Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk. Ali Mohamed Shein Ajumuika na Wananchi wa Zanzibar Katika Maziko ya Aliyekuwa Mbunge Jimbo la Mpendae na Mgombea Ubunge Kwa Tiketi ya CCM Jimbo la Mpendae Zanzibar Salim Hassan Abdallah Turky (Mr.White)


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk. Ali Mohamed Shein, akiweka mchanga katika kaburi lililowekwa mwili wa aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Mpendae kupitia CCM Marehemu Salim Hassan Abdallah Turky, yaliofanyika katika makaburi ya Fuoni Kijitoupele Jijini Zanzibar Wilaya ya Magharibi "B" Unguja.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein  leo ameongoza mazishi ya Mwanasiasa Mkongwe na Mgombea nafasi ya Ubunge Jimbo la Mpendae Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Salim Hassan Abdullah Turky yaliyofanyika katika makaburi ya Kijitoupele Mkoa wa Mjini Magharibi.

Viongozi mbali mbali wa vyama vya siasa, dini, serikali na  sekta binafsi pamoja na wananchi, wafanyabiashara, ndugu na jamaa walihudhuria  katika mazishi hayo akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania Ali Hassan Mwinyi.

Wengine ni Makamo wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Mohamed Gharib Bilal, Mgombea nafasi ya Urais wa Zanzibar kupitia CCM Dk. Hussein Ali Hassan Mwinyi,  Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kabih pamoja na Naibu  Kadhi Mkuu wa Zanzibar Sheikh Hassan Othman Ngwali.

Mapema Alhaj Dk. Shein aliungana na viongozi, ndugu, jamaa, marafiki na wananchi mbali mbali katika dua na sala ya kumsalia Marehemu  Salim Hassan Abdullah Turky (Mr. White) katika Msikiti wa “Noor Muhammad” uliopo Mombasa  Mjini Unguja.

Akisoma wasifu wa Marehemu huko Kijitoupele katika eneo la makaburi alipozikwa Marehemu, Waziri Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mohammed Aboud Mohammed alisema kuwa Marehemu Salim Hassan Abdullah Turky (Mr. White), aliyezaliwa Februari 11 mwaka 1963 amefariki dunia usiku wa kuamkia leo Septemba 15, 2020 huko katika Hospitali ya Tasakhtaa Global Jijini Zanzibar.

Waziri Aboud alieleza kuwa Marehemu Salim Turky alikuwa mfanyabiashara maarufu Zanzibar na muda mrefu hapa nchini ambapo ameanza shughuli zake za Biashara tangu miaka ya 1980 kwa kujishughulisha na uagiziaji na uuzaji wa bidhaa mbali mbali.

Aliongeza kuwa katika mwaka 1990 alijiunga na kuwa Mjumbe wa Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wakulima Zanzibar (Zanzibar National Chamber of Commence) na mwaka 2006 aliteuliwa kuwa Mdhamini wa Jumuiya hiyo hadi kifo chake.

Aidha, alisema kuwa katika shughuli zake za biashara Marehemu alikuwa ni mwanzilishi na Mwenyekiti wa “Turky Group of Company”, Kampuni ambayo inajishughulisha na Biashara za Utalii, mafuta na gesi, huduma za afya, viwanda, usafirishaji wa Baharini na kadhalika.

Kwa maelezo ya Waziri Aboud katika harakati za siasa tokea mwaka 1992 Marehemu alishiriki kikamilifu katika shughuli za kisiasa nchini ambapo alikuwa mpenzi thabiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambapo katika mwaka 2010-2020 alikuwa Mbunge wa kuchaguliwa na Wananchi katika Jimbo la Mpendae.

Alisema kuwa Katika kuelekea uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020 Marehemu alikuwa tayari ameteuliwa na (CCM) kuwa Mgombea wa kiti cha Ubunge katika Jimbo la Mpendae.

Aidha, Waziri Aboud alisema kuwa katika shughuli za Kibunge Marehemu aliteuliwa kuwa Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Viwanda na Biashara na Kamati ya Kudumu ya Ardhi Maliasili na Utalii katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kutokana na umahiri wake wa kufanyakazi kwa bidii katika Bunge, alisema kuwa Marehemu aliteuliwa kuwa Kamishna wa Tume ya Huduma za Bunge pamoja na kuwa Mjumbe katika mradi wa Umoja wa Mataifa wa Huduma za Bunge (Legislative Support Project) unaosimamiwa na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Mpango wa Maendeleo (UNDP).

Sambamba na hayo, katika masuala mazima ya kujitolea katika jamii, Waziri Aboud akisoma wasifu wa Marehemu Turky alisema kuwa mbali na kuwa mfanyabiashara na mwanasiasa pia alijitolea katika kusaidia masuala mbali mb ali ya kijamii bila ya kujali itikadi yake ya kisiasa ambapo aliweza kuwasidia watu mbali mbali kutokana na mahitaji yao.

Wasifu huo ulieleza kuwa Marehemu pia, alijitolea kikamilifu katika kuunga mkono juhudi za Serikali za kupambana na umasikini na kukuza uchumi.

Waziri Aboud alisema kuwa Marehemu atakumbukwa katika juhudi za kukuza sekta ya michezo na elimu ambapo katika mwaka 1993 alichaguliwa kuwa Meneja wa timu ya mpira wa miguu ya “Shangani Football Club” na ilifanikiwa kuchukua kombe la ubingwa wa ligi Kuu ya Zanzibar na mwaka 1995 alikuwa ni miongoni mwa waanzilishi wa Skuli ya Sunni Madrassa Jamat iliyopo Mkunazini.

Hivi karibuni katika Mkutano wa uzinduzi wa Kampeni za (CCM) zilizofanyika katika viwanja vya Kimandamaiti maarufu viwanja vya Demokrasia, Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alimnadi Marehemu Turky pamoja na wagombea nafasi wengine za uongozi ndani ya chama hicho.

Marehemu Turky ameacha kizuka na watoto watatu, Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahala pema peponi, Amin.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.