Habari za Punde

KARATE-DO NI NIDHAMU YA MAISHA

Sensei Rumadha Fundi mwalimu wa karate wa kimataifa akiwa katika mazoezi ya pampja na walimu wengine wa kimataifa katika semina maalumu

Na.Mchambuzi Sensei Rumadha Fundi
Mwana-Karate au kama ajulikanavyo kwa lugha ya mchezo huo uitwa kwa jina la “Karateka”. Karateka hubeba dhamana kubwa sana katika maisha yake ya kila siku kuhakikisha kwamba nidhamu ya mafunzo na desturi za uadilifu zinaenda sambamba na kuwa mfano bora wa kauli na matendo ya Sensei au mwalimu. Hivyo basi, hata wanafunzi wote wa Karate hufuata nyayo hizohizo kama jinsi ilivyo rithiwa toka vizazi na vizazi huko katika visiwa vya Okinawa,Japan kwa karne tofauti hadi hivi leo mfumo huo unaendelea.
Hazina hii muhimu ipo pia katika Sanaa zinginezo za mapambano toka Japan, kama vile Judo, Kendo, Aikido, Kobudo, Kenpo, Jiu – Jitsu, na Karate pia. Fahari hii ya Sanaa hizi za mapambano tokea Japan ambacho ni kisiwa kidogo na uwezo mkubwa wa kina katika sayansi ya mapambano, iliweza kumudu na kuwa na tofauti zote bila kuwa na kashfa, matusi, dharau, ubadhilifu kwa wanafunzi, hata kusengenya Sanaa au chama chochote nyingine kati yao na wafuasi au wanafunzi wake. Isitoshe basi, huko Japan,ususani visiwani Okinawa, kuna shule, au Dojo za mitindo au sanaa hizo mbalimbali kila mji na wilaya zote, lakini, hautasikia wala kuona moja ya kundi, chama au wanafunzi wakiwadharau wengine au kuwaongelea vibaya wale wasio kuwa chini ya mtindo wa aina moja, sababu tu dojo zao jirani au baadhi ya wanafunzi wao wanapenda kujifunza mfumo tofauti wa Karate na wenzao sasa unaanza uhasama wa mafunzo.
Kihistoria na hadithia za kweli tulizosikia hasa endapo unatembelea visiwani Okinawa kwenye chimbuko na sehemu takatifu kwa Sanaa ya Karate, jambo moja nililo weza shuhudia kwa macho na kimwili ni kwamba, hizi ni Sanaa za Japan na wajapan wote wanajivunia, bila shaka wanaziwakilisha vyema sana utamaduni hu una hata kushirikiana kwa maonyesho ya kikukuu ya kila mwaka ya Karate inayo wakusanya walimu, nanafunzi na masters wa mitindo yote ya Karate “KARATE DAY” katika mji mkuu wa Naha City, shehemu ya mtaa maarufu huko Naha uitwao “Kokusai Dori”, na kuonyesha mbini na Kata za Karate mitindo hiyo tofauti bila kujali tofauti zao kimwenendo na Maisha binafsi ya mtu kama jamii.
Pia, Okinawa utumia fursa hii kuwa enzi wale magwiji waliochangia mbinu na ubunifu wa kuendeleza Sanaa hii na pia kuisambaza duniani kote, na hatimae hata kwetu Tanzania ilifika miaka zaidi ya 47 iliyopita, yaani shule halali ya kutambulika, Hekalu la Kujilinda ilifunguliwa rasmi 1973 na Hanshi Nantambu Camara Bomani sensei, hatimae mwaka 1976 kutoa mikanda miesi wa kwanza wa tano Tanzania kwa majina: Zebedayo Mapfumo Gamanya sensei, Tola Sodoinde Malunga sensei, Magoma N.Sarya sensei, Adombe Mabruki sensei na Abome Mabruki sensei.
Jambo muhimu kwa wafuasi wa Karate tuzingatie sana maadili kwa weledi wa kimafunzo yetu, hususani kama jinsi ilivyo huko visiwani Okinawa, ni heshima, nidhamu na adabu ya kuwaheshimu wana karate wenzio, hata kama sio chama kimoja au mitindo isiyo sambamba na kujivunia jinsi gani sanaa hii imewezesha watu toka tabaka tofauti za maisha,hali ya kiuchumi, elimu tofauti , mataifa tofauti, lugha tofauti, na hata imani za dini tofauti wake kwa waume. Hivyo basi, hatuna budi tujifunze kwetu hapa Tanzania, lipi la kufanya ilituweze kuiwakilisha sanaa ya Karate kwa ubora wake na sio kuwa kana kwamba ni makundi ya kipinzani au kama jambo la kihuni na ubabe wa kutojuwa au kuifahamu historia na urafiki wa karibu kwa kila chama na mitindo tofauti kwa kuishi mji au mkoa mmoja kama jinsi ilivyo huko Okinawa, Japan ambako kuna maelfu ya Dojo na mitindo mbalimbali na hakuna uhasama wala utovu wa lugha za maneno machafu yasio na nidhamu ya mfano tunayojifunza na pia kuwafunza watoto katika kizazi kijacho kuepuka shari za ulevi, madawa ya kulevya na uhuni kupitia nguzo za ukumbi wa mafunzo “Dojo Kun”. Mfano: “Chunga tabia yako”, “Usiwe mwenye kujiaminisha sana mwenyewe”, “Ishi Maisha ya kawaida na yasio na makuu”, “Mafunzo hayana mwisho”.
Pia, kila mwana Karate mahili au Karateka, inampasa kuwa muadilifu na mwenye kujaribu kufuata historia ya kweli ya Karate kupitia mitindo yao na kuwa na elimu ya maelezo ya chama anacho kiwakilisha na kujenga weledi wa mafunzo ya filosofia hii. Waasisi muhimu na adimu kwa wafuasi wa Karate dunuani, hasa visiwani Okinawa, kupitia makumbusho ya Taifa ya Karate kwenye mji wa Tomigusuku, Okinawa katika ukumbi wa “Okinawa Karate Kai Kan”, kuna mengi ya kujifunza kana vile nilivyoshuhudia wakati wa maadhimisho ya miaka 65 ya chama cha “Jundokan” toka kilivyo anzishwa na master Eiichi Miyazato mwaka 1957 huko Asato, Naha City, Okinawa, Japan alikuwa ni mwanafunzi wa master Chojun Miyagi, mwanzilishi wa mtindo wa Okinawa Goju Ryu. Miyagi Chojun, wanafunzi wake wakiwemo kama vile, master Eiichi Miyazato sensei wa Jundokan Goju Ryu, master Seiko Higa sensei, master Tatsuo Shimabuku sensei, mwanzilishi wa Isshin Ryu, master Meitoku Yagi sensei, mwanzilishi wa chama cha Meibuka Goju Ryu, master Seikichi Toguchi sensei, mwanzilishi wa Shorei Kan Goju Ryu, master Gichin Funakoshi, mwanzilishi wa Goju Kai, niliweza shuhudia pia majina ya waasisi wakuu hawa kama ifuatavyo:
  • Sokon Matsumura. Matsumura sensei aliishi kati ya miaka ya 1809 hadi kufariki mwaka 1899, alizaliwa mji wa Shuri, Okinawa, alijifunza mbinu za awali za mapambano toka kwa mtu ajulikanae kwa jina la Kanga Sakukawa.
  • Anko Itosu. Itosu sensei hadi sasa huitwa “Father of Karate” yaani Baba wa Karate huko Okinawa. Alizaliwa mwaka 1831 mjini Shuri, Okinawa, Japan hadi mwaka 1915. Alitowa wanafunzi na waanzilishi wa mitindo mingi toka Okinawa kama vile kwa majina:
  • Gichin Funakoshi, mwanzilishi wa Shotokan, Kenwa Mabuni, mwanzilishi wa Shito Ryu, Choshin Chibana, mwanzilishi wa Shorin Ryu. Motobu Choki, mkufunzi wa Shuri-te na Tomari-te.

Walimu au masters wengine mitindo au vyama tofauti toka Okinawa ni: Kanryo Higaonna, Chojun Miyagi, Kyan Chotoku, Anko Sato, Kanbun Uechi, mwanzilishi wa mtindo wa Uechi Ryu. Haya yote niliyo yaeleza hapo, nikuzihilisha kwamba hesabu za watu hao maarufu visiwani Okinawa, waliweza kuisambaza Sanaa yao ya Karate vyema duniani hadi hii leo na kutufikia hata sisi nchini Tanzania bila utovu wa nidhamu, kejeli, matusi na lugha za kihuni kama jinsi baadhi ya watu wasio na upeo kifikra na kutoelewa kuifundisha Karate asilia. Ni wito na ombi kubwa kwangu kwa vyama na shule za Karate nchi Tanzania, kuimarisha haya maadhimio adimu tuliyo yapata kupitia sanaa ya mapambano na Karate za mitindo tofauti, kuimarisha na kujenda mwili na fikra kuwa kitu kimoja. Kutokuwa na kiburi, dharau na makuu kwa walimu wadogo, wenye nia nzuri wanafuatao nidhamu za wakuu wao wa dojo kuheshimiwa kama jinsi ilivyo desturi za kwenye chimbuko huko Japan. Tunaamini jinsi sanaa hii ilivyo na nguvu ya kuweza kuleta na kuwaunganisha watu, mataifa tofauti bila kujali tofauti zao chini ya imani moja tu, nayo ni moyo juu, mbinu na falasafa ya nidhamu ya mafunzo ya Karate. Tujenge tunacho amini, katika nguzo zetu za ukumbi wa mafunzo ili iwe msingi mkuu wa kizazi kijacho kwa ubora na umadhubuti, ushupavu kulinda usalama wa nchi yetu kwa mifano bora ya mafunzo ya Karate Tanzania na hata Afrika nzima.
Usia wangu, ukiambatana na uzoefu wa miaka takriban 42 ya weledi wa mafunzo ya Karate mpaka sasa, ushiriki wa semina “Gasshuku” kwenye mabara ya Marekani Kaskazini, Marekani ya kati, Ulaya na pia Japan kwenyewe chini ya walimu wakuu wa Karate maarufu duniani, nimejifunza na kuona walimu wa kuu au masters wengi sana ikiwa ni bahati kwangu ninayo ishukuru kwa yote niliyojifunza na kujenga urafiki wa kina toka kwa kila mmoja wao. Sikuwa na budi, bali kushiriki na kujadili njia sahihi na kukipa kipau mbele heshima stahiki kwa dojo zote tukijuwa kwamba kuna umuhimu wa kujua na kuelewa historia na chimbuko zake. Mwelekeo wa makundi au vyama na mitindo ya walimu wa Karate Tanzania, hauna budi kuutambua ukweli kwamba mafunzo hayana aidha umri au sababu hutokubali kufunzwa mbinu “Bunkai” na iliyemfunza mafunzo ya awali, endapo anauzoefu wa elimu na mbinu kadhaa zilizo sahihi. Maoni na mchango wa hoja hizi toka katika majarida ya makumbusho ya Karate “Okinawa Karate Kaikan”, wakati wa ziara yangu mwaka 2018 ya maadhimisho ya 65 ya chama chetu cha Jundokan toka kizaliwe iliyofanyika kwenye mji wa Tomigusuku, Okinawa, Japan.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.