Habari za Punde

Endeleeni Kufanyakazi Kwa Uadilifu na Kutoa Huduma Bora.

Watumishi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) wameaswa kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu na kwa misingi ya uwajibikaji ili kutoa huduma bora kwa wadau wake.

Rai hiyo imetolewa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Bw. Tixon Nzunda alipotembelea ofisi za Mfuko kwa ajili ya kufuatilia shughuli zinazofanywa na WCF.

“Nimefanikiwa kuzungumza na watendaji wa idara na vitengo vyote na moja ya maelekezo yangu ni kuwahimiza kutoa huduma kwa umma kwa kuzingatia misingi ya ueledi, uwajibikaji na usikivu na kuzingatia misingi na miongozo ya uendeshaji kazi serikalini”, alisema Bw. Nzunda.

“Pia nawasisitiza kuhakikisha kuwa utendaji wa shughuli za umma unazingatia misingi ya kujenga ustawi wa wananchi. Tumieni rasimilimali zilizopo kwa kuzingatia thamani ya fedha na uwekezaji ufanyike katika maeneo yenye tija ili kulinda amali za fidia kwa wanachama”.

Bw. Nzunda ameelekeza Mfuko kuhakikisha unaimarisha zaidi mifumo ya kielektroniki kutoka asilimia 80 hadi 100 ili huduma zote za madai ya fidia zifanyike kwa njia ya kielektroniki.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) Dkt. John Mduma, amesema Mfuko utazingatia kuimarisha huduma za kielektroniki ambapo pia unaendelea kuutangazia umma kuhusu punguzo la Tozo ya michango lililofanywa na Serikali kwa sekta binafsi kutoka asilimia 1.0 hadi 0.6. Aidha, Dkt. Mduma ameishukuru Serikali kwa hatua hiyo muhimu na kuwasisitiza waajiri sekta binafsi kuzingatia mabadiliko husika.

Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Bw. Tixon Nzunda (katikati), akisikiliza maelezo kutoka kwa Mkuu wa Kitengo cha Mifumo ya Computer, Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Stephen Goyayi, (kushoto) huku Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko huo, Dkt. John Mduma akisikiliza wakati wa ziara ya Bw. Nzunda aliyoifanya Julai 19, 2021 kwenye ofisi za Mfuko huo kwa nia ya kuangalia utendaji na utoaji huduma wa Mfuko.
Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Bw. Tixon Nzunda (wapilia kushoto), Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma (Wakwanza kushoto) na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusoiano, Bi. Laura Kunenge wakimsikiliza Bw. Yusuph Kihiyo, Meneja wa Kitengo cha Kumbukumbu WCF wakati wa ziara ya Bw. Nzunda kutembelea ofisi za Mfuko kwa ajili ya kufuatilia shughuli zinazofanywa na WCF.
Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Bw. Tixon Nzunda alipotembelea ofisi za Mfuko kwa ajili ya kufuatilia shughuli zinazofanywa na WCF.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.