Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ofisi ya Makamu wa Rais Taarifa kwa vyombo vya Habari Iliotolewa na Mhe. Selemani Said Jafo (MB.) Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira katika Kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Hifadhi ya Tabaka la Ozoni 16 SEPTEMBA, 2021
Ndugu Wananchi,
1. Tarehe 16 Septemba mwaka huu tutaungana
na Jumuiya ya Kimataifa kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Hifadhi ya Tabaka la
Ozoni kama ilivyoagizwa na Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Azimio lake nambari
49/114 la tarehe 19 Desemba 1998 kama kumbukumbu ya tarehe ya kutiwa saini Itifaki
ya Montreal (Montreal Protocol - 1987)
kuhusu kemikali zinazomong’onyoa Tabaka la Hewa ya Ozoni angani.
Ozoni ni hewa iliyoko kwenye angahewa ya juu, takribani kilometa 10 hadi 50 juu ya ardhi. Kazi yake kubwa ni kuchuja sehemu kubwa ya mnururisho wa mionzi kama “Ultraviolet B” isifike kwenye uso wa dunia. Ujumbe wa mwaka huu ni “Montreal Protocol - Keeping us, our food and vaccines cool”. Mkataba wa Montreal: Tulinde Afya ya Binadamu, Hifadhi ya chakula na kuhakikisha chanjo za Uviko 19 ni salama” Ujumbe wa maadhimisho haya una lengo la kukumbusha Jumuiya ya Kimataifa kuwa utekelezaji wa Itifaki ya Montreal kuhusu udhibiti wa kemikali zinazomong’onyoa tabaka la ozoni umeweka mfumo thabiti wa kuhakikisha kuwa afya ya binadamu na mazingira zinalindwa ikiwemo tabaka la ozoni.
Vilevile, ujumbe huu unazikumbusha nchi wanachama wa Itifaki ya Montreal kuhakikisha kemikali mbadala (gesi) zinapatikana kwa urahisi na kwa gharama nafuu ili kuchangia katika hifadhi ya chakula na jitihada za kupambana na janga la maambukizi ya Ugonjwa wa virusi ya Korona (UVIKO – 19) katika kuhakikisha kuwa chanjo zinakuwa salama.
2. Tabaka la Ozoni linapoharibiwa huchangia kuruhusu mionzi zaidi ya “Ultraviolet B” kufika kwenye uso wa
dunia na hivyo kusababisha kuongezeka kwa magonjwa kama vile saratani ya ngozi,
uharibifu wa macho yaani "mtoto wa jicho" unaosababisha upofu,
upungufu wa kinga dhidi ya maradhi na kujikunja kwa ngozi. Aidha, madhara
mengine ni kuharibika kwa mimea hasa mazao ya kilimo kutokana na kuathirika kwa
maumbile na mifumo ya ukuaji. Vile vile, baadhi ya kemikali hizi husababisha
kuongezeka kwa joto duniani na hivyo kuchangia katika mabadiliko ya tabianchi.
3. Ili kulinda tabaka la Ozoni, Serikali za mataifa mbalimbali zilikubaliana
kuunda Mkataba wa Vienna (Vienna Convention) wa Hifadhi ya Tabaka la Ozoni
mwaka 1985. Mkataba huu unasisitiza ushirikiano katika utafiti, usimamizi na
ubadilishanaji wa taarifa za hali ya Tabaka la Ozoni kutokana na kupungua kwa
matumizi yake. Vile vile ilianzishwa Itifaki ya Montreal (Montreal Protocol) inayohusu
udhibiti wa kemikali zinazomong'onyoa Tabaka la Ozoni na Itifaki hii ilipitishwa tarehe 16 Septemba, 1987. Lengo kuu la
Itifaki hii ni kupunguza uzalishaji na matumizi ya kemikali zinazomong'onyoa
Tabaka la Ozoni kwa ratiba maalum ili kutoa nafasi kwa mabadiliko ya teknolojia na upatikanaji wa kemikali mbadala hasa kwa nchi
zinazoendelea.
Ndugu Wananchi,
4.
Aidha,
baadhi ya kemikali mbadala zilizopendekezwa kuwa rafiki kwa Ozoni,
zimegunduliwa kuwa zinachangia ongezeko la joto duniani na kusababisha
mabadiliko ya tabianchi.
5. Itifaki ya Montreal imefanyiwa marekebisho mara tano (5) hadi sasa kufuatia ongezeko la orodha ya kemikali ambazo ama zina athari kwa tabaka la ozoni au ni rafiki kwa ozoni lakini zinachangia mabadiliko ya tabianchi. Marekebisho ya hivi karibuni yalifanyika Kigali, Rwanda mwaka 2016. Mwezi Novemba, 2019 Tanzania iliridhia Marekibisho ya Kigali yenye lengo la kupunguza na baade kuondosha uzalishaji na matumizi ya kemikali ambazo hapo awali zilikuwa ni mbadala wa kemikali zinamong'onyoa Tabaka la Ozoni na baadae kugundulika kuchangia katika ongezeko la joto duniani na kusababisha mabadiliko ya tabianchi. Kupitishwa kwa marekebisho haya kutachangia katika jitihada za kukabiliana na kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi. Baada ya kuridhia marekebisho ya Kigali Tanzania inafanya mapitio ya Kanuni za Usimamizi wa Kemikali Zinazomong’onyoa Tabaka la Ozoni za Mwaka 2007 ili kuhuisha marekebisho ya Kigali katika kanuni husika.
6. Hadi sasa Itifaki ya Montreal imepata mafanikio makubwa ya kupunguza takribani
ya kiasi cha asilimia 98 (takribani tani 1.8) ya uzalishaji wa matumizi ya
kemikali zinazomong’onyoa Tabaka la Hewa ya Ozoni. Punguzo hilo la matumizi ya
kemikali hizi limechangia katika juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi
kwa sababu baadhi ya kemikali zinazomong’onyoa tabaka la Ozoni pia husababisha
kuongezeka kwa joto duniani. Kwa mfano, kiasi cha kemikali kilichoondolewa
katika matumizi ni takriban tani bilioni 135 za hewa ukaa na hivyo kuchangia
kwa kiasi kikubwa katika kukabiliana na ongezeko la joto duniani na mabadiliko
ya tabianchi. Aidha, matokeo ya tafiti yanathibitisha kwamba kiwango cha
kemikali zinazoharibu tabaka la Ozoni angani kinaendelea kupungua na
inakadiriwa kuwa iwapo jitihada za utekelezaji wa Itifaki hii zitaendelea,
Tabaka la Ozoni litarudi katika hali ya kawaida ifikapo katikati ya karne hii.
Ndugu Wananchi,
7. Ili kufanikisha utekelezaji wa Itifaki ya Montreal, mwaka 1996 Serikali iliandaa na kutekeleza Programu ya Taifa ya kuondosha matumizi ya kemikali hizi. Mikakati ya kitaifa ndani ya Programu hii ni pamoja na:
i) Kujenga uwezo wa Taasisi zinazosimamia utekelezeji wa Mkataba;
ii) Kuweka takwimu za kemikali hizo;
iii) Kutoa elimu kwa wadau na kwa umma wa Watanzania kuhusu umuhimu wa Tabaka la
Ozoni na hatari zinazolikabili;
iv) Kusambaza habari kuhusu kemikali na tekinolojia mbadala;
v) Kubadilisha tekinolojia katika viwanda vinavyotumia kemikali haribifu;
vi) Kutoa mafunzo yanayolenga kuimarisha ujuzi katika sekta ya kuhudumia
viyoyozi na majokofu;
vii) Kuimarisha mbinu za upunguzaji wa matumizi ya kemikali husika kwa kuanzisha
mtandao wa kunasa, kusafisha na kurejeleza vipoza joto;
viii)
Kuhamasisha na kuhimiza
matumizi ya kemikali na tekinolojia mbadala na rafiki kwa tabaka la Ozoni; na
ix)
Kuweka taratibu za
kudhibiti uingizaji na matumizi ya kemikali zinazodhibitiwa na Mkataba wa
Montreal.
8. Hatua hizi zimewezesha Tanzania kuondosha kemikali hizi kwa mujibu wa
ratiba iliyowekwa na Itifaki kwa kudhibiti uingizaji wa kemikali husika kupitia
mipaka ya nchi yetu.
Aidha, wafanyabishara wengi ambao ni
wauzaji wa kemikali husika wamekuwa na uelewa mkubwa na hivyo biashara ya
kemikali mbadala imeendelea kukua mwaka hadi mwaka.
9. Chini ya Programu ya Taifa ya kuondosha matumizi ya kemikali haribifu,
Serikali iliandaa Mpango wa Usimamizi wa Vipozi (Refrigerant Management Plan) ambao utekelezaji wake umefanyika kama
ifuatavyo:
i.
Kuandaa Kanuni za
Usimamizi wa Kemikali Zinazomong’onyoa Tabaka la hewa ya Ozoni na zilianza
kutumika tarehe 7 Desemba 2007 ambayo inafanyiwa mapitio ili kuhuisha
marekebisho ya Kigali katika kanuni husika;
ii.
Jumla ya mafundi mchundo
wa viyoyozi na majokofu 500 wamepatiwa mafunzo kuhusu njia bora za kuhudumia
vifaa hivyo bila kuathiri Tabaka la hewa ya Ozoni;
iii.
Kusambazwa kwa Vitambuzi
vya kemikali hizi vipatavyo 18 kwa ajili ya usambazaji katika vituo vilivyo
mipakani mwa nchi yetu;
iv.
Mashine 20 za kunasa na
5 za kunasa na kurejeleza gesi chakavu
zimenunuliwa na kusambazwa kwa karakana 20 na Vituo vitano vya Kikanda vya
kunasa na kusafisha gesi chakavu za Majokofu na Viyoyozi katika vyuo vya VETA
vya Mwanza, Chang’ombe - Dar es salaam, Kigoma, Mbeya na Mkokotoni-Zanzibar;
v.
Jumla ya maafisa forodha
na wasimamizi wa sheria 200 wamepatiwa mafunzo kuhusu udhibiti wa kemikali
zinazomong’onyoa Tabaka la hewa ya Ozoni.
Ndugu Wananchi,
10. Hapa nchini maadhimisho haya yatafanyika kwa njia ya uelimishaji umma
kuhusu Tabaka la Ozoni, faida zake, madhara ya kuharibika kwa Tabaka hili na
matumizi salama ya bidhaa zenye kemikali rafiki kwa Tabaka la ozoni. Aidha,
mafunzo yatatolewa kwa maafisa forodha na wasimamizi wa sheria kuhusu namna ya
kudhibiti uingizaji wa kemikali zinazoharibu tabaka la ozoni. Hivyo kupitia
kwenu wanahabari naamini elimu hii itaendelea kutolewa kwa jamii ya Watanzania
ili kuongeza ushiriki wao katika kutekeleza jukumu hili muhimu la kulinda
sayari hii.
11. Ni muhimu tuzingatie kwamba juhudi za kila mmoja wetu zinatakiwa ili
kupunguza na kuondosha madhara katika Tabaka la Ozoni yanayosababishwa na
bidhaa tunazonunua na kutumia majumbani au sehemu za biashara. Natoa wito kwa
kila mwananchi kushiriki katika kuhifadhi Tabaka la Ozoni kwa kuzingatia mambo
yafuatayo:
i.
Kuepuka kuingiza nchini gesi zilizopigwa
marufuku na vifaa vinavyotumia gesi haribifu kama vile majokofu na viyoyozi vilivyokwishatumika (mitumba) na ambavyo vinatumia
vipoozi aina ya R22 na R134.
ii.
Kuingiza nchini vipoozi mbadala na rafiki kwa tabaka la Ozoni kama vile R209, R407, R404 na R717.
iii.
Kununua bidhaa
zilizowekwa nembo rasmi isemayo “Ozone
friendly” yaani “sahibu wa Ozoni” au “CFC-free”
ikiashiria haina wala haikutengenezwa na kemikali zinazomong’onyoa Tabaka la Ozoni.
iv.
Kuepuka kutupa ovyo
majokofu ya zamani ama vifaa vya kuzima moto vyenye kemikali zinazomong’onyoa Tabaka
la Ozoni aina ya “CFCs” na “halon”. Hivyo, ushauri wa kitaalamu
kutoka kwa mafundi ama mamlaka zinazohusika.
v.
Kuepuka matumizi ya kemikali aina ya
“Methyl bromide” kufukizia udongo, na
badala yake kutumia mbinu mbadala na salama pamoja na mbinu tungamanishi za
udhibiti wa wadudu waharibifu yaani “integrated
pest management”.
vi.
Mafundi wa majokofu na
viyoyozi wahakikishe kuwa wananasa
na kutumia tena vipoozi (refrigerants)
kutoka kwenye viyoyozi, na majokofu wanayohudumia badala ya kuviachia huru visambae
angani. Aidha, mafundi watoe elimu kwa
wateja wao juu ya njia rahisi za kutambua uvujaji wa vipoozi kutoka katika
majokofu na viyoyozi wanavyotumia.
12. Nawatakieni maadhimisho mema ya Siku ya Kimataifa ya Hifadhi ya Tabaka la
Ozoni.
SELEMANI SAIDI JAFO (MB.)
WAZIRI WA NCHI OFISI YA MAKAMU WA RAIS
MUUNGANO NA MAZINGIRA
No comments:
Post a Comment