Habari za Punde

Marehemu Dkt.John Magufuli Alikuwa Kiongozi Mwenye Kumtegemea Sana Mwenyenzi Mungu.

 
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la MapinduziDk. Hussein Ali Mwinyi amesema kuwa maisha ya Marehemu Dk, John Pombe Magufuli yalikuwa ni darasa tosha kwa viongozi na Watanzania wote juu ya namna wanavyotakiwa kuishi.

Rais Dk. Hussein Mwinyi ameyasema hayo leo katika salamu zake alizozitoa huko katika ukumbi wa Chimwaga Jijini Dodoma katika Kongamano la kumuombea dua Marehemu Dk. John Pombe Magufuli ambalo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan alikuwa mgeni rasmi.

Katika salamu hizo, Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa Rais Magufuli alikuwa kiongozi mwenye kumtegemea sana Mwenyezi Mungu na kuamini kuwa yeye ndiye Muweza wa kila jambo.

Alisema kuwa Hayati Magufuli alipigania umoja na alikuwa karibu sana na viongozi na waumini wa dini na madhehebu yote  na kila mara aliwataka waumini wa dini zote kuiombe nchi na pia, hakusita kusaidia maendeleo ya dini bila ya ubaguzi.

Alisema kuwa imani yake hiyo ilimfanya ajiamini na kuwa na uthubutu wa kuchukua maamuzi mazito kwa yale aliyoamini na yenye manufaa kwa wananchi wa Jamhuri ya Muuugano wa Tanzania.

Alieleza kuwa Marehemu kila mara alikuwa akihimiza kufanyakazi kwa bidii kwa kutumia wito wake wa “ Hapa Kazi tu” na maneno aliyoyatohoa kutoka kwenye vitabu vya vitakatifu yasemayo “ Asiyefanya kazi asile” maneno ambayo yatakumbukwa kama dira ya uwajibikaji.

Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa Hayati Magufuli aliwafunza Watanzania kuwafikiria zaidi wanyonge na watu wenye mahitaji maalum mambo ambayo alitekeleza kwa vitendo ikiwemo kutoa elimu bure, ujenzi wa hospitali za kisasa, kuweka mkazo juu ya usambazaji wa huduma za maji, umeme vijijini, ujenzi wa miundombinu ya barabara pamoja na kushughulikia kero za wafanyabiashara wadogo wadogo.

Katika salamu zake hizo, Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa Hayati Magufuli hakuwa na kigugumizi katika kukemea na kupiga vita vitendo vya rushwa, wizi, uzembe na ubadhirifu wa mali ya umma ambapo ameacha mfano katika usimamizi wa matumizi bora ya fedha na rasilimali za taifa.

Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ina upekee wa kuwa na rasilimali mbali mbali na kuwa ni mfano Barani Afrika na duniani kote katika kudumisha amani, umoja na mshikamano.

Alisema kuwa Tanzania inaendelea kuonesha ukomavu katika kudumisha demokrasia na utawala bora ambapo Tanzania ina utaratibu mzuri wa Kikatiba wa kubadilisha uongozi hata pale ambapo Mwenyezi Mungu analeta mtihani wa kuomdokewa na viongozi wa Kitaifa, Tanzania huwa inafuvu.

Aliongeza kuwa hivi sasa Tanzania imekuwa mfano wa kuigwa duniani  kwa kuwa na Rais mpya ambaye ni Samia Suluhu Hassan ambae ni Mama wa kwanza kushika nafasi hiyo kubwa  hapa nchini na pia katika eneo la Afrika Mashariki.

Aidha, alisema kuwa Rais Samia ana mchango mkubwa katika kuiongoza Tanzania kufikia maono ya Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Magufuli sambamba na kuendeleza fira zake.

Kwa msingi huo, Rais Dk. Mwinyi aliwaomba Watanzania kumpa mashirikiano ya kutosha ili aendelee kusimamia kazi iliyoanzishwa na Hayati Rais Magifuli.

Rais Dk. Mwinyi aliahidi kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itampa ushirikiano wa kutosha Rais Samia katika kufanikisha majukumu yake.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Miwnyia lsiema kuwa anaungana na viongozi wa dini katika kumuombea dua Hayati Magufuli pamoja na nchi kwa ujumla.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.