Habari za Punde

Zawadi 'NMB MastaBata - Kivyako Vyako' zafikia Mil. 30/-

 

Ofisa Huduma kwa Wateja Makao Makuu NMB, Suzan Manga (kulia) akizungumza na mmoja wa washindi wa droo ya tatu ya NMB MastaBata Kivyakovyako iliyochezeshwa leo jijini Dar es Salaam. Katikati ni Ofisa Mwandamizi Idara ya Kadi NMB, Bw. Said Kiwanga pamoja na Mwakilishi wa Bodiya Michezo ya Kubahatisha Nchini, Elibariki Sengasenga wakifuatilia tukio hilo.

Ofisa Mwandamizi Idara ya Kadi NMB, Said Kiwanga akibofya kitufe kutafuta washindi kwenye droo ya tatu ya NMB MastaBata Kivyakovyako iliyochezeshwa leo jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mwakilishi wa Bodiya Michezo ya Kubahatisha Nchini, Elibariki Sengasenga pamoja na Ofisa Huduma kwa Wateja Makao Makuu NMB, Suzan Manga.

Na.Mwandishi Wetu.

WATEJA 100 wa Wiki ya Tatu ya Kampeni ya 'NMB MastaBata - Kivyako Vyako,' wamepatikana jana (Alhamisi Januari 20), na kutwaa jumla ya Sh. Milioni 10, hivyo kufanya zawadi zilizotolewa hadi sasa kufikia Sh. Mil. 30 kati ya zaidi ya Sh. Mil. 200 zinazoshindaniwa.

NMB MastaBata ni kampeni ya wiki 10 inayoendeshwa na Benki ya NMB, ikilenga kuhamasisha wateja kufanya malipo na manunuzi kwa njia ya kadi za MasterCard, Masterpass QR, Vituo vya Mauzo (PoS) na mtandaoni, ambako zaidi ya wateja 1,080 watazawadiwa pesa taslimu.

Katika kampeni hiyo (ambayo huu Ni msimu wake wa tatu), wateja 100 kila wiki huzawadiwa Sh. 100,000 kila mmoja, huku washindi 25 wa droo za mwisho wa mwezi wakijishindia kiasi hicho cha pesa, ambako 'Grande Finale' ikitarajia kutoa washindi 30 watakaojinyakulia Sh. Milioni 3 kila mmoja.

Akizungumza kabla ya droo hiyo iliyofanyika jijini Dar es Salaam, Ofisa Mwandamizi wa Biashara ya Kadi wa NMB, Saidi Kiwanga, alisema kampeni hiyo imeonesha ufanisi mkubwa katika kuelimisha wateja wao kuwa kadi ni zaidi ya kutolea pesa, badala yake ni njia salama na nafuu ya kufanya malipo ya manunuzi mbalimbali.

"Katika wiki mbili zilizopita, wateja 200 wamejishindia Sh. Mil. 20 na leo tutapata washindi wengine 100 na hivyo kufikisha watu 300 walionufaika na zawadi za Sh. Mil. 30. Hakuna changamoto yoyote katika wiki tatu za kampeni hii, zaidi ya ufanisi na elimu pana kwa wateja wetu ya kutambua uwanda mpana unaopatikana kupitia kadi zao na PoS.

"Kiasi hiki cha Sh. Mil. 30 ni kati ya zaidi ya Sh. Mil. 200 zinazoshindaniwa kwa wiki 10, ambako kila wiki tunawazawadia washindi 100, droo za mwisho wa mwezi tutatoa zawadi kwa wateja 25 na katika fainali mwishoni mwa kampeni hii mwezi Machi, tutakuwa na washindi 30 ambao watajitwalia Sh. Mil. 3 kila mmoja," alisema Kiwanga.

Kwa upande, Ofisa Msimamizi kutoka Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania (GBT), Elibariki Sengasenga, aliwahakikishia wateja wa NMB kuwa kampeni hiyo inaendeshwa kwa kufuata taratibu zote zinazosimamia na bodi yake na kuwataka kuondoa shaka juu ya upatikanaji wa washindi wake.

"GBT ni waratibu na wasimamizi wakuu wa Michezo ya Kubahatisha Tanzania. Jukumu letu ni kuhakikisha sheria, kanuni na taratibu zinafuatwa. Tunawahakishia wateja wa NMB kuwa kampeni hii inatoa washindi kihalali, wawe huru kufanya matumizi kwa kadi ambacho ndio kigezo kikuu cha kuingia katika droo na bahati zao zitaamua ushindi wao," alisisitiza Sengasenga.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.