RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi ameahidi kutekeleza ahadi yake ya kupambana na rushwa, ubadhilifu wa mali ya umma na uzembe katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) ambacho hivi sasa anakiongoza rasmin.
Rais Dk.Mwinyi aliyasema
hayo leo katika hotuba yake aliyoitoa katika sherehe za mahafali ya 16 ya Chuo
Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), mara baada ya kutawazwa rasmin kuwa Mkuu
wa Chuo hicho, hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Dk. Shein, ndani ya kampasi
ya Chuo hicho huko Tunguu, Mkoa wa Kusini Unguja. Hafla iliyohudhuriwa na
viongozi mbali mbali wa vyama na Serikali akiwemo Makamo
wa Kwanza wa Rais Maalim Seif Sharif Hamad.
Katika hotuba yake,
Rais Dk. Hussein Mwinyi alisema kuwa akiwa Mkuu wa Chuo, atafuatilia kwa karibu
makusanyo ya ada, ruzuku kutoka Serikalini na kwa wahisani, matumizi ya thamani
ya vitu vinavyonunuliwa pamoja na vianzio mbali mbali.
Rais Dk. Mwinyi
aliutaka uongozi wa Chuo hicho kusimamia vizuri na kwa umakini na uadilifu
rasilimali za chuo, watunze vizuri nyaraka mbali mbali zenye kuonesha mali
zinazomilikiwa na chuo zikiwemo hati miliki za ardhi, nyumba na majengo
mengineyo huku akihiza haja ya kufanyiwa matengenezo nyumba na majengo ya chuo na
nyumba zote zinakaliwa wakati wote.
Aliwataka wahadhiri na
wafanyakazi kufanya kazi kwa bidii na nidhamu kwa kuzingatia sheria na maadili
yanayoongoza kazi zao pamoja na kujiandaa kitaaluma ili wawe wanapanda daraja
kwa kulingana na taratibu zilizopo.
Alisisitiza umuhimu wa
usafi wa mazingira na kuutaka uongozi kuhakikisha unaweka mazingira katika
Kampasi zao ili yaweze kuvutia kwa kuwa na miti ya vivuvi na bustani huku
akiwataka kujiandaa kwani hivi karibuni atafanya ziara katika Kampasi zote
kuangalia hayo yote aliyoyasema.
Aidha, Rais Dk.
Hussein mwinyi alisema kuwa Rais Mstaafu wa Awamu ya Saba Dk. Ali Mohamed Shein
ameonesha njia kwamba Chuo hicho ni miliki ya Watu wa Zanzibar na kinaendeshwa
na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa hivyo ni lazima kifundishe masomo
yanayoendana na mahitaji ya wananchi kiuchumi na kijamii.
Kwa msingi huo Rais
Dk. Mwinyi aliitaka (SUZA) kuwa mfano wa Chuo chenye mitaala na programu mbali
mbali za ufundishaji zinazozingatia mahitaji ya nchi pamoja na sera na mipango
ya maendeleo ya muda mfupi, muda wakati na muda mrefu.
Alieleza kuwa (SUZA)ina
kazi kubwa ya kufundisha wataalamu wa kutosha wanaohitajika kusimamia uchumi wa
Buluu.
Rais Dk. Mwinyi alitumia
fursa hiyo kumpongeza Rais Mstaafu Dk. Shein kwa kumkabidhi Chuo kikiwa
kimepiga hatua kubwa za maendeleo katika kipindi cha miaka 10 cha uongozi wake
ambapo miundombinu imeimarika, idadi ya Kampasi na idadi ya wanafunziimeongezeka,
wahadhiri na wafanyakazi pamoja na programu zinazofundishwa na hadhi na sifa ya
elimu inayotolewa imekuwa.
Rais Dk. Hussein ameitaka
(SUZA) kuandaa utaratibu mzuri zaidi wa kufanya tafiti na kuweka mkazo wa
matumizi ya tafiti katika maeneo mbali mbali yanayohusu uchumi wa Buluu na
sekta nyengine za uchumi.
Alieleza kuwa ni kazi
ya (SUZA) kwa kushirikiana na taasisi nyengine za Elimu ya Juu ikiwemo Tume ya
Sayansi na Teknolojia Tanzania (COSTECH) kufanya tathmini ya tafiti
zilizofanywa ndani ya kipindi cha 2015-2020 na uhalisia wa tafiti hizo kwa
mahitaji ya nchi.
Hivyo, alieleza kuwa
Zanzibar ina haja ya kuwa na ajenda mpya ya utafiti wa Kitaifa na kusisitiza
kuachana na tabia ya kutegemea wahisani hata katia mambo muhimu ya maendeleo
wanayoweza kufanywana Wazanzibari wenyewe.
Alisisitiza kwamba
atahakikisha wataalmu wote walioajiriwa na wanaolipwa mishahara wanatumia
taaluma na uzoefu wao kwa faida ya wananchi na wao wenywe kwani chuo hicho ni
lazima kiongeze kasi katika kufanya tafiti mbali mbali.
Alieleza kuvutiwa na
dhamira iliyokuwepo ya kuifanya (SUZA) kuwa ni Oxford ya Kiswahili na iwe
chimbuko la wataalamu, waandishi na malenga wa mashairi na kwa kushirikiana na
Baraza la Kiswahili la Zanzibar (BAKIZA), iwe ni kitovu cha kutoa Kamusi
zinazopendwa na zinazoaminika katika lugha ya Kiswahili.
Aidha, ameutaka
uongozi wa (SUZA), kuandaa mikakati mizuri ya kulinda lahaja za Kizanzibari, kuwa wepesi, kubuni misamiati
na istilahi zinazohitajika ili kuweza kwenda sambamba na mabadiliko ya
teknolojia.
Rais Dk. Mwinyi alitoa
kazi kwa uongozi wa (SUZA)kushirikiana na uongozi wa (BAKIZA) katika kuandaa
mikakati na kufanya jitihada za kutafuta ajira za Kiswahili nje ya nchi kwa
ajili ya wataalamu mbali mbali waliopo Zanzibar.
“Lazima tuwe na
mipango ya kutumia hazina yetu, kiswahili, katika kukuza ajira pamoja na
kuhakikisha kwamba tuna mipango imara ya kufundisha na kukieneza katika mataifa
mengine”.
Pia, alieleza haja ya
kwa Chuo hicho kuangalia upya mitaala yake na mbinu za ufundishaji kwani
wawekezaji wengi katika sekta ya utalii wanapenda kuajiri wafanyakazi kutoka
nje ya Zanzibar jambo ambalo yeye haridhishwi kuona hali hiyo licha ya kuwa wahitimu
wengi wanatolewa katika eneo hilo lakini bado vijana hawapati ajira.
Kwa wale walioomba
mikopo ya elimu ya juu na wakapata, Rais Dk. Mwinyi aliwahimiza wawe tayari
kulipa deni liliopo kwa kuzingatia sheria na makubaliano yaliyo katika mikataba
waliyoijaza.
Aliwapongeza wahitimu
wote na kuwataka kujiepusha na vishawishi na anasa vinavyoweza kuathiri masomo
yao huku akieleza kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuweka
mkazo kwenye sekta ya elimu katika ngazi zote kwa misingi na dhamira ile ile ya
waasisi wa Mapinduzi matukufu ya Zanzibar ya Januari 12. 1964.
Wakati huo huo, Rais
Dk.Mwinyi alimtunuku Shahada ya Heshima ya Udaktari wa Falsafa katika Sayansi
za Tiba, Rais Mstaafu wa Zanzibar Awamu ya Saba Dk. Ali Mohamed Shein na
kumpongeza huku akisisitiza kwamba wananchi wa Zanzibar wataendelea kumkumbuka
kwa ubunifu wake wa kuanzisha mambo mazuri ambayo watu wengi walihisi
hayawezekani.
Rais Mstaafu Dk. Shein
nae wka upande wake akitoa salamu zake za shukurani aliupongeza uongozi wa Chuo
hicho kwa kumtunuku Shahada hiyo ambayo itaendelea kumpa hadhi huku akieleza
imani yake kwamba Rais Dk. Mwinyi atakiendeleza vyema chuo hicho.
Nae Waziri wa Elimu na
Mafunzo ya Amali Simai Mohamed Said alieleza jinsi Wizara yake itakavyoendelea
kumuunga mkono Rais Dk. Hussein Mwinyi pamoja na kueleza mikakati mbali mbali
iliyowekwa na Wizara hiyo ili iweze kuleta manufaa katika sekta ya elimu.
Mapema Makamu Mkuu wa
Chuo cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) Dk. Zakia Mohammed Abubakar alimueleza Rais
Dk. Mwinyi kwamba Jamii ya Chuo hicho cha (SUZA), iko tayari kwa moyo mkunjufu
kufanya kazi na yeye kwa kufuata kikamilifu ushauri na maelekezo katika
kukiendeleza chuo hicho.
Aidha, alimpongeza
Rais Mstaafu Dk. Ali Moahmed Shein ambaye alikuwa Mkuu wa Chuo tokea mwaka 2010
hadi 2020 kwa juhudi zake kubwa za kukitumikia chuo hicho ambapo kwa juhudi
hizo ndipo chuo hicho kikaamua kumtunuku Shahada ya Udaktari wa Falsafa katika
Sayansi za Tiba kwa sababu sheria inaruhus kufanya hivyo.
Makamu Mkuu huyo wa
(SUZA), alieleza kuwa mwaka huu chuo hicho kinawahitimu jumla ya wanafunzi 1524
ambao Rais Dk. Mwinyi aliwatunuku vyeti
vyao kutoka programu 56 zinazofundishwa na
chuo hicho cha (SUZA).
Mkuu huyo alieleza
kwamba katika wahitimu wa mwaka wa masomo 2019/2020 jumla ya wanafunzi ambao
wamefanya vizuri zaidi ni 41 ambao kati yao 24 (52%) ni wanawake na 17 (48%) ni
wanaume na wanafunzi bora ni watatu.
Katika hafla hiyo,
Rais Dk. mwinyi aliwatunuku wanafunzi 244 wa ngazi ya Cheti, 799 kwa ngazi ya
Stashahada, 453 kwa ngazi ya Shahada na 28 kwa ngazi ya Uzamili huku
akiwakabidhi vyeti na zawadi wanafunzi bora watatu akiwemo Nassra Suleiman
Mohammed wa Shahada ya Kwanza aliyepata GPA 4.9, Ali Abdalla Moh’d wa
Stashahada aliyepata GPA 5.0 na Hanafi Abdallah Moh’d aliyepata GPA 4.9.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment