MakamuMwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akihutubia wakati wa mkutano wa mapokezi ya Mgombea wa Urais wa Zanzibar kupitia CCM Mhe.Dkt. Hussein Mwinyi, mkutano huo umefanyika katika viwanja vya Afisi Kuu ya CCM Zanzibar.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi ambae pia ni Makamo Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Zanzibar
Dk. Ali Mohamed Shein amesema uamuzi wa CCM kumteua Dk. Hussein Ali Hassan Mwinyi kuwa mgombea wa kiti cha Urais kupitia chama
hicho katika uchaguzi mkuu ujao, umezingatia uwezo mkubwa na uaminifu alionao
mgombea huyo.
Dk. Shein amesema hayo leo katika
viwanja vya Ofisi Kuu ya CCM Kisiwandui katika hafla ya mapokezi ya Mgombea wa
Chama hicho kuelekea uchaguzi mkuu ujao Dk. Ali Hussein Mwinyi, baada ya kukamilika
kwa mchakato wa kumpata mgombea kupitia vikao mbali mbali.
Alisema Dk. Mwinyi ni mzaliwa wa Zanzibar na mwanachama kindakindaki, akiwa kiongozi muaminifu alielitumikia taifa kwa juhudi kubwa na
mwenye kutoa maamuzi kwa hekima busara.
Alisema mwanachama huyo ni mtaratibu
na ana mahusiano mema na watu, akibainisha chama hicho kutokuwa na mashaka yoyote na
uwezo na uadilifu wake.
Aidha, alisema kutokana mwenendo bora
wa kiongozi huyo, CCM ina hakika kuwa atayalinda, kudumisha na kuyaenzi
Mapinduzi ya Zanzibar ya 1964.
Rais Dk. Shein alieleza kuwa CCM iko
tayari kuingia katika kinyang’anyiro cha uchaguzi mkuu, akibainisha kuwa na
matarajio makubwa ya kupata ushindi wa kishindo katika uchaguzi huo. .
“Serikali iko makini kwa uchaguzi,
fedha kwa ajili ya uchaguzi huo zipo”, alisema.
Nae, mgombea wa kiti cha Urais kupitia
chama hicho, Dk. Hussein Ali Mwinyi alisema azma ya kugombea wadhifa huo ni
kuwatumikia Wazanzibar pamoja na Watanzania wote kwa uwezo wake wote,
akibainisha dhamira ya kuwaletea maendeleo na ustawi katika maisha yao.
Alisema miongoni mwa vipaumbele vyake
ni pamoja na kuendeleza amani iliopo ili Zanzibar iweze kupiga hatua zaidi za
maendeleo, huku akiahidi kazi hiyo kufanyika kwa ushirikiano kati ya wananchi na vyombo vya ulinzi na usalama.
Alisema analenga kuimarisha umoja
na mshikamano wa Kitaifa miongoni mwa
Wazanzibari wote ili kuondokana na hatari ya kuibuka kwa ubaguzi wa kimajimbo.
Aidha, alieleza kuwa ataendeleza kasi
ya maendeleo iliyoanzishwa na mtangulizi wake na kukamilisha miradi yote ya
maendeleo kwa maslahi ya Wazanzibari.
Katika utekelezaji wa majukumu yake,
Dk. Mwinyi alisema hatakuwa na muhali, huruma wala na atasimamia vita dhidi ya
rushwa, ubadhirifu wa mali ya umma, uzembe pamoja na watendaji wote wasiowajibika
ipasavyo.
Aliwataka viongozi wa chama hicho
kuanzia ngazi ya shina hadi Taifa kujiweka tayari kwa kazi ili kuweza kukipatia
ushindi chama hicho, kupitia kampeni zitakazoendeshwa kisayansi ili hatimae kushika Dola.
Katika hatua nyengine, Dk. Mwinyi
aliahidi kutetea maslahi ya Zanzibar kupitia Jumuiya zote za Kikanda na zile za
kimataifa.
Mapema, Naibu Katibu Mkuu wa CCM
Zanzibar Juma Abdalla Sadalla alisema hatua ya kwanza ya uteuzi wa mgombea wa chama
hicho imekamilika, kupitia vikao halali vilivyoendeshwa kwa uwazi na bila
makundi.
Alimsifia mgombea huyo kuwa ni
mwanachama mchapakazi, mweledi, mwenye uelewa wa mambo na uwezo mkubwa katika kutoa maamuzi kwa hekima na
busara.
Mapema kiongozi huyo alipata mapokezi
makubw akutoka kw awnanachi na wanachama wa CCM, waliojikusanya kutoka uwanja wa
Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume hadi Ofisi Kuu ya CCM Kisiwandui,
akiwemo msanii maarufu wa kizazi kipya kutoka Tanznaia Bara Ali Kiba.
Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024
2231822
E-mail: abdya062@gmail.com
No comments:
Post a Comment