RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akishuhudia utiaji wa saini kwa ajili ya ujenzi wa bandari mpya ya Malindi ambayo itakuwa ya kitalii pamoja na mji wa kisasa katika eneo la Bwawani Mjini Zanzibar.akisaini kulia)Mkurugenzi wa Shirika la Bandari Zanzibar. Nahaat Mahfoudh na (kushoto) Bw.Mohamed Al Taooq alisaini kwa niaba ya Mamlaka ya Uwekezaji ya Oman.(Picha na Ikulu)
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza baada ya utiaji wa saini wa mpango mkuu na utafiti na uembuzi yakinifu kwa ajili ya ujenzi mpya wa bandari ya malindi Zanzibar, Mamlaka ya Uwekezaji ya Oman, hafla hiyo iliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar.(Picha na Ikulu)
KATIBU Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Mhandisi Zena Ahmed Said na Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi Zanzibar.Mhe Rahma Kassim Ali wakimsikiliza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi (hayupo pichani) akizungumza baada ya kumalizika kwa wa utiaji wa saini ya Ujenzi wa Bandari Mpya ya Malindi Zanzibar, hafla hiyo iliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo 20-1-2022.(Picha na Ikulu)
/BALOZI Mdogo wa Oman anayefanyia kazi zake Zanzibar Mhe.Said Salim Al Sinawi na (kushoto kwake) Sheikh. Nasser Al Harthy wakiwa na Maofisa wa Mamlaka ya Uwekezaji ya Oman Taasisi ya Serikali ya Oman, wakimsikiliza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi (hayupo pichani) akizungumza baada ya kumalizika kwa ya utiaji wa saini ya ujenzi wa Bandari Mpya Malindi Zanzibar hafla hiyo imefanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar.(Picha na Ikulu)
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Sheikh.Nasser Al Harthy (kulia kwa Rais) Balozi Mdogo wa Oman Anayefanyika Kazi zake Zanzibar Mhe Balozi.Said Salim Al Sinawi, baada ya kumalizika kwa Hafla ya utiaji wa Saini ya Ujenzi wa Bandari ya Malindi Zanzibar iliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar.(Picha na Ikulu)
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 20.01.2022
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali
Mwinyi ameshuhudia utiaji saini mpango mkuu na kufanya utafiti na upembuzi
yakinifu kwa ajili ya ujenzi wa bandari mpya ya Malindi ambayo itakuwa ya
kitalii pamoja na mji wa kisasa katika eneo Bwawani Mjini Zanzibar.
Utiaji saini huo umefanyika leo Ikulu
Zanzibar ambapo kwa upande wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar saini iliwekwa
na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi Amour Hamil Bakari
na kwa upande wa Mamlaka ya Uwekezaji ya Oman ambayo ni taasisi ya Serikali ya nchi
hiyo saini iliwekwa na Sheikh Nasser Al Harthy ambapo pia Mkurugenzi wa Shirika
la Bandari Nahaat Mahfoudh naye aliweka saini kwa upande wa Wizara hiyo na
Mohamed Al Taooq alisaini kwa niaba ya Mamlaka hiyo.
Akizungumza mara baada ya utiaji wa
saini huo, Rais Dk. Mwinyi alieleza kwamba katika mradi huo bandari mpya ya
Malindi ambayo inatarajiwa kujengwa mara baada ya kujengwa bandari ya mpya ya
Makontena huko Mangapwani itageuzwa kuwa bandari ya kitalii pamoja na kulitengeneza
eneo lote kutoka Bandarini Malindi hadi Bwawani Hoteli ili eneo hilo liwe na
majengo mapya ya burdani, hoteli na majengo ya kuishi.
Alisema kuwa eneo hilo ambalo
litakuwa la mji mpya wa kitalii linakisiwa kuwa na ukubwa wa hekta 30 ambazo
zitatokana baada ya kufukia Bahari katika eneo hilo ambalo litakuwa la mji mpya
wa kitalii.
Alieleza kwamba amefurahishwa
kutokana na hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kutafuta wawekezaji katika
maeneo mbali mbali, Serikali ya Oman mbali ya kutiliana saini na Serikali juu
ya ujenzi wa Bandari ya Makontena leo imetiliana saini tena na Serikali katika
ujenzi huo utakaopelekea kuwa na mji mpya wa kisasa hapo Malindi.
Rais Dk. Mwinyi alitoa shukurani kwa
kujitokeza kwa wawekezaji hao na kusema kwamba kiasi cha Dola milioni 500
zitatumika katika ujenzi wa mradi huo mkubwa wa kimkakati.
Alitumia fursa hiyo kuwapongeza
wawekezaji hao waliokuwa na nia ya kuekeza hapa Zanzibar na kusema kwamba
Zanzibar inaendelea kutafuta wawekezaji katika maeneo mbali mbali ambapo lengo
na madhubuni ni kwamba mpango wa maendeleo ya Zanzibar wa miaka mitano unatakiwa
kuwashirikisha sekta binafsi katika kusaidia na Serikali katika kujenga miradi
ya maendeleo yenye tija na ile ya kibiashara.
Aliongeza kuwa Serikali itaendeleza
jukumu lake la kuweka mazingira mazuri pamoja na kuwavutia wawekezaji ambapo kwa
yale mambo ambayo wawekezaji hawatoweza kuingia yatafanywa na Serikali kama
vile ujenzi wa barabara.
Aidha, Rais Dk. Mwinyi alieleza kwamba
wawekezaji hao kutoka Serikali ya Oman
wana moyo mkubwa hiyo ni kutokana na kuweka fedha nyingi katika mradi huo.
Nae Waziri wa Ujenzi,
Mawasiliano na Uchukuzi, Rahma Kassim Ali alisema kuwa ujenzi wa mradi huo
utasaidia kwa kiasi kikubwa katika kuiletea mendeleo endelevu Zanzibar.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya
Uwekezaji ya Oman Sheikh Mohamed Al Taooqi kwa upande wake alimuhakikishia Rais
Dk. Mwinyi kwamba Mamlaka hiyo itahakikisha mradi huo unafanikiwa na kufikia
malengo yaliyokusudiwa.
Mapema uongozi huo wa Mamlaka ya
Uwekezaji ya Oman ulimuonesha Rais Dk. Mwinyi michoro na ramani za mradi huo
ambao utakuwa wa aina yake na utaweza kuinua uchumi na maendeleo ya Zanzibar
ambapo Rais kwa upande wake alitoa shukurani zake na kupongeza hatua hiyo
iliyofikiwa.
Mamlaka ya Uwekezaji ya Oman pia,
ilishawahi kulitiliana saini na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar mnamo Januari
18 mwaka 2021 juu ya ujenzi wa bandari ya Mangapwani ambayo itajumuisha bandari
tofauti ikiwemo ya makontena na mizigo mchanganyiko kazi ambayo hivi sasa
inakwenda vizuri na iko katika hatua ya Upembuzi yakinifu na hatimae itaingia
katika utekelezi wa ujenzi.
Imetayarishwa na Kitengo cha Habari
Ikulu Zanzibar.
No comments:
Post a Comment