Habari za Punde

Serikali itaendelea kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu katika mazingira mazuri



Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar  Mhe. Simai Mohammed Said akifanya mahojiano maalum na Kituo cha Habari Elimu na Mawasiliano Kwarara (KMEC)
 Na Maulid Yussuf na Fat-hiya Mohammed, WEMA


Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar  Mhe. Simai Mohammed Said amesema Serikali ya awamu ya nane itaendelea kuhakikisha Wanafunzi wote wanapati elimu katika mazingira mazuri na salama.

Amesema hayo wakati alipofanya ziara Katika Skuli ya Sekondari Kwarara  Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja na kuzungumza na Wanafunzi  wa kidato cha pili ambao wanarudia darasa baada ya kukosa vigezo vya kuungia kidatu cha tatu.

Amesema  Wizara inaendelea na juhudi za kuwataka Walimu kuhakikisha wanakua karibu na Wanafunzi ili waweze kutoa hisia zao kwani hali hiyo itasaidia kujua mbinu za kuweza kujua ni namna gani wataweza kuhakikisha Mwanafunzi anafaulu vizuri.

Amesema kutokana na umuhimu wa elimu kuna haja ya kushirikiana baina ya wazazi, walimu na jamii kwa ujumla ili kuhakikisha  watoto wote wanapata  haki hiyo  wakiwa karibu na wasimamizi wao kwa upendo wa hali ya juu.

Pia amewasisitiza wazazi na jamii kuwasimamia  watoto  kudurusu masomo yao wanapokuwa katika mazingira ya nje ya skuli ili kusaidia kupata ufaulu katika masomo yao.  

Aidha amewasisitiza Wanafunzi hao kuwa na moyo wa kusoma zaidi pamoja na kuwapa hamasa ya kuwa   kurudia kwao sio mwisho wa kutimiza ndoto zao bali wawe  na matumaini ya kusoma na kupasi zaidi.

Amesema akiwa yeye ni  Waziri anayesimamia elimu yupo tayari kuhakikisha anashirikiana na wadau wote wa elimu ili Taifa liweze kuzalisha wataalamu wa fani mbalimbali.

Katika hatua nyengine Mhe Simai amemtaka Mwalimu Mkuu wa Skuli hiyo kuhakikisha anashirikiana na Uongozi wa Kituo cha Habari Elimu na Mawasiliano kwa  kupanga utaratibu wa kuwafundisha Wanafunzi wa Skuli hiyo namna ya kutumia teknolojia ya Tehama ili waweze kunufaika na uwepo wa Kituo hicho.  

Nae Mwalimu Mkuu wa Skuli ya Sekondari Kwarara mwalimu Hussein Ali amesema wanachangamoto ya upungufu wa Walimu hasa wa masomo ya Sayansi pamoja na mrundikano wa Wanafunzi madarasani ambapo wameombwa kujengewa madarasa pamoja na holi ili yawese kusaidia kupunguza changamoto hiyo.

Kwa upande wao Wanafunzi hao wamesema wamefarijika sana kuonana waziri  wao na kujua changamoto zao ambapo amesema upungufu wa walimu ni chanzo cha ufaulu mdogo.

Wamesema kua Mwalimu mmoja anapokua na vipindi vingi kwa siku hupelekea kukosa kusoma kwa utulivu na kupelekea wao kutofahamu somo husika.

Wakati huo Mhe Simai  alifika katika  Kituo cha Habari Elimu na Mawasiliano Kwarara (KMEC) na kufanya mahojiano maalumu kupitia chanali ya EZ tv, ambapo  amewashauri wamiliki wa Skuli binafsi kukitumia kituo hicho kwa kupeleka vipindi vyao mbalimbali vya kielimi ili kuweza kuisaidia jamii kujifunza kupitia televisheni.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.