengwa kwa siku moja. Nakuhakikishieni kwamba suala hili mkiliendeleza na kulifanyia kazi kwa moyo mmoja, basi Wilaya ya Kaskazini “B” itakuwa na hospiali ya Wilaya baada ya miaka michache ijayo.  Ninakuhimizeni mlifanyie kazi wazo hilo, nami naliunga mkono kwa moyo wangu wote.  Serikali inawaunga mkono, jiandaeni na jipangeni.   

Mambo mbali mbali ya maendeleo yamefanyika katika Mkoa huu kwenye kipindi cha miaka kumi ya uongozi wangu.  Hata hivyo, ninaamini kwamba bado yapo mambo kadhaa yanayopaswa yatekelezwe.  Lakini ninamaliza muda wangu wa uongozi, nikiwa nimeridhika sana  na mafanikio makubwa tuliyoyapata katika kuimarisha miundombinu mbali mbali katika Mkoa huu, na Mikoa mengine ya Unguja na Pemba.  Nadhani, sitokosea nikisema kwamba Mkoa huu wa Kaskazini Unguja hivi sasa unaongoza hapa Zanzibar  kwa  kuwa na barabara mpya, nzuri na za kisasa. Haya ni matunda ya juhudi zetu za pamoja.  Natoa pongezi zangu za dhati, kwa wananchi waliokubali bila ya masharti kuondosha vitu na mali zao kwa ajili ya kupisha miradi ya ujenzi wa barabara tuliyoitekeleza katika Mikoa yote ya Unguja na Pemba.

Tuhakikishe kwamba tunazitumia barabara zetu kwa kuongeza kasi ya maendeleo. Barabara hizi, ziwe ni neema kwa  wakulima, wafugaji, wavuvi, wafanyabiashara, wafanyakazi, wanafunzi, watalii, wawekezaji na wananchi wote kwa jumla.

Kwa upande mwengine, nafahamu kwamba, siwezi kuja Bumbwini na niondoke bila ya kukumbushiwa juu ya mpango wa Serikali wa kuimaliza barabara ya Makoba-Kiongwe pamoja na ujenzi wa Barabara ya Bumbwini Mahonda.  Nataka nikuhakikishieni kwamba hizi ni ahadi za Serikali na kwa vyo vyote vile tutazitekeleza. Barabara hii ya Bumbwini-Mahonda ni muhimu katika kutekeleza dhamira yenu ya ujenzi wa hopitali ya Wilaya, kuendeleza  ujenzi wa bandari ya mafuta na gesi ya Mangapwani, pamoja na kuliunganisha eneo la Pangatupu na Zingwezingwe  na maeneo mengine ya Wilaya hii.

Nimepata taarifa juu changamoto zilizopo kwa Wananchi wa Wilaya hii baada ya kuporomoka kwa daraja la Mperura linalounganisha eneo la   Bumbiwini Misufini na Pangatupu. Serikali inaandaa mipango ya  kulifanyia matengenezo daraja lenu hilo, na panapomajaliwa, baada ya kipindi kifupi kijacho daraja hilo litatengenezwa na litaweza kupitika vizuri. 

Ndugu Wananchi,
Miongoni mwa  miji ya Zanzibar inayoendelea kukuwa kwa kasi hivi sasa ni Mji wa Nungwi ambao upo kwenye Mkoa huu wa Kaskazini. Mji huu umebahatika kuwa na mazingira mazuri, fukwe za kupendeza na kama walivyo watu wa Zanzibar, wakaazi wake ni wakarimu. Kwa jumla  Visiwa vyetu vya Unguja na Pemba  vinasifika kwa kuwa na mazingira mazuri na fukwe za kuvutia. Sijui kama wananchi wengi wa Zanzibar, wanajua kwamba, mitandao mingi inayotangaza utalii inausifu na kuutangaza ufukwe wa Nungwi kuwa  ni miongoni mwa fukwe  20 bora duniani. Kwa hivyo, tunakazi kubwa ya kuuendeleza mji wa Nungwi hivi sasa. Tujifunze kutokana na shida tunazozipata hivi  sasa katika utoaji wa huduma katika maeneo tuliyojenga bila ya kuzingatia mipango miji. Tusijikwae hapo hapo kila mara.

Kwa kutambua umuhimu wa Mji huu wa Nungwi, Serikali imeamua kujenga  Kiwanja cha Ndege kidogo, katika eneo la Kigunda karibu na mji wa Nungwi, kiwanja hicho hivi sasa kimeshafikia hatua nzuri. Katika  Shamshara za Maadhimisho ya Sherehe za Mapinduzi Matukufu, tarehe 10 Januari, 2020  kiwanja hiki kiliwekewa jiwe la msingi na Naibu Spika wa Baraza la Wawakilishi Mheshimiwa Mgeni Hassan Juma. Hivi sasa kinatumika  kwa safari za ndege ndogo ndogo za utalii na hapo baadae kitatiwa lami na kitakuwa cha kisasa.

Imani yangu ni kwamba kitakapomalizika kiwanja hicho kitazidi kufungua milango ya maendeleo na kuharakisha kasi ya ukuaji  Mji wa Matemwe.

Kwa hivyo,  kwa mara nyengine, nawahimiza viongozi wa Mikoa na  Wilaya zote za Unguja na Pemba mhakikishe kwamba Miji yote mipya tunayoijenga, inaendelezwa kwa kuzingatia utekelezaji wa  mipango miji. Migogoro ya ardhi iliyopo na itakayojitokeza itatueni kwa kuzingatia sheria na kanuni za Serikali ziliopo.

Ndugu Wananchi,
Sote tunafahamu kwamba baada ya kufanyika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu wa 2020, na kupatikana Rais mwengine wa Zanzibar, kwa mujibu wa  Katiba ya Zanzibar ya 1984, ndio itakuwa mwisho wa uongozi wangu sitoongeza hata dakika moja seuze sekunde moja. 

Kwa hivyo, hapana shaka kwamba, shughuli hii ya  Baraza hili la Idd el  Hajj tunayoifanya leo,  Mwenyezi Mungu akipenda itakuwa ni ya mwisho kwangu kuhudhuria na kutoa hutoba  nikiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.  Nikialikwa kama mgeni mwalikwa nitahudhuria na nina uhakika nitaalikwaKwa hivyo, natoa shukurani zangu za dhati  kwa wananchi wote wa  Zanzibar  na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jumla, kwa mapenzi makubwa mliyoonesha kwangu na kwa  kuiunga mkono Serikali yetu katika kuyatekeleza majukumu yetu kwa vipindi vyote viwili vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba. Kwa furaha kubwa ninawashukuru wananchi wote kwa kuendelea kuniunga mkono wakati wote, katika utekelezaji wa mipango yetu mbali mbali na kudumisha amani, mshikamano na upendo miongoni mwa wananchi wa Zanzibar.

Kwa pamoja, tumeweza kuyapanga na kuyatekeleza mambo mengi mazuri na makubwa kwa maendeleo ya nchi yetu. Tumeshirikiana kwa dhati kwa hali ya juu katika kuzitafutia ufumbuzi changamoto mbali mbali zilizokuwa zikijitokeza. Ni hivi karibuni tu nilipokuwa nikilihutubia Baraza la Tisa la Wawakilishi la Zanzibar, tarehe 20 Juni, 2020, nilielezea kwa kina  mafanikio tuliyoyapata na changamoto zilizojitokeza katika kuijenga nchi yetu.

Ndugu Wananchi,
Namalizia hotuba yangu, kwa kutoa shukurani zangu za dhati na naipongeza sana Kamati ya Kitaifa ya Sala na Baraza la Idd kwa kushirikiana vyema na uongozi wa Mkoa, Wilaya na wananchi wote kwa ajili ya  kuzifanikisha sherehe hizi. Natoa shukurani zangu za dhati kwa wananchi wa Mkoa wa Kaskazini, ambao ndiyo wenyeji wetu katika  sikukuu hii kwa mwaka huu wa 2020. Mashirikiano mazuri ya wananchi wa Mkoa huu ni kielelezo cha umoja, mshikamano na mapenzi kwa Serikali yenu, pamoja na uzalendo wa nchi yenu. Hongereni sana.

Vile vile, natoa shukurani kwa Vyombo vya Habari ambavyo vimewawezesha wananchi kuyafuatilia matangazo ya Baraza hili la Idd katika maeneo yao. Nawashukuru na nawapongeza Makamanda, Viongozi na wapiganaji wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama kwa uwajibikaji wao kwenye shughuli yetu hii adhimu na nyenginezo. Kadhalika, nakupongezeni na nakutakieni wananchi nyote kheri na baraka katika kuisherehekea sikukuu hii ya Idd el Hajj. Namuomba Allah Subhaanahu Wa Taala aturejeshe nyumbani sote kwa salama na furaha.

Asanteni sana.
WAKULLU AAMUN WA ANTUM BIKHEIR.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.