Habari za Punde

Wawakilishi wajinoa kuwakabili Arusha Wazee Club.



Kikosi cha Timu ya Baraza la Wawakilishi Sport Club kwa upande wa Mpira wa Pete (Netball) kinaendelea kujinoa vikali ili kuakabiliana vyema na mashindano  ya kirafiki mara tu baada ya kumalizika kwa Mkutano wa Bajeti.

Wakizungumza katika mazoezi ya pamoja katika viwanja  Vya Baraza la wawakilishi Chukwani, Kocha na wachezaji wa kikosi hicho  wameahidi kufanya vizuri  katika mashindano hayo.

Kocha mkuu wa Timu hiyo, Amina Khamis Kapenta amesema,  ana matumaini makubwa ya kushinda  kutokana na mwamko na maandalizi mazuri ya  mazoezi kwa wachezaji wake.

Nae mlinda mlango  wa kikosi hicho yaani GK – goal keeper Mgeni Hassan Juma ambae pia ni Naibu Spika wa Baraza la Wawakilishi pamoja   na Mshambuliaji Lela Muhammed Musa wameahidi kuchukua ushindi huku wakitoa wito kwa wawakiishi wengine kuendelea kushiriki katika mazoezi hayo jambo ambalo pia litawasaidia katika kuimarisha afya zao.

Baraza  la Wawakilishi Sport Club kwa miaka mingi sasa imekuwa na kawaida ya kufanya ziara ya kimechezo Jijini Arusha  baada ya Mkutano wa Bajeti kila mwaka,  ikiwa ni wenyeji wa Arusha Wazee Club ambapo timu hiyo nayo hupata nafasi ya kuja Zanzibar wakati wa Msimu wa tamasha la Pasaka kila mwaka.

 

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.