Habari za Punde

Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Mhe Dk. Ali Mohamed Shein Amdadi Mgombea Urais wa Zanzibar Mhe.Dk. Hussein Mwinyi Viwanja vya Jamahuri Makunduchi Mkoa wa Kusiniu Unguja leo 1/10/2020.Pekee mee \\\\

 

Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Zanzibar ambae pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akihutubia katika mkutano wa kampeni ya Mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM Mhe.Dk.Hussein Mwinyi, iliofanyika katika Uwanja wa Jamuhuri Makunduchi Mkoa wa Kusini Unguja leo 1/10/2020 na kumuombea Kura pamoja na Wabunge Wawakilishi na Madiwani wa CCM.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema CCM ndio chama pekee chenye uwezo wa kuongoza Dola na  hivyo amewataka wananchi na wanachama wa chama hicho kutofanya utani kukiweka madarakani.

 

Dk. Shein ambae ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, amesema hayo katika mkutano wa Kampeni ya chama hicho uliofanyika katika uwanja wa Jamhuri Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja.

 

Aliwataka wananchi hao kumchaguwa Dk. Hussein Ali Mwinyi, Wabunge, Wawakilishi na Madiwani wote wa CCM, akibainisha hatua hiyo itafanikisha azma yake ya kumkabidhi kijiti cha uongozi mgombea huyo.

 

Alisema kuna ulazima wa kumchagua Dk. Hussein Mwinyi, ikiwa ni hatua sahihi katika kudumisha Muungano wa Tanzania  pamoja na kuimarisha Mapinduzi ya Zanzibar ya 1964.

 

Alisema sifa za mgombea huyo hazina shaka, zikithibitishwa kutokana na historia ya utumishi wake katika nafasi mbali mbali serikalini.

 

Alisema umuhimu wa kuendeleza umoja na mshikamano ni jambo linaloeleweka vyema na mgombea huyo, hivyo akatowa wito kwa wanachama na wananchi wote kumchagua.

 

Alisema kwa kushirikiana na Rais John Pombe Magufuli, viongozi hao watashirikiana kuendeleza Muungano pamoja na kudumisha  Mapinduzi ya 1964.

 

Rais Dk. Shein aliwataka vijana kufahamu historia ya Zanzibar kuwa inatokana na Mapinduzi ya 1964, hivyo akabainisha kuwa maendeleo yote nchini yanatokana na Mapinduzi hayo, hivyo akasema  wana wajibu wa kuyalinda na kuyadumisha.

 

Aidha,  aliwataka kukataa rai za baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani watakaowaomba kuvipigia kura vyama vyao.

 

 Alisema Mapinduzi ndio ngao ya Zanzibar sambamba na Muungano kuwa  muhimili mkuu wa uhai Taifa hilo, hivyo ni lazima mambo hayo mawili yawepo, akibainisha Muungano huo umetokana na muungano wa Serikali mbili huru, jambo alilosema limebainishwa katika Ilani ya CCM.

 

Aliwataka wananchi na wanachama waliohudhuria mkutano huo  kuwakataa wapinzani kwa kigezo kuwa watalitia  Taifa kwenye misukosuko na akasisitiza umuhimu wa kudumisha sifa ya Mkoa huo ya kuwa ngome ya Chama hicho.

 

Nae, Mgombea wa Kiti cha Urais kupitia CCM Hussein Ali Mwinyi alisema katika kufanikisha dhana ya Uwajibikaji kazini, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar awamu ya nane inakusudia kuangalia stahiki zote za wafanyakazi katika utumishi wa umma.

 

Alisema Serikali itahakikisha stahiki zote za wafanyaakazi zinatolewa kwa wakati pamoja na  kuimarishwa kwa kuwaongezea mishahara kadri uchumi utakavyoimarika.

 

Alisema kuna umuhimu wa haki na wajibu kwenda sambamba , hivyo Serikali italenga kusimamia haki hizo pamoja na kusimamia uwajibikaji kikamilifu.

 

Alieleza kuwa dhamira ya kuimarisha sekta mbali mbali ikiwemo za kijamii, kunalenga kuhakikisha kila mmoja anawajibika kwa nafasi yake, hivyo akasisitiza umuhimu wa wafanyakazi kuondokana na wizi, rushwa na ubadhirifu wa  mali ya umma.

 

Katika hatua nyengine, Dk. Mwinyi alieleza vipaumbele vya serikali ya awamu ya nane Mkoani humo kuwa ni pamoja na kuajiri walimu wa Sayansi na Hesabati ili kuondokana na upungufu wa walimu katika fani hizo, sambamba na kujikita katika utoaji wa mafunzo katika vyuo vya amali ili kukidhi soko  la ajira.

 

Alisema katika kuimarisha sekta ya Ustawi wa jamiii, Serikali itaendeleza kazi nzuri iliofanywa na serikali ya awamu ya saba kwa kuendelea kuwapatia wazee posho la pensheni jamii la shilingi 20,000 kwa mwezi pamoja na kuangalia uwezekano wa kuwaongezea kadri hali ya uchumi itakavyoimarika.

 

Alieleza kuwa makundi ya walemavu na wanawake nayo yatapewa kipaumbele ili kuleta ustawi wa jamii.

 

Alisema pamoja na kazi nzuri ya kuipandisha daraja hospitali ya Makunduchi kuwa ya Wilaya iliofanywa na serikali ya awamu ya saba, Serikali ya awamu ya nane itaendelea kuiimarisha kwa kuiongezea wafanyakazi, vifaa pamoja na kuongeza bajeti ya gharama za madawa na vifaa tiba.

 

Akigusia changamoto mbali mbali zinazowakabili wananchi wa Mkoa huo, Dk. Mwinyi alisema Serikali atakayoiongoza itaimarisha miundombinu ya barabara mbali mbali ziliomo mkoani humo, ikiwemo ile ya Tunguu – Makunduchi  yenye urefu wa  kilomita 48 pamoja ya  Kitogani – Paje (kilomita 11).

 

Alisema sekta ya utalii ambayo ni muhimu katika kuimarisha uchumi itaimarishwa kwa kuhakikisha unawanufaisha wananchi na kubainisha kuwa utaratibu utaandaliwa ili kuwawezesha vijana kupata ajira,

 

Alisema vijana watapatiwa mafunzo ili kwenda sambamba na mahitaji pamoja na wananchi na wajasiriamali kupata soko la uhakika katika maeneo hayo  kutokana na bidhaa wanazozalisha.

 

Alisema Serikali itahakikisha  wananachi wote wanapata haki zao, hususan katika suala la umiliki wa ardhi na hivyo kuondokana na uonevu unaofanywa na baadhi ya watendaji wasio waaminifu pamoja na kuhakikisha wawekezaji wanalipa fidia katika maeneo wanayowekeza.

 

Dk. Mwinyi alisema changamoto za upatikanji wa  huduma za maji safi na salama, umeme pamoja na afya katika maeneo mbali mbali ya Mkoa huo zitashughulikiwa na kuzimariha kwa kuongeza wafanyakazi, kuwekewa vifaa,  kujenga miundombinu pamoja na kujenga matangi mapya.

 

 

Mapema, Katibu wa CCM Taifa, Dkt. Bashiru Ali Kakurwa, alisema Mkoa wa Kusini Unguja una rekodi ya kufanya vizuri katika chaguzi mbali mbali zilizopita, hivyo akawataka wanachama wa Chama hicho kuendeleza utamaduni huo, kwa kigezo kuwa ni ngome ya CCM.

 

Alisema mgombea wa Chama hicho Dk. Hussein Ali Mwinyi ana sifa kubwa miongoni mwa wanachama wote 16 waliogombea nafasi hiyo, sambamba na kumpongeza kwa kuendeleza utamaduni wa Maraisi waliotangulia wa kuwatembelea wazee.

 

Alimpongeza Dk. Shein kwa kuasisi utoaji wa Pensheni jamii kwa wazee wote waliofikia umri wa miaka 70, akibainisha hatua hiyo  ni jambo kubwa la kihistoria na kusema Serikali zote mbili zitaendelea kuzisimamia Serikali zake kuliendeleza jambo hilo.

 

Aidha, Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja, Ayoub Mohamed Mahamoud, ambae pi ni Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya Mkoa huo, akigusia utekelezaji wa Ilani ya CCM kwa kipindi cha 2015-2020, alisema sekta ya Afya imeimarika sana Mkoani humo, akibanisha  kabla ya kipindi hicho wananchi walikuwa wakipata huduma za afya katika Hospitali ya Cottage, ambapo hivi sasa imepandishwa daraja na kuwa Hospitali ya Wilaya, hatua iliyoimarisha upatikanaji wa huduma bora za afya.

 

Alisema katika kipindi hicho ujenzi wa Hospitali ha Rufaa katika eneo la Binguni Wilaya Kati umeanza, ikiwa ni juhudi za Serikali katika  kuimarisha sekta ya afya nchini.

 

Vile vile alisema sekta ya Elimu nayo imeimarika, ambapo pamoja na mambo mengine ujenzi wa Chuo cha Amali Makunduchi ulikamilika na hivyo kuwa tayari kwa ajili ya kuendesha mafunzo mbali mbali yatakayowawezesha vijana kuweza kujitegemea. 

 

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kusini Unguja, Ramadhan Abdalla Ali “Kichupa”  alimhakikishia mgeni rasmi kuwa wanachama wa Chama hicho katika Majimbo yote matano  Mkoani humo watampigia kura mgombea wa Chama hicho na kupata ushindi mkubwa.

 

Katika mkutano huo, viongozi mbali mbali wa CCM walishiriki, akiwemo Rais mstaafu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania mzee Ali Hassan Mwinyi,  Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Katibu mkuu wa CCM Taifa Dkt. Bashiru Ali Kakurwa,Waziri Kiongozi mstaafu Shamsi Vuai Nahodha pamoja na wake wa Viongozi wakuu.

 

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 

 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.