Habari za Punde

Waziri Mhe.Jafo Atoa Rai Kwa Wakaazi wa Kongwa.

 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Selemani Jafo akizungumza na wakazi wa Kongwa kuhusu agenda ya mazingira mara baada ya kufanya ziara ya kikazi ya siku moja Wilayani hapo, Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Bw. Remidius Emmanuel

Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Bw. Remidius Emmanuel akizungumza na wananchi wa Wilaya ya Kongwa kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Selemani Jafo kuzungumza nao. Waziri Jafo amefanya ziara ya kikazi ya siku moja Wilayani hapo kuhimiza agenda ya mazingira.

Sehemu ya wakazi wa Kongwa wakimsikiliza Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Selemani Jafo (hayupo pichani) aliyefanya ziara ya siku moja Wilaya hapo hii leo.


Na Lulu Mussa KONGWA.                                                                                                             

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Selemani Jafo ametoa rai kwa wakazi wa Kongwa kutoa msukumo wa dhati katika agenda ya mazingira ikiwa ni pamoja na kupanda miti rafiki kwa mazingira.

Akiwa katika ziara ya kikazi ya siku moja Wilayani Kongwa Waziri Jafo ametoa rai hiyo leo kwa wana Kongwa na kuwataka kuunga mkono juhudi za Serikali za kuifanya Dodoma kuwa ya Kijani.

 "Ndugu zangu Kampeni ya kukijanisha Dodoma ni endelevu, na Kongwa ni sehemu ya Mkoa wa Dodoma, natoa rai kwenu mpande miti kwa wingi, sambamba na kilimo cha Korosho kama zao la kimkakati" Jafo alisisitiza.

Amesema agenda ya mazingira iende sambamba na upandaji wa miti kwa kila kaya walau miti mitatu ikiwemo ya kivuli na matunda ili jamii iweze kunufaika nayo sambamba na hifadhi ya mazingira ikiwa ni pamoja na ulinzi endelevu wa miundombinu kama vile barabara na madaraja.

Amesema Kongwa ya sasa si sawa na Kongwa ya zamani kutokana na uharibifu mkubwa wa mazingira unaotokana na shughuli za kibinadamu zisizo endelevu kama Ukataji wa miti kwa matumizi ya kuni na mkaa.

Waziri Jafo amesema Ofisi ya imezindua Kampeni Kabambe ya Kitaifa ya Uhifadhi na Usafi wa Mazingira kwa lengo la kunusuru taifa na majanga yatokanayo na uharibifu wa mazingira.

Ametoa wito kwa kila kaya kupanda miti walau mitatu, ikiwa ni pamoja na miti ya kivuli pamoja na matunda. Amesema upandaji wa miti utasaidia kuhifadhi miundombinu ya barabara na madaraja.

Nae Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Bw. Remidius Emmanuel amesema Wilaya ya yake inaendelea kuhamasisha jamii kutambua umuhimu wa kutunza mazingira ikiwemo kutokata miti, kutoharibu vyanzo vya maji, kutovamia misitu, kupanda miti na kuhifadhi visiki asili na takribani visiki hai 1,470,252 vimeainishwa na kutunzwa katika maeneo mbalimbali ya Wilaya hiyo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.