Habari za Punde

Wizara ya elimu na mafunzo amali kuendelea kushirikiana na wadau kuipeleka mbele sekta ya elimu

Na mwandishi wetu
WAZIRI wa Elimu na Mafunzo  ya Amali Zanzibar Riziki Pembe Juma amesema Wizara yake itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali  wa maendeleo  ili kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kupiga hatua nchini.

Akizungumza katika kikao cha matayarisho ya makabidhiana ya Skuli mpya ya  Sekondari Donge baina ya Wizara ya Elimu na wafadhili wa Skuli hiyo  huko Donge mkoa wa Kaskazini Unguja amesema  Wizara yake
ilionesha mashirikiano mazuri na wafadhili kutoka Indonesia  ili kuhakikisha Skuli hiyo inakamilika ikiwa katika kiwango bora na salama  kwa Wanafunzi.


Aidha Riziki amesema  ili Taifa liongeze kiwango cha ufaulu kinahitaji Kua na Walimu wabunifu na  majengo mazuri yatakayokidhi Haja na kuleta ufanisi mzuri wa Elimu.

Hivyo amewataka wazazi kuhakikisha wanawahamasisha watoto wao kusoma kwa bidiii ili kuhakikisha kiwango cha ufaulu kinaongezeka katika Mkoa wao na kurejesha heshima ya Mkoa wao katika Elimu.

Sambamba na hilo Pembe  amewashukuru wafadhili wanaomalizia ujenzi huo na kuwataka kujitahidi kufanya matengenezo madogo madogo yaliobaki ili wanafunzi waweze kusoma kwa haraka.

Mapema Katibu Mkuu Wizara ya Elimu Zanzibar  injinia Idrisa Muslim Hija  amesema ni jukumu la  Wizara ya Elimu kuhakikisha  Wanafunzi wanapata Elimu katika mazingira salama, na ndio maana ikaamua kufanya
matengenezo yaliobainika ili kuwa na ubora zaidi.


Nae Mwenyekiti wa kamati ya maendeleo ya Donge Yahya Ali Ussi   amesema kamati yake ilikua mstari wa mbele kuhakikisha  ujenzi wa Skuli hiyo unaendelea vizuri ili uweze kusaidia kupunguza tatizo la uhaba wa madarasa katika Skuli ya  Donge.

Kwa upande wake  mwakilishi wa jimbo la Donge Dkt. Khalid Salum Mohammed ameipongeza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar kwa kuonesha mashirikiano mazuri kwa wananchi wa Donge hadi kuhakikisha
ujenzi wa Skuli hiyo unamalizika.


Ujenzi wa Skuli ya Sekondari  Donge ulianza 1993 kwa nguvu za wananchi kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.